MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
ODC : MADA YA 1: LUGHA NI NINI?

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
ODC : MADA YA 1: LUGHA NI NINI?
#1
ODC : MADA YA 1: LUGHA NI NINI?
YALIYOMO
1.1 UTANGULIZI
 Ukitaka kuelewa  lugha ni nini uwe unawasikiliza watu wanapozungumza lugha ambayo huielewi huku jambo lililozungumzwa linakuhusu moja kwa moja .Katika hali kama hiyo wewe mwenyewe mazungumzo hayo yataonekana ni mwingiliano wa sauti tu ambazo zinakuletea kelele tu.Lakini wahusika yamkini utawaona wakicheka,wakikutazama ,wakihuzunika ,wakioneshana ishara na kuonesha hisia zao.Wewe  yamkini utaambulia kuona ishara na kupata hisia kutokana na uzoefu wa jamii utokayo.kimsingi wao huelewana kwa lugha waitumiayo  hali hii ndio hujumuiswa na kutoa jibu la kwamba lugha ni chombo cha mawasiliano.
Swali la kujiuliza :ni kwa namna gani kelele zinazosikika zikitamkwa mara kadhaa na kwa namna fulani tofauti tofauti ,zinawezesha kuelewana ,kupeana maelekezo ,kuwasilisha ujumbe na kupeana habari kwa kila muhusika wa kelele hizo.Yamkini wazo unaloweza kupata kwa haraka linaweza kuwa lazima kelele zitolewazo na wahusika zina maana fulani ijulikanayo kwa wasemaji /watamkaji wa kelele hizo.Kwa hakika kelele za namna hiyo zikifikia kiwango cha kuweza kufikisha mawasiliano  juu ya masuala  yanayojitokeza katika jamii fulani ndipo kelele hizo huitwa lughaya jamii husika.
1.2 MADHUMUNI YA MHADHARA
                 Baada ya kusoma muhadhara huu utaweza:

(i) kueleza asili ya lugha
(ii) kueleza maana /dhana ya lugha
(iii) kujadili aina za lugha
(iv)kujadili mitazamo mbalimbali ya fasili ya dhana ya lugha
(v) kujadili tabia za  lugha.
(vi) kufafanua sifa za lugha
1.3 KIINI
1.3.1 Asili ya Lugha
Ni dhahiri kuwa kila jamii ina hadithi zake kuhusu jinsi lugha yake ilivyozaliwa/kuanza.Lakini katika historia  kuna hadithi nyingi zinazohusu asili/chimbiko la lugha zote za binadamu.Mojawapo ya hadithi hizo ile inayosimuliwa katika kitabu maarufu kama Biblia inayohusu chanzo cha watu kunena lugha mbalimbali  wakati wa ujenzi wa mnara wa Babeli.Ambapo inasemekana kwamba kulitokea kutoelewana kwa kila mmoja kuzungumza lugha yake na huo ukawa mwanzo wa lugha mbalimbali Duniani.Hadithi hii yaelekea kuwa na ukweli kiimani zaidi kwani watu wa imani hii  huamini kuwa ni kweli  lakini kitaalumu hakuna kigenzo chochote ambacho kinaweza kidhibitisha ukweli huo.
1.3.1.1 Mtazamo wa kiisimu
Kiisimu asili ya lugha huweza kutazamwa kwa namna mbili .namna ya kwanza ni ile  inayoangalia hali za mabadiliko ya binadamu toka kale hadi kupata lugha asili ambazo zote ni kamili  kwa kiwango cha kukidhi mahitaji ya jamii fulani. Katika mtazamo huu inaelezwa kwamba lugha huweza kuzuka kukua na kufa.Namna ya pili ya mtazamo juu ya asili ya lugha ni ule unaozingatia namna motto anavyoipata lugha.Kimsingi ni dhahiri kwamba hakuna motto anayezaliwa akiwa na lugha au uwezo wa kuzungumza lugha fulani . Badala yake kila motto huzaliwa katika hali ya kawaida bila lugha lakini huwa na uwezo wa kupata lugha yeyote ya jamii inayomlea au jamii inayomzunguka.ukiangalia namna hii utagundua kuwa ili mtoto aweze kupata lugha ni lazima awe miongoni mwa jamii ya watu.mpaka sasa wataalamu hawajasema lolote iwapo mtoto ataachwa mahali bila kuwa na mwingiliano na watu /jamii yeyote atakuwa na lugha au atakuwa na athari gani kilugha kutokana na upweke huo.
