MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
UHAKIKI WA RIWAYA YA KUFIKIRIKA KINADHARIA

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
UHAKIKI WA RIWAYA YA KUFIKIRIKA KINADHARIA
#1
UHAKIKI WA RIWAYA YA KUFIKIRIKA KINADHARIA
UTANGULIZI
JINA LA KITABU          : KUFIKIRIKA
JINA LA MWANDISHI  : SHAABAN ROBERT
MWAKA                         : 1998
WACHAPISHAJI                       : MKUKI NA NYOTA PUBLISHER
HISTORIA YA MWANDISHI
Shaaban Robert alizaliwa tarehe 1/1/1909 katika kijiji cha Vibandani mkoani Tanga. Alipata elimu yake mkoani Dar es Salaam na kufanikiwa kuhitimu darasa la 11. Shaaban Robert alikuwa mtunzi maarufu wa vitabu mbalimbali kama vile Kusadikika, Siku ya watenzi Wote na Maisha yangu na Baada ya miaka Hamsini na vitabu mbalimbali vya mashairi. Kwa zaidi ya miaka 15 vitabu vya Shaaban Robert vilipata umaarufu kushinda vyote katika jamii ya aAfrika Mashariki na kati. Mbali na maandiko yake alikuwa na athari kubwa katika maendeleo ya lugha ya Kiswahili akiwa mjumbe wa kamati za East Africa Swahili Committee, East Africa Literature Bureau na Tanganyika Languages Board. Shaaban Robert alifariki tarehe 20/6/ 1962.
Matukio katika kitabu hiki ni ya fantasia (ya ajabu ajabu) kwani Kufikirika ni nchi ambayo ramani yake ni adimu kupatikana sababu nchi yenyewe haiandikiki ila hufikirika kwa mawazo tu. Pia riwaya hii ni riwaya chuku kwa sababu imetiwa chumvi nyingi katika matukio ya kitabu hiki.
NADHARIA ZILIZOTUMIKA
Mwandishi ametumia nadharia mbalimbali katika kuwandika riwaya hii, nadharia hizo ni kama zifuatazo;
Nadharia ya Udhanaishi: hii ni nadharia inayoshughulikia masuala kuhusu maisha yaani mwandishi anachukuliaje suala la maisha katika kitabu hiki Shaaban Robert anaona maisha hayana maana kwa kumtumia Mfalme ambaye baada ya kukosa mtoto aliona kuwa maisha hayana maana bila kuwa na mtoto.
 
Nadharia ya Saikochanganuzi. Hii ni nadharia inayojikita katika kusoma saikolojia ya mtu. Katika kitabu hiki imeelezwa kwamba baada ya mtoto yule wa l kufundishwa kwa mfululizo bila kupumzishwa alipata tatizo la kisaikolojia na baadaye kuugua sana.
Pia Mfalme baada ya kuwambiwa mtoto anatakiwa kufanywa kafara ilimuathiri kisaikolojia kwani kafara ilikuwa hairuhusiwi katika nchi ile.
Nadharia ya Usababishi: hii ni nadharia ambayo inaelezea utokeaji wa tukio moja unasababisha tukio lingine jipya litokee, katika kitabu hiki matukio yake ni ya usababishi kwa sabau tukio la kwanza limesababisha utokeaji wa tukio la pili. Mfano, tukio la ukosefu wa mtoto kwa Mfalme ndilo lilisababisha kuwepo kwa utabiri na pia kafara.
Nadharia ya Muingiliano Matini. Pia katika kitabu hiki kuna mchanganyiko wa matini mbalimbali mfano shairi Uk. 43, hadithi, Utenzi na Nyimbo.
MUHTASARI WA RIWAYA KWA UFUPI
Nchi ya Kufikirika ni nchi iliyojawa na utajiri mwingi kwani ilijaliwa mali nyingi na zenye thamani kubwa. Iliongozwa na Mfalme ambaye katika maisha yake yeye na Malkia hawakufanikiwa kupata mtoto. Jambo hili lilimuhuzunisha sana Mfalme wa nchi ya Kufikirika. Mfalme huyu alijitahidi kuomba msaada wa kila aina ya makundi ya waganga kama waganga wa mizimu, makafara, mazinguo, hirizi na mashetani ili kupata ufumbuzi wa tatizo lake lakini ilishindikana.
