MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
UFUNDISHAJI WA LUGHA YA PILI

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
UFUNDISHAJI WA LUGHA YA PILI
#1
Utangulizi
Kuna mikabala/ mikondo mbalimbali katika historia ya ufundishaji wa lugha ya pili  ambayo  imewahi  kutumiwa.  Baadhi  ya  mikabala  hiyo,  mpaka  sasa  imeendelea kuathiri ufundishaji wa lugha ya pili. Ujuzi wa mikabala hiyo ni jambo muhimu kwa mwalimu wa Kiswahili kwa sababu unaweza kumsaidia kupata fununu kuhusu asili ya mbinu  tofauti  tofauti  zinazotumiwa  kufundisha  lugha  ya  pili. Hapo  awali  mbinu  hizi zililenga hasa ufundishaji wa lugha ya Kingereza kama lugha ya pili. Hata hivyo, baadhi ya  mambo  ambayo  hupendekezwa  katika  mbinu  hizo  yanaweza  kumsaidia  mwalimu ambaye anajishughulisha na ufundishaji wa Kiswahili kama lugha  ya pili.
Madhumuni Ya Somo
Kufikia mwisho wa somo hili utaweza kutoa mifano ya mbinu za kufundishia lugha na kueleza jinsi kila mojawapo ya mbinu hizo inaweza kutumiwa katika ufundishaji wa Kiswahili.
Mbinu Ya Kimapokeo
Hii ni mbinu ambayo hapo awali ilitumika kama njia ya kufundishia lugha za kijadi  kama  vile  Kiyonani  na  Kilatini.  Ilitawala  ufundishaji  wa  lugha  za  kizungu  na kigeni kati ya miaka 1840 na 1940. Lengo kuu la mbinu hii ni kufanikisha ufahamu wa sarufi  pamoja  na  uwezo  wa  kuandikia  kwa  usahihi  katika  lugha  inayolengwa.  Pia inalenga kuwezesha mwanafunzi kuwa na upeo mpana wa msamiati unaotumika sana katika lugha ya uandishi katika lugha husika, ili hatimaye aweze kuthamini umuhimu pamoja na thamani ya nakala zinazohusika.
Katika mazingira ya darasani, mwalimu anatazamiwa kutekeleza malengo haya kwa kushirikisha wanafunzi katika kazi ya kutafsiri mara kwa mara kutoka lugha zao hadi  katika  lugha  inayofunzwa.  Kabla  ya  kutafsiri,  wanafunzi  wanapaswa  kwanza kijifunza maneno ya lugha inayolengwa ili waweze kutafsiri katika lugha mpya. Pamoja na  hayo,  wanafunzi  wanapewa  maelezo  marefu  kuhusu  sheria  za  kisarufi.  Kisha wanapewa zoezi la kutunga sentensi ili kubainisha ufahamu wao wa sheria hizo. Uwezo wa  mwanafunzi  katika  kutafsiri  huwa  ndicho  kigezo  muhimu  kinachotumiwa  kama chombo cha kupima ustadi wake katika kipengele cha sarufi na msamiati.
Udhaifu hasa wa mbinu hii ni kwamba haitilii mkazo juu ya matamshi sahihi pamoja na stadi za kimawasiliano. Inasisitiza sana ujuzi wa sheria za kisarufi bila kupatia wanafunzi nafasi ya kutosha kujieleza kutokana na nafsi zao. Matokeo ya kujishughulisha sana na ufundishaji wa kanuni na vighairi ni kwamba waalimu huishia kwa kufundisha wanafunzi lugha ya ulimwengu wa vitabu, lugha isiyokuwa na uhai, na ambayo mara nyingi haina manufaa katika ufanikishaji wa mawasiliano ya kawaida.
Utumiaji wa mbinu hii unalifanya somo la lugha kukosa ubunifu unaotakikana. Wanafunzi hawapati nafasi ya kutumia lugha kama chombo wanachoweza kukitegemea kutekeleza mahitaji yao ya kimawasiliano. Shughuli ya kujifunza lugha inageuka kuwa zoezi la kukariri maneno chungu nzima na kanuni kemkem za kisarufi. Hakuna hakikisho kwamba baada ya kukariri maneno na kanuni wanafunzi watakuwa na uwezo wa kutumia kanuni  na  maneno  vilivyokaririwa  katika  mawasiliano  ya  nje  ya  darasa.  Shughuli  ya kufundisha na kujifunza lugha inakuwa kama zoezi la kuchemsha bongo tu.