Katika ujumla wake umejifunza kwamba chimbuko la lugha linafungamana sana na maumbile pamoja na mazingira ya mtu binafsi na jamii yake kwa mda mrefu.katika kipengele cha muda haijajulikana vema muda kamili ni upi na hivyo kupelekea kuwepo na simulizi kuhusu chimbuko la binadamu na lugha yake.
1.3.2 Maaana ya Lugha
Fasili ya lugha kwa mujibu wa wa crystal (1992) anasema :”lugha ni mfumo wa sauti nasibu, ishara au maandishi kwa ajili ya mawasiliano na kujieleza katika jamii ya watu”
Katika fasili yake ametaja mambo makuu matano ambayo ni mfumo,sauti za nasibu, sautialama na ishara,jamii ya wanadamu, mawasiliano na kujieleza/kujitambulisha.
Ili kupata dhana nzima ya fasili hii ni muhimu tuangalia kila kipengele katika fasili yake:
1.3.2.1 Mfumo
Kila lugha ina muundo wake ambao huwa ni fofauti na lugha nyingine.kwa maana hii kila lugha ni kijisehemu cha miundo iliyopo katika kundi zima la miundo ya lugha duniani.miundo hiyo yaweza kuwa jinsi maneno yalivyoundwa jinsi maneno yalivyofuatana.hivyo kila lugha ina ruwaza maalumu.
1.3.2.2 Sauti Nasibu
Hapa ina maana kuwa hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya neno na kile kinachowakilishwa katika lugha.Hivyo maana inayowakilishwa huwa ni ya kinasibu tu au inatokana na makubaliano ya wanajamii/watumiaji wa lugha fulani katika mazungumzo yao ambayo huwa yanatofautiana kutoka rika moja hadi jingine.
   Mfano Neno MEZA halina maana ya moja kwa moja na umbo linalowakilishwa.
1.3.2.3 Sauti, Alama na Ishara
  Kimsingi kila lugha huteua sauti ,alama au ishara zianazowakilisha wazo au ujumbe.lugha nyingi hutumia sauti katika mazungumzo wakati baadhi ya lugha hutumia ishara za maandishi katika mawasiliano na lugha nyingine hutumia alama katika kukamilisha mawasiliano.
1.3.2.4 Jamii ya Wanadamu
Kimsingi ni wanadamu pekee ndio watumiao lugha  na ni jamii zao pekee zinazoteua maneno na kuyapa maana waitakayo katika jamii hiyo sambamba na jinsi gani miundo ya lugha zao wanataka ziwe.Viumbe wengine wana njia za mawasiliano  ambazo zinatofautiana kabisa na njia za mawasiliano ya wanadamu.Hivyo lugha huwa ni kwa wanadamu tuu.
1.3.2.5 Mawasiliano
Katika kueleza dhana nzima ya lugha inafaa kugusa dhima ya lugha hiyo kwa wale waitumiayo.Lugha hutumika kama njia kuu ya mawasiliano.Kwa kupitia lugha watu huweza kutoa  na kupokea ujumbe pamoja na kutolea hisia zao.Kwa kutumia lugha tunasema  tukitakacho ili kukidhi mahitaji yetu.Mawasiliano katika lugha kunaajumuisha kuzungumza ,kuandika,kusoma na hata kutumia mifumo mingine ya ishara.njia zote hizi ni njia za mawasiliano kwa kutumia lugha.