Badaye lilijitokeza kundi la waganga wa utabiri. Kundi hili lilibashiri kwamba Mfalme anaweza kupata mtoto ambaye ni mwanaume, atazaliwa siku ya jumatano ila mtoto huyo atakapofikisha umri wa miaka kumi atasumbuliwa na magonjwa na ili kumnusuru mtoto huyo wa Mfalme hawana budi kutoa kafara ya watu wawili Mwerevu na Mjinga.
Baada ya miezi kadhaa kupita Malkia alipata mimba na baadaye kapata mtoto ambaye alipofikisha miaka ya kwenda shule Mfalme aliajiri mwalimu aliekuwa anakuja kumfundisha akiwa nyumbani. Mtoto Yule alikuwa na uwezo mkubwa sana wa akili lakini Mfalme hakuruhusu motto Yule kujihusisha na masuala ya michezo na wenzake jambo ambalo lilimkosesha raha mtoto yule.
Alipofikisha umri wa miaka kumi mtoto huyo alishambuliwa na maradhi ambapo kama walivyosema watabiri, ili kumnusuru maisha yake Mfalme hana budi kufanya kafara ya watu wawili lakini kafara ilikuwa hairuhusiwi katika nchi ya Kufikirika. Mfalme aliamua watu wawili watafutwe na baadaye walipatikana, Mwerevu (mfanya biashara) na Mjinga. Watu hao walifungwa gerezani kusubiri siku ya hukumu.
Ilipofika siku hiyo Mjinga alimuahidi Mwerevu kufanya kila njia kujiokoa na kumwokoa mwenzie. Siku ilipofika alipokamatwa aliomba kuongea na Mfalme jambo la mwisho akasema “kama kafara hii ilitaka kuchinjwa kwa Mwerevu na Mjinga kwa hali werevu wa mwenzangu haukuthibitika na ujinga wangu hauna ushahidi” Mjinga huyo alimshauri Mfalme kumpeleka mwanawe hospitali kwani madaktari ndio wana majukumu ya kutibu magonjwa na sio kafara.
Mfalme alipokea ushauri wa Mjinga na kumpeleka mwanawe hospitali na baadaye mwanawe alipona. Mfalme alifurahi sana na kumtunuku Mjinga yule kuwa waziri wa nchi ya Kufikirika. Hivyo basi kitabu hiki kinaeleza kwamba nchi ya Kufikirika ilitawaliwa na mila na desturi potofu ambazo zinapitwa na wakati kama vile kafara, kupiga ramli, mazinguo na mashetani ambayo yamepitwa na wakati ambayo hayana budi kutotiliwa maanani na kupigwa marufuku kwani hayana maana.
MAUDHUI.
Ni jumla ya yale yote ambayo mwandishi ameyazungumzia katika kazi yake, maudhui hujumuisha vipengele vya dhamira, ujumbe, migogoro, mtazamo, na falsafa.
DHAMIRA
Ni lengo kuu la mtunzi wa kazi ya riwaya alilokusudia kufikisha katika jamii.
DHAMIRA KUU
Ujenzi wa jamii mpya: mwandishi Shaaban Robert amekusudia kuelimisha jamii ya Kufikirika kuwachana na mila na desturi zilizopitwa na wakati kama vile kuwamini imani za waganga wa kienyeji, kutoa watu kafara, kutokusoma elimu ya sayansi na kuendelea kusoma haswa sinazohusu miungu yao ya kimila na desturi za Kufikirika, pia anamtumia mhusika mwalimu kama mpenda mabadiliko na kuwachana na mila na desturi zilizopitwa na wakati katika jamii ya Kufikirika.
DHAMIRA NDOGONDOGO
Elimu, katiaka nchi ya Kufikirika elimu haikuwa na nafasi kwani Mfalme alikuwa anaamini elimu ama imani za kishirikina na ndio maana alimwambia mwalimu mtoto wake amfundishe elimu inayohusu mila na desturi za Kufikirika hivyo swala la elimu halikutiliwa maanani, pia kwa upande wa pili elimu inaoneshwa kuwa ndio chombo cha ukombozi pindi mwalimu anaamua kumfundisha  mtoto wa  Mfalme elimu ya sayansi (kigeni) hii inaonesha kuwa elimu inajitokeza pale ambapo mkulima alimshauri kwenda kwa daktari kupima ugonjwa wa kisaikolojia ambao ulimfanya mtoto kudhoofika hivyo badala ya kutoa kafara aende hospitali kupima kwa daktari hivyo elimu ikitumiwa vizuri inaweza kubadili  jamii kutoka katika mila na desturi zilizopitwa na wakati na kuweza kuleta mabadiliko katika jamii.