Mbinu Ya Moja Kwa Moja
Hali ya kutoridhika na mbinu ya kimapokeo ni miongoni mwa mambo ambayo yalichangia kuibuka kwa mbinu ya moja kwa moja. Iliibuka katika karne ya 19 kuchukua mahali  pa  mbinu  ya  kimapokeo.  Wanaopendelea  mbinu  hii  hushikilia  kwamba  njia mwafaka ya kujifunza lugha ya pili ni kukabiliana nayo moja kwa moja na kuitumia kama vile mtoto mdogo anavyofanya anapojifunza lugha ya mama. Kulingana na mbinu hii ni marufuku kutumia lugha ya wanafunzi au lugha nyingine yo yote ile.
Mbinu hii husisitiza umilisi wa lugha bila tafsiri wala maelezo rasmi juu ya sheria za kisarufi. Wanafunzi wanatakiwa kijifunza lugha kwa kushirikishwa kikamilifu kama wahusika watendaji katika matumizi tofauti tofauti ya lugha. Inasisitizwa kwamba ikiwa maana inaweza kuwasilishwa moja kwa moja kwa kushirikisha maono au vitendo hakuna haja ya kutafsiri.
Kwa upande wa sarufi, mbinu hii inashikilia kwamba njia bora ya kuendeleza ufahamu wake ni kutokana na uzoefu wa kutumia mara kwa mara lugha inayohusika. Mwanafunzi akipewa fursa ya kutosha kukumbana na matumizi ya lugha, itakuwa rahisi kwake kutambua na kujifunza sheria zinazotawala sarufi ya lugha hiyo. Mbinu hii inasisitiza haja ya kutoa nafasi kwa mwanafunzi ya kujifunza lugha kama vile mtoto anavyojifunza lugha yake ya kwanza. Mtoto anajifunza na kuimudu lugha kwa kukumbana nayo moja kwa moja katika mkutadha maalum wa mawasiliano.
Hakuna mtu anayemfafanulia kanuni za kisarufi za lugha yake. Hata hivyo anazing’amua kanuni hizo yeye mwenyewe baada ya kushuhudia matumizi yake katika vielelezo vya sentensi. Huwa anajifunza lugha ya jamii yake katika mazingira yanayoshirikisha vitendo na maono. Ushirikishaji wa maono na vitendo unachangia kujenga hali ambayo husaidia mtoto  kukisia  maana  ya  kile  kinachosemwa. Anajifunza  lugha  ya  jamii  yake  kwa kusikiliza kwanza na baadaye kuigiza yale anayosikiza.
Kwa mujibu wa mbinu hii mwalimu anapofundisha lugha ya pili anashauriwa kutotegemea  tafsiri.  Anashauriwa  vile  vile  kutofundisha  moja  kwa  moja  sheria  za kisarufi.  Ana  wajibu  wa  kuambatanisha  ufundishaji  wake  na  vitendo,  uigizaji  na mazungumzo. Lakini ikiwa mwalimu hana budi kufundisha sarufi, inafaa ufundishaji wa sarufi uzingatie kiwango cha matumizi ya lugha huko mkazo ukitiliwa juu ya madondoo ya kisarufi yanayotumika sana sana hasa katika mazungumzo.
Kwa mujibu wa mbinu hii, dhima ya mwalimu ni kupanga na kufanikisha utumizi wa lugha badala ya kujishughulisha na ufafanuzi pamoja na uchambuzi wa kanuni za kisarufi. Ili mwalimu aweze kufaulu kutumia mbinu hii anapaswa kuwa na ujuzi wa kiwango cha hali ya juu katika lugha anayofundisha. Ni lazima pia awe na ubunifu wa kumwezesha kuwasilisha maana bila kutumia lugha nyingine yo yote zaidi ya ile ambayo anafundisha.  Anatarajiwa  pia  kujitahidi  kujenga  mazingira  ya  kufundishia  ambayo yanakaribia kufanana yale ya lugha ya kwanza. Mazingira hayo yanatarajiwa kufanikisha ufahamu wa lugha kupitia mazoezi ya kusikiliza pamoja na mazungumzo. Lazima yawe mazingira   ambayo   yanaweza   kuchangia   katika   kuhamasisha   mwanafunzi   kutaka kujifunza lugha inayohusika.
