MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
<![CDATA[JIFUNZE KISWAHILI - Riwaya]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/ Sun, 28 Apr 2024 11:52:10 +0000 MyBB <![CDATA[SAFARI YA BULICHEKA NA MKE WAKE]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2824 Mon, 05 Sep 2022 09:07:07 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2824
.pdf   Safari ya Bulicheka na mke wake .pdf (Size: 2.29 MB / Downloads: 37) ]]>

.pdf   Safari ya Bulicheka na mke wake .pdf (Size: 2.29 MB / Downloads: 37) ]]>
<![CDATA[JANGA SUGU LA WAZAWA]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2797 Sat, 30 Jul 2022 16:41:27 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2797
.docx   JANGA SUGU LA WAZAWA.docx (Size: 29.96 KB / Downloads: 6) ]]>

.docx   JANGA SUGU LA WAZAWA.docx (Size: 29.96 KB / Downloads: 6) ]]>
<![CDATA[MAISHA YANGU NA BAADA YA MIAKA 50]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2790 Mon, 25 Jul 2022 05:12:14 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=2790
.pdf   Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini (Shaaban Robert) (z-lib.org).pdf (Size: 16.8 MB / Downloads: 18) ]]>

.pdf   Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini (Shaaban Robert) (z-lib.org).pdf (Size: 16.8 MB / Downloads: 18) ]]>
<![CDATA[RIWAYA TEULE ZA KARNE YA ISHIRINI NA MOJA NA UDURUSU WA NADHARIA ZA FASIHI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1810 Sat, 25 Dec 2021 12:19:31 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1810 Utangulizi
Sifa bainifu ya baadhi ya kazi za fasihi ya Kiswahili za karne ya ishirini na moja ni matumizi makubwa ya mbinu za kiuandishi za kimajaribio. Msomaji wa kazi hizi aghalabu hujikuta ameghumiwa na wingi wa urejeleo matini, uhalisia mazingaombwe pamoja na vipande vidogo vidogo vya visa ambavyo hutumika kuungia simulizi hizo zilizochupwa huku na huko (Bertoncini 2006: 93; Khamis 2003: 78). Kwa jinsi hali ilivyo riwaya hizi zinaelekea kutangaza upenuni kwamba enzi na dola ya uandishi wa kazi za kihalisia imepitwa na wakati na umefika muda wa kutoa wasaa kwa majaribio haya mapya. Ni maoni ya makala kuwa fauka ya mbinu hizi kuwa na natija pamoja na dosari zake bado kuna baadhi ya waandishi ambao bado wanaongozwa na misingi ya kihalisia.
Mbali na uwezekano wa kazi hizi za kimajaribio za kuitenga sehemu ya hadhira (wakiwemo wale wasiozifahamu nadharia za fasihi) kwa kumkumbatia zaidi msomaji aliyesoma na kuzamia fani adimu za kijamii, fasihi ya karne ya ishirini na moja ni njia jarabati ya kumkomaza msomaji ashiriki kikamilifu katika kufuatilia viini vya simulizi mbalimbali anazozikuta humo. Ndani ya riwaya hizi, msomaji anapambana na fikra za wanafalsafa, wanasiasa mashuhuri pamoja na vitimvi vyao, maswala ya utandawazi na athari zake, madondoo ya vitabu vya kidini, visa(a)sili, mighani,
majinamizi, na hata kazi nyingine za kifasihi za wasomi watajika. Makala hii inazamia kipengele kimoja tu cha mafunzo ya nadharia za fasihi ambazo huwa muhimu hasa kwa wanafunzi wa vyuo vya ualimu na hususani vyuo vikuu pale inapowabidi wazungumzie kitaaluma kazi za fasihi. Makala imetumia riwaya ya Musaleo! (2004) ya Kyallo WadiWamitila na riwaya nyingine mbili za Said Ahmed Mohamed za Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010) kama mifano mahususi ya namna waandishi wanavyozungumzia kwa dhahiri nadharia za fasihi. Nadharia katika Uhakiki wa Fasihi: Kipi kwanza? Katika jadi ya uhakiki wa kazi za fasihi, swala mojawapo lililozingatiwa kwa makini ni iwapo wahakiki wanastahili kuzingatia kile kinachosemwa na matini ili kielezwe kwa misingi ya kinadharia au kufanya kinyume chake.
Ingawa kuna kila ithibati kuwa wapo wataalamu waliofuata mojawapo kati ya njia hizo, ushahidi umeonyesha kuwa wengi wa wahakiki hupendelea kufuatiliwa zaidi kwa matini na kisha kuamua nadharia mwafaka itakayofafanua kwa uwazi kile kilichomo ndani ya matini. Said Khamis (2008) amelizungumzia hili kwa mapana na ametoa sababu ambayo naona niitaje hapa kwa kuwa inawafiki nadharia-tete inayoendelezwa na makala hii. Anasema: Nadharia zinabadilika taratibu zaidi kwa sababu mabadiliko ya nadharia mara nyingi huongozwa na mabadiliko ya mitindo na tanzu za fasihi yenyewe. Kinyume cha mambo kilichopo ni kwamba kila siku nadharia hujaribu kama inavyowezekana iwe na uwezo wa muda mrefu wa kuchambua na kuzieleza kazi za fasihi mbalimbali.
Lakini, kwa upande mwingine, hakuna nadharia inayoweza kufaa katika resi ambamo utoaji wa kazi za kubuni situ una wepesi zaidi, lakini mara zote unazingatia upya na mabadiliko. Hii ina maana nadharia fulani moja au zaidi zinaweza kufaa kwa muda fulani tu mpaka pale zinapojikuta, kwa sababu moja au nyingine, zinakumbwa na matatizo ya kutoweza kuzichambua vyema kazi zinazoibuka na upya na mabadiliko.
Wakati huu ndipo nadharia mpya inapohitajika. (Khamis 2008: 12) Nimemnukuu Khamis kwa mapana kutokana na kile anachokiona kama umuhimu wa nadharia za fasihi kuizingatia matini ambayo kama anavyosema daima imo mbioni kuzua mabadiliko.
Katika vitu viwili hivi vinavyotegemeana, matini inayobuniwa ndiyo inayosababisha zaidi haja ya mabadiliko katika nadharia ambayo huenda ikashindwa kuzizungumzia kazi mpya za kifasihi, hususani zile za kimajaribio. Pamoja na kuwafiki hoja anayoitoa Khamis, makala inazamia nadharia-tete ambayo inahusu uhakiki wa nadharia kama msingi huo wa ubunifu wa kimajaribio ambao unahitaji uteguliwe na nadharia.
Riwaya Tatu Teule kwa Muhtasari na Misingi ya Uteuzi wake Mbali na Euphrase Kezilahabi, wanariwaya Said Ahmed Mohamed na Kyallo Wadi Wamitila wametajwa kama waandishi wanaoongozwa na fikra mpya za kiuandishi, yaani uandishi wa kimajaribio ukiwemo ule wa kihalisia-mazingaombwe (Waliaula 2010: 143; Bertoncini 2006: 93; Khamis
RIWAYA TEULE ZA KARNE YA ISHIRINI NA MOJA
Makala inatambua kuwepo kwa sifa hizo za uhalisia mazingaombwe ndani ya riwaya miongoni mwa mambo mengi yaliyofumbatwa humo. Aidha, riwaya hizi zina sifa za kiusasabaadaye ambamo mna vipande vidogo vidogo vya simulizi zisizokuwa na muwala wala zisizochukuana vyema kama zilivyo hadithi za paukwa pakawa zinazoishilia na harusi au wahusika wanaoishi raha mustarehe. Kwa utaratibu wa sifa hizo, nimeteua riwaya husika za Musaleo! (2004), Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010) kwa kuwa zote zinaagua nadharia za fasihi kama sehemu mojawapo ya dhamira zilizomo ndani ya matini hizi. Musaleo! (2004) inajumuisha simulizi inayoenda mbele na nyuma na iliyofichama hadithi mbili tofauti na umazingaombwe usioweza kutabirika.
Ni hadithi inayomsukuma msomaji mbele na nyuma na mwingiliano matini uliokithiri unaohitaji umakinifu ili msomaji apate kuelewa fikra mbinu, njama, vitimbi na hila wanazotumia wakoloni mamboleo katika kuwazuga wale wanaosimama kidete kuzitetea haki zao katika jamii. Nyuso za Mwanamke (2010) nayo inamwendeleza nguli wa kike, Nana, na jinsi anavyojinasua kimawazo kutokana na wavu wa ulimwengu wa kiume kwa kufuata kile kinachoridhiwa na moyo wake.
Ni safari ya msichana, mwanagenzi wa maisha, anayeabiri kujua utu wake na sifa zinazomfafanua binafsi kama mwanamke, tofauti na wanavyotarajia wahusika wengine wa kike na wa kiume wa riwayani. Dunia Yao (2006), kwa upande wake, imesheheni mijadala ya kifalsafa inayozamia fani mbalimbali za sanaa na swala zima la ubunifu. Ninachokiona zaidi ni swala la uendelevu wa sanaa ukiwemo uhai na ufaafu wake katika kuzungumzia visa visivyowaelea watu katika ulimwengu mamboleo.
Dunia, inavyosema Dunia Yao, ni bahari isiyotabirika kina chake na sanaa haiwezi kuwekewa mipaka tunapoabiri kuizungumzia. Kama ilivyoparaganyika dunia, sanaa nayo haina budi kufuata mkondo huo kwani kuifuatilia dunia kwa mstari ulionyooka kama zilivyo kazi za kihalisia ni kuishi katika njozi.
Kuelewa nadharia za fasihi ni miongoni mwa njia adimu za kuelewa mafumbo ya kisanii na ya kimaisha yaliyoatikwa katika riwaya hizi. Makala imezamia baadhi ya nadharia za kifasihi ambazo zimejitokeza wazi wazi katika riwaya hizo tatu. Uhakiki wa Nadharia ya Mwigo Katika kitabu chake maarufu cha Poetics, Plato anaelezea asili na chanzo cha sanaa. Miongoni mwa mambo mengine, Plato humo anaelezea uhusiano wa karibu uliopo kati ya msanii na Mungu ambaye anachukuliwa kuwa mfalme wa sanaa zote. Hususani, Plato anamtaja Mungu wa sanaa aitwaye Muse ambaye huwapanda wasanii vichwani na kuwafanya wabubujikwe na mawazo ya kisanii pindi anapowakumba (kufuatana na Plato kama inavyofafanuliwa katika Tilak, 1993: 29).
Kwa mujibu wa Plato, Mungu huyu huwapagawisha wasanii tu na kuwapa ufunuo au wahyi unaowawezesha kuwasiliana moja kwa moja na wasanii (Habib 2005: 24; Wafula & Njogu 2007: 24).
Kwa sababu hiyo, Plato aliwaona wasanii kama watu wenye vipaji maalum vinavyotoka kwa Mungu na kwa sababu hiyo, siyo kila mtu angeweza kuwa msanii. Katika riwaya tatu zilizoteuliwa Dunia Yao, na kwa kiasi fulani Musaleo!, inafuatilia kwa makini nadharia hii ya Plato kuhusu mwigo na imethubutu hata kumchukua mhusika wake mmoja, Muse ambaye anahusishwa na ghamidha na kariha ya utoaji wa sanaa za kiubunifu huko Ugiriki, kuwa mshirika wa kiroho wa mhusika mkuu aitwaye ‘Ndi-‘. Mhusika Bi Muse (wakati mwingine Mize) wa Dunia Yao anazua mjadala mpevu wa swala zima la sanaa na hulka yake kama inavyowasilishwa na Mohamed. Mhusika huyu ambaye amechukuliwa moja kwa moja kutoka kwa maandishi ya wahakiki wa Kiyunani, Plato na Aristotle, anakuwa kiunzi muhimu cha kujadili swala zima la usanii. Haya yanadokezwa ipasavyo katika riwaya hii pale Bi Muse anapoeleza asili yake.
Ufunguzi wa sura ya tanounadokeza asili ya mhusika huyu, Bi Muse, ambaye ni yule yule aliyezungumziwa na Plato tangu jadi, tofauti hapa ikiwa Bi Muse ni mhusika wa hadithini. Sura inaanza hivi: “Mimi ni Muse” […] “Kwa asili hasa, Ugiriki – lakini siku hizi naishi popote. Mara nyingine hujificha katika vina virefu vya ardhi kabla sijachomoza kumzuru niliyemchagua. Na leo nimekuchagua wewe.
Kwa hivyo nimechomozekea chini ya mnazi palipofukiwa kitovu chako, baada ya kupiga mbizi Bahari ya Hindi kuja kukuingia kichwani mwako…” (Mohamed 2006:61) Sawa na anavyopendekeza Plato kuhusu namna wigo wa kisanaa unavyojiri, hapa mwandishi anaendeleza hoja hiyo hiyo ya namna Ndi- anavyosababishwa atunge kazi yake na Bi Muse.
Naye ni kiumbe anayetangaza kuwa asili yake ni Ugiriki (alikotoka Plato) na hamkumbi Mgiriki pekee bali humkumba mtunzi yeyote wa kazi za kubuni. Ana nguvu za kichawi za kumsababisha msanii apagawe kama riwaya inavyodokeza: “Kwa kawaida,” aliendelea, “sina umbo maalum. Ni aina ya jeteta linalochanua jinsi andasa zangu na zako zinavyokubaliana kuchanua. Sikuzaliwa katika dhati na bayana ya mambo.
Mimi ni binti wa Zeus na Mnemosyne. Asili yangu inasimamia kumbukizi na dhana tu. Ndio maana nina majina mengi kwa mujibu wa kazi yangu ya kutia ilhamu. Calliope, Clio, Erato, Euterpe, Melpomene, Polyhymnia, Terpsichore, Thalia, Urania.
Hata unaweza kuniita Bi Mize, kwa jina la kikwenu. Kwani hapa nilipo nimekuja kwa sura ya kikwenukwenu, kipande samaki, kipande mtu na kipande ndege.” (Ivi: 68f) Huyu anayefahamika kama Bi Muse katika riwaya anaeleza namna anavyoweza kubadili umbo na kuwa mwenza wa kila msanii duniani. Ingawa amezaliwa na Mungu Mkuu wa Kigiriki, Zeus, Bi Muse ana uwezo wa kuwa binti wa kifalme au wa kijini kwa kuzingatia utamaduni wa msanii husika. Ndiyo sababu hapa anamwambia Ndi- kuwa akipenda anaweza kumwita Bi Mize ili afahamu kwa ukaribu nguvu zake anapomkumba. Mize au Mwanamize ni mhusika wa Waswahili anayefahamika kwa vitimvi vyake na nguvu za kiuchawi za kugeuka umbo kama inavyosemwa kwenye dondoo.
Muse, kama anavyotangaza, ana nguvu za kichawi za kumzuga mtu na kummiliki pale anapomchagua na kumfanya kuwa kiti chake. Kitendo hiki cha kupandwa na jazba na kupagawa ndicho kinachojitokeza mwanzoni mwa riwaya pale Ndi- anapoeleza namna swala zima la utunzi linavyohusiana na nguvu hizo za Muse ambapo utunzi unakua hatua baada ya nyingine hadi kukamilika kwake: Katika kubuni na kuumba – ‘Bi Muse’ anapokujia na kukuchota kwa uzuri wake – kama koja la ajabu, unatunga sauti na sauti, ileile au tofauti, na kupata silabi. Silabi na silabi, unapata neno! Neno, maneno. Ibara na sentensi. Ibara na sentensi huzaa matini. Na vyote hivyo ni sehemu muhimu ya simulizi – maandishi. (Ivi: 9) Dondoo hili linaeleza kwa muhtasari uhakiki wa ki-Plato na ki-Aristotle unaohusisha uandishi na kujazibika kwa mwandishi. Safari inayoanza na sauti au fonimu moja inakua na kupea hadi kufikia kuwa matini nzima. Inapotokea hivyo, mwandishi na mungu huyu wa sanaa, Muse, huwa kitu kimoja. Ndi- anaelekea kukiri kuwa uandishi hufatwa na ghamidha na kariha inayomjia mwandishi na wala si jambo la vivi hivi tu, chambilecho Ndi- kuwa Muse si kiumbe wa ‘sasambura turore’ au anayejitoa hadharani kuonekana. Ni kana kwamba Ndi- hushindwa kujizuia na kuhamasika kuendeleza kazi yake ya kiubunifu pale anapotawaliwa kihisia na kifikra na Bi Muse.
Hujikuta tu akiongozwa asikokufahamu ingawa anavyokiri mwenyewe huwa ni wakati adimu wa kutamanika. Hii ndiyo sababu Dunia Yao inaufafanua uhusiano wa Ndi- na Bi Muse kuwa wa mke na mume wanaoliwazana na kubembelezana hadi wanapooana na kuwekana nyumbani. Ni taswira ya unganiko la kipekee ambalo hufukuza utasa na badala yake huzalisha kazi za kisanaa baada ya wahusika hawa kusuhubiana na hata kupata mtoto, yaani kazi inayotungwa. Hatua zote hizi zinaelezwa na Ndi- hivi: Ndiyo, jina lake nimekuwa nikilisikia na kulisoma siku nyingi. Kama alivyosema mwenyewe, si kiumbe wa sasambura turore. Hujifichua anapohitajiwa kwa mapenzi ya dhati au kwa kutoa msaada.
Na mimi, nimefikia baleghe ya kusalitika naye. Nina haja naye. Ninamhitaji. Ninataka anisaidie. Anisaidie kuwasaidia wengine ikiwezekana. Anisaidie kuukata ugumba wa utunzi. Nina hamu kurutubisha na kutia mbolea pahala fulani. Nipate kizazi kipya cha sanaa katika ukame wa ubunifu. Nipate kurutubisha kizazi kipya cha utu katika ukame usio na utu. Ninahitajia mtekenyo wake unipandishe jazba. (Ivi:61f) Swala la kupandwa na jazba linajitokeza pia katika Musaleo!. Katika riwaya hii, Kingunge anaonyesha kuwa uandishi wake hutokana na jazba na kariha inayomsukuma kuandika kile ambacho yeye mwenyewe hana maarifa nacho. Tunaelezwa hivi: Lakini mara hii alipomweleza mkewe uandishi wenyewe alilazimika kusikiliza kwa makini. “Mara hii ni tofauti. Inajisimulia mimi naandika tu. Ni kitu kama ndoto. Yaani kazi yangu ni kuandika yanayonijia. Ngoja niimalizapo utajua tofauti yake na nyingine…” (Wamitila 2004: 12).
Tofauti na riwaya ambazo Kingunge anadai amezipa majina, riwaya anayoandika kwa wakati huu ni ya kipekee na imepokea nguvu maalum asizoweza kuzidhibiti. Ni kariha ya kipekee inayomsibu na ambayo inamsukuma kuandika mambo asiyoyaelewa. Si ajabu basi anapodai kwamba riwaya hii itajipa yenyewe jina badala ya yeye kufanya hivyo (k.10f). Nadharia za Umaumbo wa Kirusi na Umuundo katika Dunia Yao Dunia Yao pia inahakiki kwa uwazi dhana za nadharia ya umuundo za uhusiano wamaneno kimfululizo na kiwimawima. Msingi unaochukuliwa na riwaya hii ni ule wa ki-Saussure, na ulioendelezwa baadaye na Roman Jakobson, unaohusiana na dhana zake za uhusiano wa ishara wimawima au kimfululizo (Eagleton 1996: 85f).
Katika Dunia Yao Mohamed anatueleza hivi: Uhusiano wima wa maneno unakuhakikishia uteuzi. Uhusiano mlalo unakuhakikishia mpangilio wa kisarufi.Unatii amri za lugha au unavunja kanuni za lugha wakati mmoja. Unajenga kutoka kipashio cha chini kwenda kipashio cha juu kabisa. Au unaweza kushuka kutoka juu kwenda kipashio cha chini kabisa. Madhumuni ni kujenga maana kwa njia ya kubomoa maana. Kujenga mvuto wa kisanaa. (Mohamed 2006:9; msisitizo wangu) Mohamed katika Dunia Yao anataja na kuzifafanua dhana mbili muhimu za umuundo ambazo anazirejelea kama “uhusiano wima” na “uhusiano mlalo” wa maneno. Mahusiano haya ya maneno, tunaelezwa, yana natija zake hasa kwa mwanafasihi.
Uhusiano wima wa maneno, tunaambiwa, huhakikisha uteuzi. Swala muhimu hapa ni kujua namna uteuzi huu unavyohakikishwa kwani haujabainishwa waziwazi kwenye dondoo. Mwamzandi (2007: 71) ametoa mfano ambao kwa muhtasari unafafanua swala hili la uteuzi: mchuti kiki Abasi aliupiga teke mpira mkwaju Katika mfano huu, neno ‘teke’ limechukuliwa kama neno la kawaida au la wastani ambalo msemaji wa Kiswahili angelitumia.
