MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
PROF SAID AHMED MOHAMED: AMECHANGIA KWA TANZU ZOTE ZA FASIHI

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
PROF SAID AHMED MOHAMED: AMECHANGIA KWA TANZU ZOTE ZA FASIHI
#1
PROF SAID AHMED MOHAMED: AMECHANGIA KWA TANZU ZOTE ZA FASIHI YA KISWAHILI; SI RIWAYA, SI TAMTHILIYA, SI HADITHI FUPI, SI USHAIRI
[Image: SAM-300x158.jpg]
Msomi wa Kiswahili na mwandishi maarufu wa riwaya, tamthilia, mashairi, kazi za watoto na vitabu vya kiada Profesa Said Ahmed Mohamed Khamis
Kwa Mukhtasari
KUISHI kuna nafuu na gharama juu yake. Ingawa kila jambo maishani hustahili kugharimiwa, gharama kubwa zaidi ni ile ya amani.
Kuandika kazi yoyote ya fasihi kunahitaji wakati, utulivu na wito wa ndani ya nafsi. Huwezi kujilazimisha kutunga. Kila kazi ya fasihi katika utanzu wake ni kama mtoto uliyemzaa.
Haiwezekani mtoto mmoja awe sawa na mwingine wa tumbo moja. Huu siku zote utasalia kuwa ukweli katika uandishi wa kubuni.
 
Ingawa kila mwandishi ana msimamo na falsafa yake, mimi siwezi hata kidogo kuwafanya wahusika katika kazi zangu wakate tamaa. Bila ya tamaa binadamu hawezi kujikomboa.
Kukaa nje ya Zanzibar na Tanzania kumenipa uzoefu ambao umechangia pakubwa ubunifu wa mandhari, maudhui na fani katika kazi zangu.
Itakulazimu kupenda lugha, kusikiliza sana na kusoma kwingi ili uwe mwandishi bora wa Fasihi.
Ingawa si kosa kwa mtunzi kuiga baadhi ya mawazo kutoka kwa watangulizi wake, mwandishi lazima awe mweledi na mwepesi wa kutumia misemo ya kuvutia na kushangaza.
Huu ndio ushauri wa Profesa Said Ahmed Mohamed Khamis – msomi wa Kiswahili na mwandishi maarufu wa riwaya, tamthilia, mashairi, kazi za watoto na vitabu vya kiada.
MAISHA YA AWALI
Alizaliwa Pemba, Zanzibar mnamo Desemba 12, 1947. Hakubahatika kupata malezi ya baba na mama ipasavyo kwani wazazi wake walitengana akiwa na umri mdogo sana.
Alilelewa na mama zake “wakubwa”, Bi Jokha na Bi Rukia. Alisomea Wete Boys, Pemba kabla ya kuhamia Kiembe Samaki kisha Darajani, Unguja alikohitimu elimu ya shule ya msingi.
Baadaye alijiunga na shule ya upili ya Gulioni (awali ikiitwa King George The VI). Baada ya kuhitimu masomo ya sekondari, alijiunga na Chuo cha Ualimu cha Nkurumah, Zanzibar mnamo 1966.
Hakujiunga na Kidato cha Tano na Sita kwa sababu wakati huo aliyekuwa kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi nchini Zanzibar, Hayati Abeid Amani Karume alipiga marufuku masomo ya kiwango hicho.
USOMI NA UTAALAMU
Baada ya kuhitimu Ualimu mnamo 1966, alifundisha katika shule ya msingi ya Kizimbani kwa wiki mbili tu, halafu akahitajika kwenda kufundisha Biolojia, Hisabati, Kemia na Kiswahili katika shule ya upili ya Utaani hadi 1974.
Alibahatika kujiunga na shule ya International Correspondence alikosomea masomo ya Sanaa katika kiwango cha Kidato cha Tano na Sita.
Mnamo 1976, alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kusomea Shahada ya Kwanza katika Elimu. Alijikita katika Isimu na Fasihi ya Kiswahili.
Baada ya kufuzu, alirejea Zanzibar na kuwa Mwalimu Mkuu katika shule za msingi na upili za Hamamni kwa miaka mitatu.
Baadaye alirejea Chuo Kikuu cha Dar es salaam kusomea shahada ya Uzamili katika Isimu Tekelezi.
Upekee wa umilisi wake wa Kiswahili ulimvutia mwalimu Siegmund Brauner, Mjerumani aliyemfundisha kozi za Isimu Linganishi na Isimu Historia. Said alipata fursa ya kuelekea Ujerumani kusomea shahada ya Uzamifu (PhD).
Alijiunga na Chuo Kikuu cha Karl Marx Leipzig, Ujerumani mwishoni mwa 1981 na kukamilisha masomo yake mnamo 1985.
Miezi michache baadaye, aliteuliwa na Rais wa Zanzibar wakati huo, Mzee Idris Abdul Wakil kuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya  Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI) ambayo baadaye iliitwa Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA).
Alielekea Kenya mnamo 1987 na kuwa Mwenyekiti wa kwanza wa Idara ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Moi, Eldoret na baadaye kufundisha Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Nairobi hadi 1990.
Kisha alitua Japan kufundisha Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Osaka akiwa Mkuu wa Idara ya Lugha za Kigeni. Alipata Uprofesa na kuhamia Chuo Kikuu cha Bayreuth, Ujerumani alikofundisha Kiswahili kati ya 1997 na 2012.
