MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
Dhana ya Uhuru wa Mwandishi

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
Dhana ya Uhuru wa Mwandishi
#1
Dhana ya Uhuru wa Mwandishi
E. Kezilahabi
Dhana ya Uhuru
Tunapozungumzia uhuru kama dhana ya kifalsafa mara nyingi huwa tunafikiria uwezo wa mtu binafsi wa kufanya uamuzi, kujijua, kujiendesha kujirekebisha. Lakini pia huwa tunatia maanani mkondo ambao uko nje ya nafsi. Mkondo huu wa nje huwa na uwezo wa kuathiri na wakati mwingine huongoza moja kwa moja na kutoa kauli ya mwisho kuhusu jambo la kutenda. Wakati mwingine nguvu za ndani au utashi wa nafsi ya mtu huweza kuwa na nguvu zaidi ya mkondo wa nje.
Kwa muda mrefu katika historia ya falsafa ya Kimagharibi kulikuwa na imani iliyotawala – kwamba uwezo wa kutoa sababu au utumiaji wa akili ndilo jambo limtofautishalo binadamu na mnyama. Kufuatana na falsafa hii binadamu anatakiwa kuzitawala hisia zake kwa kutumia akili. Hisia zikiachwa peke vake haziaminiki kwa sababu mara nyingi huoneoza kwenve njia ambayo hatima yake ni madhara. Kwa sababu hii mwanafalsafa wa Kiyunani, Plato, hakuwa na imani na ushairi.
Lakini, je ni kweli kwamba kwa muda wote huu katika historia binadamu amekuwa akitumia akili? Swali hili linakuwa gumu tunapokumbana na ukweli wa mambo kama: utumwa, vita vya dunia, ubaguzi wa rangi, nafasi finyu aliyonayo mwanamke katika jamii, hatari ya kuteketezwa kwa dunia na silaha kali za nyukliya, na njama za ubeberu.
Ukweli wa mambo haya umeleta fikra mpya katika mijadala ya kifalsafa na kielimu jamii. Wanafalsafa wa existentialism ndio waliokuwa wa kwanza kufikiria upya misingi ya falsafa iliyopita. Waliona kwamba mambo haya yote yanaambatana na uhuru pamoja na mtazamo rahisi kuhusu maisha aliokuwa nao mwanadamu. Waliona kuwa masuala yote yanahusiana na kuwako (existence au being there) au kutokuwako (nothingness). Haya ni maswali muhimu yanayomkabili binadamu wa leo. Kwa hiyo uhuru ni katika kuwako na kutokuwako (being & nothingness) na uamuzi (choice) anao binadamu mwenyewe. Katika aya zinazofuata nitajaribu kueleza zaidi dhana hii ya uhuru.
Tunaweza kusema kwamba binadamu katika kuusaka uhuru ni kama mtoto mdogo ambaye ameanza kufurahia uwezo wake wa kutembea. Mtoto huyu anaona kipepeo mwenye rangi nzuri ametua juu ya ua. Anataka amshike kwa mkono. Kila anapomkaribia anaruka. Mtoto, bila kukata tamaa, anaendelea kumfuata hadi anapojikuta msituni; mwishowe giza linaingia, haoni njia ya kurudi, woga unamwingia, anatoa kilio kuomba msaada akifikiri wazazi wake wako karibu. Uhuru basi haushikiki. Ubora na umuhimu wake vimo katika kutoshikika au kutopatikana. Tungekuwa nao tusingeishi maana maisha yasingekuwa na kitu kijulikanacho kama telos, yaani kile kinachosakwa au nia. Tunaweka juhudi katika shughuli zetu za kila siku kwa sababu ya utupu (nothingness) ambao hutakiwa kujazwa lakini haujaziki. Ni kama kujaza maji ndani ya pakacha. Katika kufanya hivyo tunaishi. Uhuru basi umo katika utupu, katika kutokuwa nao.
Ni kweli tunaweza kupata uhuru wa bendera, tukashangilia sana. Mara tunajikuta katika mfumo wa jitihada – jitihada ya kufanya hali ya uchumi iwe nzuri zaidi. Kubadilisha hali ya maisha ya watu. Kwa hiyo tunakata mirija yote ya unyonyaji. Tunajikuta katika mfumo mwingine – mfumo wa kukata na kukatwa. Katika vita hivi mkulima anaumia zaidi. Polepole neno ushindi linabadilishwa kuwa kujaribu. Kila kiongozi anayekuja anasema atajaribu, atajitahidi kubadilisha hali. Kwa hiyo tunaweza kuongezea kwamba uhuru umo katika kujaribu na kujitahidi, na tunasukumwa mbele na mabadiliko ambayo yana rangi ya kipepeo.