Maneno yaliyoandikwa kwa mlazo na ambayo yamejipanga juu na chini ya neno ‘teke’ ndiyo tunayoweza kusema kuwa yanahakikisha uteuzi unaozungumziwa na dondoo. Maneno hayo yanaeleza namna na jinsi mbalimbali za kuupiga mpira na mwanafasihi anaweza kuchangua neno mahsusi kwa kutegemea hisia maalum anayotaka kuibua kwa msomaji wake (Mwamzandi 2007: 71). Uhusiano mlalo wa maneno nao, kama unavyofafanuliwa ndani ya dondoo, una uwezo wa kuidumisha au kuivunja sarufi ya lugha, matokeo ambayo yanatokana na jinsi mwanafasihi, kwa mfano, atakavyochagua kuyapanga maneno yake katika sentensi. Katika sentensi, lugha yoyote huwa na matarajio na sheria zake za kisintaksia na kisarufi. Kwa sababu hiyo, kulibadilisha neno
moja katika sentensi na kuliweka mahala tofauti na pale panapotarajiwa na wanalugha husika kuna athari kubwa, ikiwemo ile ya kuzua maana tofauti na ile inayoweza kukubalika. Neno hilo linaathiriana kivingine na maneno mengine ya sentensi na kuzua maana mpya inayoweza kutegua uzoefu wetu wa lugha hiyo. Huu ndio ule mpangilio wa kisarufi unaoweza kutii au kuvunja kanuni za lugha na ambao unaozungumziwa na dondoo hapo juu na tunaweza kuutolea mfano huu: kitabu kizuri mtu mnene Hebu tazama sasa tunapobadilisha na kuanza na vivumishi na kisha nomino, na kuikaidi sarufi ya Kiswahili kama inavyotarajiwa: kizuri kitabu mnene mtu Ingawa maana iliyokusudiwa bado ipo, mabadiliko ya pale zilipo nomino na vivumishi kumesababisha ugeni fulani. Huu si muundo wa wastani wa Kiswahili ingawa unaweza ukakubalika katika miktadha mahsusi, ukiwemo fasihi.
Huku ndiko kujenga maana kwa njia ya kuibomoa kama kunavyozungumziwa na dondoo. Uhakiki wa Kidenguzi: Nyuso za Mwanamke na Dunia Yao Mbali na kushughulikia maelezo ya kinadharia kuhusu nadharia ya udenguzi, riwaya za Nyuso za Mwanamke na Dunia Yao pia zinashughulikia zoezi lenyewe la kuchanganua maana kwa kuongozwa na fikra hiyo ya kidenguzi. Ili tufuatilie kila kinachosemwa katika riwaya hizi mintarafu ya udenguzi ni vyema tuangazie, walau kwa muhtasari, fikra kuu ya nadharia yenyewe.
Udenguzi ni nadharia inayohusishwa na Mfaransa Jacques Derrida (1930-2004). Hapa nitafafanua misingi miwili tu ya nadharia hii kama ilivyofafanunuliwa na wataalamu mbalimbali (taz. Burman & McLure 2005: 284-286; Schmitz 2007: 115f). Mosi, mbinu kuu na muhimu inayotumiwa wa wanaudenguzi ni ukinzani wa jozi za maneno. Tasnifu ya Derrida kuhusu jozi hizo ni kuwa jamii za Kimagharibi zimejenga upendeleo wa wazi pale neno moja katika jozi husika daima linawakilisha utukufu au kile kinachopaniwa kufikiwa kama kitu adili huku dhana ya pili ya jozi hiyo hiyo ikiangaliwa kama ghushi, isiyo safi na ya daraja ya chini. Wanafilosofia wa awali, kama anavyodokeza Derrida, waliuona ulimwengu katika muktadha huo – jambo lililowafanya kuuona upande wa kwanza wa jozi za maneno kama unaojengwa na vitu vya kimsingi na vinavyostahili kupewa kipaumbele kama vilivyo safi, vya wastani na vilivyokamilika huku upande wa pili wa jozi nao ukifafanuliwa na vitu vilivyotandwa na utata, vyenye doa na umahuluti. Kwa sababu hiyo, usanifu wa hoja katika nchi za kimagharibi una tabia ya kuviona vitu na hali mbalimbali kwa namna ya upendeleo.
Pamoja na mgao huo ambao wanafilosofia wa kijadi walipania kuujenga, wanaudenguzi hulenga kufutilia mbali mipaka hiyo na kuonyesha kuwa jozi za maneno ni mfano wa sarafu moja yenye pande mbili. Udenguzi hubainisha kuwa nuru na kiza ni vitu ambavyo wanafilosofia wa kijadi wangevitenganisha kwa kupendelea nuru kuliko kiza. Kwa wadenguzi, nuru sawasawa na kiza vimechangamana na huwezi kukielewa kimoja bila kingine. Hatungeweza kumaizi kile tunachokifahamu kama nuru iwapo lugha tunayoitumia haingekuwa imeratibu ndani yake dhana ya kiza. Pili, udenguzi hushughulikia kwa pamoja jozi ya maneno yanayokinzana na wakati huo huo kubainisha itikadi kuu inayojitokeza na inayostahili kusailiwa upya. Kupitia uchanganuzi makini wa lugha ya matini, wadenguzi hudhihirisha ukinzani na utepetevu wa matini hizo.
Hili ndilo linalowapelekea wadenguzi kudai kuwa matini hujiumbua na kujibomoa yenyewe na wala sio wao wanaofanya hivyo. Wanavyodai, hii ni sifa ya azali na iliyomo katika lugha kwani tangu jadi lugha imejengeka kama mfumo wenye ukinzani na unaotofautisha maana. Lugha yenyewe imejengeka kiudenguzi kwani hubainisha tofauti zilizomo ndani yake – za kimaana na za kiitikadi. Kipengele cha kwanza kinaingiliana moja kwa moja na fasiri inayotolewa na mhusika mkuu wa Nyuso za Mwanamke, Nana, pale anapotoka nyumbani kwao na kuabiri safari ndefu ya kuutafuta uhuru wake binafsi baada ya kuamua kutoroka nyumbani kwao. Anaanza somo lake la kidenguzi kwa kuzamia jozi zilizomo katika dhana mbalimbali zinazokinzana: Kwa kawaida nafsi yangu ilinifanya niamini kwamba hakuna utenganisho mkamilifu baina ya kuwepo na kutokuwepo. Sisi binadamu tupo kama hatupo au hatupo kumbe tupo.
Basi, maisha ya siku hizi ni kama kuwepo ndani ya kutokuwepo au katika kutokuwepo na kuwepo. Ni hali ya kudinda ndani ya ukweli na uwongo. Au baina ya nafsi moja na ndani ya nyingi na nyingi ndani ya moja: utambulisho wetu ni wa weusi na weupe, majilio yetu ni nidhamu na machafuko. Tunavunga ndani maumbile yanayovunjwa na utamaduni wa pupa, katika dunia isiyobagua tena kati ya wema na uovu, uke na uume, kitovu na pembezoni… (Mohamed 2010: 59; msisitizo wangu). Lakini kama Derrida anavyotambua kuwa watu hupania tu kuweka mipaka kati ya vitu, mipaka hiyo kwa hakika huwa ya kufikirika na udenguzi hutuelekeza tuangalie kwa makini ukinzani unaojitokeza ndani ya matini (Carter 2006: 111).
Nana anatutanabahisha juu ya jozi tofauti tofauti zikiwemo kuwepo/kutokuwepo, ukweli/uwongo, umoja/wingi, weusi/weupe, wema/uovu, uke/uume, kitovu/pembezoni ambazo tunastahili kuzifikiria kwa pamoja ili tuone namna jozi hizi zinavyojengana na kuumbuana1. Hii ndiyo sababu Nana wakati mwingine anazibadilisha jozi za maneno kama vile kuwepo/kutokuwepo hadi kutokuwepo/kuwepo, na “moja/nyingi” – “nyingi/moja”. 1 Kwa ufafanuzi zaidi wa fikra ya kidenguzi kama zoezi la uchanganuzi wa jozi za maneno msomaji anashauriwa asome makala ya Mwamzandi (2011: 1-14). Humo ataona namna maneno jozi yanavyoumbuana na pia kujengana kimaana. Aidha, ningependa kuwashukuru wahariri kwa ushauri na mapendekezo yao, hususani kuhusu sifa na hulka ya fasihi ya kiusasa-baadaye.
Mipaka ya jozi za maneno huwa myembamba sana na hili ndilo linaloendelezwa na Nana kwa utaratibu huu: Mkinzano unaishi ndiyo, na kwa kweli lazima uishi kwani mkinzano ndiyo maisha yenyewe. Lakini kila mkinzano una mstari mwembamba usioonekana kwa macho. Ndiyo unatenganisha mambo, lakini ni mwembamba mno kutenganisha kwa ukamilifu kitu kimoja na cha pili. Hapana kitu kimoja na cha pili, pana kimoja kinachoshibishana na kugombana na cha pili. Ndivyo dunia yetu ilivyoanza tokea mwanzo katika hali ya uwili inayotegemeana na kutofautiana […] Pana kuvuka mipaka pande mbili. Hiki cha huku kinaweza kwenda kule na cha kule kinaweza kuja huku. Nguvu za hiki zinajengwa na kile. Kuwepo kwa hiki ni sababu ya kuwepo kile. Huo ndio uwili unaotegemeana, lakini unaovunjana kwa wakati mmoja. Anayejiona ameshinda hatimaye ni yule mwenye nguvu, lakini ukitazama sana, hapana anayeshinda. Kuna kushindwa kwa wote. (Ivi: 59f) Katika dondoo hili, uwili unaozungumziwa na Derrida umekaririwa mno hapa. Kila mahali, kunatajwa kitu kimoja na jinsi kinavyosuhubiana na kuathiriana na kile cha pili.
Dunia, kama asemavyo Nana, imejengwa na uwili huu wa ukinzani. Maneno ya Nana yanadokeza muktadha mahsusi unaohusu ugomvi wake na babake. Baba alidhamiria kushinda kwa kumlazimisha Nana awe chini ya mamlaka yake. Nana naye anajiona ni mtu mzima wa kujiamulia watu anaotaka kutangamana nao. Hili ndilo analosisitiza Nana katika mvutano wake na babake. Baba anapania mwanawe atangamane na watu wa aila ya juu kama alivyo yeye mwenyewe na haelekei kuufurahia uhusiano wa bintiye na Mpiga Gita (Faisal).
Mwishoni, tunaonyeshwa kwamba baina ya kushinda na kushindwa, kushinda kunawavutia wengi ingawa kwa hakika hakuna mshindi. Nana anatoroka nyumbani na katika vita hivi vya baba na mwana, hakuna anayeshinda – kila mmoja anashindwa! Baadaye kidogo, Nana anatueleza waziwazi chanzo cha mawazo haya anapotuambia: Hapo nilimkumbuka Derrida na ubomozi wake anaouita (de)construction. Kila kitu lazima kiwe deconstructed. Naye hakuchukua muda kunijia katika fikra hii ya (de)construction. […] Falsafa si mijineno tu. Si ubingwa tu wa kushindana ili mmoja amwone mwingine duni, ili yeye aonekane bingwa au gwiji. Falsafa ni maisha yenyewe. (Ivi:60) Udenguzi au ‘ubomozi’ kama unavyorejelewa kwenye Nyuso za Mwanamke unahusishwa na usomaji uliopea wa kutazama kila neno katika jozi kwa jicho pekuzi. Usomaji huu umependelewa sana na wadenguzi wanaodai kuwa matini za fasihi zina tabia ya kuzungumzia kile zisichokidhamiria (Burman & MacLure 2005: 284f). Hii ni mianya inayostahili kufuatiliwa na msomaji ili aweze kuidengua kikamilifu matini husika. Dunia Yao, kupitia Ndi- inazungumzia hatua hii muhimu katika usomaji wa kidenguzi kwa kusema:
Madhumuni ni kujenga maana kwa njia ya kubomoa maana. Kujenga mvuto wa kisanaa. Ndiyo, unaweza kujenga maana hata katika mwanya mtupu. Hata ukitaka, unaweza kwa makusudi kupoteza maana kabisa kwa vivuli vya maana. (Mohamed 2006: 9) Katika dondoo hili kile kinachorejelewa kama kivuli cha maana ni ile sehemu ya pili ya neno au dhana katika jozi ambayo aghalabu huenda ikaachwa nje na isizungumziwe wazi wazi na mwandishi. Wadenguzi wanafuatilia maneno kama hayo kama linavyotarajia zoezi la kidenguzi ili kubainisha kile kisichosemwa na athari yake katika uwanja mzima wa maana (Schmitz 2007: 118; Carter 2006: 111). Uhalisia, Sanaa Faafu na Nadharia ya Usasa-baadaye Swala jingine muhimu linaloibuliwa na riwaya zilizoteuliwa katika makala hii ni mazingatio ya kile tunachoweza kukitambua kama sanaa stahiki kwa waandishi na hadhira lengwa.
Kama nilivyotanguliza hapo awali, riwaya hizi zimesheheni majaribio mengi na kwa namna zilivyoandikwa msomaji huenda akatanzwa na mbinu tata zilizomo za kiuandishi. Waandishi wa riwaya hizi wanaelekea kulitambua hilo na Dunia Yao inazamia mjadala huu wa sanaa faafu dhidi ya ile iliyopitwa na wakati, hasa kwa kuzingatia kipindi mahsusi cha kihistoria na mbinu sadifu za kuwasilishia sanaa. Kama tapo la kiuandishi, uhalisia umekuwa na uzuri wake ingawa kile kilichoonekana kitu adimu ndani ya uhalisia kimeanza kutiliwa shaka. Ndi- katika Dunia Yao anadokeza hivi: Alisita hapo. Nilifahamu amekusudia nini. Wakati wa sanaa ya uhalisia nilijua umeshapita.
Kwa kweli wakati ule nilipoanza, nisingeweza kuandika vingine nje ya uhalisia. Kanuni zake zisingekubali. Nani angenichapisha? Nani angenisoma? Jambo moja muhimu lililoshikamana na sanaa wakati ule lilikuwa dukuduku la watu. Tamaa zao za dhahiri. Nusura iliyoonekana iko njiani. Ingefika kesho kama si sasa hivi. (Mohamed 2006: 71) Kama mhusika, Ndi- anaona kwamba yeye pia amekuwa katika hali ya mpito. Uhalisia aliouenzi sasa hauna nafasi kwake kwa kuwa wasomaji sasa wako tayari kuzipokea kazi zake za kimajaribio.
Hapo awali, hakuwa na budi ila kutunga kazi za kihalisia na anazo sababu zake za kufanya hivyo kama inavyoelezwa katika majadiliano haya ya Ndi- na Bi Muse. Jambo la kwanza ni kuwa wasomaji wenyewe walikuwa na matarajio au dukuduku lao kuhusu kazi za fasihi ambazo walitarajiwa ziandikwe kwa mtindo huo wa kihalisia. Pili, wachapishaji nao hawangethubutu kuchapisha kazi za kimajaribio kwa kuwa wanunuzi hawangeziona za manufaa kwao. Hivyo mwandishi wa wakati huo hangekuwa na hiari ya kiuandishi ila kuwatii wachapishaji ambao waliongozwa zaidi na faida inayotokana na mauzo yao kuliko ujasiri wa kisanii wa mwandishi. Swala hili la kuthaminiwa kwa fedha kuliko waandishi limezungumziwa pia katika Musaleo! kama tatizo mojawapo linaloathiri kutolewa kwa sanaa nzuri, tena faafu. Sanaa nzuri, kama inavyoelekea kujadiliwa humo, ni ile
ambayo itakidhi haja za kibinafsi za waandishi na aila zao. Hususani, Musaleo! inalalamikia namna waandishi wanavyopunjwa na kuchezwa shere na wachapishaji. Zamda, mkewe Kingunge, analalamika jinsi mumewe anavyotumia muda wake mwingi kuandika riwaya huku akikosa namna za kuikimu familia yake. Zamda anasema: Sasa huu uandishi nao naona umekuwa kama kufungukwa na uganga. Heri siku zilizopita na hata kulipa haulipi huu! Uandishi! Uandishi! Uandishi wa nini? (Wamitila 2004: 12) Ndi- katika Dunia Yao anaelekea kupendelea fani ya usasa mamboleo au usasa wa kisasa katika maswala ya uwasilishaji wa kazi za sanaa. Sanaa, kwa mujibu wa mhusika huyu, huenda na wakati na mahitaji ya mwanadamu.
Na hapo anaeleza kwa nini uhalisia ulifaa katika kipindi fulani cha uandishi kuliko uandishi wa aina yoyote na ilipodhihiri kwamba uhalisia haungeweza kushughulikia dhamira za kisasa, basi ilibidi nao utupiliwe mbali kama kinavyotarajia kipindi cha hivi leo. Ndi- anasema: “Hii ni bustani iliyopitwa na wakati,” nilimsikia akisema hatimaye, “inafanana na mantiki ya mambo ya miaka ile iliyopita. Ni bustani ya ukame na kifo. Ni ukaukivu wa mambo unaoashiria ufu wa bongo lako lisiloweza tena kusimulia kwa mantiki. Hakuna tena mantiki. Hakuna tena umajimaji wa ubichi wa mambo. Uhai haupo tena mbali na kifo, na kwa hivyo hauwezi kuwepo ukweli, ukweli. Wigo wa ukweli wa moja kwa moja haudindi tena. Na kusema kweli, tokea mwanzo haukuwepo.
Iliyokuwepo ni ndoto. Ndoto ya bustani hai. Kumbe kavu na teketevu namna hii.” (Mohamed 2006: 64) Hapa, Ndi- anaulinganisha uhalisia na kifo cha kiakili, yaani kukosekana kwa ubunifu katika fasihi. Hata kile kilichothaminiwa kuwa uhalisia kiliishi katika njozi za watu na kamwe haukuwa ubunifu kama anavyodai Ndi-. Anachosisitiza Ndi- ni kuwa kuzingatia uhalisia kwa kipindi cha leo ni kuishusha hadhi fasihi. Mawazo sawa na hayo yamezungumziwa pia na Kingunge katika Musaleo! pale anapokutana na mhariri wake ili wazungumzie maendeleo ya mswada wa hadithi yake.
Mhariri anabishana juu ya mwelekeo mpya aliouchukua Kingunge kwa kusema: “Wasomaji wako watalalamika sana mara hii. Mbona usitumie mtindo rahisi ambao wanaufahamu: unajua watu hawapendi mabadiliko bali huyapenda mazoea na ukale…” alilalamika mhariri. “Na hilo ndilo kosa kubwa. Maendeleo hayamo katika ukale!” (Wamitila 2004: 41) Sawa na anavyodai Ndi- wa Dunia Yao, katika Musaleo! naye mhusika Kingunge anayaona maendeleo yakiwemo katika kuhimiza kuwepo kwa majaribio katika uandishi na wala sio katika kuwa wahafidhina. Lakini je, sanaa mamboleo inayopendelewa na riwaya hizi ni ipi?
Waonavyo waandishi hawa wa kimajaribio uhalisia umepitwa na wakati na wamehoji kuwa sanaa kamwe haiwezi kuwekewa mipaka. Mintarafu ya riwaya hizi, sanaa nzuri ni ile itakayojumuisha mbinu za kuelezea dunia ya sasa iliyojaa miujiza na mambo mengi ambayo hayawezi kueleweka kwa njia iliyo rahisi. Uzuri wa sanaa kwao si kuyaeleza mambo yalivyo kihalisia na, chambilecho Dunia Yao, “kuzipata maana kibungabunga” (Mohamed 2006: 9). Msomaji sharti ashiriki kikamilifu katika kuzipekua maana za kazi anazozisoma na kukubali kuzugwa pale inapobidi.
Sanaa nzuri kwao ni ile itakayomlazimisha msomaji kusaili ishara tofauti tofauti atakazotumia mwandishi na kisha kuzihusisha ishara hizo na muktadha wa maisha yake halisi. Hatimaye, ufaafu wa sanaa huamuliwa na namna itakavyomtumikia yule anayelengwa. Haya ndiyo mawazo makuu yanayoendelezwa katika sura yote ya tano ya Dunia Yao. Katika Musaleo! naye mhusika Kingunge anayakubali mawazo haya anaposema: “Siandiki? Naandika sana. Tena mara hii riwaya ya kisawasawa itakayojisoma yenyewe pamoja na kuyasoma maisha yetu. Naandika riwaya itakayojihakiki yenyewe!” (Wamitila 2004: 10) Kingunge, kama inavyodhihirika hapa, anashadidia wazo kuwa kitendo cha uandishi huvuka mawanda ya matini kwa kuhakiki mchakatowenyewe wa uandishi.
Katika muktadha huu, riwaya za kisasa zinamaizi hali hiyo na kuhimiza wingimatini uliomo duniani – jambo ambalo wasomaji hawana budi kuliafiki na kulikubali kama dira inayochukuliwa na fasihi ya kisasa ya Kiswahili. Baada ya kuzungumzia uhalisia na ufaafu wake wa kukidhi matakwa ya binadamu, riwaya teule pia zinafafanua viunzi vilivyotumika kuzijenga.