1.3.2.6.Kujieleza/kujitambulisha
Ni dhahiri kabisa kwamba wanajamii huitumia lugha kwa ajili ya mawasiliano katika Nyanja zote za kimaisha ( kisiasa kiuchumi na kiutamaduni)inafaa ikielewa pia kuwa katrika kuizunguma, kuiandika  kuisoma na pengine kuzitumia ishara fulani,mtumiaji kwa namna moja ama nyingine hujitambulisha na kujieleza kwa hadhira kwamba yeye ni nani, anazungumzia nini, na nani,  wa utamaduni gani,na pengine hata eneo analotokea ni wapi?yote haya huweza kudhihirika kutokana na ukweli kwamba lugha huwa na sifa kubwa ya kubeba utamaduni wa mahali lugha inapozungumzwa.hivyo lugha ni kielelezo chako katika mazingira na utamaduni wa unamoishi.ikitokea lugha unayiozungumza si ya utamaduni wako au asili yako, basi utatambulika tu na wanajamii wenye utamaduni wa lugha yao.
Japokuwa watanzania wote twaweza kuzungumza Kiswahili kama lugha ya taifa na ni lugha ya mawasiliano kwa taifa letu lakini wazungumzaji huweza kujitambulisha maeneo watokayo katika sehemu mbalimbali za Tanzania.si jambo geni kusikia wazungumzaji wakisema huyo atakuwa mhehe wa mfundi au mbena wa njombe kwa maana hawa hawana “s” ila wana ‘z’ au huyu mtu wakusini maana hawa hawaa “m” badala yake wana “n.kwa mfano hii lugha huweza kutambulisha eneo mtu atokako.
Katika ufafanuzi  wa dhana ya lugha ni muhimu kuzingatia vipengele vilivyojadiliwa hapo juu ilio kutoa dhana ya lugha kwa upana wake.
 
1.3.3 Aina za Lugha
Kwa kutumia msingi wa kutazama hali halisi na mifumo ya sauti na ishara anayoitumia binadamu kwa ajili ya kukidhi mahitaji yake ya lugha katika jamii,wataalamu wa lugha wameafikiana kutenga lugha katika aina kuu mbili ambazo ni lugha asili na lugha unde.
 
1.3.3.1 Lugha za Asili
Lugha asili ni ile lugha inayohusisha mfumo wa sauti zinazotolewa kwa kutumia ala katika chemba ya mdomo wa binadamu Lugha asili ina sifa za kuwa na viwango tofauti katika  muundo wake,na huwa na uwezo wa kuzalisha tungo zisizo na ukomo/kikomo.kwa mujibu wa mwanaisimu John Lyons,lugha asili ina viwango viwili muhimu vya muundo ambavyo ni :
(i)Kiwango cha msingi kinachohusisha vipashio kamili vyenye maana kama vile maneno
(ii)Kiwango kisicho msingi kinachihusisha vipashio ambavyo vyenyewe havina maana lakini hutumika katika kuunda vipashio vipashio vya msingi.vipashio hivi huwa ni sauti katika lugha (Lyons 1970:11-13)
Sifa hii ya uwezo wa kuzalisha tungo zisizo na ukomo kimsingi inahusu hasa uwezo wa binadamu wa kuunda na kuelewa idadi isiyo kikomo ya maumbo ya maneno na sentensi katika lugha  yake.hii hufanyika kiasili bila mhusika kukusudia kutumia kanuni fulani za kisarufi katika lugha yake.Katika uzalishaji huu mtumiaji wa lugha hutumia sauti  fulani ili kupata maneno ya aina fulani.Kwa mfano kwa kutumia sauti i,m,l na a katika mipangilio mbalimbali ,katika Kiswahili tunaweza kupata maneno kama imla,lima,lami.
Pia kwa kutumia muundo wa aina moja kuweza kuzalisha sentensi nyingi mbalimbali.kwa mfano kwa kutumia muundo wa wenye KIIMA, KITENZI NA YAMBWA ianwezekana kupata sentensi kama:
Tembo amemla mtu
Mtu amemla tembo
Mwalimu anasoma gazeti
Mama anapika ugali
Mkulima analima karanga.n.k.