Suala la uongozi, Ungozi ni ile hali ya kutoa ama kuongoza jamii ama watu wakati wa jambo fulani. Mwandishi Shaaban Robert hakupuuzia suala la uongozi katika riwaya hii, anaonesha kuwa viongozi wa nchi ni lazima wawe mstari wa mbele katika kuhakikisha maslahi ya nchi yanalindwa na wananchi wanaishi kwa amani. Mwandishi anabainisha suala hili kwa kumtumia mhusika Mfalme (uk 1-2)
          “Nimejaliwa kupata ufalme kuliko wafalme wengine walio majirani zangu. Binafsi yangu nimepigana vita nyingi kulinda nchi isitekwe na adui. Ushindi wa kila vita umenipa utukufu wa namna ya peke yake. Milki yangu pana imeenea kaskazini, kusini, mashariki na magharibi.”.
Pia amemchora Mfalme kama kiongozi aliyetaka kujitimizia yeye matakwa yake mwenyewe bila kuwangalia jamii inayomzunguka. Hili linajitokeza pale ambapo Mfalme anatafuta njia ya kuondoa tatizo la ugumba/ kukosa mtoto na kutumia mali yote ya Kufikirika kwa ajili ya tatizo hilo bila kujali maslahi na ustawi wa wana Kufikirika, wengi tunaweza kujiuliza je katika jamii ile hajawahi tokea mtu mwingine akakosa mtoto? Na je naye alitumia mali ya nchi kutatua tatizo hilo? (uk. 8-11). Pia tunamwona Mfalme akikubali kutolewa kwa kafara ya damu ili kumponya mwanawe. Hili limekubalika kwa sababu yeye ni kiongozi ameshinda kusimamia haki za binadamu au wananchi wake anaowaongoza. (uk. 32)
 
Suala la ugumba na utasa, mwandishi Shaaban Robert hakusita kulielezea suala la ugumba na utasa katika riwaya hii ambalo ndio lilisababisha kuibuka dhamira mbalimbali. Mwandishi anamtumia mhusika Mfalme na Malkia katika kuonesha tatizo hili. Mwandishi anaonesha kuwa licha ya ujasiri, uzalendo na furaha yote aliyokuwa nayo Mfalme na Malkia lakini walijiona sio kitu kutokana na kukosa mtoto, ambaye angekuja kurithi madaraka mara baada ya kufa kwa Mfalme.(uk 3)
Usaliti, mwandihi ametumia wahusika ambao ni Mfalme na mwalimu pindi ambapo Mfalme alimwambia mwalimu amfundishe mtoto wake elimu ya mila na desturi za Kufikirika hivyo mwalimu hakumfundisha na kuwanza kumfundisha elimu ya sayansi ya kigeni. Hivyo mwalimu alimsaliti Mfalme kwa kukiuka maafikiano yao. (uk.22-23).
Mila na desturi, mwandishi Shaaban Robert ameonesha mila na desturi zilizopitwa na wakati ama zilizokuwa zinapatikana katika jamii ya Kufikirika, hivyo Shaaban Robert anamtumia Mfalme na mwalimu kuonesha jinsi gani mila zilizopitwa na wakati kama vile kutoa kafara, kuwamini waganga wa kienyeji, elimu ya mila na desturi zilizopitwa na wakati.
Imani potofu, mwandishi anamtumia Mfalme kama mtu anayeamini mila na desturi zilizopitwa na wakati kama vile anaamini uchawi, uganga, kafara katika jamii ya Kufikirika hivyo Shaaban Robert anamtumia Mfalme kuiasa jamii hiyo ili kuweza kuwachana na desturi zilizopitwa na wakati.
Uharibifu wa mazingira, Shaaban Robert anamtumia Mfalme kama kiongozi aliyekuwa mharibifu wa mazingira kwani alileta waganga mbalimbali ili kuweza kupata mtoto ambao baadhi yao waliamuru miti kukatwa yote, maji kukauka hivyo ikasababisha kuwathiri mazingira katika jamii ya Kufikirika.
ONTOLOJIA
Hili ni jambo au wazo linalobeba imani ya jamii juu ya jambo fulani. Uzazi ukikosekana basi ni lazima waganga wa kienyeji na utabiri uhusishwe ili kutafuta sababu ya ukosefu huo (uk 7-13). Jamii ya Kufikirika iliamini kuwa mtoto huleta furaha katika ndoa na jamii (uk. 17)
Ujumbe.
  • Mwandishi Shabarn Robert katika kazi yake ya Kufikirika anakusudia kuikomboa jamii kutoka katika ujinga na kujenga jamii ya kisomi na kisasa.
  • Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Mfano wananchi wa Kufikirika walikuwa na umoja katika kufanikisha ustawi wa nchi yao hali kadhalika watu wa Kufikirika walikuwa na umoja na ushirikiano katika kufanikisha Mfalme wao kupata mtoto.
  • Kwenye upendo, umoja na ushirikiano hakuna vurugu na matatizo mbalimbali. Ustawi wa nchi ya Kufikirika umetokana na umoja na ushirikiano waliokuwa nao.
  • Jamii isijiegemeze katika imani za kimila na kitamaduni tu bali iangalie upande mwingine. Hii inatokana na ukweli kwamba wanaKufikirika walikuwa hawaamini masuala ya hospitali badala yake walikuwa wanaamini mambo ya kimila na kitamaduni.
  • Ujinga na werevu wa mtu hupimwa kwa matendo na sio kazi anayoifanya. Hii inatokana na watu wa Kufikirika ambao walikuwa wanapima werevu na ujinga wa mtu kutokana na kazi zao.
  • Ujumbe mwingine ni kwamba viongozi lazima wadumishe sheria za nchi ili kuleta usawa na amani katika nchi.
Hivyo Shaaban Robert anaitaka jamii ibadilike kwa kuzingatia maonyo na maadili yapatikanayo katika riwaya ya Kufikirika.
Falsafa.
Falsafa ya mwandishi Shaaban Robert katika kazi yake hii ya Kufikirika anaamini kuwa kuna maisha baada ya kifo. Hivyo basi anawaasa wanajamii wajitahidi kutenda mema kwa sababu kuna maisha baada ya kifo.
 
Msimamo, msimamo ndio uwezao kuwatofautisha wasanii wawili wanaotunga kazi za fasihi zilizo na kiini na chimbuko moja. Katika kazi hii mwandishi Shaaban Robert anaonekana kuwa na msimamo wa kimapinduzi. Kwa mujibu wa mwandishi anaona katika kipindi cha sayansi na teknolojia mila na tamaduni za zamani zisipewe nafasi.
 Mtazamo, mwandishi Shaaban Robert anaonekana kuwa na mtazamo wa kiyakinifu, mwandishi anaona kuwa jamii isiangalie mila na tamaduni tu bali iangalie mambo ya sayansi na teknolojia.
Migogoro, mgogoro ni mvutano kati ya pande mbili au zaidi, mwandishi Shaaban Robert katika riwaya hii ya Kufikirika anaonesha migogoro mbalimbali kama vile mgogoro wa kiuchumi, kijamii, kisiasa, utamaduni na mgogoro wa nafsi.
Tukianza na mgogoro wa kiuchumi, Mwandishi anaonesha jinsi nchi ya Kufikirika ilvyoyumba kiuchumi kutokana na mali zote za nchi zilivyotumika katika kumtibu Mfalme na Malkia na mwishowe shughuli za nchi zilisimama. (uk (8-12).
Pia kuna mgogoro wa kijamii, mwandishi anaonesha mgogoro wa Mfalme na Malkia kwa kukosa mtoto, kwa kuwa walijiona hawana  umuhimu katika jamii ingawa walikuwa na mali nyingi. Uk(1-6).
Pia mgogoro mwingine wa kijamii ni kati ya Mfalme na waganga kwamba makundi matano ya waganga  waliokusudiwa kumtibu Mfalme na Malkia walishindwa kuwatibu. (uk(8-13).
Mgogoro mwingine wa kijamii ni kati ya Mfalme na waliotakiwa kutolewa kafara, kwamba katika nchi ya Kufikirika suala la mtu kutolewa kafara ni suala ambalo haliendani na sheria za nchi ya Kufikirika.
Vilevile kuna mgogoro wa nafsi uliojitokeza kwa Mfalme, jinsi Mfalme alivyokuwa akiumia juu ya kukosa mtoto kwa muda mrefu takribani miaka kumi baada ya kuoana na Malkia.
Pia Malkia alikuwa na mgogoro na nafsi yake juu ya kukosa mtoto kwa muda mrefu tangu kuoana kwao.
Hali kadhalika kuna mgogoro kati ya waziri mkuu na wajumbe juu ya kubadili mfumo wa uongozi.
Pia kuna mgogoro kati ya ukale na usasa, kwamba wananchi wa Kufikirika waliamini sana mambo ya kishirikina wakati Utubusara alikuwa akijaribu kuwaelimisha juu ya mambo ya sayansi na teknolojia na waachane na mambo ya zamani.