Riwaya za kisasa, kama inavyopendekezwa, zimejengwa na vipande vya ngano au simulizi fupi fupi zisizokuwa na uaushi, tofauti na simulizi kuu ambazo aliziona kama zilizopoteza uthabiti wake (Lyotard 1984: 37). Simulizi hizi hutokeza kwa muda mfupi ndani ya riwaya na hazilengi kuhodhi ukweli kama zilivyo simulizi za jadi ambazo zililenga kukongomea ukweli kama zilivyouona. Lyotard, kwa mfano, amenukuliwa na Barry (2002: 86) akisema kuwa simulizi kuu hubuniwa kwa azma ya kusawazisha ukinzani na kusababisha urajua ambao kwa hakika hauna mashiko. Mtazamo sawa na huu unachukuliwa na riwaya teule kutokana na kile anachokirejelea Baudrillard (1983: 142-156) kama “kupotea kwa uhalisi” ambapo mpaka kati ya uhalisi na kinachodhaniwa kuwa maana yake haupo. Anachodhamiria Baudrillard (ibid) ni kuwa viashiria vimepoteza uwezo wake wa uashiriaji na kwa sababu hiyo, uhalisi haurejelei chochote kilicho nje ya kiashiria bali kiashiria hutuelekeza katika viashiria vinginevyo. Maana, hivyo basi, hubakia ikiselea kutokana na wingi wa viashiria. Hii ndiyo sababu riwaya za usasa-baadaye zikakosa muungano na muumano wa hadithi tangu mwanzo hadi mwisho ingawa huo unakuwa msingi wa kuchachawiza hadithi yenyewe inayosimuliwa. Katika Musaleo! inadaiwa kwamba sanaa ya siku hizi imefanana sana na uhalisia wenyewe wa maisha na waandishi wanafuata mkondo tu wa uhalisi huo. Mawazo haya yanachukuana
na yale ya Baudrillard, anayedai kwamba mahala pa uhalisi wa siku hizi umechukuliwa na mbinu za uashiriaji au uwasilishaji wa ukweli huo (1983: 142-156). Mjadala wa Kingunge na mhariri unafafanua zaidi uhusiano kati ya uhalisia wa maisha na sanaa sadifu ya kuuzungumzia: “[…] Uhalisi wa siku hizi umevunjikavunjika hauna pa kujishikiza; hauna mshikamano imara. Hakuna njia nyingine ya kuukabili isipokuwa kwa mtindo wa uhalisi wenyewe; hujasikia mjinga hunyolewa jinsi anavyojipaka maji? Lazima tudadisidadisi kila kitu: siasa, uchumi, mapenzi hata miundo ya hadithi pamoja na hata lugha yenyewe. Hii sio dunia ya kuridhika na tulichozoea,” alisema Kingunge. (Wamitila 2004: 41) Msimulizi katika Dunia Yaoanazungumzia hili pia: Katika simulizi na mapito yake, vipandevipande – si lazima vishikane. Unavimwaga tu vipande vyenyewe kama unaatika mbegu kwenye shamba la sanaa. Unafanya hivyo kuwaacha wasomaji waunge wenyewe vipande vya maana zao, huku maneno mengine ukiyajengea vivuli ili kuwategea makusudi watafute maana zao badala ya kuzipata maana kibungabunga. (Mohamed 2006: 9) Kwa kuwa muda wa kimajaribio umefika na kazi zenye sifa hizo kukubalika na kuchapishwa, basi msimulizi katika Dunia Yao anaeleza kile kinachokuwa kiungo muhimu cha kazi kama hizi: Naam, nilikiri. Hii ndiyo itakuwa simulizi yangu mpya katika mchanganyondimi.
Kipande hapa…kipande pale. Vipande vya ‘allegory’. Vipandevipande vya ngano mpya. Ngano ya tafrani-za-kileo katika usogori mpya. Aaaaa, ikiwa zamani sikukujua Bi Muse, sasa nakuhitaji mara milioni moja. Nataka niwe nawe pachapacha. Nikukumbatie unikumbatie, unikoleze ilhamu, nilimwambia. (Ivi: 68) Huu ni mdokezo unaotolewa na riwaya kuhusu kile kitakachopatikana humu. Tunatanabahishwa kuwa riwaya hii itakuwa ni mchanganyiko wa simulizi za kila aina na wingimatini wa “kipande hapa…kipande pale” (ibid.).
Kwa yakini, hii ni sifa inayojitokeza katika riwaya zote tatu ambazo zimenakili kazi mbalimbali za waandishi tofauti tofauti. Mimi/Wengine, Kitovu/Pembezoni: Mazingatio ya Nadharia ya Ukoloni-baadaye Kipindi mahsusi cha kustawi kwa nadharia ya ukoloni-baadayeni katika mwaka wa 1978 baada ya Edward Said kuchapisha kitabu chake cha Orientalism (Said 1978). Nadharia yenyewe inajihusisha na mambo mawili makuu yaani ukoloni-baadaye wenyewe na kazi za kisanaa zinazouhusu. Riwaya teule zinazoshughulikiwa na makala hii zimezingatia mambo yote haya mawili kwa njia tofauti. Musaleo! inagusia mada muhimu ya Said iliyomo katika Orientalism. Riwaya inazunguzmia dhana za ‘mimi’ na ‘wengine’ – mbeya mbili muhimu zinazotofautisha Umagharibi na Umashariki. Umagharibi ulihusu nchi za Ulaya na Marekani ambazo zilihusishwa na ustaarabu pamoja na maendeleo makubwa katika nyanja zote huku Umashariki ukinasibishwa na nchi zilizokuwa na umasikini uliokithiri, maendeleo duni na ushenzi. Kile ambacho Said alikirejelea kama Orient (‘WENGINE’ katika Musaleo!) na kilicholengwa na watu wa Ulaya Magharibi kilijumuisha nchi za Mashariki ya Kati pamoja na zile za watu lugha za Kisemitiki pamoja na mataifa ya Asia Kusini.
Mataifa haya, na hasa yale ya Uarabuni ya Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, ndiyo yaliyobeuliwa na kuonekana kama yenye dosari mbele ya macho ya wazungu wa Ulaya Magharibi (Said 1978: 99). Umagharibi nao ulichukuliwa kama kitovu cha ustaarabu na maendeleo ya kisayansi na kijamii. Hiyo ndiyo misingi anayoitumia mhusika Ukolongwe katika Musaleo! katika kujitofautisha na wanajamii: “Sasa kuanzia leo, na wala si kuanzia leo ni tangu zama na azali, kuna MIMI na WENGINE tu. Mimi ndimi msingi wa kila kitu. Mimi sio kama nyie!” (inasemwa alikuwa na rangi nyepesi na nywele zake zilikuwa mbuyembuye, ambazo hazikuiva) […] Alisema mengi lakini kufupisha habari kadai rangi yake ilikuwa bora na iliashiria ubora wa akili.
Ukolongwe alishikilia kuwa kauli zake ziliwekewa misingi imara na Sayansi [sic]. Inasemekana siku moja alitokeza hadharani huku ameshikilia kitabu kimoja kiitwacho The Wild Man’s Pedigree. Humo aliwasomea watu sehemu fulani aliyodai kuwa ilizieleza sifa zao. “Weusi: wasiochangamka, watulivu, wenye pua pana, wajanja, wazembe na wanaotawaliwa na ugeugeu!” Ajabu ni kwamba mwenyewe alikuwa na sifa hiyo hiyo ya kubadilikabadilika kama kinyonga. (Wamitila 2004: 26f; herufi za mlazo hivyo hivyo katika matini ya awali) Kinachohadithiwa katika riwaya ya Kingunge ni juhudi za wakoloni za kukuza uwingine kupitia maumbile kama vile rangi na nywele. Aidha, madai ya wakoloni kuwa wao ni bora yanajitokeza pia katika maandiko yao wanayoyaenzi kama vile The Wild Man’s Pedigree ambamo wanaendeleza propaganda kwamba wao ni bora kuliko wanajamii wengine.
Humo, twapata Waafrika wakifafanuliwa kama wenye sifa hasi za uzembe, ujanja, kutokuwa na msimamo na hata walioumbuka kimaumbile kama inavyoashiriwa na pua zao pana. Kwa upande wao, wakoloni wanajiona kama wenye rangi bora inayoashiria akili iliyopevuka, waliostaarabika na wanaofuata maadili ya kisayansi. Pamoja na kutambua hila za wakoloni, Musaleo! inajusurisha kubainisha mbinu mbalimbali zilizotumiwa na wakoloni katika kuwatawala wenyeji Waafrika. Ukolongwe, mhusika mkuu wa riwaya ya Kingunge, kwa mfano, anapiga marufuku kile alichoshindwa kukifahamu na ambacho wenyeji walikifahamu. Pia aliamrisha watoto wafunzwe nyimbo mpya, tofauti na zile walizoziimba hapo awali.
Vilevile, tunaelezwa namna alivyoiteka nyara lugha na kubadilisha maana za maneno kiasi kwamba pale panapozungumziwa ‘uhuru’ au ‘uzalendo’ wenyeji walisikia badala yake ‘kufuru’ na ‘uvundo’ mtawalia (Ivi: 26). Kwa utaratibu huo Musaleo!, kupitia kwa riwaya ya Kingunge, inaingia katika hatua ya utekelezaji wa nadharia ya ukoloni-baadaye kwa kuzingatia namna fasihi ya ukoloni-baadaye inavyoweza kuweka upenuni kwa uwazi au kwa mafumbo hila na hilaki wanazotumia watawala kwa watawaliwa (Tyson 2006: 431). Musaleo! ni zoezi la kina la uchanganuzi wa njama, hulka na athari za ukoloni mkongwe pamoja na ukoloni mamboleo wa viongozi wa zama za leo. Riwaya hii ina zoezi maalum la utekelezaji wa uhakiki wa nadharia ya ukoloni-baadaye. Humu, ukoloni mamboleo unawakilishwa na kina ‘Musaleo’ wa siku hizi, yaani viongozi, wanaotumia njama za kila aina za kuwakandamiza wale
waliowapa madaraka. Hapa na pale, riwaya hii inazungumzia kwa mafumbo namna nchi za Kimagharibi zinavyowazuga wale walioko pembezoni kama inavyobainishwa na kile kisa cha “ardhi kuwa pande kubwa lililovunjika na kuwa Godi-Wana na Huraa-Asi na mengine madogo madogo mpaka yakafikia matano” (Wamitila 2004: 89). Katika kisa hiki, kunatajwa sumaku inayozivuta ardhi mahala pamoja na yule buibui aliyesakini pale kwenye kiini ambaye aliwala nzi waliozongwa na utandu – sitiari ambazo zinafafanua mahusiano hayo ya kitovu (wenye nguvu, wakoloni au mataifa ya ulimwengu wa kwanza) dhidi ya pembezoni (wanyonge, watawaliwa au mataifa ya ‘ulimwengu wa tatu’). Nadharia ya ukoloni-baadaye haiishii katika kumlaumu mkandamizaji kama anavyodhihirisha Said katika kitabu chake Culture and Imperialism (Said 1993). Anatambua kuwa ingawa nchi za Asia, Afrika na Amerika ya Kilatini zina uhuru wa kisiasa bado zinatawaliwa na kutegemea nchi za Kizungu (Said 1993: 20). Pamoja na ukweli huo, Said anaona kwamba haifai kuzimwagia nchi za Kimagharibi lawama kwa kuwa nchi hizo zinastahili kujilaumu zenyewe kwa kutoichanganua vyema mifumo adili ya kuleta mageuzi ya dhati ya kisiasa na kitamaduni katika jamii (Said 1993: 277). Ni hapa ambapo viongozi walioshika hatamu za utawala baada ya kuondoka kwa wakoloni wakongwe waliendeleza na bado wanaendeleza uongozi wa kiimla na kuwanyanyasa wananchi wenzao. Kulingana na Said hali ilivyo baada ya ukoloni wa Kimagharibi ni aina ya mduara wa kibeberu unaoturejesha katika hali iliyokuwa wakati wa mkoloni. Bado kuna tamaa za kichoyo ambapo watu wanataka kujinufaisha kibinafsi na kuwabagua wenzao kidini, kirangi na kikabila (Said 1993: 275-276). Na hapa ndipo Nana katika Nyuso za Mwanamke anavyotaka watu waangazie kitovu na pembezoni kama chanzo cha uovu uliosakini duniani: Sikubaliani nao wanaotilia mkazo kitovu cha duara. Nguvu tunazoambiwa zimeumbwa makusudi ili wanaoishi pembezoni lazima wavutwe ndani kusujudia kitovu.
Nionavyo mimi, lazima ukingo wa duara uvunjwe ili viliyomo ndani vimiminike nje na vya nje viweze kupenya ndani kutafiti kilicho ndani na kitovu chenyewe kinachotoa fikra mbaya na ovu. Bila ya hivyo walioko pembezoni maisha watajikuta wako pembezoni – wamezugwa kabisa na maneno ya kukuza njugu maganda. (Mohamed 2010: 60) Anavyoona Nana, swala la kitovu na pembezoni ni fikra potofu iliyomo vichwani mwa watu na kwa sababu hiyo wakati umefika wa kila mtu kujituma ili kuifanya dunia kuwa mahala bora badala ya kuishi kwa visingizio vya ukoloni na athari zake mbaya. Anima na Mamanchi wa Musaleo!:Wahusika katika Saikolojia Changanuzi Musaleo! imetumia mawazo ya mwanasaikolojia Carl Gustav Jung2 hasa katika ujenzi wake wa wahusika Anima na Mamanchi. Kimsingi, Jung alidai kwamba kila binadamu, awe mke au mume, 2 Carl Gustav Jung (1895-1961) ni mwanafunzi wa Sigmund Freud na kwa mujibu wa Wamitila (2003: 298) ni mwanasaikolojia anayefahamika kwa kuendeleza dhana ya ‘ung’amuzi jumuishi’ ambayo aliitumia kuelezea sehemu ya akili ya binadamu ambayo hurithiwa na kufanana kwa kila binadamu. Sehemu hii, anavyoeleza Wamitila, ndiyo huwa amebeba chembechembe za hulka za jinsia tofauti na yake. Hivyo ni kusema kwamba mwanamume huwa na sifa za kike zilizofichika katika ung’amuzibwete wake na aghalabu sifa hizo hujitokeza katika umbo la msichana bikira au mwanamke mwenye sifa za kiungu na ambaye hufahamika kama Anima. Vivyo hivyo, mwanamke naye huhodhi sifa za kiume katika ung’amuzibwete wake na hudhihirika katika umbo la kikongwe mwenye busara aitwaye Animus (Carter 2006: 79). Kudhihirika kwa wahusika hawa huwa katika ndoto na ishara mbalimbali na wanasaikolojia huamini kuwa wahusika hawa huwa njia ya kuimarisha tabia ya mtu binafsi ambayo huwa imeficha mawazo na mitazamo hasi (Schmitz 2007: 200).
Mawazo ya Jung yanabainika ndani ya riwaya hasa tunapozingatia uhusika wa Anima na Mamanchi na jinsi wanavyomdhihirikia Mugogo Wehu. Wote wanatokea pale Mugogo anapokunywa sumu aliyotegewa na watu wasiojulikanana kupoteza fahamu nyumbani mwake, ingawa Mugogo mwenyewe alihisi machovu na hivyo kujilaza kitandani (Wamitila 2004: 8). Yote anayoyafanya Mugogo ndani ya hadithi kwa hakika si mambo yakinifu bali yanatokea ndani ya ‘ndoto’ anayoipata katika ‘usingizi’ huu – yakiwemo kukutana kwake kwanza na Anima, na kisha, Mamanchi. Akiwa katika ndoto yake kuu, Mugogo anakutana kisadfa na Anima (Ivi: 28). Kukutana kwao kwa hakika si kwa kisadfa kama anavyodai Mugogo mwenyewe bali ni njiamaalum inayotolewa na riwaya kwa msomaji ya kuona wasiwasi na hofu zilizofichika katika ung’amuzi bwete wa Mugogo. Tangu mwanzoni mwa riwaya, tayari msomaji ameshamuona Mugogo kama mhusika anayeishi maisha yaliyojaa shauku, hofu na wasiwasi mwingi. Kwa mfano, alikuwa na yakini kuwa aliusikia mlio wa bunduki na kushuhudia kishindo cha vijana waliokimbilia huku na huko ili wazinusuru roho zao. Kisha akawaona vijana waliopigwa risasi nje ya nyumba yake ambao wanatoweka kimiujiza (Ivi: 1). Yote haya yanamfanya atoke kwa azma ya kufanya uchunguzi iwapo aliyoyashuhudia ni ya kweli. Anachohadithiwa huko nje ni tofauti na watu wanamdhania kuwa mwehu.
Anashauriwa apuuze yasiyomhusu kwani hakuna aliyesikia bunduki anazozungumzia Mugogo (Ivi 6). Anaporudi nyumbani kutoka ulevini, ndipo “anapojipumzisha kitandani” (Ivi: 8) ilhali ukweli ni kuwa makali ya sumu aliyokuwa ametiliwa yalikuwa yamekolea na kumfanya apoteze fahamu. Hapo ndipo riwaya inapomdhihirisha Anima kama mhusika ambaye, katika misingi ya Jung, anajitokeza kamanjia mbadala ya kutufunulia wazi wazihofu na wasiwasi aliokuwa nao Mugogo akilini mwake. Mbali na hayo Anima wa Musaleo!, kama alivyo Anima wa Jung, pia ni mwanamke na Mugogo anaelekea kuathirika naye kimapenzi kama anavyolazimishwa akiri hilo na Mamanchi ambaye awali anajitambulisha kama “siri ya Mashamba ya Mawe” (Ivi: 22): inayohodhi vikale ambavyo hujitokeza kwa njia ya ishara na ndoto. Wahusika wake wa kisaikolojia, Anima na Animus, ni vielelezo vya visakale anavyozungumzia na ambavyo vimo katika ung’amuzi jumuishi wa kila binadamu.
“Mugogo, unamjua Anima?” Nitakosaje kumjua mtu kama huyu jamani? Alikuwa rafiki yangu wa kike; mwanamke mwenye ujasiri mkubwa na mapenzi yasiyojua kukimwa. (ibid.) Katika safari yake kwenda katika shamba la mawe, Anima anajitokeza tena – wakati huu katika umbo la mhusika Mamanchi. Katika njozi hii ambayo Mugogo anapata ufumbuzi wa mambo mengi kupitia Mamanchi, Anima sasa si msichana tena bali ni mwanamke mkongwe, mwenye busara na anayejua mambo mengi. Aidha, Mamanchi ana sifa za kiungu, sawa na zile zilizozungumziwa na Jung. Mamanchi, kwa mfano, amezaliwa akafa, akazaliwa akafa, na akazaliwa upya (Ivi: 60). Anamfahamisha Mugogo katika ziara yao ya shamba la mawe hila na vituko vinavyotumiwa na kina ‘Ukolongwe’, jina tunaloweza kulichambua kama kifupi cha ‘ukoloni mkongwe’ na kina Musaleo au viongozi wa siku hizi katika kuendeleza utawala wao wa kiimla. Weledi wa mambo alionao Mamanchi kuhusu vitimvi vya wakoloni wakongwe na wakoloni mamboleo unaelekea kumtanza Mugogo. Mapenzi na ufahamu wa Mamanchi kwake unamkumbusha uhusiano maalum aliokuwa nao na Anima kiasi cha kumfanya Mugogo ashuku kuwa Mamanchi na Anima ni mtu mmoja anapouliza: “Mbona sauti yako inafanana na ya mtu ninayemjua?” Mamanchi: Nani? Anima! Mamanchi: Anima ni mimi pia! Mimi naye ni sawa! (Ivi: 86) Kumbe Anima na Mamanchi ni wamoja ingawa wamejitokeza katika maumbo tofauti: Anima akiwa msichana huku Mamanchi akiwa ajuza. Kinachounganisha umbile lao, hata hivyo, ni msaada mkubwa unaotokana na ukweli na uthabiti wao kwa Mugogo Wehu katika kuuelewa ulimwengu unaoelekea kumtanza.
Kupitia wahusika hawa, Mugogo anatoa harara zake, shida, hofu na kupata mtazamo wa maisha. Mwishoni anaporejelewa na fahamu zake, tunamwona akiwa kiumbe tofauti na vile alivyokuwa hapo awali ingawa hayo yanadokezwa kwa mafumbo na Msimulizi: Ung’amuzi wa mambo wa Mugogo Wehu umepiga hatua kubwa. Macho ambayo alishindwa kuyafungua jana ameyafungua. Ameweza hata kusema mambo kadha. (Ivi: 100) ‘Kufungua’ na ‘kufunga’ macho kunakorejelewa hapa kunahusiana na kule kuzindukana kwa Mugogo Wehu kutoka lindi la kutofahamu (kupoteza kwake fahamu) ambako kulielekea kumtia woga hadi hali ya matumaini (kufungua macho) kama inavyoashiriwa na uwezo wa ‘kusema mambo kadha’.