UANDISHI
Alipenda kusoma, kutunga mashairi na hadithi fupi tangu alipokuwa mwanafunzi wa darasa la tano. Alitunga mashairi ambayo mengi yalitumiwa na walimu kufundishia madarasa ya juu.
‘Nimfuge Ndege Gani Ili Nipate Salama’ ni shairi lake la kwanza alilolitunga mnamo 1960.
Mengi ya mashairi yake yalighaniwa katika Radio Zanzibar. Alipata motisha zaidi kutoka kwa walimu wake, Mohamed Abdallah na Kindi Abubakary waliomhamasisha pakubwa.
Anakiri kurithi kipawa cha usanii kutoka kwa mama yake “mkubwa” aliyekuwa nyakanga. Mama huyu alikuwa bingwa wa kuimba nyimbo za unyago.
Pia alikuwa mtunzi mzuri wa mashairi na alipenda sana hadithi za jadi za fasihi simulizi. Zaidi ya kurithi kipaji kutoka kwa mama yake, uandishi wa Said ulitokana na mafunzo ya elimu ya dini ya Kiislamu aliyopata  katika madrassa.
Aliwahi kushiriki mashindano ya Uandishi wa Hadithi Fupi za Kiswahili yaliyodhaminiwa na Shirika la Habari la BBC katika miaka ya 90.
Nyingi za hadithi zake pia zilisomwa katika kituo cha Deutsche Welle (DW), Ujerumani. Hali hii ilimhimiza kuandaa diwani Sadiki Ukipenda na Hadithi Nyingine, kitabu kilichochapishwa na Jomo Kenyatta Foundation (JKF) mnamo 2002.
Said alidhihirisha uwezo alio nao katika kutunga visa bunilizi vilivyoelezea maisha halisi ya kila siku katika jamii.
Upekee wa kisanaa katika riwaya za Mohamed Suleiman Mohamed, Kiu (1972) na Nyota ya Rehema (1976) ulimpa Said hamu na shauku ya kuandika riwaya yake ya mwanzo, Asali  Chungu (1977). Baadaye alitunga Utengano na Dunia Mti Mkavu vitabu vilivyochapishwa mnamo 1980.
Kazi hizo zilimzidishia umaarufu na kumfungulia milango ya kupokezwa tuzo za haiba kubwa ndani na nje ya Afrika.
Akiwa mshairi mahiri, Said ametunga diwani mbalimbali zikiwa ni pamoja na Sikate Tamaa (1980), Kina cha Maisha (1984) na Jicho la Ndani (2002), kazi zinazozamia masuala ya kisiasa, kiuchumi, mapenzi na utamaduni.
Ujuzi wa fani katika utunzi wa fasihi ni sifa iliyomfanya kufaulu kutumia mtindo wa uhalisia mazingaombwe katika Kivuli Kinaishi (1990), Amezidi (1995), Babu Alipofufuka (2001) na Sadiki Ukipenda (2002).
Ametumia kwingi mbinu za bunilizi, utomeleaji na taswira katika tamthilia za Pungwa (1988), Kitumbua Kimeingia Mchanga (2004) na Posa za Bi Kisiwa (2007) aliyoiandika kwa kumshirikisha Profesa Kitula King’ei wa Chuo Kikuu cha Kenyatta.
Nyuso za Mwanamke (2010) ni riwaya aliyoitunga Said miaka 36 baada ya kuchapishwa kwa Utengano (1980). Anajivunia pia riwaya Kiza  Katika Nuru (1988), Tata za Asumini (1990), Dunia Yao (2006), Mhanga Nafsi Yangu (2012) na Mkamadume (2013).
Ameandika zaidi ya vitabu 60, cha karibuni zaidi kikiwa Mashetani Wamerudi,tamthilia iliyozinduliwa rasmi Oktoba 10, 2016 katika Tuzo za Kumi – Kumi  za WASTA.
Gharama ya Amani (2014) ni kitabu chake cha hadithi kinachosisitiza umuhimu wa utu, uadilifu na utaifa miongoni mwa wanajamii.
Akiwa miongoni mwa waandishi wa riwaya za kimapinduzi na kifalsafa, baadhi ya kazi zake zimetafsiriwa kwa lugha za kigeni.
Ametajwa kuwa mwandishi mashuhuri zaidi Afrika Mashariki kutokana na ukamilifu wake katika kuandika riwaya, tamthilia, mashairi, hadithi fupi, kazi za watoto na hata vitabu vya kiada vya kufundishia shule za msingi, upili na vyuo.
Ameandika zaidi ya vitabu 60, cha karibuni zaidi kikiwa Mashetani Wamerudi, tamthilia iliyozinduliwa rasmi Oktoba 10, 2016 katika Tuzo za Kumi – Kumi ambazo hutolewa kila mwaka na mwasisi wa WASTA Kituo cha Kiswahili Mufti, Guru Ustadh Wallah Bin Wallah.
FAMILIA
Said ana mke mmoja, Rahma na watoto wawili. Msichana Najima, jina lenye maana ya nyota.
Jina la mvulana ni Mahir, neno la Kiarabu linalomaanisha mwenye ujuzi. Wote hawa wamemaliza kusomea Shahada ya Kwanza.
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)