Pia kuna mgogoro wa kisiasa, mwandishi anaonesha jinsi Mfalme alivyokuwa ameegemea kuongoza nchi yake kupitia mila na desturi, lakini tunaona jinsi Utubusara alivyokuwa akijaribu kuishauri jamii ya Kufikirika kuepukana na mila zilizopitwa na wakati na waegemee katika sayansi na teknolojia ili waweze kuleta mabadiliko.
FANI
Fani katika kitabu cha Kufikirika imejumuisha, muundo, mtindo, whusika na matumizi ya lugha.
Muundo.
Ni msuko wa visa na matukio katika uwasilishaji wa kazi ya fasihi. Muundo uliotumika katika kazi ya kitabu au riwaya ya Kufikirika ni wa moja kwa moja (muundo wa msago). Visa na matukio vimejengwa kama ifuatavyo;
Mfalme anaonekana kukosa mtoto kwa kipindi kirefu sana, analalamika na kujaribu kutafuta ufumbuzi.
Waganga walioko katika nchi ya kufikirka wanakutana pamoja na kutafuta namna  yoyote ya kupatikana kwa mtoto/kuzaliwa kwa mtoto/kuondoa ugumba katika nyumba ya Mfalme.
Matokeo ya utabiri kwa kupatikana kwa mtoto, mtoto anazaliwa baada ya mwaka na miezi tisa.
Mtoto wa Mfalme anaugua baada ya kufikia ule umri wa kumwaga damu kama kafara kwa mtoto. Kupatikana kwa watu wawili Mjinga na mwenye busara kutolewa kama kafara.
Mtoto wa Mfalme anapona baada ya kupelekwa hospitali na kufanyiwa vipimo.
Mtindo.
Ni namna ya uwasilishaji wa kazi za fasihi. Mwandishi ametumia mtindo wa masimulizi kwa nafsi ya tatu na ya kwanza.
Vilvile ametumia ushairi na tenzi katika uboreshaji wa kazi yake. Mfano katika ukurasa wa 18 na 43.
Mwandishi ametumia usababishi, mfano Mfalme kutopata mtoto ndicho chanzo cha kuitisha waganga na matokeo ya uganga.
Pia katika kuboresha mtindo wake mwandishi ametumia taharuki, mfano taharuki imetokea pale ambapo amri ya kukamatwa watu wawili Mjinga na mwerevu kwa ajili ya kutolewa kafara
Pia Motifu, Ni wazo au jambo linalojitokeza mara kwa mara katika kazi ya fashihi. Katika riwaya ya Kufikirika tunaona kuna motifu ya msako. Mfalme anafanya kila njia ili apate mtoto. Motifu ya mtoto wa pekee, Mfalme alipata mtoto wa pekee, Mfalme alipata mtoto mmoja tu. Motifu ya uaguzi, tunaona uaguzi unafanywa kwa Malkia na Mfame ili waweze kupata mtoto, pia inajitokeza kwa mtoto wa Mfalme kuangaliwa baada ya kuugua.
Mandhari
Mandhari ni mahali au sehemu ambayo kazi ya fasihi inatendeka. Katika riwaya ya Kufikirika mwandishi Shaaban Robert ametumia mandhari ya Kufikirika, kwani hata nchi inayozungumziwa ni ya Kufikirika, nchi ambayo ni Kufikirika haionekani kwa macho ipo angani ni kubwa na watu wake ni wengi. Pia mwandishi ametumia muktadha halisi kama vile Gerezani, Nyumbani kwa Mfalme, Bustanini ( uk.1) na shambani. Kupitia mandhari hizi mwandishi Shaaban Robert ameibua dhamira mbalimbali ambazo zimejadiliwa hapo awali.
Wahusika.
Ni wawakilishi wa kazi ya fasihi na ni mdomo wa msanii. Wahusika wanaoonekana katika kitabu cha Kufikirika ni kama wafuatao;
Mfalme; ni mtawala wa saba katika nchi ya Kufikirika, wafalme waliotangulia ni sita. Ametawala nchi yake vizuri pamoja na kwamba anatumia mila na desturi za zamani za watawala waliotangulia na vile vile alikosa mtoto kwa kipindi kirefu, kwa jinsi hiyo akatafuta ufumbuzi wa kupatikana kwa mtoto kwa kuitisha waganga  ili wamsaidie tatizo hilo.