Hitimisho hili linawafiki uhakiki wa ki-Jung kwa jinsi linavyoagua hofu, wasiwasi na jumla ya mitazamo hasi iliyofichika katika ung’amuzibwete hadi kuleta satua kwa waathiriwa, wakiwemo Mugogo Wehu. Hitimisho Mapitio ya riwaya za Dunia Yao, Nyuso za Mwanamke na Musaleo!yamebainisha wazi kwamba fasihi ni nyenzo mbadala, tena ya kiubunifu, ya kuzizungumzia nadharia za fasihi kwa njia ya ukakamavu zaidi. Uaguzi wa makini wa nadharia za fasihi katika riwaya teule umeziweka kazi hizi katika medani ya kipekee ya kuzungumzia mambo ambayo yangepatikana katika matini mahususi za nadharia za fasihi. Miongoni mwa mambo mengine mengi, riwaya hizi, kwa ustadi, zimeatika mawazo ya wananadharia mbalimbali wa fasihi wakiwemo wanaumaumbo wa Kirusi, wanaumuundo, wanaudenguzi na hata wanasaikolojia changanuzi katika bunilizi za Kiswahili. Wahakiki, walimu na wapenzi wa fasihi wanaweza kuzitumia riwaya husika kama matini za kiziada katika somo la nadharia.
ukakamavu zaidi. Uaguzi wa makini wa nadharia za fasihi katika riwaya teule umeziweka kazi hizi katika medani ya kipekee ya kuzungumzia mambo ambayo yangepatikana katika matini mahususi za nadharia za fasihi. Miongoni mwa mambo mengine mengi, riwaya hizi, kwa ustadi, zimeatika mawazo ya wananadharia mbalimbali wa fasihi wakiwemo wanaumaumbo wa Kirusi, wanaumuundo, wanaudenguzi na hata wanasaikolojia changanuzi katika bunilizi za Kiswahili. Wahakiki, walimu na wapenzi wa fasihi wanaweza kuzitumia riwaya husika kama matini za kiziada katika somo la nadharia.
Marejeleo
  • Barry, Peter. 2002. Beginning Theory. Manchester: Manchester University Press.
  • Baudrillard, Jean. 1983. Simulations. New York: Semiotext(e).
  • Bertoncini, Elena. 2006. Globalization Unmasked in Two Kiswahili Novels. Makala ya Kongamano la Kimataifa la Jubilei ya TUKI – 2005, ed. by Seleman S. Sewangi & Joshua S. Madumulla. Dar es Salaam: TUKI, pp. 84-94.
  • Burman, Erica&Magie MacLure. 2005. Deconstruction as a Method of Research. Research Methods in the Social Sciences, ed. by Bridget Somekh & Cathy Lewin. New Delhi: Vistaar Publications, pp. 284-292.
  • Carter, David. 2006. Literary Theory. Reading: Cox & Wyman.
  • Eagleton, Terry. 1996. Literary Theory: an Introduction. Oxford: Blackwell Publishing.
  • Habib, Rafey M.A. 2005. A History of Literary Criticism. Malden: Blackwell Publishing
  • Khamis, Said A.M. 2003. Fragmentation, Orality and Magic Realism in Kezilahabi’s Novel “Nagona”. Nordic Journal of African Studies 12(1): 78-91.
  • Khamis, Said A.M. 2008. Nadharia, Ubunifu, Uchambuzi na Taaluma ya Kiswahili. Nadharia katika Taaluma ya Kiswahili na Lugha za Kiafrika, ed. by Nathan O. Ogechi, Naomi L. Shitemi & K. Inyani Simala. Eldoret: Moi University Press, pp. 3-23.
  • Lyotard, Jean-François. 1984. The Postmodern Condition. A Report on Knowledge. Trans. Geoff Bennington and Brian Massuni. Minneapolis: University of Minnesota Press.
  • Mohamed, Said Ahmed. 2006. Dunia Yao. Nairobi: Oxford University Press.
  • Mohamed, Said Ahmed. 2010. Nyuso za Mwanamke. Nairobi: Longhorn Publishers.
  • Mwamzandi, Issa Y. 2007. Utandawazi na Teknolojia ya Mawasiliano katika Umalenga wa Waswahili: Mfano wa Sitiari za Taarab. Kiswahili na Elimu Nchini Kenya, ed. by Kimani Njogu. Nairobi: Twaweza Communications, pp. 68-82.
  • Mwamzandi, IssaY. 2011. Derridean Thought in Practice: an Examination of the Kiswahili Proverb. Journal of Intra-African Studies 5: 1-14. Said, Edward. 1978. Orientalism. New York: Pantheon Books.
  • Said, Edward. 1993. Culture and Imperialism. London: Chatto and Windus.
  • Schmitz, Thomas A. 2007. Modern LiteraryTheory and Ancient Texts: an Introduction.
  • Malden: Blackwell Publishing. Tilak, Raghukul. 1993. History and Principles of Literary Criticism. New Delhi:
  • Rama Brothers Educational Publishers. Tyson, Lois. 2006. Critical Theory Today. New York:
  • Routledge & Taylor and Francis. Wafula, Richard & Kimani Njogu. 2007. Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.
  • Waliaula, Ken W. 2010. Uhalisia na Uhalisiamazingaombwe: Mshabaha kati ya Dunia Yao na The Tin Drum. Swahili Forum 17: 143-157.
  • Wamitila, Kyallo W. 2003. Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Books. Wamitila, KyalloW. 2004. Musaleo!. Nairobi: Vide-Muwa.
]]>
Utangulizi
Sifa bainifu ya baadhi ya kazi za fasihi ya Kiswahili za karne ya ishirini na moja ni matumizi makubwa ya mbinu za kiuandishi za kimajaribio. Msomaji wa kazi hizi aghalabu hujikuta ameghumiwa na wingi wa urejeleo matini, uhalisia mazingaombwe pamoja na vipande vidogo vidogo vya visa ambavyo hutumika kuungia simulizi hizo zilizochupwa huku na huko (Bertoncini 2006: 93; Khamis 2003: 78). Kwa jinsi hali ilivyo riwaya hizi zinaelekea kutangaza upenuni kwamba enzi na dola ya uandishi wa kazi za kihalisia imepitwa na wakati na umefika muda wa kutoa wasaa kwa majaribio haya mapya. Ni maoni ya makala kuwa fauka ya mbinu hizi kuwa na natija pamoja na dosari zake bado kuna baadhi ya waandishi ambao bado wanaongozwa na misingi ya kihalisia.
Mbali na uwezekano wa kazi hizi za kimajaribio za kuitenga sehemu ya hadhira (wakiwemo wale wasiozifahamu nadharia za fasihi) kwa kumkumbatia zaidi msomaji aliyesoma na kuzamia fani adimu za kijamii, fasihi ya karne ya ishirini na moja ni njia jarabati ya kumkomaza msomaji ashiriki kikamilifu katika kufuatilia viini vya simulizi mbalimbali anazozikuta humo. Ndani ya riwaya hizi, msomaji anapambana na fikra za wanafalsafa, wanasiasa mashuhuri pamoja na vitimvi vyao, maswala ya utandawazi na athari zake, madondoo ya vitabu vya kidini, visa(a)sili, mighani,
majinamizi, na hata kazi nyingine za kifasihi za wasomi watajika. Makala hii inazamia kipengele kimoja tu cha mafunzo ya nadharia za fasihi ambazo huwa muhimu hasa kwa wanafunzi wa vyuo vya ualimu na hususani vyuo vikuu pale inapowabidi wazungumzie kitaaluma kazi za fasihi. Makala imetumia riwaya ya Musaleo! (2004) ya Kyallo WadiWamitila na riwaya nyingine mbili za Said Ahmed Mohamed za Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010) kama mifano mahususi ya namna waandishi wanavyozungumzia kwa dhahiri nadharia za fasihi. Nadharia katika Uhakiki wa Fasihi: Kipi kwanza? Katika jadi ya uhakiki wa kazi za fasihi, swala mojawapo lililozingatiwa kwa makini ni iwapo wahakiki wanastahili kuzingatia kile kinachosemwa na matini ili kielezwe kwa misingi ya kinadharia au kufanya kinyume chake.
Ingawa kuna kila ithibati kuwa wapo wataalamu waliofuata mojawapo kati ya njia hizo, ushahidi umeonyesha kuwa wengi wa wahakiki hupendelea kufuatiliwa zaidi kwa matini na kisha kuamua nadharia mwafaka itakayofafanua kwa uwazi kile kilichomo ndani ya matini. Said Khamis (2008) amelizungumzia hili kwa mapana na ametoa sababu ambayo naona niitaje hapa kwa kuwa inawafiki nadharia-tete inayoendelezwa na makala hii. Anasema: Nadharia zinabadilika taratibu zaidi kwa sababu mabadiliko ya nadharia mara nyingi huongozwa na mabadiliko ya mitindo na tanzu za fasihi yenyewe. Kinyume cha mambo kilichopo ni kwamba kila siku nadharia hujaribu kama inavyowezekana iwe na uwezo wa muda mrefu wa kuchambua na kuzieleza kazi za fasihi mbalimbali.
Lakini, kwa upande mwingine, hakuna nadharia inayoweza kufaa katika resi ambamo utoaji wa kazi za kubuni situ una wepesi zaidi, lakini mara zote unazingatia upya na mabadiliko. Hii ina maana nadharia fulani moja au zaidi zinaweza kufaa kwa muda fulani tu mpaka pale zinapojikuta, kwa sababu moja au nyingine, zinakumbwa na matatizo ya kutoweza kuzichambua vyema kazi zinazoibuka na upya na mabadiliko.
Wakati huu ndipo nadharia mpya inapohitajika. (Khamis 2008: 12) Nimemnukuu Khamis kwa mapana kutokana na kile anachokiona kama umuhimu wa nadharia za fasihi kuizingatia matini ambayo kama anavyosema daima imo mbioni kuzua mabadiliko.
Katika vitu viwili hivi vinavyotegemeana, matini inayobuniwa ndiyo inayosababisha zaidi haja ya mabadiliko katika nadharia ambayo huenda ikashindwa kuzizungumzia kazi mpya za kifasihi, hususani zile za kimajaribio. Pamoja na kuwafiki hoja anayoitoa Khamis, makala inazamia nadharia-tete ambayo inahusu uhakiki wa nadharia kama msingi huo wa ubunifu wa kimajaribio ambao unahitaji uteguliwe na nadharia.
Riwaya Tatu Teule kwa Muhtasari na Misingi ya Uteuzi wake Mbali na Euphrase Kezilahabi, wanariwaya Said Ahmed Mohamed na Kyallo Wadi Wamitila wametajwa kama waandishi wanaoongozwa na fikra mpya za kiuandishi, yaani uandishi wa kimajaribio ukiwemo ule wa kihalisia-mazingaombwe (Waliaula 2010: 143; Bertoncini 2006: 93; Khamis
RIWAYA TEULE ZA KARNE YA ISHIRINI NA MOJA
Makala inatambua kuwepo kwa sifa hizo za uhalisia mazingaombwe ndani ya riwaya miongoni mwa mambo mengi yaliyofumbatwa humo. Aidha, riwaya hizi zina sifa za kiusasabaadaye ambamo mna vipande vidogo vidogo vya simulizi zisizokuwa na muwala wala zisizochukuana vyema kama zilivyo hadithi za paukwa pakawa zinazoishilia na harusi au wahusika wanaoishi raha mustarehe. Kwa utaratibu wa sifa hizo, nimeteua riwaya husika za Musaleo! (2004), Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010) kwa kuwa zote zinaagua nadharia za fasihi kama sehemu mojawapo ya dhamira zilizomo ndani ya matini hizi. Musaleo! (2004) inajumuisha simulizi inayoenda mbele na nyuma na iliyofichama hadithi mbili tofauti na umazingaombwe usioweza kutabirika.
Ni hadithi inayomsukuma msomaji mbele na nyuma na mwingiliano matini uliokithiri unaohitaji umakinifu ili msomaji apate kuelewa fikra mbinu, njama, vitimbi na hila wanazotumia wakoloni mamboleo katika kuwazuga wale wanaosimama kidete kuzitetea haki zao katika jamii. Nyuso za Mwanamke (2010) nayo inamwendeleza nguli wa kike, Nana, na jinsi anavyojinasua kimawazo kutokana na wavu wa ulimwengu wa kiume kwa kufuata kile kinachoridhiwa na moyo wake.
Ni safari ya msichana, mwanagenzi wa maisha, anayeabiri kujua utu wake na sifa zinazomfafanua binafsi kama mwanamke, tofauti na wanavyotarajia wahusika wengine wa kike na wa kiume wa riwayani. Dunia Yao (2006), kwa upande wake, imesheheni mijadala ya kifalsafa inayozamia fani mbalimbali za sanaa na swala zima la ubunifu. Ninachokiona zaidi ni swala la uendelevu wa sanaa ukiwemo uhai na ufaafu wake katika kuzungumzia visa visivyowaelea watu katika ulimwengu mamboleo.
Dunia, inavyosema Dunia Yao, ni bahari isiyotabirika kina chake na sanaa haiwezi kuwekewa mipaka tunapoabiri kuizungumzia. Kama ilivyoparaganyika dunia, sanaa nayo haina budi kufuata mkondo huo kwani kuifuatilia dunia kwa mstari ulionyooka kama zilivyo kazi za kihalisia ni kuishi katika njozi.
Kuelewa nadharia za fasihi ni miongoni mwa njia adimu za kuelewa mafumbo ya kisanii na ya kimaisha yaliyoatikwa katika riwaya hizi. Makala imezamia baadhi ya nadharia za kifasihi ambazo zimejitokeza wazi wazi katika riwaya hizo tatu. Uhakiki wa Nadharia ya Mwigo Katika kitabu chake maarufu cha Poetics, Plato anaelezea asili na chanzo cha sanaa. Miongoni mwa mambo mengine, Plato humo anaelezea uhusiano wa karibu uliopo kati ya msanii na Mungu ambaye anachukuliwa kuwa mfalme wa sanaa zote. Hususani, Plato anamtaja Mungu wa sanaa aitwaye Muse ambaye huwapanda wasanii vichwani na kuwafanya wabubujikwe na mawazo ya kisanii pindi anapowakumba (kufuatana na Plato kama inavyofafanuliwa katika Tilak, 1993: 29).
Kwa mujibu wa Plato, Mungu huyu huwapagawisha wasanii tu na kuwapa ufunuo au wahyi unaowawezesha kuwasiliana moja kwa moja na wasanii (Habib 2005: 24; Wafula & Njogu 2007: 24).
Kwa sababu hiyo, Plato aliwaona wasanii kama watu wenye vipaji maalum vinavyotoka kwa Mungu na kwa sababu hiyo, siyo kila mtu angeweza kuwa msanii. Katika riwaya tatu zilizoteuliwa Dunia Yao, na kwa kiasi fulani Musaleo!, inafuatilia kwa makini nadharia hii ya Plato kuhusu mwigo na imethubutu hata kumchukua mhusika wake mmoja, Muse ambaye anahusishwa na ghamidha na kariha ya utoaji wa sanaa za kiubunifu huko Ugiriki, kuwa mshirika wa kiroho wa mhusika mkuu aitwaye ‘Ndi-‘. Mhusika Bi Muse (wakati mwingine Mize) wa Dunia Yao anazua mjadala mpevu wa swala zima la sanaa na hulka yake kama inavyowasilishwa na Mohamed. Mhusika huyu ambaye amechukuliwa moja kwa moja kutoka kwa maandishi ya wahakiki wa Kiyunani, Plato na Aristotle, anakuwa kiunzi muhimu cha kujadili swala zima la usanii. Haya yanadokezwa ipasavyo katika riwaya hii pale Bi Muse anapoeleza asili yake.
Ufunguzi wa sura ya tanounadokeza asili ya mhusika huyu, Bi Muse, ambaye ni yule yule aliyezungumziwa na Plato tangu jadi, tofauti hapa ikiwa Bi Muse ni mhusika wa hadithini. Sura inaanza hivi: “Mimi ni Muse” […] “Kwa asili hasa, Ugiriki – lakini siku hizi naishi popote. Mara nyingine hujificha katika vina virefu vya ardhi kabla sijachomoza kumzuru niliyemchagua. Na leo nimekuchagua wewe.
Kwa hivyo nimechomozekea chini ya mnazi palipofukiwa kitovu chako, baada ya kupiga mbizi Bahari ya Hindi kuja kukuingia kichwani mwako…” (Mohamed 2006:61) Sawa na anavyopendekeza Plato kuhusu namna wigo wa kisanaa unavyojiri, hapa mwandishi anaendeleza hoja hiyo hiyo ya namna Ndi- anavyosababishwa atunge kazi yake na Bi Muse.
Naye ni kiumbe anayetangaza kuwa asili yake ni Ugiriki (alikotoka Plato) na hamkumbi Mgiriki pekee bali humkumba mtunzi yeyote wa kazi za kubuni. Ana nguvu za kichawi za kumsababisha msanii apagawe kama riwaya inavyodokeza: “Kwa kawaida,” aliendelea, “sina umbo maalum. Ni aina ya jeteta linalochanua jinsi andasa zangu na zako zinavyokubaliana kuchanua. Sikuzaliwa katika dhati na bayana ya mambo.
Mimi ni binti wa Zeus na Mnemosyne. Asili yangu inasimamia kumbukizi na dhana tu. Ndio maana nina majina mengi kwa mujibu wa kazi yangu ya kutia ilhamu. Calliope, Clio, Erato, Euterpe, Melpomene, Polyhymnia, Terpsichore, Thalia, Urania.
Hata unaweza kuniita Bi Mize, kwa jina la kikwenu. Kwani hapa nilipo nimekuja kwa sura ya kikwenukwenu, kipande samaki, kipande mtu na kipande ndege.” (Ivi: 68f) Huyu anayefahamika kama Bi Muse katika riwaya anaeleza namna anavyoweza kubadili umbo na kuwa mwenza wa kila msanii duniani. Ingawa amezaliwa na Mungu Mkuu wa Kigiriki, Zeus, Bi Muse ana uwezo wa kuwa binti wa kifalme au wa kijini kwa kuzingatia utamaduni wa msanii husika. Ndiyo sababu hapa anamwambia Ndi- kuwa akipenda anaweza kumwita Bi Mize ili afahamu kwa ukaribu nguvu zake anapomkumba. Mize au Mwanamize ni mhusika wa Waswahili anayefahamika kwa vitimvi vyake na nguvu za kiuchawi za kugeuka umbo kama inavyosemwa kwenye dondoo.
Muse, kama anavyotangaza, ana nguvu za kichawi za kumzuga mtu na kummiliki pale anapomchagua na kumfanya kuwa kiti chake. Kitendo hiki cha kupandwa na jazba na kupagawa ndicho kinachojitokeza mwanzoni mwa riwaya pale Ndi- anapoeleza namna swala zima la utunzi linavyohusiana na nguvu hizo za Muse ambapo utunzi unakua hatua baada ya nyingine hadi kukamilika kwake: Katika kubuni na kuumba – ‘Bi Muse’ anapokujia na kukuchota kwa uzuri wake – kama koja la ajabu, unatunga sauti na sauti, ileile au tofauti, na kupata silabi. Silabi na silabi, unapata neno! Neno, maneno. Ibara na sentensi. Ibara na sentensi huzaa matini. Na vyote hivyo ni sehemu muhimu ya simulizi – maandishi. (Ivi: 9) Dondoo hili linaeleza kwa muhtasari uhakiki wa ki-Plato na ki-Aristotle unaohusisha uandishi na kujazibika kwa mwandishi. Safari inayoanza na sauti au fonimu moja inakua na kupea hadi kufikia kuwa matini nzima. Inapotokea hivyo, mwandishi na mungu huyu wa sanaa, Muse, huwa kitu kimoja. Ndi- anaelekea kukiri kuwa uandishi hufatwa na ghamidha na kariha inayomjia mwandishi na wala si jambo la vivi hivi tu, chambilecho Ndi- kuwa Muse si kiumbe wa ‘sasambura turore’ au anayejitoa hadharani kuonekana. Ni kana kwamba Ndi- hushindwa kujizuia na kuhamasika kuendeleza kazi yake ya kiubunifu pale anapotawaliwa kihisia na kifikra na Bi Muse.
Hujikuta tu akiongozwa asikokufahamu ingawa anavyokiri mwenyewe huwa ni wakati adimu wa kutamanika. Hii ndiyo sababu Dunia Yao inaufafanua uhusiano wa Ndi- na Bi Muse kuwa wa mke na mume wanaoliwazana na kubembelezana hadi wanapooana na kuwekana nyumbani. Ni taswira ya unganiko la kipekee ambalo hufukuza utasa na badala yake huzalisha kazi za kisanaa baada ya wahusika hawa kusuhubiana na hata kupata mtoto, yaani kazi inayotungwa. Hatua zote hizi zinaelezwa na Ndi- hivi: Ndiyo, jina lake nimekuwa nikilisikia na kulisoma siku nyingi. Kama alivyosema mwenyewe, si kiumbe wa sasambura turore. Hujifichua anapohitajiwa kwa mapenzi ya dhati au kwa kutoa msaada.
Na mimi, nimefikia baleghe ya kusalitika naye. Nina haja naye. Ninamhitaji. Ninataka anisaidie. Anisaidie kuwasaidia wengine ikiwezekana. Anisaidie kuukata ugumba wa utunzi. Nina hamu kurutubisha na kutia mbolea pahala fulani. Nipate kizazi kipya cha sanaa katika ukame wa ubunifu. Nipate kurutubisha kizazi kipya cha utu katika ukame usio na utu. Ninahitajia mtekenyo wake unipandishe jazba. (Ivi:61f) Swala la kupandwa na jazba linajitokeza pia katika Musaleo!. Katika riwaya hii, Kingunge anaonyesha kuwa uandishi wake hutokana na jazba na kariha inayomsukuma kuandika kile ambacho yeye mwenyewe hana maarifa nacho. Tunaelezwa hivi: Lakini mara hii alipomweleza mkewe uandishi wenyewe alilazimika kusikiliza kwa makini. “Mara hii ni tofauti. Inajisimulia mimi naandika tu. Ni kitu kama ndoto. Yaani kazi yangu ni kuandika yanayonijia. Ngoja niimalizapo utajua tofauti yake na nyingine…” (Wamitila 2004: 12).
