MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
TASWIRA YA MWANAMKE KATIKA RIWAYA YA NYOTA YA REHEMA

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
TASWIRA YA MWANAMKE KATIKA RIWAYA YA NYOTA YA REHEMA
#1
Taswira ya Mwanamke katika Riwaya ya Mohamed (1976) Nyota ya Rehema
Nyota ya Rehema ni riwaya iliyoandikwa na Mohamed (1976). Riwaya hii inamsawiri
na kumjadili Rehema ambaye ndiye mhusika mkuu. Riwaya inatuonesha jinsi Rehema
alivyozaliwa na kukulia kwenye unyanyaswaji mkubwa wa mama yake mzazi kwa
sababu alizaliwa mweusi tititi, wakati ambapo wazazi wake wote wawili ni wa
asili ya Kiarabu. Mwandishi anaelezea maisha ya jadi katika visiwa vya Zanzibar
kabla ya mapinduzi ya mwaka 1964 yaliyomng’oa Sultani. Kuzaliwa kwa Rehema
kulisababisha mfarakano baina ya wazazi wake wawili, ambapo mama yake Rehema,
bi. Aziza alipewa talaka na kuhamishiwa nyumba nyingine. Akapewa kisogo na
Fuad: ambaye alioa mke mwingine aliyeitwa bi. Adila. Baada ya kifo cha mama
yake, Rehema alirejea na kuishi kwa baba yake pamoja na mama yake wa kambo.
Maisha ya malezi ya mama wa kambo yalikuwa magumu mno kwa Rehema. Rehema
aliamua kuyatoroka maisha haya, hatimaye alijikuta akiokolewa na Sulubu huko
msituni. Baada ya kukaa na Sulubu kwa muda, Rehema aliamua  kukimbilia mjini ambako aliona raha na taabu
za dunia. Kwa kifupi Riwaya ya Nyota ya
Rehema imemsawiri Rehema katika taswira mbalimbali zinazomfanya mwanamke
awe kiumbe duni na dhalili.
Taswira ya Mwanamke kama Chombo cha
Starehe
Taswira
mojawapo ni ile mwandishi aliyomchora mwanamke kama chombo cha kumliwaza na
kumstarehesha mwanamume. Mwandishi anatuchorea tabia dhalimu walizokuwa nazo
baadhi ya wanaume, ikiwa ni pamoja na kuwabaka mabinti wanaokataa kufanya ngono
nao. Haya yanathibitishwa na mwandishi wakati Rehema aliposikika akisema:
….Ngojea
kwanza bwana Mansuri; Rehema alisema, huku akishindana kuuzuia mwili mzito
uliokuwa ukimwelemea, Unataka kufanya nini? Usijifanye mtoto, Rehema unajua
mimi nakupenda, alisema Mansuri sauti yake ikiwa imebadilika. Rehema akijibu,
mimi si… sitaki … (uk. 65).
Mansuri
alitumia nguvu na uwezo wake aliokuwanao alipokuwa juu ya Rehema, ingawa Rehema
alijitahidi kujizuia asifanyiwe tendo kama hili. Lakini hatimaye Rehema
anabakwa na Mansuri.
Aidha,
mwandishi anatuonyesha jinsi Rehema alivyotumiwa na Mansuri ili kumfurahisha;
ingawa alikuwa ni mfanyakazi wa ndani wa Mansuri. Mansuri alipomletea Rehema
zawadi ya nguo, alimbusu kwa shauku kuu ikiwa ni ishara ya kumtaka kimapenzi.
Hapa mwandishi anatuonyesha Mansuri akimwambia Rehema:
…Ah,
hiyo ndiyo iliyokuchukua kuliko zote; huku akinyanyuka na kumsogelea Rehema.
Alimshika mikono yote miwili na kwa ghafula, bila ya Rehema kutarajia, Mansuri
aligusisha midomo yake juu ya shavu la Rehema, na kuondoa. Akisema umeonaje
Rehema, ugumu upo katika mara ya kwanza na ya pili tu. Sasa nenda kajitazame
kiooni….(uk. 63).
