MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
Eleza kwa mifano ya kutosha ngeli za upatanisho wa Kisarufi. Onesha uzuri na upungufu

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
Eleza kwa mifano ya kutosha ngeli za upatanisho wa Kisarufi. Onesha uzuri na upungufu
#1
SWALI: Eleza kwa mifano ya kutosha ngeli za upatanisho wa Kisarufi. Onesha uzuri na upungufu wake.                          
Fasili ya ngeli imejadiliwa na wataalamu na wanazuoni mbalimbali, huku kila mtaalamu akiwa na mtazamo wake juu ya dhana hii. Baadhi ya wataalamu na wanazuoni hao ni kama hawa wafuatayo:
Mgullu (1999: 148) anasema istilahi “ngeli” imechukuliwa kutoka lugha ya Kihaya (Tanzania). Katika lugha ya kihaya neno “ngeli” lina maana ya aina ya kitu.
Mgullu (1999: 148) akiinukuu Kamusi ya Kiswahili Sanifu (1981) anaeleza kuwa ngeli ni utaratibu wa taaluma ya Sarufi ya lugha katika kupanga aina za majina (nomimo) kama vile ki-vi, ma, n.k.
Mgullu anaendelea kusema kuwa fasili hii inapotosha. Tunaamini ya kuwa ngeli ni kundi la nomino za aina moja na si ule utaratibu wa kupanga nomino katika makundi kama fasili ya hapo juu inavyodai.
TUKI (1990) wanaeleza kuwa ngeli za nomino ni kundi moja la majina yaliyo na upatanisho wa kisarufi unaofanana na viambishi vya umoja na wingi vinavyofanana. Fasili hii inaonekana ni bora lakini tatizo lake ni kuwa imeweka pamoja vigezo viwili, yaani kigezo cha kisintaksia na kile cha kimofolojia. Kwa maoni yangu ni kuwa vigezo hivi haviwezi kutumika pamoja kwa sababu havina uhusiano wa moja kwa moja. Wanaisimu na wachambuzi wengi wa awali walijaribu kuvitumia vigezo vyote viwili kwa pamoja wakati wa kuainisha ngeli za nomino za Kiswahili lakini walishindwa. Hali hii imesababisha uainishaji wa ngeli katika lugha ya Kiswahili uonekane kuwa wa kutatanisha.
Massamba, D.P.B na Wenzake (2012) wanasema kwamba ngeli ni mgawanyiko wa aina mbalimbali za nomino katika mtazamo wa kisarufi katika fikra ya viashirio vya nomino katika aina nyingine za maneno zinazoandamana nazo. Kwa maelezo mafupi tunaweza kusema ngeli za nomino huhusu makundi ya majina; kila kundi likiwa na mabadiliko ya aina moja ya viambishi vya umoja na wingi vyenye kuleta upatanisho wa kisarufi wa namna moja katika vitenzi, vivumishi na viwakilishi. Kila ngeli ina kiambishi cha nomino zake ambacho kinatawala viambishi vinavyorejelea nomino hiyo katika aina hizo nyingine ziandamanazo nayo.
Massamba na Wenzake wanaendelea kufafanua kuwa kila lugha inayotumia utaratibu wa ngeli huwa ina idadi fulani ya ngeli. Si rahisi kusema kwa yakini hapo zamani lugha za kibantu zilikuwa na ngeli ngapi, lakini tunajua kwamba kwa wastani lugha nyingi zina ngeli zisizopungua kumi na zisizozidi ishirini.
Wanaisimu wengine Ashtoni (1944) na Broomfield (1930) waliainisha majina baada ya Meinhof, walifuatisha mtindo wa Meinhof, isipokuwa wanayaweka katika ngeli moja majina ya umoja na uwingi ambayo yanachangia mzizi mmoja badala ya kuyaona kuwa ni tofauti. Kwa uainishaji huu walipunguza idadi ya ngeli  hadi kufikia 9 tu.
Uainishaji wa akina Ashton na Broomfield unafanana na ule wa Meinfoh kwa sababu wote wameegemeza uainishaji wao katika umbo la viambishi awali vya majina. Hata hivyo uainishaji wao umekuwa mwepesi zaidi kwa mtu anayejifunza ngeli za majina kwa vile unaonesha uhusiano wa umbo la umoja na uwingi la majina ya aina moja. Zaidi ya hayo uchache wa ngeli hizi unamfanya mwanafunzi azikumbuke kwa urahisi.