Tofauti na riwaya ambazo Kingunge anadai amezipa majina, riwaya anayoandika kwa wakati huu ni ya kipekee na imepokea nguvu maalum asizoweza kuzidhibiti. Ni kariha ya kipekee inayomsibu na ambayo inamsukuma kuandika mambo asiyoyaelewa. Si ajabu basi anapodai kwamba riwaya hii itajipa yenyewe jina badala ya yeye kufanya hivyo (k.10f). Nadharia za Umaumbo wa Kirusi na Umuundo katika Dunia Yao Dunia Yao pia inahakiki kwa uwazi dhana za nadharia ya umuundo za uhusiano wamaneno kimfululizo na kiwimawima. Msingi unaochukuliwa na riwaya hii ni ule wa ki-Saussure, na ulioendelezwa baadaye na Roman Jakobson, unaohusiana na dhana zake za uhusiano wa ishara wimawima au kimfululizo (Eagleton 1996: 85f).
Katika Dunia Yao Mohamed anatueleza hivi: Uhusiano wima wa maneno unakuhakikishia uteuzi. Uhusiano mlalo unakuhakikishia mpangilio wa kisarufi.Unatii amri za lugha au unavunja kanuni za lugha wakati mmoja. Unajenga kutoka kipashio cha chini kwenda kipashio cha juu kabisa. Au unaweza kushuka kutoka juu kwenda kipashio cha chini kabisa. Madhumuni ni kujenga maana kwa njia ya kubomoa maana. Kujenga mvuto wa kisanaa. (Mohamed 2006:9; msisitizo wangu) Mohamed katika Dunia Yao anataja na kuzifafanua dhana mbili muhimu za umuundo ambazo anazirejelea kama “uhusiano wima” na “uhusiano mlalo” wa maneno. Mahusiano haya ya maneno, tunaelezwa, yana natija zake hasa kwa mwanafasihi.
Uhusiano wima wa maneno, tunaambiwa, huhakikisha uteuzi. Swala muhimu hapa ni kujua namna uteuzi huu unavyohakikishwa kwani haujabainishwa waziwazi kwenye dondoo. Mwamzandi (2007: 71) ametoa mfano ambao kwa muhtasari unafafanua swala hili la uteuzi: mchuti kiki Abasi aliupiga teke mpira mkwaju Katika mfano huu, neno ‘teke’ limechukuliwa kama neno la kawaida au la wastani ambalo msemaji wa Kiswahili angelitumia.
Maneno yaliyoandikwa kwa mlazo na ambayo yamejipanga juu na chini ya neno ‘teke’ ndiyo tunayoweza kusema kuwa yanahakikisha uteuzi unaozungumziwa na dondoo. Maneno hayo yanaeleza namna na jinsi mbalimbali za kuupiga mpira na mwanafasihi anaweza kuchangua neno mahsusi kwa kutegemea hisia maalum anayotaka kuibua kwa msomaji wake (Mwamzandi 2007: 71). Uhusiano mlalo wa maneno nao, kama unavyofafanuliwa ndani ya dondoo, una uwezo wa kuidumisha au kuivunja sarufi ya lugha, matokeo ambayo yanatokana na jinsi mwanafasihi, kwa mfano, atakavyochagua kuyapanga maneno yake katika sentensi. Katika sentensi, lugha yoyote huwa na matarajio na sheria zake za kisintaksia na kisarufi. Kwa sababu hiyo, kulibadilisha neno
moja katika sentensi na kuliweka mahala tofauti na pale panapotarajiwa na wanalugha husika kuna athari kubwa, ikiwemo ile ya kuzua maana tofauti na ile inayoweza kukubalika. Neno hilo linaathiriana kivingine na maneno mengine ya sentensi na kuzua maana mpya inayoweza kutegua uzoefu wetu wa lugha hiyo. Huu ndio ule mpangilio wa kisarufi unaoweza kutii au kuvunja kanuni za lugha na ambao unaozungumziwa na dondoo hapo juu na tunaweza kuutolea mfano huu: kitabu kizuri mtu mnene Hebu tazama sasa tunapobadilisha na kuanza na vivumishi na kisha nomino, na kuikaidi sarufi ya Kiswahili kama inavyotarajiwa: kizuri kitabu mnene mtu Ingawa maana iliyokusudiwa bado ipo, mabadiliko ya pale zilipo nomino na vivumishi kumesababisha ugeni fulani. Huu si muundo wa wastani wa Kiswahili ingawa unaweza ukakubalika katika miktadha mahsusi, ukiwemo fasihi.
Huku ndiko kujenga maana kwa njia ya kuibomoa kama kunavyozungumziwa na dondoo. Uhakiki wa Kidenguzi: Nyuso za Mwanamke na Dunia Yao Mbali na kushughulikia maelezo ya kinadharia kuhusu nadharia ya udenguzi, riwaya za Nyuso za Mwanamke na Dunia Yao pia zinashughulikia zoezi lenyewe la kuchanganua maana kwa kuongozwa na fikra hiyo ya kidenguzi. Ili tufuatilie kila kinachosemwa katika riwaya hizi mintarafu ya udenguzi ni vyema tuangazie, walau kwa muhtasari, fikra kuu ya nadharia yenyewe.
Udenguzi ni nadharia inayohusishwa na Mfaransa Jacques Derrida (1930-2004). Hapa nitafafanua misingi miwili tu ya nadharia hii kama ilivyofafanunuliwa na wataalamu mbalimbali (taz. Burman & McLure 2005: 284-286; Schmitz 2007: 115f). Mosi, mbinu kuu na muhimu inayotumiwa wa wanaudenguzi ni ukinzani wa jozi za maneno. Tasnifu ya Derrida kuhusu jozi hizo ni kuwa jamii za Kimagharibi zimejenga upendeleo wa wazi pale neno moja katika jozi husika daima linawakilisha utukufu au kile kinachopaniwa kufikiwa kama kitu adili huku dhana ya pili ya jozi hiyo hiyo ikiangaliwa kama ghushi, isiyo safi na ya daraja ya chini. Wanafilosofia wa awali, kama anavyodokeza Derrida, waliuona ulimwengu katika muktadha huo – jambo lililowafanya kuuona upande wa kwanza wa jozi za maneno kama unaojengwa na vitu vya kimsingi na vinavyostahili kupewa kipaumbele kama vilivyo safi, vya wastani na vilivyokamilika huku upande wa pili wa jozi nao ukifafanuliwa na vitu vilivyotandwa na utata, vyenye doa na umahuluti. Kwa sababu hiyo, usanifu wa hoja katika nchi za kimagharibi una tabia ya kuviona vitu na hali mbalimbali kwa namna ya upendeleo.
Pamoja na mgao huo ambao wanafilosofia wa kijadi walipania kuujenga, wanaudenguzi hulenga kufutilia mbali mipaka hiyo na kuonyesha kuwa jozi za maneno ni mfano wa sarafu moja yenye pande mbili. Udenguzi hubainisha kuwa nuru na kiza ni vitu ambavyo wanafilosofia wa kijadi wangevitenganisha kwa kupendelea nuru kuliko kiza. Kwa wadenguzi, nuru sawasawa na kiza vimechangamana na huwezi kukielewa kimoja bila kingine. Hatungeweza kumaizi kile tunachokifahamu kama nuru iwapo lugha tunayoitumia haingekuwa imeratibu ndani yake dhana ya kiza. Pili, udenguzi hushughulikia kwa pamoja jozi ya maneno yanayokinzana na wakati huo huo kubainisha itikadi kuu inayojitokeza na inayostahili kusailiwa upya. Kupitia uchanganuzi makini wa lugha ya matini, wadenguzi hudhihirisha ukinzani na utepetevu wa matini hizo.
Hili ndilo linalowapelekea wadenguzi kudai kuwa matini hujiumbua na kujibomoa yenyewe na wala sio wao wanaofanya hivyo. Wanavyodai, hii ni sifa ya azali na iliyomo katika lugha kwani tangu jadi lugha imejengeka kama mfumo wenye ukinzani na unaotofautisha maana. Lugha yenyewe imejengeka kiudenguzi kwani hubainisha tofauti zilizomo ndani yake – za kimaana na za kiitikadi. Kipengele cha kwanza kinaingiliana moja kwa moja na fasiri inayotolewa na mhusika mkuu wa Nyuso za Mwanamke, Nana, pale anapotoka nyumbani kwao na kuabiri safari ndefu ya kuutafuta uhuru wake binafsi baada ya kuamua kutoroka nyumbani kwao. Anaanza somo lake la kidenguzi kwa kuzamia jozi zilizomo katika dhana mbalimbali zinazokinzana: Kwa kawaida nafsi yangu ilinifanya niamini kwamba hakuna utenganisho mkamilifu baina ya kuwepo na kutokuwepo. Sisi binadamu tupo kama hatupo au hatupo kumbe tupo.
Basi, maisha ya siku hizi ni kama kuwepo ndani ya kutokuwepo au katika kutokuwepo na kuwepo. Ni hali ya kudinda ndani ya ukweli na uwongo. Au baina ya nafsi moja na ndani ya nyingi na nyingi ndani ya moja: utambulisho wetu ni wa weusi na weupe, majilio yetu ni nidhamu na machafuko. Tunavunga ndani maumbile yanayovunjwa na utamaduni wa pupa, katika dunia isiyobagua tena kati ya wema na uovu, uke na uume, kitovu na pembezoni… (Mohamed 2010: 59; msisitizo wangu). Lakini kama Derrida anavyotambua kuwa watu hupania tu kuweka mipaka kati ya vitu, mipaka hiyo kwa hakika huwa ya kufikirika na udenguzi hutuelekeza tuangalie kwa makini ukinzani unaojitokeza ndani ya matini (Carter 2006: 111).
Nana anatutanabahisha juu ya jozi tofauti tofauti zikiwemo kuwepo/kutokuwepo, ukweli/uwongo, umoja/wingi, weusi/weupe, wema/uovu, uke/uume, kitovu/pembezoni ambazo tunastahili kuzifikiria kwa pamoja ili tuone namna jozi hizi zinavyojengana na kuumbuana1. Hii ndiyo sababu Nana wakati mwingine anazibadilisha jozi za maneno kama vile kuwepo/kutokuwepo hadi kutokuwepo/kuwepo, na “moja/nyingi” – “nyingi/moja”. 1 Kwa ufafanuzi zaidi wa fikra ya kidenguzi kama zoezi la uchanganuzi wa jozi za maneno msomaji anashauriwa asome makala ya Mwamzandi (2011: 1-14). Humo ataona namna maneno jozi yanavyoumbuana na pia kujengana kimaana. Aidha, ningependa kuwashukuru wahariri kwa ushauri na mapendekezo yao, hususani kuhusu sifa na hulka ya fasihi ya kiusasa-baadaye.
Mipaka ya jozi za maneno huwa myembamba sana na hili ndilo linaloendelezwa na Nana kwa utaratibu huu: Mkinzano unaishi ndiyo, na kwa kweli lazima uishi kwani mkinzano ndiyo maisha yenyewe. Lakini kila mkinzano una mstari mwembamba usioonekana kwa macho. Ndiyo unatenganisha mambo, lakini ni mwembamba mno kutenganisha kwa ukamilifu kitu kimoja na cha pili. Hapana kitu kimoja na cha pili, pana kimoja kinachoshibishana na kugombana na cha pili. Ndivyo dunia yetu ilivyoanza tokea mwanzo katika hali ya uwili inayotegemeana na kutofautiana […] Pana kuvuka mipaka pande mbili. Hiki cha huku kinaweza kwenda kule na cha kule kinaweza kuja huku. Nguvu za hiki zinajengwa na kile. Kuwepo kwa hiki ni sababu ya kuwepo kile. Huo ndio uwili unaotegemeana, lakini unaovunjana kwa wakati mmoja. Anayejiona ameshinda hatimaye ni yule mwenye nguvu, lakini ukitazama sana, hapana anayeshinda. Kuna kushindwa kwa wote. (Ivi: 59f) Katika dondoo hili, uwili unaozungumziwa na Derrida umekaririwa mno hapa. Kila mahali, kunatajwa kitu kimoja na jinsi kinavyosuhubiana na kuathiriana na kile cha pili.
Dunia, kama asemavyo Nana, imejengwa na uwili huu wa ukinzani. Maneno ya Nana yanadokeza muktadha mahsusi unaohusu ugomvi wake na babake. Baba alidhamiria kushinda kwa kumlazimisha Nana awe chini ya mamlaka yake. Nana naye anajiona ni mtu mzima wa kujiamulia watu anaotaka kutangamana nao. Hili ndilo analosisitiza Nana katika mvutano wake na babake. Baba anapania mwanawe atangamane na watu wa aila ya juu kama alivyo yeye mwenyewe na haelekei kuufurahia uhusiano wa bintiye na Mpiga Gita (Faisal).
Mwishoni, tunaonyeshwa kwamba baina ya kushinda na kushindwa, kushinda kunawavutia wengi ingawa kwa hakika hakuna mshindi. Nana anatoroka nyumbani na katika vita hivi vya baba na mwana, hakuna anayeshinda – kila mmoja anashindwa! Baadaye kidogo, Nana anatueleza waziwazi chanzo cha mawazo haya anapotuambia: Hapo nilimkumbuka Derrida na ubomozi wake anaouita (de)construction. Kila kitu lazima kiwe deconstructed. Naye hakuchukua muda kunijia katika fikra hii ya (de)construction. […] Falsafa si mijineno tu. Si ubingwa tu wa kushindana ili mmoja amwone mwingine duni, ili yeye aonekane bingwa au gwiji. Falsafa ni maisha yenyewe. (Ivi:60) Udenguzi au ‘ubomozi’ kama unavyorejelewa kwenye Nyuso za Mwanamke unahusishwa na usomaji uliopea wa kutazama kila neno katika jozi kwa jicho pekuzi. Usomaji huu umependelewa sana na wadenguzi wanaodai kuwa matini za fasihi zina tabia ya kuzungumzia kile zisichokidhamiria (Burman & MacLure 2005: 284f). Hii ni mianya inayostahili kufuatiliwa na msomaji ili aweze kuidengua kikamilifu matini husika. Dunia Yao, kupitia Ndi- inazungumzia hatua hii muhimu katika usomaji wa kidenguzi kwa kusema:
Madhumuni ni kujenga maana kwa njia ya kubomoa maana. Kujenga mvuto wa kisanaa. Ndiyo, unaweza kujenga maana hata katika mwanya mtupu. Hata ukitaka, unaweza kwa makusudi kupoteza maana kabisa kwa vivuli vya maana. (Mohamed 2006: 9) Katika dondoo hili kile kinachorejelewa kama kivuli cha maana ni ile sehemu ya pili ya neno au dhana katika jozi ambayo aghalabu huenda ikaachwa nje na isizungumziwe wazi wazi na mwandishi. Wadenguzi wanafuatilia maneno kama hayo kama linavyotarajia zoezi la kidenguzi ili kubainisha kile kisichosemwa na athari yake katika uwanja mzima wa maana (Schmitz 2007: 118; Carter 2006: 111). Uhalisia, Sanaa Faafu na Nadharia ya Usasa-baadaye Swala jingine muhimu linaloibuliwa na riwaya zilizoteuliwa katika makala hii ni mazingatio ya kile tunachoweza kukitambua kama sanaa stahiki kwa waandishi na hadhira lengwa.
Kama nilivyotanguliza hapo awali, riwaya hizi zimesheheni majaribio mengi na kwa namna zilivyoandikwa msomaji huenda akatanzwa na mbinu tata zilizomo za kiuandishi. Waandishi wa riwaya hizi wanaelekea kulitambua hilo na Dunia Yao inazamia mjadala huu wa sanaa faafu dhidi ya ile iliyopitwa na wakati, hasa kwa kuzingatia kipindi mahsusi cha kihistoria na mbinu sadifu za kuwasilishia sanaa. Kama tapo la kiuandishi, uhalisia umekuwa na uzuri wake ingawa kile kilichoonekana kitu adimu ndani ya uhalisia kimeanza kutiliwa shaka. Ndi- katika Dunia Yao anadokeza hivi: Alisita hapo. Nilifahamu amekusudia nini. Wakati wa sanaa ya uhalisia nilijua umeshapita.
Kwa kweli wakati ule nilipoanza, nisingeweza kuandika vingine nje ya uhalisia. Kanuni zake zisingekubali. Nani angenichapisha? Nani angenisoma? Jambo moja muhimu lililoshikamana na sanaa wakati ule lilikuwa dukuduku la watu. Tamaa zao za dhahiri. Nusura iliyoonekana iko njiani. Ingefika kesho kama si sasa hivi. (Mohamed 2006: 71) Kama mhusika, Ndi- anaona kwamba yeye pia amekuwa katika hali ya mpito. Uhalisia aliouenzi sasa hauna nafasi kwake kwa kuwa wasomaji sasa wako tayari kuzipokea kazi zake za kimajaribio.
Hapo awali, hakuwa na budi ila kutunga kazi za kihalisia na anazo sababu zake za kufanya hivyo kama inavyoelezwa katika majadiliano haya ya Ndi- na Bi Muse. Jambo la kwanza ni kuwa wasomaji wenyewe walikuwa na matarajio au dukuduku lao kuhusu kazi za fasihi ambazo walitarajiwa ziandikwe kwa mtindo huo wa kihalisia. Pili, wachapishaji nao hawangethubutu kuchapisha kazi za kimajaribio kwa kuwa wanunuzi hawangeziona za manufaa kwao. Hivyo mwandishi wa wakati huo hangekuwa na hiari ya kiuandishi ila kuwatii wachapishaji ambao waliongozwa zaidi na faida inayotokana na mauzo yao kuliko ujasiri wa kisanii wa mwandishi. Swala hili la kuthaminiwa kwa fedha kuliko waandishi limezungumziwa pia katika Musaleo! kama tatizo mojawapo linaloathiri kutolewa kwa sanaa nzuri, tena faafu. Sanaa nzuri, kama inavyoelekea kujadiliwa humo, ni ile
ambayo itakidhi haja za kibinafsi za waandishi na aila zao. Hususani, Musaleo! inalalamikia namna waandishi wanavyopunjwa na kuchezwa shere na wachapishaji. Zamda, mkewe Kingunge, analalamika jinsi mumewe anavyotumia muda wake mwingi kuandika riwaya huku akikosa namna za kuikimu familia yake. Zamda anasema: Sasa huu uandishi nao naona umekuwa kama kufungukwa na uganga. Heri siku zilizopita na hata kulipa haulipi huu! Uandishi! Uandishi! Uandishi wa nini? (Wamitila 2004: 12) Ndi- katika Dunia Yao anaelekea kupendelea fani ya usasa mamboleo au usasa wa kisasa katika maswala ya uwasilishaji wa kazi za sanaa. Sanaa, kwa mujibu wa mhusika huyu, huenda na wakati na mahitaji ya mwanadamu.
Na hapo anaeleza kwa nini uhalisia ulifaa katika kipindi fulani cha uandishi kuliko uandishi wa aina yoyote na ilipodhihiri kwamba uhalisia haungeweza kushughulikia dhamira za kisasa, basi ilibidi nao utupiliwe mbali kama kinavyotarajia kipindi cha hivi leo. Ndi- anasema: “Hii ni bustani iliyopitwa na wakati,” nilimsikia akisema hatimaye, “inafanana na mantiki ya mambo ya miaka ile iliyopita. Ni bustani ya ukame na kifo. Ni ukaukivu wa mambo unaoashiria ufu wa bongo lako lisiloweza tena kusimulia kwa mantiki. Hakuna tena mantiki. Hakuna tena umajimaji wa ubichi wa mambo. Uhai haupo tena mbali na kifo, na kwa hivyo hauwezi kuwepo ukweli, ukweli. Wigo wa ukweli wa moja kwa moja haudindi tena. Na kusema kweli, tokea mwanzo haukuwepo.
Iliyokuwepo ni ndoto. Ndoto ya bustani hai. Kumbe kavu na teketevu namna hii.” (Mohamed 2006: 64) Hapa, Ndi- anaulinganisha uhalisia na kifo cha kiakili, yaani kukosekana kwa ubunifu katika fasihi. Hata kile kilichothaminiwa kuwa uhalisia kiliishi katika njozi za watu na kamwe haukuwa ubunifu kama anavyodai Ndi-. Anachosisitiza Ndi- ni kuwa kuzingatia uhalisia kwa kipindi cha leo ni kuishusha hadhi fasihi. Mawazo sawa na hayo yamezungumziwa pia na Kingunge katika Musaleo! pale anapokutana na mhariri wake ili wazungumzie maendeleo ya mswada wa hadithi yake.