Hayo
ni baadhi ya matukio yanayochora hali ya matendo machafu na ya kudhalilisha
anayotendewa mwanamke katika fasihi ya Kiswahili. Mwanamke anachorwa kama
chombo cha starehe na kiburudisho kwa mwanamume. Hapa mara moja tunaoneshwa
kuwa mwanamke hapati starehe yoyote ile mbali na kupata karaha kutoka kwa
mwanamume huyo. Hapa yanajitokeza maswali kwa mtafiti katika suala zima la
mapenzi na kumwona mwanamke kama chombo cha starehe. Hii ni kutokana na ukweli
kwamba, kitendo hiki kinachowashirikisha jinsia zote mbili zinatumia tendo hili
liitwalo tendo la ndoa kufurahishana, kustareheshana na kuoneshana mapendo.
Hivyo waandishi hawana budi kuandika ukweli juu ya suala hili kwani jinsia zote
zinastareheshana na sio mwanamke pekee.
Taswira ya Umalaya
Taswira
hii ya umalaya unaofanywa na wanawake kujiuza miili yao ili kujipatia riziki
zao za kila siku ndiyo tunayoiongelea hapa. Kwa mfano mwandishi amewachora
Rehema, Kidawa na Ruzuna wakiwa katika harakati za kufanya umalaya ili waweze
kukidhi haja zao.
Mwandishi
anamsawiri Rehema akiendesha ukahaba wa hali ya juu mara alipoacha kazi kwa
Mansuri. Hapa mwandishi anathibitisha umalaya wa Rehema asemapo:
….Palikuwa
na vijana kemkem wa kitajiri waliomwomba aishi naye… Alitembea nao na kufanya
nao Ukahaba na baadhi yao alikaribia kuwapenda. Walimchukua hotelini, Vilabuni
na michezoni ambako wenzake walikuwa wakikulilia. Walimwambia wanampenda,
akaona ladha na maneno yao walimridhi aliyoyataka, akadeka na upole wao…..(uk.
78).
Hivyo
taswira ya umalaya inasababisha ugomvi kati ya wanaume, ambapo mhusika Chiku aliwagonganisha
wanaume hao na kuwafanya wagombane. Mwandishi anatueleza tukio hili kama
ifuatavyo:
…muda
si muda, wanaume wawili waliingiana maungoni. Mishindo ya ngumi ilisikika
waziwazi…. Yule bwana aliyeachwa uchi alipokimbilia kuficha sehemu ya siri,
adui yake alimpiga mweleka akamtupa chini (uk. 56-57).
Hapa
wahusika wanawake wanasawiriwa kuwa malaya na chanzo cha ugomvi kati ya
wanaume. Hili linasababishwa na kuyageuza mapenzi na tendo la kujamiana liwe na
sura ya kibiashara. Taswira hii inamsukuma mtafiti kujiuliza kuwa, Je wale
wanawake wanaowahonga wanaume fedha kwa ajili ya kufanya nao ngono watawekwa
katika kundi gani? Je wakati wa biashara hizo za ngono, jinsia zote hazifaidiki
kwa namna yoyote ile katika kujamiana huko? Maswali haya yatafumbuliwa katika
sura ifuatayo.
Taswira ya Wanawake kupenda Starehe
na Raha
Taswira
hii imejitokeza katika riwaya Nyota ya Rehema, Rehema amesawiriwa kuwa mhusika
asiyethamini kazi kuwa ndio msingi wa uhai na utu wa binadamu. Rehema anaamua
kuacha kazi kwa Mansuri na Rozi baada ya kuona kuwa anajitesa, mwandishi
anatueleza:
….Rehema
hakuona taabu ya kukosa kazi kwa Mansuri na Rozi na kusema kweli alishukuru
mapenzi aliyoonyeshwa yaliuviza unyonge wake; alitanabahi kuwa umbo lake ni
rasilimali yenye kutumainika. Maadam mwanamume yeyote aliyepishana naye, akiwa
topasi na ufagio wake au mtaalam wa kalamu yake wote hawakuweza kujizuia
wasigeuke kumtazama (uk. 78).