1.3.3.2 Lugha Unde
Lugha unde ni ile inayohusu mfumo wa ishara ambazo binadamu amezibuni na huzitoa kwa kutumia viungo vyake vya mwili kama mikono,vidole kope za macho n,k maandishi pia huingia kwenye kundi la hili kwani ni nyenzo mojawapo anazoziunda mwanadamu ili kikidhi mahitaji yake ya mawasiliano.katika hali ya kawaida lugha hii huwa na maana tofautitofauti kutokana na rika la watu uhusiano wao,mahali, tukio napengine mahitaji yake.
Hadi leo haijajulikana kama wanyama wana aina gani ya lugha kati ya hizi.chakujiuliza ni je wanyama wana lugha ?na kama wanayo ipo katika kundi gani?aidha sifa zilizobainishwa zinaelezea kitu kinachoitwa lugha na kudokeza kwamba si kila njia ya  mawasiliano ni lugha katika  maana ileile ya lugha.
1.3.4  Mitazamo Mbalimbali Juu ya Fasili ya Dhana ya Lugha
Wataalamu wengi wameileza dhana ya lugha tangu miaka ya 1920 na 1930 hususan wanaisimu wa skuli ya isimu-miundo ambao ni Leonard Bloomfield na Edward Sapir.mawazo yao kuhusu ni lugha ni kwamba (i)lugha ni ishara (ii)ishara hizo huzihusisha moja kwa moja na ala za sauti zilizomo katika bomba la sauti,(iii)sauti hizo zimo katika mfumo maalumu,(iv)mfumo huo wa sauti ni wanasibu(V)kwa kutumia mfumo huo wa nasibu, jamii inayoitumia lugha husika huwasiliana.zipo fafanuzi nyingine za lugha ambazo zimejikita katika misingi ya Nyanja totauti ya kitaaluma kama ifuatavyo:
Kwa wanafalsafa wanaona lugha ni chombo cha fikra. Wao huona kwamba mtu hawuzi kufkiri bila kuwa na lugha hivyo lugha ni chombo cha fikra.
Kwa wanazuoni /wanaelimu jamii wanaona kwamba lugha ni namna fulani ya tabia.wao huhusiana namna mtu anavyotumia /anavyoongea na tabia yake kama mtu anaongea maneno yote kwa ukali hiyo ndio tabia yake na tofauti yake ni sahihi.
Kwa wanasaikolojia wanaona lugha ni mlango wa kutambua akili za binadamu wao wanaamini kwamba bila lugha huwezi kutambua akili za watu.
Ama kwa hakika wapo wataalamu wengine ambao huenda wamefafanua zaidi juu ya dhana nzima ya neno lugha ni jukumu,lako kutafua zaidi juu ya dhana hii.
1.3.5 Tabia za Lugha
Ama kwa hakika zipo tabia ambazo zinajitokeza kwa kila lugha ,tabia hizo zinaihalalisha lugha fulani kuwa lugha kwa maana halisi ya lugha.
1.3.5.1 Tabia ya kukua
Lugha ina tabia ya kukua,lugha inavyozidi kutumika katika jamii huongeza maneno kulingana na mahitaji, kitendo hicho hupelekea lugha kuwa na tabia ya kukua.Katika mchakato huu maneno ya zamani hubadilika na maneno mapya hujitokeza,mabadiliko haya hujitokeza kutokana na maendeleo ya kijamii,maendeleo ya sayansi na teknolojia.mabadiliko haya huwa yanajikita katika nyanja zote za kimaisha yaani kisiasa kiuchumi na kiutamaduni,kwa mfano kipindi cha maendeleo ya vyama vingi ndipo tulipopata misamiati ya ngangari ngunguri n.k pia kuna misamiati kama kasheshe,kilimo kwanza,kompyuta n.k.
