MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
SHAIRI: WAOAJI, NUDHUMU IPOKEENI

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
SHAIRI: WAOAJI, NUDHUMU IPOKEENI
#1
Naingia kilingeni, nna ujumbe wa dhati, 
ninalokuleteeni, lifikile kwa wakati, 
Mijini na vijijini, pembeni na katikati, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
E Mungu muumba wetu, uketie juu mbinguni, 
pokea shukrani zetu, twakuomba kwa imani, 
matashi haya si yetu, yote ni yako hisani, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
‘litupatia habari, tangazo tukalipata, 
hatutaraji kabari, ni wako umempata, 
Uonyeshe umahiri, walahi usije juta, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Zenu ndoa zilindeni, msigeze kwa mwingine, 
uwe wewe namba wani, mwandanio mbebane, 
Ogopa purukushani, ujipange kama chane, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Mubebe hii nudhumu, sibeze huu mtindo, 
tena msije laumu, kuanza tafuta tindo, 
Nafusi usidhulumu, ‘pate kutilia pondo, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Maisha ni mapatano, uliza na utajuzwa, 
itisha na makutano, ni mengi utaelezwa, 
Na hayana mfanano, jumbe zinavyokolezwa, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Usisikize mayowe, chunga na usidharau, 
ndoayo uikowe, haya usiyasahau, 
Mwenye mpini ni wewe, lea jipandishe dau, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Yanapokuja magumu, mbambe mtu muhimu, 
Tena siishiwe hamu, kuishia kutuhumu, 
Mpigie japo simu, usidhani afahamu, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Waamba zi rangi zote, ndani mkishaingia, 
Wapo wanosema yote, ‘mradi wamesikia, 
Kama ingekuwa vyote, usingejichagulia, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Chuja changanya za kwako, himili chako kifua, 
Jenga na ujenge yako, mbio ongeza hatua, 
Mthamini mke wako, kama tende na halua, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Ubaya usimtende, kumtafutia visa, 
Usimtwishe makonde, kwacho utachojiasa, 
Kwa udi na umpende, usisambaze siasa, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Mbinu mpya ujifunze, ukilinde chombo chako, 
Raha na dhiki mtunze, hata kibidi uwinde, 
Huyo ni wako mfunze, usimpige makonde, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Ulijaa ukumbini, u nahodha naamini, 
Na sasa upo melini, mtunze huyo mwendani, 
Chombo tayari majini, wamiliki usukani, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Chombo chako kimiliki, kiwe cha kwako thamani, 
Unayo hati miliki, uzidi kuwa makini, 
Uikabili mikiki, kamwe sianguke tini, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Hii uliihiyari, sote tunakupongeza, 
Siku uliisubiri, jiko ukalisogeza, 
Leo i yako fahari, upendo kuuongeza, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Zidisha uaminifu, katika hii safari, 
Uisome misaafu, wala sione hatari, 
Mwenza umtaarifu, aijue misitari, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Yaache ya mitaani, hili liwe akilini, 
Ndoa uliitamani, sasa umeingia ndani, 
Na yale ya kizamani, uyatupe baharini, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Tena so masihara, ukweli ninawajuza, 
Usidhani ni mikwara, na wala si ya kubeza, 
Mwapewa nyingi hongera, waja wanawachunguza, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Maisha yaliyo bora, ukweli muweke mbele, 
Msiikwae minara, kupigizana kelele, 
Yote yale ya dharura, mjuze usinyamale, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Gumzoni msitiwe, kufurahisha wa’mbaji, 
Na wala usiwe wewe, kuwaita wasemaji, 
Hata ukipigwa jiwe, tafakari mlengaji, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Pingu hii tangu kale, ni mbegu yenye shinale, 
Upendo furaha tele, muwaonyeshe wavyele, 
Si kipele wala kidole, hili ulipambanule, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Haya yamewaingiya, vifuani yametuwa, 
Sitarajii kuliya, ni wenzi mmeshakuwa, 
Japo mmoya mmoya, kila mja ajijuwa, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Ipo mingi miongozo, mengine kitaalamu, 
Yapo mengi machangizo, mengine huyafahamu, 
Yapo mengine uozo, chagua yalo muhimu, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Usiudharau Uzi, unao wake hishima, 
Usidhani u mjuzi, ujuaye kutuama, 
Uwakumbuke wazazi upate kuchuma mema, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Kuna wa juzi na Leo, wa Jana na yeye pia, 
Ah! mla mla Leo, hili nasisitizia, 
Mshike wako wa leo, wa jana mpishe ndia, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Uisuke yako ndoa, ukilee chako chungu, 
Usikubali madoa, yakakutia machungu, 
Upendo wa kweli toa, usitowe kwa mafungu, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Hila mbaya uzipinge, Mungu umtangulize, 
Nyumba yenu muijenge, na moto muukoleze, 
Wanaoleta mawenge, wote muwatokomeze, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Waanza Maisha mapya, siambe hujui hili, 
Tena usipige chafya, hili lako hutungui, 
Usiseme yaogofya, na weye siyo bedui, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Pole nayo samahani, vitawale ndani yenu, 
Usione tafrani, kusema chumbani kwenu, 
Utaona burudani, nakupa hii fununu, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Likitokea jeraha, moyowe ukapondeka, 
Usitibu kwa karaha, misumari kuchomeka, 
Mjiane kwa staha, mpate kufurahika, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Hadhiye ilinde vyema, hili nataka ujue, 
Wewe ni yake salama, usimwate augue, 
Mkumbushiane zama, maisha msijutie, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.

Ndiye wa kwako muhibu, usiku hata mtana, 
Uyakwepe majaribu, haki mtatulizana, 
Atazishika shurubu, na raha mtapeana, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Kusiwepo vurumai, mioyo mkaumiza, 
Dosari hatukatai, ni bora kuzieleza, 
Usiseme bai bai, tena kwa kujiapiza, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Mazuri yalo mwangani, kweli huleta hishima, 
Raha ilo kivulini, mabaya inayazima, 
Mnapokuwa rahani, penzi hupanda kilima,
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Usiitumie nguvu, hata pasipotakiwa, 
Tumia wako werevu, mengi kuyadadavua, 
Zile lugha mbovumbove, ndoa itaichafua, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Uyajue majukumu, usiyafumbie macho, 
Nunua hata kalamu, kwa hicho ulichopata, 
Umfanye afahamu, kiduchu ulichonacho, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Kuna fupa na mnofu, mawimbi na hata mawimbwi, 
Kabati na majokofu, manda pia nazo bumbwi, 
Karaha na pia hofu, hata kujikuta bubwi, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Yatakutoka matozi, usipandwe na hasira, 
Yapo ya uchokonozi, yanoyoleta kufura, 
Usipange malipizi, wajiona uko imara, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Hata pano kashikashi, jifunze kusawazisha, 
Maisha utayaishi, bendera tapeperusha, 
Utapata bakshishi, haya nakuelimisha,
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Mgande wako mwandani, awe yeye si mwingine, 
Umfanye abaini, hauna penzi kwengine, 
Mzamishe mahabani, kwa upole msemezane, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Msisikize maneno, yatayowaharibia, 
Kwenu iwe tu miguno, na raha kujipatia, 
Mpange maelewano, msiishie kulia, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
Ndooni nahitimisha, msiambe sijaaga, 
Huu si muwashawasha, wala ngoma ya kupiga, 
Nalonga na si kuchosha, ni kweli pasi kuzuga, 
Nasema na WAOAJI, nudhumu ipokeeni.
©Mary Marcus
15.10.2019 2:33Am
Barua pepe: marymarcusg@gmail.com
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)