Mhariri anabishana juu ya mwelekeo mpya aliouchukua Kingunge kwa kusema: “Wasomaji wako watalalamika sana mara hii. Mbona usitumie mtindo rahisi ambao wanaufahamu: unajua watu hawapendi mabadiliko bali huyapenda mazoea na ukale…” alilalamika mhariri. “Na hilo ndilo kosa kubwa. Maendeleo hayamo katika ukale!” (Wamitila 2004: 41) Sawa na anavyodai Ndi- wa Dunia Yao, katika Musaleo! naye mhusika Kingunge anayaona maendeleo yakiwemo katika kuhimiza kuwepo kwa majaribio katika uandishi na wala sio katika kuwa wahafidhina. Lakini je, sanaa mamboleo inayopendelewa na riwaya hizi ni ipi?
Waonavyo waandishi hawa wa kimajaribio uhalisia umepitwa na wakati na wamehoji kuwa sanaa kamwe haiwezi kuwekewa mipaka. Mintarafu ya riwaya hizi, sanaa nzuri ni ile itakayojumuisha mbinu za kuelezea dunia ya sasa iliyojaa miujiza na mambo mengi ambayo hayawezi kueleweka kwa njia iliyo rahisi. Uzuri wa sanaa kwao si kuyaeleza mambo yalivyo kihalisia na, chambilecho Dunia Yao, “kuzipata maana kibungabunga” (Mohamed 2006: 9). Msomaji sharti ashiriki kikamilifu katika kuzipekua maana za kazi anazozisoma na kukubali kuzugwa pale inapobidi.
Sanaa nzuri kwao ni ile itakayomlazimisha msomaji kusaili ishara tofauti tofauti atakazotumia mwandishi na kisha kuzihusisha ishara hizo na muktadha wa maisha yake halisi. Hatimaye, ufaafu wa sanaa huamuliwa na namna itakavyomtumikia yule anayelengwa. Haya ndiyo mawazo makuu yanayoendelezwa katika sura yote ya tano ya Dunia Yao. Katika Musaleo! naye mhusika Kingunge anayakubali mawazo haya anaposema: “Siandiki? Naandika sana. Tena mara hii riwaya ya kisawasawa itakayojisoma yenyewe pamoja na kuyasoma maisha yetu. Naandika riwaya itakayojihakiki yenyewe!” (Wamitila 2004: 10) Kingunge, kama inavyodhihirika hapa, anashadidia wazo kuwa kitendo cha uandishi huvuka mawanda ya matini kwa kuhakiki mchakatowenyewe wa uandishi.
Katika muktadha huu, riwaya za kisasa zinamaizi hali hiyo na kuhimiza wingimatini uliomo duniani – jambo ambalo wasomaji hawana budi kuliafiki na kulikubali kama dira inayochukuliwa na fasihi ya kisasa ya Kiswahili. Baada ya kuzungumzia uhalisia na ufaafu wake wa kukidhi matakwa ya binadamu, riwaya teule pia zinafafanua viunzi vilivyotumika kuzijenga.
Riwaya za kisasa, kama inavyopendekezwa, zimejengwa na vipande vya ngano au simulizi fupi fupi zisizokuwa na uaushi, tofauti na simulizi kuu ambazo aliziona kama zilizopoteza uthabiti wake (Lyotard 1984: 37). Simulizi hizi hutokeza kwa muda mfupi ndani ya riwaya na hazilengi kuhodhi ukweli kama zilivyo simulizi za jadi ambazo zililenga kukongomea ukweli kama zilivyouona. Lyotard, kwa mfano, amenukuliwa na Barry (2002: 86) akisema kuwa simulizi kuu hubuniwa kwa azma ya kusawazisha ukinzani na kusababisha urajua ambao kwa hakika hauna mashiko. Mtazamo sawa na huu unachukuliwa na riwaya teule kutokana na kile anachokirejelea Baudrillard (1983: 142-156) kama “kupotea kwa uhalisi” ambapo mpaka kati ya uhalisi na kinachodhaniwa kuwa maana yake haupo. Anachodhamiria Baudrillard (ibid) ni kuwa viashiria vimepoteza uwezo wake wa uashiriaji na kwa sababu hiyo, uhalisi haurejelei chochote kilicho nje ya kiashiria bali kiashiria hutuelekeza katika viashiria vinginevyo. Maana, hivyo basi, hubakia ikiselea kutokana na wingi wa viashiria. Hii ndiyo sababu riwaya za usasa-baadaye zikakosa muungano na muumano wa hadithi tangu mwanzo hadi mwisho ingawa huo unakuwa msingi wa kuchachawiza hadithi yenyewe inayosimuliwa. Katika Musaleo! inadaiwa kwamba sanaa ya siku hizi imefanana sana na uhalisia wenyewe wa maisha na waandishi wanafuata mkondo tu wa uhalisi huo. Mawazo haya yanachukuana
na yale ya Baudrillard, anayedai kwamba mahala pa uhalisi wa siku hizi umechukuliwa na mbinu za uashiriaji au uwasilishaji wa ukweli huo (1983: 142-156). Mjadala wa Kingunge na mhariri unafafanua zaidi uhusiano kati ya uhalisia wa maisha na sanaa sadifu ya kuuzungumzia: “[…] Uhalisi wa siku hizi umevunjikavunjika hauna pa kujishikiza; hauna mshikamano imara. Hakuna njia nyingine ya kuukabili isipokuwa kwa mtindo wa uhalisi wenyewe; hujasikia mjinga hunyolewa jinsi anavyojipaka maji? Lazima tudadisidadisi kila kitu: siasa, uchumi, mapenzi hata miundo ya hadithi pamoja na hata lugha yenyewe. Hii sio dunia ya kuridhika na tulichozoea,” alisema Kingunge. (Wamitila 2004: 41) Msimulizi katika Dunia Yaoanazungumzia hili pia: Katika simulizi na mapito yake, vipandevipande – si lazima vishikane. Unavimwaga tu vipande vyenyewe kama unaatika mbegu kwenye shamba la sanaa. Unafanya hivyo kuwaacha wasomaji waunge wenyewe vipande vya maana zao, huku maneno mengine ukiyajengea vivuli ili kuwategea makusudi watafute maana zao badala ya kuzipata maana kibungabunga. (Mohamed 2006: 9) Kwa kuwa muda wa kimajaribio umefika na kazi zenye sifa hizo kukubalika na kuchapishwa, basi msimulizi katika Dunia Yao anaeleza kile kinachokuwa kiungo muhimu cha kazi kama hizi: Naam, nilikiri. Hii ndiyo itakuwa simulizi yangu mpya katika mchanganyondimi.
Kipande hapa…kipande pale. Vipande vya ‘allegory’. Vipandevipande vya ngano mpya. Ngano ya tafrani-za-kileo katika usogori mpya. Aaaaa, ikiwa zamani sikukujua Bi Muse, sasa nakuhitaji mara milioni moja. Nataka niwe nawe pachapacha. Nikukumbatie unikumbatie, unikoleze ilhamu, nilimwambia. (Ivi: 68) Huu ni mdokezo unaotolewa na riwaya kuhusu kile kitakachopatikana humu. Tunatanabahishwa kuwa riwaya hii itakuwa ni mchanganyiko wa simulizi za kila aina na wingimatini wa “kipande hapa…kipande pale” (ibid.).
Kwa yakini, hii ni sifa inayojitokeza katika riwaya zote tatu ambazo zimenakili kazi mbalimbali za waandishi tofauti tofauti. Mimi/Wengine, Kitovu/Pembezoni: Mazingatio ya Nadharia ya Ukoloni-baadaye Kipindi mahsusi cha kustawi kwa nadharia ya ukoloni-baadayeni katika mwaka wa 1978 baada ya Edward Said kuchapisha kitabu chake cha Orientalism (Said 1978). Nadharia yenyewe inajihusisha na mambo mawili makuu yaani ukoloni-baadaye wenyewe na kazi za kisanaa zinazouhusu. Riwaya teule zinazoshughulikiwa na makala hii zimezingatia mambo yote haya mawili kwa njia tofauti. Musaleo! inagusia mada muhimu ya Said iliyomo katika Orientalism. Riwaya inazunguzmia dhana za ‘mimi’ na ‘wengine’ – mbeya mbili muhimu zinazotofautisha Umagharibi na Umashariki. Umagharibi ulihusu nchi za Ulaya na Marekani ambazo zilihusishwa na ustaarabu pamoja na maendeleo makubwa katika nyanja zote huku Umashariki ukinasibishwa na nchi zilizokuwa na umasikini uliokithiri, maendeleo duni na ushenzi. Kile ambacho Said alikirejelea kama Orient (‘WENGINE’ katika Musaleo!) na kilicholengwa na watu wa Ulaya Magharibi kilijumuisha nchi za Mashariki ya Kati pamoja na zile za watu lugha za Kisemitiki pamoja na mataifa ya Asia Kusini.
Mataifa haya, na hasa yale ya Uarabuni ya Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, ndiyo yaliyobeuliwa na kuonekana kama yenye dosari mbele ya macho ya wazungu wa Ulaya Magharibi (Said 1978: 99). Umagharibi nao ulichukuliwa kama kitovu cha ustaarabu na maendeleo ya kisayansi na kijamii. Hiyo ndiyo misingi anayoitumia mhusika Ukolongwe katika Musaleo! katika kujitofautisha na wanajamii: “Sasa kuanzia leo, na wala si kuanzia leo ni tangu zama na azali, kuna MIMI na WENGINE tu. Mimi ndimi msingi wa kila kitu. Mimi sio kama nyie!” (inasemwa alikuwa na rangi nyepesi na nywele zake zilikuwa mbuyembuye, ambazo hazikuiva) […] Alisema mengi lakini kufupisha habari kadai rangi yake ilikuwa bora na iliashiria ubora wa akili.
Ukolongwe alishikilia kuwa kauli zake ziliwekewa misingi imara na Sayansi [sic]. Inasemekana siku moja alitokeza hadharani huku ameshikilia kitabu kimoja kiitwacho The Wild Man’s Pedigree. Humo aliwasomea watu sehemu fulani aliyodai kuwa ilizieleza sifa zao. “Weusi: wasiochangamka, watulivu, wenye pua pana, wajanja, wazembe na wanaotawaliwa na ugeugeu!” Ajabu ni kwamba mwenyewe alikuwa na sifa hiyo hiyo ya kubadilikabadilika kama kinyonga. (Wamitila 2004: 26f; herufi za mlazo hivyo hivyo katika matini ya awali) Kinachohadithiwa katika riwaya ya Kingunge ni juhudi za wakoloni za kukuza uwingine kupitia maumbile kama vile rangi na nywele. Aidha, madai ya wakoloni kuwa wao ni bora yanajitokeza pia katika maandiko yao wanayoyaenzi kama vile The Wild Man’s Pedigree ambamo wanaendeleza propaganda kwamba wao ni bora kuliko wanajamii wengine.
Humo, twapata Waafrika wakifafanuliwa kama wenye sifa hasi za uzembe, ujanja, kutokuwa na msimamo na hata walioumbuka kimaumbile kama inavyoashiriwa na pua zao pana. Kwa upande wao, wakoloni wanajiona kama wenye rangi bora inayoashiria akili iliyopevuka, waliostaarabika na wanaofuata maadili ya kisayansi. Pamoja na kutambua hila za wakoloni, Musaleo! inajusurisha kubainisha mbinu mbalimbali zilizotumiwa na wakoloni katika kuwatawala wenyeji Waafrika. Ukolongwe, mhusika mkuu wa riwaya ya Kingunge, kwa mfano, anapiga marufuku kile alichoshindwa kukifahamu na ambacho wenyeji walikifahamu. Pia aliamrisha watoto wafunzwe nyimbo mpya, tofauti na zile walizoziimba hapo awali.
Vilevile, tunaelezwa namna alivyoiteka nyara lugha na kubadilisha maana za maneno kiasi kwamba pale panapozungumziwa ‘uhuru’ au ‘uzalendo’ wenyeji walisikia badala yake ‘kufuru’ na ‘uvundo’ mtawalia (Ivi: 26). Kwa utaratibu huo Musaleo!, kupitia kwa riwaya ya Kingunge, inaingia katika hatua ya utekelezaji wa nadharia ya ukoloni-baadaye kwa kuzingatia namna fasihi ya ukoloni-baadaye inavyoweza kuweka upenuni kwa uwazi au kwa mafumbo hila na hilaki wanazotumia watawala kwa watawaliwa (Tyson 2006: 431). Musaleo! ni zoezi la kina la uchanganuzi wa njama, hulka na athari za ukoloni mkongwe pamoja na ukoloni mamboleo wa viongozi wa zama za leo. Riwaya hii ina zoezi maalum la utekelezaji wa uhakiki wa nadharia ya ukoloni-baadaye. Humu, ukoloni mamboleo unawakilishwa na kina ‘Musaleo’ wa siku hizi, yaani viongozi, wanaotumia njama za kila aina za kuwakandamiza wale
waliowapa madaraka. Hapa na pale, riwaya hii inazungumzia kwa mafumbo namna nchi za Kimagharibi zinavyowazuga wale walioko pembezoni kama inavyobainishwa na kile kisa cha “ardhi kuwa pande kubwa lililovunjika na kuwa Godi-Wana na Huraa-Asi na mengine madogo madogo mpaka yakafikia matano” (Wamitila 2004: 89). Katika kisa hiki, kunatajwa sumaku inayozivuta ardhi mahala pamoja na yule buibui aliyesakini pale kwenye kiini ambaye aliwala nzi waliozongwa na utandu – sitiari ambazo zinafafanua mahusiano hayo ya kitovu (wenye nguvu, wakoloni au mataifa ya ulimwengu wa kwanza) dhidi ya pembezoni (wanyonge, watawaliwa au mataifa ya ‘ulimwengu wa tatu’). Nadharia ya ukoloni-baadaye haiishii katika kumlaumu mkandamizaji kama anavyodhihirisha Said katika kitabu chake Culture and Imperialism (Said 1993). Anatambua kuwa ingawa nchi za Asia, Afrika na Amerika ya Kilatini zina uhuru wa kisiasa bado zinatawaliwa na kutegemea nchi za Kizungu (Said 1993: 20). Pamoja na ukweli huo, Said anaona kwamba haifai kuzimwagia nchi za Kimagharibi lawama kwa kuwa nchi hizo zinastahili kujilaumu zenyewe kwa kutoichanganua vyema mifumo adili ya kuleta mageuzi ya dhati ya kisiasa na kitamaduni katika jamii (Said 1993: 277). Ni hapa ambapo viongozi walioshika hatamu za utawala baada ya kuondoka kwa wakoloni wakongwe waliendeleza na bado wanaendeleza uongozi wa kiimla na kuwanyanyasa wananchi wenzao. Kulingana na Said hali ilivyo baada ya ukoloni wa Kimagharibi ni aina ya mduara wa kibeberu unaoturejesha katika hali iliyokuwa wakati wa mkoloni. Bado kuna tamaa za kichoyo ambapo watu wanataka kujinufaisha kibinafsi na kuwabagua wenzao kidini, kirangi na kikabila (Said 1993: 275-276). Na hapa ndipo Nana katika Nyuso za Mwanamke anavyotaka watu waangazie kitovu na pembezoni kama chanzo cha uovu uliosakini duniani: Sikubaliani nao wanaotilia mkazo kitovu cha duara. Nguvu tunazoambiwa zimeumbwa makusudi ili wanaoishi pembezoni lazima wavutwe ndani kusujudia kitovu.
Nionavyo mimi, lazima ukingo wa duara uvunjwe ili viliyomo ndani vimiminike nje na vya nje viweze kupenya ndani kutafiti kilicho ndani na kitovu chenyewe kinachotoa fikra mbaya na ovu. Bila ya hivyo walioko pembezoni maisha watajikuta wako pembezoni – wamezugwa kabisa na maneno ya kukuza njugu maganda. (Mohamed 2010: 60) Anavyoona Nana, swala la kitovu na pembezoni ni fikra potofu iliyomo vichwani mwa watu na kwa sababu hiyo wakati umefika wa kila mtu kujituma ili kuifanya dunia kuwa mahala bora badala ya kuishi kwa visingizio vya ukoloni na athari zake mbaya. Anima na Mamanchi wa Musaleo!:Wahusika katika Saikolojia Changanuzi Musaleo! imetumia mawazo ya mwanasaikolojia Carl Gustav Jung2 hasa katika ujenzi wake wa wahusika Anima na Mamanchi. Kimsingi, Jung alidai kwamba kila binadamu, awe mke au mume, 2 Carl Gustav Jung (1895-1961) ni mwanafunzi wa Sigmund Freud na kwa mujibu wa Wamitila (2003: 298) ni mwanasaikolojia anayefahamika kwa kuendeleza dhana ya ‘ung’amuzi jumuishi’ ambayo aliitumia kuelezea sehemu ya akili ya binadamu ambayo hurithiwa na kufanana kwa kila binadamu. Sehemu hii, anavyoeleza Wamitila, ndiyo huwa amebeba chembechembe za hulka za jinsia tofauti na yake. Hivyo ni kusema kwamba mwanamume huwa na sifa za kike zilizofichika katika ung’amuzibwete wake na aghalabu sifa hizo hujitokeza katika umbo la msichana bikira au mwanamke mwenye sifa za kiungu na ambaye hufahamika kama Anima. Vivyo hivyo, mwanamke naye huhodhi sifa za kiume katika ung’amuzibwete wake na hudhihirika katika umbo la kikongwe mwenye busara aitwaye Animus (Carter 2006: 79). Kudhihirika kwa wahusika hawa huwa katika ndoto na ishara mbalimbali na wanasaikolojia huamini kuwa wahusika hawa huwa njia ya kuimarisha tabia ya mtu binafsi ambayo huwa imeficha mawazo na mitazamo hasi (Schmitz 2007: 200).
Mawazo ya Jung yanabainika ndani ya riwaya hasa tunapozingatia uhusika wa Anima na Mamanchi na jinsi wanavyomdhihirikia Mugogo Wehu. Wote wanatokea pale Mugogo anapokunywa sumu aliyotegewa na watu wasiojulikanana kupoteza fahamu nyumbani mwake, ingawa Mugogo mwenyewe alihisi machovu na hivyo kujilaza kitandani (Wamitila 2004: 8). Yote anayoyafanya Mugogo ndani ya hadithi kwa hakika si mambo yakinifu bali yanatokea ndani ya ‘ndoto’ anayoipata katika ‘usingizi’ huu – yakiwemo kukutana kwake kwanza na Anima, na kisha, Mamanchi. Akiwa katika ndoto yake kuu, Mugogo anakutana kisadfa na Anima (Ivi: 28). Kukutana kwao kwa hakika si kwa kisadfa kama anavyodai Mugogo mwenyewe bali ni njiamaalum inayotolewa na riwaya kwa msomaji ya kuona wasiwasi na hofu zilizofichika katika ung’amuzi bwete wa Mugogo. Tangu mwanzoni mwa riwaya, tayari msomaji ameshamuona Mugogo kama mhusika anayeishi maisha yaliyojaa shauku, hofu na wasiwasi mwingi. Kwa mfano, alikuwa na yakini kuwa aliusikia mlio wa bunduki na kushuhudia kishindo cha vijana waliokimbilia huku na huko ili wazinusuru roho zao. Kisha akawaona vijana waliopigwa risasi nje ya nyumba yake ambao wanatoweka kimiujiza (Ivi: 1). Yote haya yanamfanya atoke kwa azma ya kufanya uchunguzi iwapo aliyoyashuhudia ni ya kweli. Anachohadithiwa huko nje ni tofauti na watu wanamdhania kuwa mwehu.
Anashauriwa apuuze yasiyomhusu kwani hakuna aliyesikia bunduki anazozungumzia Mugogo (Ivi 6). Anaporudi nyumbani kutoka ulevini, ndipo “anapojipumzisha kitandani” (Ivi: 8) ilhali ukweli ni kuwa makali ya sumu aliyokuwa ametiliwa yalikuwa yamekolea na kumfanya apoteze fahamu. Hapo ndipo riwaya inapomdhihirisha Anima kama mhusika ambaye, katika misingi ya Jung, anajitokeza kamanjia mbadala ya kutufunulia wazi wazihofu na wasiwasi aliokuwa nao Mugogo akilini mwake. Mbali na hayo Anima wa Musaleo!, kama alivyo Anima wa Jung, pia ni mwanamke na Mugogo anaelekea kuathirika naye kimapenzi kama anavyolazimishwa akiri hilo na Mamanchi ambaye awali anajitambulisha kama “siri ya Mashamba ya Mawe” (Ivi: 22): inayohodhi vikale ambavyo hujitokeza kwa njia ya ishara na ndoto. Wahusika wake wa kisaikolojia, Anima na Animus, ni vielelezo vya visakale anavyozungumzia na ambavyo vimo katika ung’amuzi jumuishi wa kila binadamu.