1.3.5.2 Tabia ya kuathiri na kuathiriwa
Lugha ina tabia ya kuathiri lugha na kuathiriwa na lugha nyingine.kwa kawaida lugha inavyochua maneno fulani kutoka lugha nyingine huwa inaathiri lugha inakochukua maneno wakati lugha inayopokea maneno yale huwa inakuwa inaathiriwa na lugha ile.ni dhahiri kwamba Kiswahili kimeathiriwa na lugha ya kiarabu,kibantu,na kiingereza,wakati huohuo Kiswahili kimeathiri lugha hizo.
1.3.5.3 Tabia ya ubora
Lugha  ina tabia ya ubora .Tabia hii ina maana kwamba  kila lugha ni bora kwa wale wanaoitumia .Hakuna lugha iliyobora kuliko nyingine kwani kwa wale wanaoitumia inawafaa.Ijapokuwa upo uwezekano wa kuwa na bora lugha, bora lugha hujitokeza sana kwenye rejesta ambazo huzingatia mawasiliano ya kundi fulani na hivyo kuwa na bora lugha badala ya lugha bora.
1.3.5.4 Tabia ya kujitosheleza
Lugha ina tabia ya kujitosheleza kulingana na mahitaji ya jamii ambayo inaitumia.Tabia hii hujipambanua wazi kutokana na kujitosheleza kimsamiati kulingana na mahitaji ya jamii husika.
1.3.6 Sifa za Lugha
Lugha huhalalishwa kuwa lugha kutokana na sifa zifuatazo:
(i) Lugha ni lazima imuhusu Mwanadamu
Ama kwa hakika hakuna kiumbe kisichokuwa mwanadamu (mtu)kinachoweza kuzungumza lugha kwa maana halisi ya lugha.Lugha ni chombo maalumu wanachotumia wanadamu kwa lengo kuu la mawasliano.Kwa mantiki hiyo basi sifa kuu ya chombo hiki ni lazima kiwe kinamhusu mwanadamu na si  vinginevyo.
(ii)  Sauti
lugha ambayo inamhusu mwanadamu,huambatana na sauti za binadamu zinazotoka kinywani mwake.Katika jambo hili ni lazima mwanadamu atamke jambo kinyani mwakekwa sauti.Ijapokuwa mwanadamu anaweza kutumia njia nyingine ya maandisha na akawa amefikia lengo lake la mawasiliano.
(iii) Lugha ni lazima iwe na utaratibu maalumu
Kama ilivoelezwa kwenye fasili ya lugha  kuwa lugha ni sauti zenye utaratibu maalumu.ambao hupangwa kwa kufuata utaratibu fulani unaokubalika kwa jamii hiyo ya watu.Kwa maana hiyo basi si kila sauti itokayo kinywani mwa mwanadamu ni lugha,itakuwa lugha iwapo itakuwa imefuata taratibu zinazokubalika katika jamii husika.mfano mtoto anapolia anatoa sauti lakini hatuwezi kusema kulia ni lugha kwa sababu ni sauti inayotoka kinywani la  hasha.Utaratibu wa sauti hizo kwa neon moja hitwa Sarufi.
Mfano:
(a)Hatusemi.
(i)  Juma wimbo anaimba.
(ii) Kitabu changu mimi nimekipoteza.
(b)Jamii imepatana kusema kwa utaratibu ufuatao:
  (i) Juma anaimba Wimbo.
 (ii)Mimi nimekipoteza kitabu changu.
(iv) Lugha huwa na misingi ya Fonimu.
 
Lugha hufuata misingi ya fonimu ,ambapo lugha ina vitakwa au vipashio ambayo huitwa fonimu.wanaisimu wanakubaliana kwa ujumla kwamba fonomu ni sauti yenye uwezo wa kuleta tofauti katika maana ikipachikwa katika neno  la lugha husika.Baadhi ya fonomu za lugha ya Kiswahili:
1./a/,/e/,/i/,/o/,/u/.