Malkia; ni mke wa Mfalme wa nchi ya Kufikirika, anaonekana kuwa na shukrani kutokana na utabiri wa kupatikana mtoto na kupona kwa mtoto wake, alitoa zawadi.
Wazee wa baraza. Wanamsaidia Mfalme katika kutawala, kufanya maamuzi na mashauri mbalimbali. Mfano; walitoa maamuzi ya kupatikana kwa watu wawili, mmoja mwerevu  na Mjinga kwa ajili ya kumwaga damu ili apone (mtoto wa Mfalme).
Mwalimu 1. (Utu busara ujinga hasara), ni mhusika aliyeibua dhamira nyingi katika riwaya hii ya Kufikirika, alikuwa ni mtu makini na mwenye upeo mkubwa katika kufikiria mambo. Huyu ndiye aliyetabiri kuzaliwa kwa mtoto wa Mfalme, baadaye akawa mwalimu wa mtoto wa Mfalme na baadaye akajiingiza katika ukulima (uk.49). Hekima na uelewa aliokuwa nao ulikuwa ngao tosha iliyomsaidia kujikomboa kutoka katika vikwazo vyote alivyokumbana navyo, hakika ni mtu anayefaa kuigwa katika jamii. Alimfundisha mtoto kwa masharti ya kazi yake bila kujali amri ya Mfalme.
Mwalimu 2; alimfundisha mtoto kwa kufuata maelekezo ya Mfalme, mtoto akaugua vibaya kwa kukosa mapumziko na michezo kwa ajili ya afya yake. Ni muhusika muwi.
Utubusara; ni mtabiri aliyemtabiria Mfalme kwamba baada ya mwaka atapata mtoto wa kiume.
Mkulima; alichukuliwa kuwa kafara na alichukuliwa kama Mjinga.
Mfanya biashara; alichuliwa kama Mwerevu katika nchi ya Kufikirika ili atolewe kafara.
Wakazi wa Kufikirika. Ni wananchi wa Kufikirika.
Waziri mkuu, huyu anawakilisha viongozi wanaopindisha sheria kwa manufaa ya watu wachache. Mwandishi anamchora mhusika huyu kama mtu ambaye anatumia vitisho na nguvu katika kushawishi wajumbe kukubaliana na ubadilishaji wa sheria. Hakika hafai kuigwa na jamii hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko.
MATUMIZI YA LUGHA.
Lugha ndio nyenzo kuu ya kazi ya fasihi na ili kuitofutisha kazi fasihi na isiyokuwa na kifasihi lugha ndio nguzo kwa kutumia tamathali, lugha ya picha na taswira, methali, nahau nakadharika.
Mwandishi ametumia lugha inayoeleweka na ameijenga kazi yake kwa lugha ya;
Picha; mfano, uk 2; chini ya bendera yangu kwa maana ya chini ya utawala wangu.
Nahau; mwenye haya hazai. Uk 6, habari iliota mbawa. Uk 17, kujiweka chini ya miguu. Uk 19, kushika mpini uk. 8, usishike tama. Uk 25.
Methali, methali zilizotumika katika riwaya hii ni kama vile, nyumba ya mgumba haina matanga (uk 5),mwenye haya hazai (uk 6),
Misemo, katika riwaya ya Kufikirika misemo iliyotumika ni kama ifuatayo. Dunia haifichi siri (uk 23), maisha ni kama kuwa katika bahari ( uk 24). mafuu ilicheleewa uk 30. Afya ya mtoto ilinyongonyea uk 29
Tamathali za semi, haya ni maneno ambayo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo na hata sauti katika maandishi au kusema. Pia tamathali za semi hutumika ili kupamba lugha au mazungumzo. Katika riwaya ya Kufikirika mwandishi Shaaban Robert ametumia tamathali mbalimbali kama ifuatavyo:
Tashibiha, katika tamathali hii watu ama vitu viwili au zaidi hulinganishwa na watu ama vitu vingine kwa kutumia maneno kama mithili, kama, n.k, katika riwaya hii tashibiha zilizojitokeza ni kama vile kichwa chake kilishindiliwa kama gunia (uk 29),sauti ya waafrika ni kali kama ile ya radi ( uk 6)waliweza kunusa kama mbwa mwitu( uk 8), akili yake kali kama wembe ( uk 38), maswali aliyamimina kama maji ( uk 29), mtu mdogo kama mbilikimo (uk 41)
Tashihisi, katika aina hii vitu visivyo na sifa walizonazo watu hupewa sifa hizo. Katika riwaya hii mwandishi Shaaban Robert anabainisha tashihisi zifuatazo,sauti ya ndege waliokuwa wakiimba matawini kwa kuwagana na mchana ilikuwa na simanzi masikioni (uk 1)
Sitiari, hii ni tamathali ambayo hulinganisha vitu bila kutumia viunganishi, mwandishi wa riwaya hii ametumia sitiari zifuatazo, Mjinga ni mnyama ( uk 41), wanawake ni malaika( uk 40).