“Mugogo, unamjua Anima?” Nitakosaje kumjua mtu kama huyu jamani? Alikuwa rafiki yangu wa kike; mwanamke mwenye ujasiri mkubwa na mapenzi yasiyojua kukimwa. (ibid.) Katika safari yake kwenda katika shamba la mawe, Anima anajitokeza tena – wakati huu katika umbo la mhusika Mamanchi. Katika njozi hii ambayo Mugogo anapata ufumbuzi wa mambo mengi kupitia Mamanchi, Anima sasa si msichana tena bali ni mwanamke mkongwe, mwenye busara na anayejua mambo mengi. Aidha, Mamanchi ana sifa za kiungu, sawa na zile zilizozungumziwa na Jung. Mamanchi, kwa mfano, amezaliwa akafa, akazaliwa akafa, na akazaliwa upya (Ivi: 60). Anamfahamisha Mugogo katika ziara yao ya shamba la mawe hila na vituko vinavyotumiwa na kina ‘Ukolongwe’, jina tunaloweza kulichambua kama kifupi cha ‘ukoloni mkongwe’ na kina Musaleo au viongozi wa siku hizi katika kuendeleza utawala wao wa kiimla. Weledi wa mambo alionao Mamanchi kuhusu vitimvi vya wakoloni wakongwe na wakoloni mamboleo unaelekea kumtanza Mugogo. Mapenzi na ufahamu wa Mamanchi kwake unamkumbusha uhusiano maalum aliokuwa nao na Anima kiasi cha kumfanya Mugogo ashuku kuwa Mamanchi na Anima ni mtu mmoja anapouliza: “Mbona sauti yako inafanana na ya mtu ninayemjua?” Mamanchi: Nani? Anima! Mamanchi: Anima ni mimi pia! Mimi naye ni sawa! (Ivi: 86) Kumbe Anima na Mamanchi ni wamoja ingawa wamejitokeza katika maumbo tofauti: Anima akiwa msichana huku Mamanchi akiwa ajuza. Kinachounganisha umbile lao, hata hivyo, ni msaada mkubwa unaotokana na ukweli na uthabiti wao kwa Mugogo Wehu katika kuuelewa ulimwengu unaoelekea kumtanza.
Kupitia wahusika hawa, Mugogo anatoa harara zake, shida, hofu na kupata mtazamo wa maisha. Mwishoni anaporejelewa na fahamu zake, tunamwona akiwa kiumbe tofauti na vile alivyokuwa hapo awali ingawa hayo yanadokezwa kwa mafumbo na Msimulizi: Ung’amuzi wa mambo wa Mugogo Wehu umepiga hatua kubwa. Macho ambayo alishindwa kuyafungua jana ameyafungua. Ameweza hata kusema mambo kadha. (Ivi: 100) ‘Kufungua’ na ‘kufunga’ macho kunakorejelewa hapa kunahusiana na kule kuzindukana kwa Mugogo Wehu kutoka lindi la kutofahamu (kupoteza kwake fahamu) ambako kulielekea kumtia woga hadi hali ya matumaini (kufungua macho) kama inavyoashiriwa na uwezo wa ‘kusema mambo kadha’.
Hitimisho hili linawafiki uhakiki wa ki-Jung kwa jinsi linavyoagua hofu, wasiwasi na jumla ya mitazamo hasi iliyofichika katika ung’amuzibwete hadi kuleta satua kwa waathiriwa, wakiwemo Mugogo Wehu. Hitimisho Mapitio ya riwaya za Dunia Yao, Nyuso za Mwanamke na Musaleo!yamebainisha wazi kwamba fasihi ni nyenzo mbadala, tena ya kiubunifu, ya kuzizungumzia nadharia za fasihi kwa njia ya ukakamavu zaidi. Uaguzi wa makini wa nadharia za fasihi katika riwaya teule umeziweka kazi hizi katika medani ya kipekee ya kuzungumzia mambo ambayo yangepatikana katika matini mahususi za nadharia za fasihi. Miongoni mwa mambo mengine mengi, riwaya hizi, kwa ustadi, zimeatika mawazo ya wananadharia mbalimbali wa fasihi wakiwemo wanaumaumbo wa Kirusi, wanaumuundo, wanaudenguzi na hata wanasaikolojia changanuzi katika bunilizi za Kiswahili. Wahakiki, walimu na wapenzi wa fasihi wanaweza kuzitumia riwaya husika kama matini za kiziada katika somo la nadharia.
ukakamavu zaidi. Uaguzi wa makini wa nadharia za fasihi katika riwaya teule umeziweka kazi hizi katika medani ya kipekee ya kuzungumzia mambo ambayo yangepatikana katika matini mahususi za nadharia za fasihi. Miongoni mwa mambo mengine mengi, riwaya hizi, kwa ustadi, zimeatika mawazo ya wananadharia mbalimbali wa fasihi wakiwemo wanaumaumbo wa Kirusi, wanaumuundo, wanaudenguzi na hata wanasaikolojia changanuzi katika bunilizi za Kiswahili. Wahakiki, walimu na wapenzi wa fasihi wanaweza kuzitumia riwaya husika kama matini za kiziada katika somo la nadharia.
Marejeleo
  • Barry, Peter. 2002. Beginning Theory. Manchester: Manchester University Press.
  • Baudrillard, Jean. 1983. Simulations. New York: Semiotext(e).
  • Bertoncini, Elena. 2006. Globalization Unmasked in Two Kiswahili Novels. Makala ya Kongamano la Kimataifa la Jubilei ya TUKI – 2005, ed. by Seleman S. Sewangi & Joshua S. Madumulla. Dar es Salaam: TUKI, pp. 84-94.
  • Burman, Erica&Magie MacLure. 2005. Deconstruction as a Method of Research. Research Methods in the Social Sciences, ed. by Bridget Somekh & Cathy Lewin. New Delhi: Vistaar Publications, pp. 284-292.
  • Carter, David. 2006. Literary Theory. Reading: Cox & Wyman.
  • Eagleton, Terry. 1996. Literary Theory: an Introduction. Oxford: Blackwell Publishing.
  • Habib, Rafey M.A. 2005. A History of Literary Criticism. Malden: Blackwell Publishing
  • Khamis, Said A.M. 2003. Fragmentation, Orality and Magic Realism in Kezilahabi’s Novel “Nagona”. Nordic Journal of African Studies 12(1): 78-91.
  • Khamis, Said A.M. 2008. Nadharia, Ubunifu, Uchambuzi na Taaluma ya Kiswahili. Nadharia katika Taaluma ya Kiswahili na Lugha za Kiafrika, ed. by Nathan O. Ogechi, Naomi L. Shitemi & K. Inyani Simala. Eldoret: Moi University Press, pp. 3-23.
  • Lyotard, Jean-François. 1984. The Postmodern Condition. A Report on Knowledge. Trans. Geoff Bennington and Brian Massuni. Minneapolis: University of Minnesota Press.
  • Mohamed, Said Ahmed. 2006. Dunia Yao. Nairobi: Oxford University Press.
  • Mohamed, Said Ahmed. 2010. Nyuso za Mwanamke. Nairobi: Longhorn Publishers.
  • Mwamzandi, Issa Y. 2007. Utandawazi na Teknolojia ya Mawasiliano katika Umalenga wa Waswahili: Mfano wa Sitiari za Taarab. Kiswahili na Elimu Nchini Kenya, ed. by Kimani Njogu. Nairobi: Twaweza Communications, pp. 68-82.
  • Mwamzandi, IssaY. 2011. Derridean Thought in Practice: an Examination of the Kiswahili Proverb. Journal of Intra-African Studies 5: 1-14. Said, Edward. 1978. Orientalism. New York: Pantheon Books.
  • Said, Edward. 1993. Culture and Imperialism. London: Chatto and Windus.
  • Schmitz, Thomas A. 2007. Modern LiteraryTheory and Ancient Texts: an Introduction.
  • Malden: Blackwell Publishing. Tilak, Raghukul. 1993. History and Principles of Literary Criticism. New Delhi:
  • Rama Brothers Educational Publishers. Tyson, Lois. 2006. Critical Theory Today. New York:
  • Routledge & Taylor and Francis. Wafula, Richard & Kimani Njogu. 2007. Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.
  • Waliaula, Ken W. 2010. Uhalisia na Uhalisiamazingaombwe: Mshabaha kati ya Dunia Yao na The Tin Drum. Swahili Forum 17: 143-157.
  • Wamitila, Kyallo W. 2003. Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Books. Wamitila, KyalloW. 2004. Musaleo!. Nairobi: Vide-Muwa.
]]>
<![CDATA[RIWAYA : MARIOO]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1731 Sun, 12 Dec 2021 08:41:48 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1731
.pdf   SURA YA KWANZA.pdf (Size: 170.51 KB / Downloads: 4)



.docx   SURA YA KWANZA.docx (Size: 45.79 KB / Downloads: 0) ]]>

.pdf   SURA YA KWANZA.pdf (Size: 170.51 KB / Downloads: 4)



.docx   SURA YA KWANZA.docx (Size: 45.79 KB / Downloads: 0) ]]>
<![CDATA[TASWIRA KATIKA DIWANI YA FUNGATE YA UHURU]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1505 Sat, 20 Nov 2021 06:38:03 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1505
.pdf   TASWIRA KATIKA FUNGATE YA UHURU.pdf (Size: 2.3 MB / Downloads: 5) ]]>

.pdf   TASWIRA KATIKA FUNGATE YA UHURU.pdf (Size: 2.3 MB / Downloads: 5) ]]>
<![CDATA[USAWIRI WA MHUSIKA PADRI KATIKA RIWAYA ZA KEZILAHABI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1440 Thu, 11 Nov 2021 03:41:08 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1440 Uchunguzi katika Rosa Mistika, Gamba la Nyoka na Nagona
BOFYA HAPA CHINI KUFUNGUA >>>>

.pdf   USAWIRI_WA_MHUSIKA_PADRI_KATIKA_RIWAYA_Z.pdf (Size: 555.1 KB / Downloads: 0)
]]>
Uchunguzi katika Rosa Mistika, Gamba la Nyoka na Nagona
BOFYA HAPA CHINI KUFUNGUA >>>>

.pdf   USAWIRI_WA_MHUSIKA_PADRI_KATIKA_RIWAYA_Z.pdf (Size: 555.1 KB / Downloads: 0)
]]>
<![CDATA[RIWAYA NA HADITHI FUPI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1250 Fri, 17 Sep 2021 03:51:33 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1250 DARASA LA RIWAYA YA KISWAHILI 
Kozi hii itajumuisha saa 3 za kujifunza kwa juma, ambapo saa 2 ni za mhadhara na saa 1 ya semina. Majuma 15 ya ufundishaji pamoja na majuma 2 ya mitihani ya chuo yatatumika kukamilisha ujifunzaji na ufundishaji wa kozi hii.
Maelezo ya msingi juu ya kozi hii
Kozi hii inalenga kutoa taaluma kunt‘u juu ya riwaya ya kiswahili kwa kuangazia chanzo na maendeleo ya riwaya sambamba na ufafanuzi wa vipera vyake. Vilevile inajadili athari zitokanazo na kuwepo kwa riwaya ndani ya jamii, mwisho, inaangazia vijenzi muhimu katika masimulizi ya kubuni.
Malengo ya kozi
Kozi hii itawawezesha wanafunzi kuuchunguza na kuutathmini muundo wa nje na wa ndani wa taaluma nzima ya riwaya ya kiswahili na riwaya zenyewe za kiswahili. 
 MUHTASARI WA KOZI
1.   Nadharia ya riwaya:
· Dhana ya riwaya
· Historia ya chimbuko la riwaya
o   Riwaya na matapo ya fasihi
o   Dhana ya ubunilizi katika riwaya
o   Muundo wa riwaya
o   Mikondo (aina) kuu za riwaya
2.   Riwaya ya kiswahili
·        Maana ya riwaya ya Kiswahili
·        Historia ya riwaya ya Kiswahilio   Kabla ya uhuruo   Baada ya uhuru
o   Kipindi cha kuanzia miaka ya 1980
o   Baada ya kutamalaki kwa zama za sayansi ya teknolojia
·        Maendeleo ya riwaya ya Kiswahili (Sababu za kuibuka, kukua na keenea ama kudumaa kwa riwaya ya Kiswahili).
·        Wanariwaya maarufu wa riwaya ya Kiswahili
3. Mbinu za kifani zinazotumika katika ujenzi wa riwaya za Kiswahili
o   Naratolojia (Usimulizi, mwendo)
o   Msuko wa vitushi na motifu zake
o   Uhusika na wahusika
o   Mtagusano wa kifasihi
o   Matumizi ya lugha
o   Mianzo na miisho ya kifomula
4. Mitazamo na mielekeo inayojichomoza katika riwaya za Kiswahili
o   Dhana ya usomaji wa riwaya za Kiswahili (maana, hadhi matatizo)o   Uhai au ufu wa riwaya za Kiswahilio   Mawazo yaliyotamalaki katika riwaya ya Kiswahili katika mapito yakeo   Masuala mtambuka katika riwaya za Kiswahilio   Tathmini ya mchango wa riwaya ya Kiswahili kwa ustawi wa waswahili
5.  Uhakiki wa riwaya Teule za Kiswahili
o   Dhana ya uhakiki na nadharia za kuhakikia kazi za fasihi
o   Kuchambua riwaya teule za Kiswahili
o   Ulinganuzi na ulinganishi wa vipengele muhimu vya kiuhakiki vijitokezavyo katika       riwaya za Kiswahili
      Riwaya Teule zitakazoshughulikiwa:
o   Nagona
o   Kusadikika
o   Kasiri ya Mwinyi Fuad
o   Mfadhili
o   Barua Ndefu kama hiio   Mirathi ya Hatari
o   Bwana Myombekele na Bibi Bugonoka
o   Hofuo   Pesa zako zinanuka
o   Mzimu wa watu wakale
         Namna ya Ufundishaji: 
Mihadhara na Mijadala.
         Saa za Ufundishaji: 
Jumla ya saa 45, saa 30 za Mihadhara na 15 za  Mijadala.
         Upimaji: 
Alama za Tamrini 40% na Mitihani ya mwisho 60%.
       
MATINI ILIYOTUMIKA 
Nadharia ya Riwaya
Kumekuwa na misuguano kadhaa kutoka kwa wanazuoni waliothubutu kutoa fasili ya riwaya. Imeonekana wazi kuwa kunakukubaliana kwa baadhi ya masuala na kutofautiana pia katika kutoa fasili hii. Miongoni mwa masuala yaliyopelekea misuguano katika utoaji wa fasili hii ni pamoja na:o   Dhima / maudhui ya riwayao   Mipaka ya riwaya pindi inapohusishwa na hadithi fupi au novelao   Ukubwa / urefu wa riwayao   Aina za riwaya
Kuna wengine huchanganya utanzu wa riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari (yaani, vile vitumiavyo lugha ya mjazo) kama vile Hadithi fupi, Novela, Tawasifu na Wasifu.
Hadithi fupi
Tofauti yake na riwaya hujikita katika upeo na uchangamani. Hii inamaana kuwa hadithi fupi huwa sahili sana ilihali riwaya huwa imetanza zaidi.
Novela
Hii huwa ni changamani zaidi kuliko hadithi fupi. Huweza kuwa na visa vingi kiasi kulinganisha na hadithi fupi.
Tawasifu
Ni utungo utumiao lugha ya mjazo ukisimulia habari za mtunzi mwenyewe.
Wasifu
Ni utungo utumiao lugha ya mjazo ambapo mtunzi husimulia habari za mtu mwingine.
Ukichunguza kwa makini vijitanzu hivyo utaona kuwa vinatofautiana na riwaya katika vigezo vya: urefu, uchangamani, idadi ya wahusika, lugha, vitushi, U―Kina, dhamira n.k.
Hivyo, mtu anayetaka kuifasili dhana ya riwaya hupaswa kumakinika katika vipengele hivyo.
Maswali ya msingi
1.  Wanazuoni mbalimbali wametoa fasili ya riwaya. Eleza fasili hizo.
2.   Kwa nini fasili zao zimetofautiana?
3.   Je, wewe unadhani riwaya ni nini?
4.   Eleza tofauti ya riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari.
5. Unadhani tofauti hizo kati ya riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari zinasababishwa na nini?
Sifa bainifu za riwaya
Ilinganishwapo na tanzu nyingine, riwaya huwa nasifa bainifu zifuatazo:
o   Kutokufungwa na sheria nyingi (kinyume na makumbo mengine ya tamthiliya na ushairi).
o   Matumizi ya lugha ya kinathari.
o   Kuwa na mawanda mapana katika urefu na kina.o   Ni zao halisi la kibepari.
o   Kuwa na uhalisi kwa kiasi kikubwa.
o   Mahitaji ya kusoma na kuandika.
o   Kuwepo kwa maisha na makazi yenye utulivu.
o   Kuwa na uwezo wa kugusia hadi vitu vionekanavyo kama vidogo (kwa maelezo       zaidi, tazama. Madumulla, 2009).
Miega ya Riwaya
Mwega ni nguzo au kiunzi kitumikacho kushikilia jambo / kitu. Kama ilivyo kwa kila kazi ya fasihi, riwaya yoyote lazima ijiegemeze katika miega au nguzo tatu muhimu za muktadha, fani na maudhui. Miega hiyo huishikilia vema riwaya katika uundwaji pamoja na utumiwaji (usomaji na uhakiki) wake. Miega yenyewe ni hii ifuatayo:
Muktadha                                                      
Muktadha ni kitu cha lazima katika kila riwaya kwasababu ndiyo huipa uhai riwaya yoyote. Riwaya yoyote hutokana na muktadha fulani au mseto wa miktadha kadhaa. Aghalabu, miega mingi ya fani na maudhui hujengwa kutoka katika nguzo hii. Hivyo, ni lazima riwaya iiakisi miktadha hiyo. Aghalabu, ni nadra sana kukuta riwaya imejikita katika muktadha wa namna moja pekee. Kwa hiyo, riwaya nyingi ni zao la mseto wa miktadha ambayo mtunzi huipitia.
Tanbihi: dhana hii ya muktadha ni vema ikachukuliwa kwa upana wake. Wengi huifinya kwa kuinasibisha na mazingira ya kijiografia (mandhari) pekee! Miktadha yaweza kuwa ya:o   Taarifa za msingi zinazomuhusu mtunzi (kuzaliwa, kazi, elimu n.k)o   Jografia (mandhari) ya maisha na mapitoo   Historia ya mapito yake / jamii yake (matukio muhimu yaliyomgusa yeye au jamii yake)o   Utamadunio   Uchumi n.k.
MAUDHUI
Nayo ni nguzo muhimu sana. Bila maudhui, hakuna riwaya. Hivyo, kila riwaya iliyosanwa vema lazima iwe na mwega huu. Ndani ya maudhui kuna mambo muhimu matatu ambayo ni: ujumbe, dhamira na vipopo vya fikra.
Dhamira
Baadhi ya wataalamu hudai kuwa dhamira muhimu zipo 4: nazo ni: kuburudisha, kuhifadhi amali na historia, kuelimisha na kupambana na maovu / madhila yaikumbayo au yatakayoikumba jamii.
Vipopo vya Fikra
Vipopo vya fikra au vitumba vya mawazo ni mawazo yajengekayo katika akili ya msomaji au mhakiki kutokana na vitushi vya riwaya, aghalabu, hutokana na utambuzi wake binafsi kuhusu mambo mbalimbali au tajiriba. Wengine huviita dhamira ndogo ndogo. Mara nyingine, vipopo vya fikra siyo lazima vijioneshe moja kwa moja riwayani. Bali, msomaji au mhakiki huweza kujiwa navyo tu kadri asomavyo riwaya huku akihusisha na utambuzi wake binafsi au tajiriba.
Ujumbe
Haya ni mavuno ayapatayo msomaji kutokana na dhamira au vipopo vya fikra. Pia, si lazima ujumbe aupatao msomaji au mhakiki ulandane na kile alichokikusudia msanii. Hii ni kwasababu, msomaji au mhakiki huweza kujenga maana ya akisomacho kutokana na kuhusisha na mazoea na utambuzi wake binafsi.
FANI
Huhusisha vipengele vitengenezavyo umbo na sura ya riwaya (mjengeko na ladha ya riwaya). Vipengele hivyo viko katika makundi mawili ya: Muundo na Ubunilizi.
Dhana ya Muundo katika Riwaya
Hii hurejelea mjengo wa kazi yenyewe. Hujumuisha vipengele mbalimbali ambavyo huiweka kazi katika umbo na muundo husika. Muundo wa kazi ya mwandishi wategemea zaidi kanuni asilia za kazi husika pamoja na jamii aiandikiayo. Ili kupata mjengeko autakao katika kazi yake, msanii hutumia mbinu mbalimbali. Mbinu hizo huhusisha vipengele kama vile:
i.      Mtindo                                  
ii.   Lugha
iii.    Vitushi                                  
vi. Migogoro
v.  Udhamira                            
vi. Muwalai
vi.     Wahusika                            
vii Mandhariv.                 
Ushikamani                                                      
Mitindo mbalimbali ya utunzi na uandishi hutokana na athari malimbali za jamii ambayo mtunzi amekulia au vionjo binafsi vya mtunzi.Kipengele kingine katika suala la mtindo ni matumizi ya nafsi. Dhana hii ya matumizi ya nafsi hurejelea matumizi ya midomo ya wahusika katika kufikisha mwazo yake. Waandishi wengi hupendelea nafsi I na ya III. Nafsi II haitumiki kwa sababu humrejelea msomaji. Hivyo, waandishi huepuka kumchoma na kumchusha msomaji. Nafsi I na III zina uhuru wa kuzitumia kwa sababu hujiweka mbali na athari zozote zimwelekeazo msomaji. Suala la nafsi ni muhimu sana katika uandishi. Kwa jumla, mbinu za kimuundo ni kipengele cha lazima cha mwega huu wa fani. Kamwe, hakiwezi kukosekana katika kazi husika na kazi hiyo ikabaki kuwa katika utanzu husika. Kipengele hiki ni tofauti na kipengele cha mbinu za kibunilizi.