Tunaweza pia kufanikiwa maishani, tukapata mali na vinginevyo. Tunaweza kutamani kujenga nyumba, tukapata pesa tukajenga. Baada ya muda tunasahau kuwa hata hiyo nyumba moja hatukuwa nayo awali, tunajenga ya pili. Katika kusahau, tunajisukuma mbele. Tunatamani kitu kingine, na katika kutamani tunajisukuma mbele. Tunaishi. Katika mtazamo huu kutamani na kusahau si ila. Si vibaya kusahau unakwenda wapi. Inapasa kuwa hivyo. Unaweza kusema unakwenda mjini. Hakuna mtu, wakati anakwenda mjini, akumbukaye kila sekunde kwamba anakwenda mjini. Unafika mjini kwa kusahau kuwa unakwenda mjini. Ni vizuri kusahau marehemu uliowafahamu, la sivyo vivuli vyao vitakutokea mara nyingi na utajiona huna uhuru. Utahama nyumba na nyumba. Ni vizuri kusahau makosa tuliyotenda. Kama binadamu angekumbuka daima makosa yake yOte, asingeishi. Hata mwaka mmoja. Kwa hiyo tunaweza kusema kuwa uhuru umo katika kusahau (forgetting). Tunasahau hata majina yetu; tunayakumbuka tunapoitwa. Katika kusahau mambo hupeana nafasi katika kichwa cha binadamu.
Tunaweza kujiuliza swali moja muhimu. Nini kitusukumacho mbele? Jibu ni utashihuru (free – will). Hapa utashihuru hauna maana ya kufanya upendalo bali linalotakiwa kuwa. Gurudumu ukilisukuma kutoka juu kilimani linatakiwa au lazima litajiviringisha lenyewe. Muundo wake, pamoja na misingi ya kisayansi, vinafanya lizunguke lenyewe bila mkondo wa nje. Hapa sina nia ya kusema kuwa gurudumu lina utashihuru bali hali ya gurudumu inalinganishwa na utashihuru wa binadamu. Utashi huu unaambatana na kutamani (desire) pamoja na mahitaji (need(s). Utashi ni moja kati ya nguzo muhimu zilizopo katika dhana ya uhuru wa mwandishi ambako mjadala huu unaendelea.
Dhana ya Uhuru wa Mwandishi
Bila utashi mwandishi atakuwa mwoga na mwepesi wa kukata tamaa. Atayumbishwa haraka kutoka kwenye msingi ya falsafa yake na imani aliyonayo juu ya mabadiliko yatokeayo katika nchi yake. Makombora ya wahakiki na wanasiasa huweza sana kuyumbisha; lakini kwa mwandishi mwenye utashi makombora haya hukomaza. Nitatoa mifano miwili ya waandishi wawili wa Kiafrika ambao wameonyesha dhahiri utashi wao. Waandishi hao ni Wole Soyinka na Ngugi wa Thiong’o. Hapa Afrika hakuna mwandishi ambaye amepata kushambuliwa na wahakiki kama Soyinka. Lakini msimamo wake ni uleule, na si mtu wa kuyumbishwa na makala. Tukumbuke kuwa amepata pia kufungwa, na alipotoka kifungoni hakubadili msimamo wake. Misukosuko iliyompata Ngugi wa Thiong’o watu wa Afrika ya Mashariki twaijua. Ngugi hajatetereka na hajayumbishwa. Waandishi hawa wawili wameweza kuwa hivyo kwa sababu ya utashi na falsafa zao.
Tunaweza kusema kwamba uhuru wa mwandishi kwanza kabisa umo katika utashi. Katika fasihi ya Kiswahili waandishi wenye utashi wapo? Bila kutaja majina nafikiri wapo. Na msingi wa kuwako kwao ni kutoyumbishwa na matamshi ya jukwaani na wahakiki ambao hawajapevuka. Msingi wa pili unawahusu hasa wale waandikao katika lugha ya Kiswahili. Kwa muda mrefu hapa nchini pamekuwa na wazo potovu linalotawala: kwamba maandishi ya Kiswahili hayana hadhi. Nimeona wanafunzi wasomao Kiswahili Chuo Kikuu wakifichaficha vitabu vya Kiswahili wasionekane kuwa wanasoma Rosa Mistika, Nyota ya Rehema, n.k. Ila wakiwa na The Interpreters, ingawa hawakielewi, watatamba nacho. Licha ya hadhi ya chini ambayo maandishi ya Kiswahili yamepewa, waandishi wa Kiswahili wanaendelea kuandika kwa sababu ya utashi walio nao. Msukumo huu ndio unaoendeleza mbele fasihi ya Kiswahili.