Katika neno {tata} tunaweza kupachika fonimu nyingine na tukapata maana tofauti tofauti kama  ifuatavyo:
{tata}={teta}={tita}={tota}={tuta}
Pia katika neno {taa} tunaweza kuzalisha maneno yafuatayo:
{taa}={tea}={tia}=[toa}={tua}
2./p/,/b/,/t/,/d/,/f/,/k/,/g/,/s/,/z/n.k
Tunaweza kupata maneno kama pawa, bawa, tawa, dawa, chawa, jawa, gawa sawa zawa na maneno mengi mengineyo.
(v) Lugha hufuata mpangilio wa vipashio unaoleta maana
Lugha ni lazima iwe na mpangilio wa vipashio mpangilio huo huwa unafahamika na watumiaji wa lugha husika. Katika mpangilio huo ndipo unapotokea muundo wa sentensi kwa maana kwamba ili sentensi iwe na maana ni lazima vijenzi vya sentensi hiyo view kwenye mpangilio unaokubalika.katika lugha ya kiwsahili mpangilio huo huanza na fonomu,neno,kirai,kshazi na hatimaye sentensi.
 (vi) Lugha Husharabu
Lugha husharabu /hushabihiana hii ina maana kwamba lugha huchukua baadhi ya maneno kutoka
Lugha nyingine ili kujiongezea msamiati wake. Tabia hii inazisaidia sana lugha
zinazokua.Katika tabia hii lugha ikishachukua neno kutoka lugha nyingine hulifanya neno lile liendae na maneno mengine ya lugha husika.Kimsingi vitu viwili vinaweza kutokea katika tabia hii,kwanza lugha inaweza kuchua neno kutoka lugha fulani na kulitumia kama lilivyo,pili lugha inaweza kuchukua neno kutoka lugha nyingine na kulirekebisha ili liendane na mfumo mzima wa lugha husika.Vitu vyote hivi kwa neno moja huitwa kusharabu .
(vii) Lugha Inajizalisha
Lugha ina sifa ya kutumia vipashio vyake kujiongezea misamiati/maneno mapya.Kujizalisha kwa lugha huweza kutokea kwa  njia ya  kunyambulishaji na  mara nyingine lugha hujipatia misamiati kutokana na urudufishaji.
Unyambulishaji hufanyika pale vipashio vinapopachikwa kwenye mzizi wa neno ili kuzalisha maneno mengine.
                                       UNYAMBULISHAJI
 
UAMBISHAJI                                                 UNYAMBUAJI
 
                                               MZIZI
 
 
KIELELEZO                         
Unyambulishaji unahusu kitendo cha kuongeza vipashio mbele na nyuma ya mzizi. Uambishaji katika Kiswahili hutokea kabla ya mzizi wakati unyambuaji hutokea baada ya mzizi.
Katika mzizi{-lim-} inawezekana kufanya unyambulishaji na  kupata maneno kama:
(a)     Yeye Analima
(b)   Wewe Unalima
©    Mimi Ninalima
(d)   Wao wanalima
 
Kutokana na mfano wa hapo juu utaona kwamba uambishaji unaopofanyika unaendana sambamba na upatanishi wa kisarufi kama inavyoonekana katika mfano hapo juu a-d
Hata hivyo katika unyambuaji Kiswahili hujiongezea msamiati kwa kuzalisha maneno mapya,angalia mifano ifuatayo:
(a)pig=>ku-pig-a=>ku-m-pig-a=>tu-li-m-pig-a
(b)pig-i-a=>pig-ish-a=>pig-ish-an-a=>pig-ik-a
© pig-ik-a
 
1.4 Hitimisho
Lugha ni lazima iwe sauti za kusemwa na binadamu. Sauti hizo za
binadamu lazima ziwe na utaratibu maalumu wa kuwasiliana, na
kama hakuna utaratibu maalumu hiyo siyo lugha. Sauti na milioiko mingi duniani, milio ile inayoweza kuwafanya binadamu
wawasiliane ndiyo tunayoita lugha.
Lugha lazima iwe na sifa zinazoambatana na tabia za
binadamu katika utamaduni wake. Vinginevyo lugha husika
itakuwa si asilia
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)