Kwa kawaida mtoto anapojifunza lugha yake ya kwanza anakuwa na hamu ya kujifunza lugha hiyo ili aweze kutangamana na jamii ya watu wanaomzunguka. Jamii hiyo pia humsaidia kuendelea kwa kumtia shime. Pamoja na hayo mtoto huwa na muda mwingi wa kusikia na kutumia lugha hiyo. Lugha inakuwa sehemu ya maisha yake ya kila siku.
Mbinu Ya Uzungumzi
Mbinu hii ilizuka na kukita mizizi katika miaka ya 1950 kutokana na mwamko mpya nchini Amerika wa kujishughulisha na ufunzaji wa lugha za kigeni. Tukio muhimu ambalo lilichangia pakubwa kuamsha ari ya Wamerika katika lugha za kigeni ilitokea mnamo mwaka wa 1957. Mwaka huo Warusi walifaulu kupeleka chombo chao (sputnik) angani. Jambo hili lilikuwa changamoto kubwa kwa taifa la Amerika. Kufuatia tukio hilo, serikali ya Amerika iliamua kujishughulisha kikamilifu katika ufundishaji wa lugha za kigeni ili isiachwe nyuma katika maendeleo ya kisayansi. Jambo ambalo linapewa kipaumbele katika mbinu hii ni ufasaha wa kuzungumza.
Ufasaha unaotarajiwa unahusu matamshi bora, sarufi, pamoja na uwezo wa kuitikia upesi na kwa urahisi katika hali tofauti zinazohusisha utumizi wa lugha katika mazungumzo.
Ufahamu  sikizi,  matamshi,  sarufi  na  msamiati  vinapofundishwa  huwa  kama  njia mojawapo   ya      kufanikisha ufasaha       wa     kuzungumza. Vilevile wanafunzi wanaposhirikishwa katika kuandika na kusoma mambo haya yanaambatanishwa na ustadi wa kutumia lugha ya mazungumzo. Kulingana na mbinu hii, stadi za lugha zinastahili kufundishwa kwa kuzingatia mfuatano huu: Kusikiliza, Kuongea, Kusoma na Kuandika.
Katika hatua za mwanzo mwanzo, kusoma na kuandika vinachukuliwa tu kama mambo  ambayo  yanaweza  kuchangia  kuimarisha  ustadi  wa  kusikiliza  na kuongea.
Vinatiliwa mkazo zaidi katika viwango vya juu wakati ambapo wanafunzi wana uzoefu unaofaa ili kuweza kukabiliana na mitindo zaidi ya lugha ya kimaandishi. Madondoo ya lugha yanapofundishwa kwa   kutumia      mbinu         hii      huwa yanawasilishwa  kupitia  mjadala  ambao  ni  chombo  muhimu  cha  kutoa  mkutadha  wa kufundishia  kile  kinacholengwa.  Zaidi  ya  kushiriki  katika  mjadala,  wanafunzi  huwa wanatakiwa, mara kwa mara, kukariri vielelezo vya sentensi.
Mbinu Ya Mawasiliano
Msingi  wa  mbinu  hii  ni  imani  kwamba  kazi  kuu  ya  lugha  ni  kufanikisha maingiliano   pamoja   na   mawasiliano   katika   jamii.   Lugha   ni   chombo   ambacho kinamwezesha binadamu kushirikiana na watu wengine na pia kutekeleza mahitaji ya maisha yake. Kwa hivyo, kulingana na waasisi wa mbinu hii, lengo kuu la kufundisha lugha  ni  kuwezesha  mwanafunzi  kuwa  na  uwezo  wa  kuwasiliana  akitumia  lugha inayohusika.