Tumetoa hoja kwamba, kwanza kabisa uhuru wa mwandishi umo katika utashi. Tuone sasa nguzo ya pili. Nguzo hii ya pili imo katika kuwa na falsafa moja inayoeleweka, falsafa ifanyayo maandishi yaonekane kama kazi moja yenye mwelekeo maalum. Falsafa ndiyo kamba ifanyayo maandishi yote ya mwandishi yawe kazi moja, siyo jina la mwandishi. Falsafa ndiyo ifanyayo maandishi ya mwandishi mmoja yawe na kitu kijulikanacho kama terminus ad quem, yaani lengo. Waandishi niliowataja hapo juu, Wole Soyika na Ngugi wa Thiong’o (na hapa nitamwongezea Leopold Senghor), ndio wanaoongoza katika kuwa na falsafa zao zinazojulikana. Katika fasihi ya Kiswahili tunao waandishi wenye falsafa inayojulikana? Wapo wachache. Wengi tulio nao wanaandika kufuatana na jambo au tukio la wakati huo bila kiunganisho. Leo ataandika juu ya mapenzi, kesho juu ya upelelezi, na kesho kutwa “mapinduzi” – mwishowe anakuwa na orodha ndefu ya vitabu visivyokuwa na terminus ad quem. Waandishi wachache tulio nao ambao waelekea kuwa na falsafa inayoongoza maandishi yao ni kama Shaaban Robert na Mohammed Suleiman. Bila kuwa na falsafa maahum ni rahisi kwa mwandishi kuyumbishwa. Tunaweza kusema kuwa uhuru wa mwandishi umo katika falsafa yake.
Hoja ya tatu itatufikisha kwenye sanaa yenyewe. Hoja hii.inasema kwamba uhuru wa mwandishi umo katika kuitawala vema sanaa yake. Kama unaandika tamthiliya na hujui misingi ya sanaa ya aina hiyo utajikuta katika kikwazo. Utajikuta huna uhuru kisanaa. Unaweza kujaribu, lakini kazi utakayoitoa itakuwa hafifu. Tunaweza kusukuma wazo hili mbele kwa kusema kuwa kazi nzuri ya kisanaa ni ile inayounganisha vema ubunifu na uhalisia. Mwandishi akielemea sana katika uhalisia kunakuwa na matatizo, na aelemeaye sana katika ubunifu anazua matatizo mengine. Kazi ngumu aliyo nayo mwandishi ni katika kuupatia barabara msitari huo. Mwandishi mwenye vitabu vingi anaweza kuwa na kitabu kimoja tu kilichoupatia vema msitari huo. Katika fasihi ya Kiswahili waandishi walioupatia msitari huu tunao: Ebrahim Hussein, Penina Muhando, Muhammed Suleiman, C.G. Mung’ong’o na A.J. Saffari. Hawa ni miongoni mwa waandishi ambao ningewataja bila kusita. Mwandishi anayeweza kuitawala vema sanaa yake anaunganisha vizuri sanaa na maudhui yake.
Lakini mwandishi hawezi kuitawala vema aina ya sanaa anayoitumia kama msingi wa lugha anayoitumia ni mbovu. Lugha ndicho kiungo maalum kati ya sanaa na kazi za kifasihi. Kama hujui vema lugha unayoitumia utajikuta huna uhuru wa kusema unachotaka kukisema. Kwa hiyo lugha ndiyo nguzo ya nne katika uhuru wa mwandishi. Waandishi wa Kiswahili niliokwisha wataja wanakitawala vema Kiswahili sanifu. Hapa nitasisitiza kwamba Kiswahili sanifu ndio msingi wa fasihi ya Kiswahili.
Tutamalizia sehemu hii kwa kusema kuwa uhuru wa mwandishi umo katika utashi, falsafa, aina ya sanaa aitumiayo mwandishi, na katika lugha.