Mubalagha, ni tamathali ya semi ambayo hutia chumvi au hukuza jambo. Katika riwaya ya Kufikirika mwandishi ametumia mbinu hii katika( uk 11) siku hiyo kuni, mkaa, na mafuta yote yalikwisha kwa kuchoma hirizi hizo, moshi mwingi uliruka juu ukatanda katika hewa kama wingu kubwa la mvua.
KUFAULU NA KUTOKUFAULU KWA MWANDISHI
Mwandishi Shaaban Robert amefanikiwa kimaudhui kwani ameadili dhamira mbalimbali zinazosawili maisha ya jamii na kuweza kuielimisha jamii kutoka hali duni na kuweza kuijenga jamii mpya kama vile kupiga vita uharibifu wa mazingira, usaliti, kuwachana na mila na desturi zilizopitwa na wakati, kutoa elimu katika jamii, uongozi mbaya hizo ni baadhi ya mbinu za ujenzi wa jamii mpya kwani Shaaban Robert amejadili kwa kina ili kuweza kuikomboa jamii.
Pia mwandishi Shaaban Robert amjadili mambo mbalimbali yanayotokea katika jamii zetu kama vile suala la elimu, usaliti, uongozi mbaya uhalibifu wa mazingira, mila na desturi, mwandishi ameonesha kukerwa na mambo kama hayo na kuona ni vema kuishauri jamii  na kuyakemea maovu yaliyopitwa na wakati ili kuwachana nayo na kujenga jamii mpya.
Hivyo mwandishi amefaulu kwani ameweza kutoa suluhisho na mwanga kwa baadhi ya mambo yanayojitokeza katika jamii zetu. Mwandish ameweza kuyaweka bayana ili kuikomboa jamii yake kwani fasihi ni zao la jamii. Mambo haya ni kama vile elimu, uongozi mbaya, uhalibifu wa mazingira, kuendeleza mila na desturi zilizopitwa na wakati, usaliti. Hivyo Shaaban Robert ametoa nasaha zake kwa jamii ili kuwachana na mambo yanayoludisha nyuma maendeleo ya jamii na kutoa suluhisho kwa baadhi ya mambo yanayotokea katika jamii.
KUFAULU KIFANI
Mwandishi Shaaban Robert amefaulu katika kuijenga kazi yake na kuweza kumvutia msomaji kwa ujuzi wake wa uandishi kwani ametumia fani mbalimbali katika uandishi wake kama vile ametumia muundo wa moja kwa moja (msonge) pia ametumia nasfi zote tatu zimetumika ili kuwakilisha ujumbe kwa jamii husika kwa lengo alilokusudia.
Pia ametumia mtindoo ambao ameweza kujenga visa na matukio kwa kutumia simulizi, tenzi, hadithi, semo, tamathali za semi, methali ili kuwakilisha mawazo yake na kuweza kuitofautisha kazi yake na kazi za waandishi wengine. Pia ametumia mtindo wa riwaya chuku kwa kutia chumvi nyingi katika kazi yake. Mtindo aliotuma ni nyimbi, masimulizi, utenzi, hadithi, semo, tamathali za semi ili kuweka kazi yake iwe na mvuto kwa msomaji kama uchuku alivyoutumia.
Suala la wahusika mwandiishi amefanikiwa kuwachora wahusika kwa sifa na tabia zao yaani wafu wa ndani na a nje zinazofaa kuigwa na jamii na zisizo faa kuigwa na jamii katika kujenga jamii mpya. Pia amewachora wahusika katika sehemu kuu tatu yaani muhusika mkuu,  na wahusika wajenzi na wahusika wadogo kuwakilisha tabia za watu katika jamii.
Pia suala la matumizi ya lugha mwandhishi Shaaban Robert amefanikiwa kwa kutumia vipengela mbalimbali kama vile tamathali za semi, Taahibiha, sitiari, mdokezo, takriri, tanakari sauti, hali iliyoifanya kazi yake kuwa na mvuto kwa msomaji, hivyo wasomaji kuweza kuipenda kazi yake na kusoma kwa makini bla kuchoka ili kulewa nini Shaaban Robert amekusudia kuiadili jamii.