Njia moja ya kuhakikisha kuwa mwanafunzi anakuwa na uwezo wa kuwasiliana ni, kwanza, kumpa fursa ya kushiriki kama mhusika mpokezi. Mwanafunzi  anapata fursa ya kupanua upeo wake wa lugha kupitia kusikiliza na kusoma. Baada ya kushiriki katika matumizi ya lugha akiwa mhusika mpokezi mwanafunzi anashirikishwa kama mhusika mwanzilishi wa mawasiliano. Kulingana na waasisi wa mbinu ya mawasiliano, lugha ambayo ni ya maana / manufaa kwa wanafunzi inatilia nguvu juhudi za kujifunza. Kwa hivyo ni muhimu kwa walimu kuhakikisha kwamba wanapochagua kazi ya wanafunzi wanatilia  maanani  uwezo  wa  kazi  hiyo  wa  kuwashirikisha  katika  matumizi  ya  lugha yenye maana na uhalisi.
Kwa kawaida, mawasiliano hufanyika katika mazingira ya watu wakiwa katika vikundi. Pia, aghalabu, mawasiliano huchukua mkondo wa mazungumzo (conversation) na  majidiliano  (discussion).  Wakizingatia  ukweli  huu,  wanaounga  mkono  mbinu  ya kimawasiliano wanapendekeza kugawanya  wanafunzi katika vikundi vidogo vidogo. Hii ni njia bora ya kuendeleza uwezo wa wanafunzi wa kuwasiliana kwa kutumia lugha inayofundishwa. Wakiwa katika vikundi vya watu wachache, wanafunzi wanakuwa na fursa bora ya kutumia lugha halisi. Pia wanapata nafasi ya kujieleza kwa ufasaha bila wasiwasi.  Ustadi  katika  kusoma  na  kuandika  unaweza  kukuzwa  kutokana  na  msingi imara wa kutumia lugha kwa uhalisi.
Je  jukumu  hasa  la  mwalimu  ni  nini?  Kwa  mujibu  wa  waasisi  wa  mbinu  hii, jukumu la mwalimu ni kuhamasisha wanafunzi na kutoa kwao nafasi ya kujieleza katika lugha  inayohusika.  Ana  wajibu  wa  kuhamasisha  wanafunzi  kutumia  lugha  kwa  njia mbalimbali. Anapaswa pia kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi anapata fursa ya kujieleza.
Pamoja na hayo, mwalimu ana wajibu kuhakikisha kwamba wanafunzi wanaelewa vizuri kwa nini wanafundishwa kile wanachofundishwa. Hivi ndivyo watakavyoweza kushiriki kwa  njia  ya  maana  na  manufaa  kwao.  Vilevile  ni  lazima  mwalimu  ahakikishe  kuwa wanafunzi wake wanahusika zaidi kuliko vile anavyohusika mwenyewe.
Aidha,  mwalimu  anashauriwa  kushirikisha  wanafunzi  katika  vitendo  ambavyo vinaweza   kuwalazimisha   kuwasiliana   kwa   kutumia   lugha   inayofaa   kulingana   na mkutadha. Kwa maneno mengine, mwalimu anapaswa kubuni hali na mazingira ambamowanafunzi  hawawezi  kukidhi  mahitaji  na  matarajio  yao  bila  kuwasiliana.  Wakijikuta katika  mazingira  ya  namna  hii  hawatakuwa na  budi  kutafuta  ufumbuzi  kwa  kutumia lugha.  Kwa  ufupi,  mwalimu  anaweza  kusaidia  kuendeleza  uwezo  wa  wanafunzi  wa kuwasiliana wakitumia lugha kwa kuzingatia mfuatano wa hatua zifuatazo:
  1. Mapokezi ya lugha.
  2. Ufafanuzi / Maelezo
  3. Majaribio ya matumizi ya lugha
  4. Mawasiliano huru
Katika hatua ya mapokezi wanafunzi wanashiriki kama wahusika wapokezi. Kazi yao katika hatua hii ni kupokea ujumbe unaowasilishwa na watu wengine na kupata maana  ya  ujunbe  unaowasilishwa.  Wanaweza  kutekeleza  jambo  hili  kupitia  zoezi  la kusikiliza au kusoma. Zoezi la kusikiliza husaidia wanafunzi kupata nafasi ya kupanua upeo  wa  lugha.  Kupitia  zoezi  hili  wanaweza  kujifunza  msamiati  mpya  na  miundo mbalimbali  ya  kisarufi.  Vilevile  wanafunzi  wanaimarisha  ujuzi  wao  wa  yale  ambayo wamejifunza tayari.