Kigezo cha sintaksia /upatanisho wa kisarufi:
   Huu ni mtazamo wa kisasa wa uainishaji wa ngeli ambao umeyagawa majina katika makundi kulingana na upatanisho wa kisarufi kati ya jina na viambishi awali vilivyo katika vitenzi. Kwa mujibu wa mtazamo huu, majina yamepangwa katika makundi tisa ambayo ni:-
  1. A -WA
Mfano; Mtoto anacheza / Watoto wanacheza.
Mzee analima / Wazee wanalima.
Mwanafunzi anasoma / Wanafunzi wanasoma.
  1. U – I
Mfano; Mkufu umekatika / Mikufu imekatika.
Mji umevamiwa / Miji imevamiwa.
Mkaa umemwagika / Mikaa imemwagika.
  1. LI – YA
Mfano; Gogo limevunjika / Magogo yamevunjika.
Gari limepotea / Magari yamepotea.
Jiko limewaka / Majiko yamewaka
  1. KI – VI
Mfano;   Kiapo kimekiukwa / Viapo vimekiukwa.
Kilima kimesawazishwa / Vilima vimesawazishwa.
Kikongwe kimeuawa / Vikongwe vimeuawa.
  1. I – ZI
Mfano; Ng’ombe imechinjwa / Ng’ombe zimechinjwa.
Nguo imechanika / Nguo zimechanika.
Nchi imekosa amani / Nchi zimekosa amani.
  1. U – ZI
Mfano; Ubao umeandikika / Mbao zimeandikika.
Ukuta umeanguka / Kuta zimeanguka.
Uzi umetumika / Nyuzi zimetumika.
  1. U – YA
Mfano; Ugonjwa unatisha / Magonjwa yanatisha.
Uasi umekithiri / Maasi yamekithiri.
  1. KU
Mfano; Kulima kunachosha.
Kuimba kwake kunafurahisha.
Kufurahi kwake kumemponya.
  1. PA – MU – KU
Mfano; Hapa pananuka.
Humu mna nzi.
Kule kumebomoka.
UZURI WA KIGEZO CHA KISINTAKSIA
  1. a)Unajitosheleza kwa kuwa kila jina linakuwa na upatanishi wake katika kitenzi.
  2. b)Kimepunguza idadi ya ngeli za nomino hivyo kurahisisha uwezo wa kuzihifadhi kichwani.
  3. c)Nomino hupangwa katika ngeli zake kulingana na sifa na hadhi yake
  4. d)Hurahisisha kubainisha umoja na wingi kwa nomino zisizo na maumbo dhahiri ya idadi
  5. e)Kigezo hiki kimepunguza kujirudiarudia kwa ngeli
  6. f)Husaidia kubaini uhusiano wa nomino na maneno ya kategoria nyingine katika tungo
  7. g)Husaidia kuonesha urejeshi wa nomino kwenye kitenzi husika
UPUNGUFU WA KIGEZO CHA KISINTAKSIA
  1.        a) Kuna viambishi vinavyojirudia. Mfano, U- imejitokeza katika ngeli ya 2, 6 na 7.
  2.        b) Huyaweka majina yenye maumbo tofauti katika ngeli moja.
  3.       c)Kunaweza kuwa na utata katika upatanisho kwa baadhi ya majina kama “makala” “Jambazi” na “Marashi”
Mfano; Makala yamechapishwa.
Makala imechapishwa.
Sentensi hizo zote zinatumika ila hatuna wingi wa makala katika Kiswahili
  1.      d) Ngeli ya kwanza umoja ina viambishi viwili Yu-/ na A-/
  2.      e) Kigezo hiki hakisaidii kutambua mofolojia ya nomino.
Hitimisho
Kwa kuwa tumeshaona upungufu na matatizo ya uainishaji wa wataalamu na wanaisimu hao, kuna haja ya wanaisimu na wanazuoni kuendelea kufanya utafiti na uchunguzi ili kuondoa upungufu huo.
MAREJELEO
 
Massamba, D.P.B. na Wenzake (1999). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA) Sekondari na Vyuo. Dar es Salaam: TUKI.
Mgullu, R.S. (1999). Mtalaa wa Isimu, Fonetiki, Fonolojia na Mofolojia ya Kiswahili. Nairobi: Longhorn Publishers.
Rubanza, Y.I. (1996). Mofolojia ya Kiswahili. Dar es Salaam: Chuo Kikuu cha Tanzania.
Taasisi ya Elimu (1996). Kiswahili Kidato 1-4. Dar es Salaam: Oxford University Press.
TUKI. (1981). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam: TUKI.
Swalo, D.B. (Muswada). Darasa la Kiswahili: Kidato cha Tano na Sita
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)