Kuwepo
kwa wanawake wanaoishi pasipo kufanya kazi halali kunadhihirisha dhana kwamba
jinsia ya kike ni mali mbele ya jamii inayohusudu kuuza utu kwa fedha.
Halikadhalika jinsia ya kiume nao wapo wanaotumia utu wao ilimradi kupata
mahitaji yao muhimu hawa ni wale wanaolelewa na wamama wenye pesa wanaojiita shuga mami. Hivyo sio wanawake tu
wanaopenda starehe na anasa kama anavyobainisha mwandishi. Hata hivyo, tofauti
za kimaumbile kati ya mwanamke na mwanamume zinaifanya jinsia ya kike ijione ni
bora na yenye thamani katika jamii hasa katika mfumo wa uchumi wa soko huria.
Taswira ya Mapenzi na Pesa kwa
Wanawake
Wapo
watu ambao wakipata fedha wanaweza kununua kitu chochote hapa duniani. Wanaweza
kununua mapenzi ya mtu, raha ya kila aina na hata ya kuupata utu wa mtu. Watu hawa
hawana imani ya kuwa hakuna uhusiano wowote ule kati ya fedha na mapenzi. Kwa
mfano, Fuad alikuwa tajiri aliyeamini kuwa Aziza atapata kila alichotaka, yaani
mambo yatakuwa sawa. Mwanamume huyu alikosea! Ilionekana kuwa fedha zilimfanya
Fuad asahau kwamba Aziza alimtaka yeye na sio fedha zake. Pia mwandishi
amemchora mwanamke akijiuza ili kupata pesa za kujikimu kimaisha. Kwa mfano,
wahusika kama wale akina Kidawa, Ruzuna na Chiku walimwingiza Rehema kwenye
maisha ya tamaa ya fedha na kujiuza pasipo binti huyu kujua hali halisi ya
dunia hasa kwenye upande wa mapenzi. Haya tunayaona mwandishi alipoandika:
Mwandishi
anasema, “Palikuwa na vijana kemkem wa kitajiri walimwomba Rehema waishi naye,
tayari kukidhi haja zao zote. Alitembea nao na kufanya nao mahaba, na baadhi
yao alikaribia kuwapenda (uk. 78).
Hali
hii aliendelea nayo akiamini kuwa fedha na mahaba vinakwenda pamoja, kwamba utu
na penzi halisi si vitu vya haja. Hadi alipochukuliwa na Bikiza ndipo
alizikumbuka zile siku nne alizoishi kwenye kibanda cha Sulubu. Ndipo
alipogundua kuwa kutembea kote huko na wanaume wote hao hakukutana na mwanamume
aliyemtosheleza na kumridhisha kama Sulubu.
Mapenzi
ya pesa yanaonekana kwa mhusika Karimu hakuwa na mapenzi ya dhati kwa Salama
bali alipenda pesa zake tu. Mapenzi ya Karimu na Salama hayawezi kulinganishwa
na yale ya Sulubu na Rehema, ambao walipendana kwa wema na sio fedha. Sulubu
alimsaidia Rehema bila tamaa isipokuwa kwa wema. Aidha, hakumpata hata mmoja
aliyekaa naye faraghani muda mfupi tu asidhihirishe uchu wake wa mapenzi
isipokuwa Sulubu.
 
Katika
sehemu hii, Rehema na Ruzuna wanawakilisha pande zote mbili za mapenzi
yanayomsibu mwanamke, yaani mapenzi ya dhati na mapenzi ya ulaghai ambayo ni ya
uongo. Rehema alichanganya mapenzi na tamaa ya fedha. Ndipo baadaye alizinduka
na kufahamu mapenzi ya kweli na hapo ndipo alipoamua kuishi na Sulubu. Kwa
upande mwingine Ruzuna alianza na mapenzi ya ukweli kati yake na Karimu lakini
baada ya kudanganywa na wanaume, akaamua kulipiza kisasi na kuingia kwenye
mapenzi ya uongo ili afurahi kuwaona waanaume wanavyopigana, ambapo tunaweza
kusema kuwa alifanya makosa makubwa.
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)