Kwa upande mwingine, katika hatua ya ufafanuzi (maelezo) mwalimu anaweza kudondoa madondoo fulani ya lugha ambayo wanafunzi wamewahi kukumbana nayo, katika zoezi la kusikia na kusoma. Kisha anatoa maelezo kuhusu madondoo hayo ili wanafunzi   wayatilie   maanani   zaidi   kuliko   mengine   kwa   wakati   huo.   Baada   ya kuhakikisha   kwamba   wanafunzi   wanafahamu   kiini   cha   somo   mwalimu   anawapa wanafunzi  nafasi  ya  kujaribu  kutumia  madondoo  hayo  katika  vielelezo  vya  sentensi wakizingatia maagizo yaliyotolewa.
Katika hatua ya mawasiliano huru wanafunzi wanapata fursa zaidi ya kujieleza bila kufuata maagizo ya mwalimu. Wanaweza kujieleza kwa njia halisi kulingana na mahitaji  ya  mawasiliano  katika  mkutadha  unaohusika.  Wanafunzi  watateua  lugha kulingana na hali halisi inayowakabili wakati huo. Mawasiliano huru huwapa wanafunzi fursa ya kutambua kuwa lugha siyo somo ambalo linajikita katika mipaka ya mazingira ya  darasani  tu,  lakini  pia  ni  chombo  cha  mawasiliano  nje  ya  mipaka  ya  darasa.
Mawasiliano huria huwapa wanafunzi nafasi ya kutumia lugha kwa njia ya ubunifu katika miktadha tofauti tofauti ya kijamii. Wanatumia lugha bila usimamizi wa mwalimu, lakini kulingana  na  hali  halisi  katika  mazingira  ya  mawasiliano.  Huwa  wajitegemea  wao wenyewe. Kadiri wanavyoshiriki katika mikutadha tofauti ya mawasiliano na kushuhudia jinsi lugha inavyotumiwa, ndivyo wanavyoendelea kukuza na kuimarisha uwezo wao wa kimawasiliano (communicative competence). Uwezo huu ni muhimu kwa mwanafunzi kwa sababu akiwa nao anaweza kufasiri lugha kwa njia iliyo sahihi akizingatia mkutadha unaohusika.  Na  akifanya  hivyo  anaweza  kuitikia  kama  inavyotarajiwa.  Kwa  mfano mwalimu  akiingia  darasani  ambamo  mna  joto  jingi  na  agundue  kuwa  madirisha yamefungwa,  anaweza  akasema:  Mbona  joto  limezidi  sana  humu  ndani.  Mwanafunzi mwenye  uwezo  wa  kimawasiliano  atatambua  kuwa  mwalimu  angetaka  madirisha yafunguliwe, na ataitikia kwa kuyafungua. Yule asiyekuwa na uwezo huo atachukulia usemi wa mwalimu kama kauli ya kawaida tu.
Msingi wa Mbinu ya Kimawasiliano
Asili ya mbinu ya kimawasiliano ni imani inayoshikilia kwamba:
(a) Lugha ni mfumo wa kueleza maana.
(b) Jukumu kuu la lugha ni kufanikisha maingiliano na mawasiliano baina ya watu.
© Shughuli  ambazo  zinachangia  kufanikisha  ufahamu  wa  lugha  ni  zile ambazo  zinatoa  kwa  wanafunzi  nafasi  ya  kushiriki  katika  mawasiliano halisi (real communication).
(d) Vitendo  vinavyohusisha  matumizi  ya  lugha  ili  kutekeleza  shughuli  za maana (meaningful tasks) husaidia kufanikisha ujuzi wa lugha.
(e) Lugha yenye maana kwa wanafunzi inaimarisha hali ya kujifunza.
(f) Mawasiliano hufanyika ikiwa wale wanaohusika wana hamu (motisha) ya
kuwasiliana.
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)