MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
NGONJERA: KUNA HAKI ZA MTOTO?

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
NGONJERA: KUNA HAKI ZA MTOTO?
#1
KUNA HAKI ZA MTOTO?
LUPOGO:
Mtoto kuwa na haki, jambo linanishangaza,
tabia hii sitaki, mtoto kumlemaza,
mtoto kumpa haki, mbona tunampoteza?
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:

Kaka Lupogo sikia, nikutie darasani,
mtoto mtu tambua, sio mbuzi wala nyani,
Hana wakumsemea, atiwapo matatani,
Mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
Bado kusema hawezi, haki mwaziimbiliza,
Waachieni wazazi, kumlea wanaweza,
Sio kitoto cha juzi, mnaanza kukikweza,
Mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
Leo taweka bayana, kwa hatua tahesabu,
Unayedhani hawana, leo utapata jibu,
Ni haki za kila mwana, hata angekuwa bubj,
Mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
hebu niambie nione, enda nikashawishika,
hata wa miaka minne? Unanifanya kucheka,
ninakungoja unene, haki ukizitamka,
Mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
Kuishi nambari wani, yake haki sikiliza,
tangu akiwa tumboni, na kuona hajaweza,
Imetiwa katazoni, maishaye kukatiza,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
Mola maisha hutoa, na kutwaa akitaka,
nyie wapi mwayatoa, mtoto kumpachika?
Mungu ndiye huamua, kusema leo ondoka,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
Sawa Mungu anatoa, na kutwaa ikibidi,
Ila wale wanoua, watoto kwa makusudi,
wengine mimba kutoa, kwa Ila na ukaidi,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO
naanza kukuelewa, nyingine ipi nambie,
mbona sasa wachelewa, kaa unisimulie,
nahofu kuongopewa, Ila wacha nitulie,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
haki ya kupumzika, ishike nambari mbili,
mtoto akishachoka, kwendelea si halali,
anataka pumzika, walezi hili tujali,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
hapo sasa umezidi, kuchoka kwa kazi gani?
mtoto inambidi, atumwetumwe dukani,
Na tena akikaidi, achapwe makalioni,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:

mtoto ni binadamu, huchoka Kama wengine,
Zikizidi ni haramu, sipewe kazi nyingine,
Kupumzika muhimu, kijana tuelewane,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
sawa bwana endelea, kwa ubishi umefuzu,
jua nakuangalia, usidhani mie zuzu,
ya tatu kiniambia, takupatia mzuzu,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
haki ya kuheshimiwa, na thamani kumtia,
mwana kudharauliwa, ni jambo lenye udhia,
jua mtoto si chawa, ni mtu ninakwambia,
Mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
aheshimike mtoto, si yeye aniheshimu?
hayo Mambo ya kitoto,  kwangu itakuwa ngumu,
hakika hiyo ni ndoto, mtoto kumuheshimu,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
LUPOGO hebu tulia, haki uzijue zote,
Ni mwiko kumbagua, watoto ni sawa wote,
hiyo ya nne sikia, Leo nitataja zote,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
Tatoka wapi usawa,  mlemavu na mzima?
wakike wa kuolewa, wakiume atasoma,
Hawawezi kuwa sawa, wazi hilo nalisema,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?



MSWAHILI:
Tena kuhusu elimu, ni haki ya kila moja,
kila mtoto muhimu, sio mtoto mmoja,
Yako maneno haramu, nazipinga zako hoja,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
mlevu usumbufu, vipi shule atafika?
wakike ni msumbufu, kesho mimba atashika,
Yake kazi maarufu, awe jikoni kupika,
mtoto ni mtu duni, haki apewe za nini?

MSWAHILI:
Mwisho nitaeleweka, kijana subira vita,
ulinzi nautamka, ana haki kuupata,
Wasije wakambaka, na madhara kuyapata,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.




LUPOGO:
Mwana kumpa ulinzi, Sasa mekuwa Rais,
kuamini sijiponzi, kitu hicho si rahisi,
Kiwa mtoto mzinzi, aitafuta mikosi,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
Wala sikati tamaa, kukupa yangu matini,
najua utasinyaa, mwenyewe taniamini,
Ya tano nakurushia, mwana msikilizeni,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
Niache muhimu kazi, mwana nimsikilize,
Braza hilo siwezi, bora nikajitembeze,
nisikilize upuzi, akili niiumize,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?




MSWAHILI:




chakula pia patiwe, kicho Bora na malazi,
Afia Bora ajawe, sitafunwe na maradhi,
wavazi anunuliwe, chakavu hayapendezi,
mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

LUPOGO:
chakula Bora cha nini, si bora kala kashiba,
hivi anajua nini, si maziwa sio jaba,
Mradi chende tumboni, aseme asante baba,
mtoto ni mtu duni, apewe haki za nini?

MSWAHILI:
Sasa nafunga darasa, elimu mekupatia,
kumbe bwana ulikosa, Mambo haya kuyajua?
leo nimekutakasa, akili kuzifunua,
mtoto si mtu duni, haki zake apatiwe.

LUPOGO:
Ukweli ninausema, Mswahili menifunza,
nitakuwa mtu mwema, mtoto vema kutunza,
Ili abaki salama, siliwe hata na funza,
Mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

WOTE:
Sisi sote mabalozi, zao haki kutangaza,
raia na viongozi, kulinda haki twaweza,
tusione upuuzi, kwa pamoja tunaweza,
Mtoto si mtu duni, zake haki apatiwe.

Mtunzi Filieda Sanga
Mama B
Mabibo Dsm
0753738704
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)