KUTOKUFAULU KWA MWANDISHI KIMAUDHUI
Mwandishi Shaaban Robert hakufanikiwa kwa baadhi ya dhamira zake kama vile suala la uongozi wa nchi kutawaliwa na kiongozi mkubwa wa nchi asiyekuwa na elimu ya kuiongoza nchi ya Kufikirika kwa kuwa na maamuzi ya misimamo yenye kufuata kanuni na taratibu za nchi husika, kwa mfano suala la kutoa kafara kanuni za taratibu za nchi hazikuhusu kutoa kafara lakini Mfalme aliruhusu kitu ambacho ni kinyume na kanuni na taratibu za nchi ya Kufikirika.
Suala la ujenzi wa jamii mpya, mwandishi Shaaban Robert hakuonesha mbinu mbadala za ujenzi wa jamii mpya kama vile umoja na ushirikiano miongoni mwa wanajamii na kuweza kuwa na lengo mahususi la kuwamua.
Suala la elimu Shaaban Robert anamtumia mtoto wa Mfalme ambaye anaonesha msimamo wa kufundishwa mtoto wake elimu ya mila na utamaduni wa Kufikirika kitu ambacho mwandishi angemtumia Mfalme kama muhusika anaye sisitiza kufundishwa kwa elimu ya kigeni katika nchi ya Kufikirika ili kuweza kujenga jamii mpya yenye maendeleo yenye kuleta tija katika jamii ya Kufikirika.
 Hivyo mwandishi Shaaban Robert ameshindwa kusimamia hizo mbinu za ujenzi wa jamii mpya kwani ndio shabaha yake lakini ameibua hizo dhamira na kushindwa kutoa suluhisho la dhamira hizo ili kujenga jamii mpya.
KUTOFAULU KWA MWANDISHI KIFANI.
Mwandishi Shaaban Robert ameshindwa  kwa baadhi ya fani alizotumia. Hapa tunaona kuwa mwandishi  ametumia uchuku mwingi katika riwaya kwa kuongeza chumvi nyingi sana kwa mfano mti yote kutumika kama dawa si waa la kawaida hali inayopelekea kutofanikiwa kwa mwandishi.
Kimaudhui Shaaban Ronert ametumia mandhari ya Kufikirika yaani nchi ambayo haishikiki, haigawanyiki wala haionekani kwani ni ni mandhari ya kubuni si lahisi kuyahusisha na jamii husika.
Hivyo mwandishi utumizi wa riwaya chuku yaani kutiwa chumvi kwa visa na matukio inakuwa vigumu msomaji kuwekza kuelewa dhamira ama lengo mahsusi la mwandishi.
MCHANGO WA MWANDISHI KWA JAMI NA WASANII WACHANGA.
Mwandishi ametoa mchango mkubwa katika jamii ameweza kukemea maovu yanayofanywa na awatu wachache wanaokandamiza jamii, kama vile uongozi mbaya (Mfalme) yeye masirahi ya tabaka la juu na kusahau tabaka la chini, mila potofu, suala la elimu, usaliti, uhalibifu wa mazingira na kutoa suluhisho la matatizo hayo ili kujenga jamii mpya na endelevu.
Mwandishi ametoa mchango kwa waandishi wachanga pindi wanaposema kazi hii wanapata kanuni na taratibu mbalimbalo za uandishi ili kuweza kupanga kazi zao na kufikisha ujumbe kwa jamii husika.
JINA LA KITABU
Kitenzi chenyewe kinatokana na neon “fikiri” lenye maana ya kudhani. Hivyo Kufikirika limesadifu yaliyomo ndani ya kitabu kwani mambo yote ni ya kutabiri kama vile utabiri wa waganga kupata mtoto Mfalme, kuumwa kwa mtoto, nchi yenyewe niKufikirika pamoja na matendo yaliyotokea ndani ya kitabu ni ya Kufikirika. Pia nchi yenyewe ni adimu kwni haikanyagiki wala kushikika. Hivyo jina la kitabu Kufikirika linasadifu yaliyomo.
JALADA LA KITABU.
Jalada la kitabu linasadifu yaliyomo ndani linaonesha picha ya mwandishi wa riwaya hii Shaaban Robert kwa sura ya kufikiri kama riwaya inavyohusika. Pia rangi ya kitabu ni ya zambarau inayoonesha matumaini. Kama watolewa kafara wawili ilipasa “kutumaini” kuwa wataweza kukwepa upanga wa chakari (uk.42)
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)