Mashetani Kama Mfano
Mashetani ni tamthiliya inayofikiriwa na wengi kuwa ya kiwango cha juu kisanaa. Ni tamthiliya ya kwanza ya Kiswahili ambayo inapenya na kujaribu kuufikia urazini. Labda ni tamthiliya ya kwanza ya Kiswahili ambayo imejadili mvutano wa kisaikolojia ulokuwa katika vichwa vya Watanzania kuhusu muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika miaka michache baada ya Azimio la Arusha. Azimio la Arusha na Mapinduzi ya Zanzibar ndiyo matukio makubwa yaliyobadilisha maisha ya watu wa tabaka la juu katika nchi hizi mbili zilizoungana.
Wahusika wakuu katika tamthiliya hii ni Kitaru na Juma. Wote ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Kitaru anasomea uwanasheria na Juma anasoma historia. Ni wanafunzi “wanamapinduzi,” wanausaka uhuru ambao umo katika ukweli. Lakini kutokana na matukio ya kihistoria pamezuka “chuki” ambayo imevuruga uhusiano kati yao. Baba yake Kitaru ambaye anatoka Bara ni bepari, na baba yake Juma ambaye mali yake ilitaifishwa Zanzibar kabla hajahamia Bara, sasa ana kijiduka. Uanamapinduzi wao unajigonga juu ya mwamba uliojikita katika tabia ya baba yake Kitaru ambaye anawachochea na mawazo ya kuchuma pesa; na katika bibi yake Juma ambaye anawachochea kwa hadithi za fahari iliyopita.
Ukweli wataupata wapi? Katika historia. Kwa hiyo historia halisia inachezwa kisanaa. Mchezo ndani ya mchezo. Hii ni mbinu ya kisanaa aitumiayo mwandishi katika kuipa historia uhai. Hadhira inapewa nafasi ya kuishi tena historia iliyopita. Sehemu ya pili ya tamthiliya hii pia ni mchezo ndani ya mchezo, lakini mchezo huu unatokea kichwani mwa Kitaru. Mchezo huu unahusu matukio yaliyotokea baada ya uhuru wa bendera na matatizo ya ukoloni mamboleo ambao lengo lake ni kichwa na uchumi. Hali ya nguvu za mkondo wa nje tunaiona katika mcheko. Baada ya maonyesho haya ya kisanaa Hussein, katika sehemu ya tatu na ya nne, anairudisha hadhira katika hali halisi.
Katika tamthiliya tunamwona mwandishi akijaribu sana kuutafuta msitari kati ya ubunifu na uhalisia. Ili kuupata msitari huu anatumia mchezo ndani ya mchezo; anatumia lugha inayowiana na wahusika, na mwanga wa spotlaiti na ndoto. Katika tamthiliya hii tunauona mvutano uliopo kati ya mkondo wa nje na nafsi. Mkondo wa nje tunauona katika sitiari ya chewa na jahazi inayofuata mkondo wa maji. Mvutano huu unawakilishwa na Binadamu na Shetani. Inavyoelekea Hussein anatoa wazo kuwa uhuru uliomo katika ukweli unapatikana katika hali ya nusu ndoto na katika hali ya nusu kichaa (neurosis), na kwamba tunaukaribia ukweli katika kazi za kisanaa kwa sababu katika sanaa tunaishi tena na tena maisha yetu. Katika sanaa tunacheza mchezo tena na tena hadi ukweli unapojidhihirisha. Wazo hili tunaliona katika maneno ya Kitaru anaposema, “Lakini katika ule mchezo, na katika ndoto, nimeona mengi niliyokuwa siyo nikiyaona” (uk. 47).
Katika Mashetani Hussein anaanza kuachana na uhalisia rahisi tuuonao tangu Wakati Ukuta hadi Kinjeketile. Anaanza kuachana na fasihi rahisi yenye nia ya kufunza (didaclic) na kuingia katika mfumo wa sanaa unaoelekea katika dhana ya uhuru wa mwandishi. Hussein anakuwa si mwandishi wa kurudia nyimbo za jukwaani. Mfululizo wa tamthiliya zake zilizofuata zimekuwa katika kiwango hicho. Mwandishi anaitawala aina ya sanaa anayoitumia, na anaonyesha dalili za kuwa na utashi thabiti.
Hitimisho
Nia ya makala haya ni kuondoa mawazo rahisi juu ya uhuru wa mwandishi. Kati ya kuwako na kutokuwako tumo katika kujaribu, katika kusahau, katika kuieleza vema falsafa inayotawala uandishi wetu, katika kuitawala lugha, na wakati huo tukisukumwa mbele na utashi. Uhuru, huo hatunao, katika kutokuwa nao tunaandika.

Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)