Dhana ya Ubunilizi katika RiwayaRiwaya, pamoja na kazi za tanzu nyingine kama vile nudhumu na tamthiliya ni kazi za kibunilizi. Neno Ubunilizi au Ubunifu linatokana na kitenzi buni. Kubuni ni kuunda jambo. Aghalabu, jambo hilo huwa katika hali ya kidhahania kabla halijaonekana au halijadhihirika kwa hadhira kupitia ogani za fahamu. Hivyo, kwa jumla, twaweza kusema kuwa ubunilizi ni uwazaji na uundaji wa wazo katika hali inayohalisika. Dhana ya ubunilizi hutusaidia kutofautisha fasihi na matukio halisi maishani. Fasihi si maisha halisi bali ni tokeo la ubunifu wa mtunzi yaani, mtunzi ana uwezo wa kubuni visa na wahusika wake kwa njia ambayo haikanganyi hali halisi ya maisha. Mambo muhimu yamwezeshayo mtu kutunga kazi bunilizi ni:
o   Silika / karama / kipawa
o   Uwezo wa kiutafiti
o   Uzoefu
o   Mawazo au fikra (taaluma)
o   Nia, lengo au azma
Misingi hii yatudokezea na kutusaidia kujibu swali la msingi tupaswalo kujiuliza tuifikiriapo kazi fulani ya kibunilizi na kuichukulia kuwa bora/nzuri ni: je, kazi hiyo ni tokeo/zao la msingi ya kitaaluma? Au silika (kipawa/karama)? Au tajiriba (uzoefu wa kimaisha)? Au ni tokeo la mseto wa vipengele hivyo vyote? Au ni tokeo la mseto wa baadhi ya vipengele hivyo?
Ubunifu wa riwaya na bunilizi za tanzu nyingine lazima uongozwe na kaida mbalimbali za hali halisi ya maisha. Mtunzi anapaswa kuufanya ulimwengu wake wa kubuni kuwa picha halisi ya maisha katika ukamilifu na ukweli wake. Uhalisia ni ukweli wa jambo kama lilivyo au linavyofahamika. Kuna ukweli wa aina 2 ambazo ni:
o   Ukweli katika hali halisi (uhalisi na uasilia wa jambo/kitu).
o   Ukweli wa kisanaa (husawiri mambo yaliyobuniwa na mtunzi).Hivyo, ubunilizi ni utengenezaji wa ukweli wa jambo kadri afikiriavyo na akusudiavyo msanii. Kwa jumla, msanii hufanya ubunilizi kwa kuzingatia vigezo muhimu vinne. Hivi ni:
o   Kaida za jamii (yake au anayoiandikia)
o   Uwezekano wa utokeaji wa jambo husika
o   Azma au lengo (hisia? ufunuo? kujibu?)
o   Hadhira 
Yafaa ubunilizi usipitilize, kwani ni rahisi kwenda mbali na jamii halisi inayoandikiwa. Hata hivyo, ifahamike kuwa kumtaka mtunzi afuate kaida fulani si kumnyima uhuru wa ubunifu. Kama mtunzi atakanganya hali halisi ya maisha kama mbinu yake ya kutunga, basi na tumpe uhuru huo ilimradi kazi yake twaielewa kwa mtizamo huo. Kazi yoyote ya kisanaa lazima iwe na vipengele muhimu vya aina/makundi mawili. Haya ni: vipengele vya kimuundo na vipengele vya kibunilizi.
Vipengele vya kimuundoHivi ni vile vinavyoifanya kazi husika iwe katika utanzu au kumbo husika. Kila utanzu una aina na namna zake za vipengele vya kimuundo. Vipengele hivyo ndivyo huwa nguzo―msingi zishikiliazo tanzu husika. Kazi fulani hujulikana kuwa ni aina ama shairi, utenzi, utendi, hadithi, fupi, riwaya au tamthiliya kutokana na vipengele hivi. Vipengele vya kimuundo hutegemeana na utanzu husika. Hata hivyo, aghalabu, huhusisha vipengele kama vile: vitushi, uhusika na wahusika, ushikamani, lugha, muwala na mandhari.
Vipengele vya kibuniliziNi jumla ya mambo ambayo mtunzi huyabuni na kuyaingiza au kuyatumia katika kazi zake ili ilete mvuto na mnato kwa hadhira. Mbinu hizi huakisi kipawa cha utunzi alichonacho mtunzi na kumtofautisha na watunzi wengine. Hii ni kwa sababu, kupitia mbinu hizo, kazi hubeba vionjo tofauti (hata kama kazi hizo tofauti zinazungumzia jambo au mada inayofanana, lazima zitatofautiana kutokana na matumizi ya mbinu tofauti za kibunilizi). Vipengele vya kibunilizi vitumiwavyo sana na watunzi wa riwaya za Kiswahili ni:
i.    Taharuki                         
ii. Kisengerenyuma
iii.  Utomeleaji                    
vi.Ufumbaji
v. Ritifaa                           
vi.Usawiri wa wahusikai
vii.  Dayolojia                      
 viii. Utanzia
xi.  Ujadi                                
x.  Ufutuhi
Taharuki Ni hali ya kuwa na dukuduku la kutaka kujua juu ya nini kitafuatia katika usimulizi wa kazi ya fasihi. Mtunzi huijengea hamu hadhira yake ya kutaka kujua zaidi. Mbinu hii hutumiwa sana/hujitokeza sana katika kazi za fasihi pendwa. Hujitokeza pia katika fasihi nenwa. Taharuki, katika kazi za fasihi simulizi hujengwa kwa kutumia:
o   Mabadiliko ya lugha―uso/sura
o   Vipashio vya fonolojia arudhi
o   MatendoNa, katika fasihi andishi, taharuki hujengwa kwa kutumia:
o   Mbinu nyingine za kibunilizi k.v. kisengerenyuma
o   Utumizi wa wahusika wa ajabu―ajabu
o   Mandhari ya ajabuajabu
Kisengerenyuma Ni namna ya kupangilia vitushi au kusimulia kwa kuanza na tukio―tokeo kisha kufuatia tukio―chanzi. Watunzi huitumia kwa namna tofautitofauti. Mbinu hii pia husaidia sana kuboresha hamu ya hadhira kutaka kujua muundo wa vitushi vya kazi husika.
UtomeleajiHujulikana pia kama mwingiliano wa tanzu. Ni kitendo cha kuchopeka/kuingiza vipande vya utanzu mwingine (ulio tofauti na utanzu ushughulikiwao) na katika utanzu mkuu ambao mtunzi anautunga. Kwa mfano, mtunzi wa hadithi fupi huweza kuchopeka mashairi/tenzi au barua katika kazi yake kuu. Utanzu wa nathari huongoza kwa uhuru wa kufanya utomelezi ulinganishwapo na tanzu nyingine. Mbinu hii huwa na tija zifuatazo:
o   Kuonesha umbuji wa tanzu hizo
o   Kuimarisha maudhui
o Kuondoa uchovu kwa wasomaji
o   Kuweka msisitizo
o   Kujikaribisha na uhalisi (senkoro, 2011:70―71).
UfumbajiNi utumiaji wa kauli zenye maana fiche. Kauli hizo huwa na maana iliyo kinyume au tofauti na umbo la nje la kazi au matini husika. Ufumbaji huweza kujitokeza katika: Anuani/mada/kichwa cha habari, majina ya wahusika, Aya, Sura ya kazi, kazi nzima n.k. tija zake ni:
o   Kuonesha umbuji wa kisanaao   Kuishirikisha hadhira kwa karibu
o   Kujitanibu na ghasia za kufuatwa―fuatwa na mkono wa dola.
UjadiHuu ni utumiaji wa kauli, matendo au mazingira ya asili yanayofungamana sana na jamii inayoandikiwa. Aghalabu, ujadi hujumuisha:o   Kauli kama vile methali, nahau, vipengele mbalimbali vya kimazungumzo ambavyo hutumiwa sana na jamii husika.o   Matambikoo   Vyakula asiliao   Watunzi hufanya hivyo ili kujiweka karibu na hadhira yao.o   Yaani, hadhira hujiona iko karibu sana na kazi husika waonapo baadhi ya vipengele vya usimulizi na kiutendaji vya kijadi wavitumiavyo kila siku vimetumiwa katika kazi fulani ya fasihi.
o   Pengine, husaidia kuongeza au kupanua hadhira.
DayalojiaHii ni mbinu ambayo mtunzi hutumia kauli za majibizano katika kuwasilisha mawazo yake. Hutumia vinywa vya wahusika wake kudokeza maudhui ayalengayo. Katika baadhi ya tanzu, dayalojia huwa ni kipengele cha kimuundo (kwa mfano, tamthiliya dayalojia ndiyo kijenzi cha msingi cha utanzu huu husika). Na kwa tanzu nyingine hujitokeza kama kipengele cha kibunilizi. Tija zake ni:
o Huondoa uchovu kwa wasomaji
o Huonesha ufundi wa mtunzi katika matendo, maneno na hadhi ya                                    wahusika.
o Husaidia kuwasilisha mawazo kwa hali ya uasili (mtunzi huwa mbali na                       uwasilishaji, hadhira hupata ladha ya maudhui kutoka kinywa asilia).
Usawiri wa wahusikaNi kitendo cha kuwachora, kuwafafanua, kuwatambulisha na kuwajenga wahusika huku wakipewa maneno, matendo, hadhi na uwezo unaolandana au unaowiana na uhusika wao. Wahusika hutumia mbinu nyingi sana katika kuwasawiri wahusika katika kazi zao. Mbinu hizo ni:
o   Majazi: utoaji wa majina kulingana na sifa, tabia au dhima. Kwa mfano,             Rosa Mistika (katika Rosa Mistika) na Sulubu (katika Nyota ya Rehema).
o   Uzungumzaji nafsi
o   Kuzungumza na hadhirao   Kuwatumia wahusika wengine (Mhusika 1                 kumfafanua mwingine).
o   Ulinganifu wa usambamba
o   Maelezo (mtunzi kumwelezea mhusika)
RitifaaNi hali ambayo mtu mmoja hufanya mawasiliano na mtu aliye mbali naye (umbali huo huweza kuwa wa kijiografia au kufariki). Aghalabu, mawazo yasawiriwayo kupitia mbinu ya ritifaa huwa na vionjo vya kihisia sana. (kila mmoja kwa wakati wake achunguze ujitokeaji wa ritifaa katika riwaya zilizoteuliwa kama zilivyoainishwa kweye muktasari wa kozi hii).
UfutuhiNi mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele mbalimbali vizuavyo ucheshi, raha, kicheko au furaha kwa hadhira yake. Vipengele hivyo huweza kujengwa na kejeli, utani, dhihaka, ubeuzi na mizaha. Miongozi mwa tija zake ni:o   Kufurahisha hadhirao   Kuwaondolea uchovuo   Kujikwepesha na nguvu za dolao   Kulainisha uwasilishaji wa maudhui yanayochoma au yenye hisia kali (utasifida).
UtanziaMbinu hii ni kinyume cha ufutuhi. Ni mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele mbalimbali vizuavyo huzuni, masikitiko, jitimai na mateso kwa hadhira yake. Vipengele hivyo huweza kujengwa na: mateso, ugumu wa maisha, vifungo, mabaa kama vile njaa, gharika, kimbunga, magonjwa na ulemavu (wa viungo au michakato ya mwili kama vile ugumba na utasa).
HISTORIA YA RIWAYA
Riwaya na Matapo ya Fasihi
Matapo ni vipindi mbalimbali vya kihistoria ambavyo fasihi au sanaa kwa jumla imevipitia. Matapo pia huweza kutafsiriwa kuwa ni mkondo au makundi makuu ya kinadharia ambayo yametawala katika fasihi/sanaa katika nyakati maalumu. sanaa/fasihi imepitia katika mikondo mingi sana. Bali ile mikuu ni minne. Nayo ni:
o   Tapo la Urasimi Mkongwe (850 ― 325 K. Y. M)
o   Tapo la Urasimi Mpya (1680 ― 1780 B. Y. M)
o   Tapo la Ulimbwende (1790 ― 1870 B. Y. M)
o   Tapo la Uhalisia (Baada ya utawala wa Malkia Viktoria na Mapinduzi ya viwanda hadi sasa).
Matapo haya yaliingiliana na kukamilisha kwa kiwango kikubwa katika muda wa kuwapo kwake. Hivyo, yawezekana kuwa matapo mawili au zaidi yakatamalaki kwa wakati mmoja.
TAPO LA URASIMI MKONGWE
Dhana ya Urasimi humaanisha mkusanyo wa mikondo ya kifikra au kimtazamo ambayo chanzo chake ni sanaa na utamaduni wa Wayunani na Warumi. Dhana hii ilijiegemeza sana katika usimikwaji wa sheria na taratibu mbalimbali za kuongoza utendekaji wa sanaa/fasihi. Sehemu kubwa ya mawazo yao katika sanaa ilimezwa na nadharia ya MWIGO. waasisi/wadau wakuu wa Urasimi mkongwe ni: Plato na Aristotle
Muhtasari wa Mawazo ya Plato Kuhusu Sanaa
o Uhusiano baina ya uwezo wa mshairi na nguvu za Mungu. Anaamini kuwa msanii ni kiumbe kitakatifu ambach
o hupokea mawazo maalumu/ufunuo kutoka kwa Mungu ili afikishe ujumbe kwa hadhira.
o Uwezo wa msanii hautokani na hekima zake, bali jazba na mpagao utokao kwa Mungu.
o Muigo si chochote, kwani msanii huigiza uhalisia wa maisha ambao hata yeye mwenyewe haujui.
o Alitoa sheria muhimu zilizopaswa kuimiliki sanaa ya utungaji mashairi (wasanii wote walipaswa kuzifuata). Sheria hizo ni:
o Kazi yoyote ya ushairi lazima ipitiwe na kamati maalumu ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 50.
o Watunga mashairi wote lazima watimize miaka 50.
o Ushairi lazima ueleze mazuri tu (kama vile juu ya mashujaa na watawala wa nchi).
o Washairi wasitunge chochote kilicho kinyume cha sheria za Jamhuri. (Rejea kitabu chake, The Laws)
Muhtasari wa Mawazo ya Aristotle juu ya Sanaa
o Kuhusu Ushairi na Tamthiliya (sanaa): Mwigo/uwakilishi ni nadharia bora. Kulingana na Aristotle, mwigo ni kiwakilishi cha maisha (uhalisi), maisha yenyewe halisi. Mwigo hupunguza au kuondoa madhara yatokanayo na woga au hasira.
o Kuhusu Hadhira: Sanaa iwe na hadhira mbili ambazo ni: Hadhira ya watu wa nasaba bora (Tanzia) na Hadhira ya watu wa nasaba duni (Futui). Tanzia: kwa mujibu wa Aristotle, ni masuala tata yenye kusikitisha na kufikirisha. Futuhi: ni masuala mepesi na yanayochekesha. Watu duni wapewe haya kwa vile akili yao haiwezi kuchambua mambo.
o Kuhusu Muundo mahususi: Sehemu za kazi ya sanaa sharti zioane/ziwiane. Kazi ya sanaa iwe na sehemu 3 ambazo ni kichwa, kiwiliwili na miguu. Miundo hii itofautiane kulingana na aina ya kazi (kama ni tanzia au futuhi). Alisisitiza kuwapo kwa nguzo muhimu katika sanaa (tamthiliya). 
Nazo ni:
ü Muundo/msuko
ü Wahusika
ü Nyimbo
ü Wazo kuu (maudhui)
ü Hadhira
ü Lugha bora kulingana na hadhira
oKuhusu Historian na ukweli katika sanaa: Sanaa ni mwigo au kiwakilisho cha ukweli na uhalisia wa maisha ya jamii. Hivyo, mwanasanaa huelezea historia kupitia sanaa. Huweza kuweka mipaka ya historia iliyopita na iliyopo. Pia huweza kuvuka mawanda ya uhalisia uliopita na uliopo. Hivyo akasema Sanaa ni halisi kuliko uhalisi wenyewe. Na ina ukweli zaidi kuliko ukweli wenyewe.
Vigezo vya Jumla vya Tapo la Urasimi
o   Kuwapo kwa fani mahsusi
o   Kuoana kwa fani na lengo/maudhui ya kazi ya sanaa (ulinganifu)
o   Kueleweka kwa kazi ya sanaa (urahisi)
o   Kutiliwa maanani kwa muundo na mpango mahususi
o   Mtindo mahsusio   Kuheshimu jadi
o   Kutotawaliwa na jazba (msanii aitawale jazba).
TAPO LA URASIMI MPYABaadhi ya wadau wake ni: Donne, Market, Herrick, Hrbvert, Cowley, Vongham, Crasha na wengine wengi.
Mambo ya Msingi Kuhusu Tapo hili ni:
o   Lilizingatia kigezo cha Mantiki na Mjadala katika kazi za sanaa (mashairi)
o   Kazi za sanaa lazima ziwe na fumbo litakalomfikirisha msomaji (hadhira)
o   Sanaa lazima iwe kwa ajili ya watu. 
Wadau wa tapo hili walimchukulia binadamu kuwa ni kiumbe mwenye kasoro asotimia; ambaye alitakiwa arekebishwe na kazi za fasihi/sanaa. Hivyo, kufaulu au kushindwa kwa kazi ya fasihi/sanaa kupimwe kulingana na kufaulu au kushindwa kwake kumzingatia/kumtumikia mtu. Yaani, sanaa lazima imfurahishe, imsahihishe na imwelimishe mtu katika maisha yake.
o   Kuwapo kwa Mpango mahsusi katika kazi ya sanaa.
o   Kuzingatiwa kwa sheria za utungaji kulingana na aina ya utanzu.
Athari za Tapo la Urasimi Mpya katika Sanaa ya sasa
o   Uteuzi mahsusi wa maneno na tungo/mishororoo   Umuhimu wa taswira katika ushairio   Matumizi ya akili kuliko jazba (hasa wakati wa utungaji wa kazi za fasihi)
TAPO LA ULIMBWENDELilishamiri barani Ulaya mnamo karne ya 18 hadi 19. Lilitokana na msisimko wa kifasihi, kifalsafa, kidini, kisiasa  na kisanaa kutokana na Urasimi mpya. Wadau maarufu wa Tapo hili ni:
o Uingereza, walikuwa: William Wordsmith na George Grabbe
o Ujerumani, walikuwa: Goethe, Holderline na Schiller
o Ufaransa: Victor Hugo
o Italia: Novalis
Mambo ya Msingi kuhusu Tapo hili:
o  Sifa yake kuu ni uhuru wa msanii. Msanii alipata uhuru wa kuchagua mada, hadhira na lugha kwa matakwa yake. Mambo ya kufikirika kama vile mambo ya ndoto/ruya yalianza kuandikwa.
o Pia wahusika wa ajabuajabu walianza kutumika kwa mfano, shetani na jangili.o   Lilizingatia hisia za ndani pamoja na mazingira ya mzungukayo mtu huyo.
o Tapo hili lilielezea maisha jinsi wao (watunzi) walivyotaka yawe.Kuzuka kwa tapo hili kulichangizwa na kuwapo kwa mambo kadhaa ambayo yalisababisha msisimko na athari za maisha ya wakati huo. Mambo hayo ni:
o  Safari za kuvumbua ulimwengu
o   Harakati za USA kudai uhuru wakati huo
o   Kuzuka kwa miji na viwanda kwa haraka
o   Ulinganishi wa nguvu za kisilaha na kisiasa baina ya mataifa mbalimbali
o   Mivutano na harakati za kitabaka.
Vigezo vya Jumla vya wana―Ulimbwende ni:
o   Kutilia mkazo mazingira na asili
o   Kuandika/kusana kazi mbalimbali zilizowazungumzia wahusika kuanzia utoto waoo   Matumizi ya wahusika wa ajabuajabu kama vile shetani, jangili, wavunja sheria, Malaya n.k.
o Kuruhusu matumizi ya ndoto zilizovuka mipaka ya uhalisi wa maisha. Hii iliruhusiwa ili kurekebisha matumizi ya fani na maudhui katika utunzi.
o Kupinga sheria zilizowekwa na Wanaurasimi: kama vile: Kutenga hadhira, kutenga mitindo ya lugha kulingana na matabaka ya hadhira na kutenga baadhi ya wahusika kulingana na nasaba.
TAPO LA UHALISIA
Uhalisia ni sawa kabisa na udodosi―mambo ambapo huwa na uzingatiaji mkubwa wa uhalisi katika kuwasilisha uhalisi huo katika fasihi. Lilielezea maisha kwa jinsi yalivyo, yaani jambo lilielezwa kwa undani na kweli. Miongoni mwa waasisi wake ni Hegel. Mazingira na wahusika walisawiri kikwelikweli kuyaakisi maisha ya kila siku (kwa kuzingatia furaha, huzuni, matumaini, matazamio na matatizo)Lilishamiri katika karne ya 20. Tapo hili lilijihusisha sana na riwaya. 
Mambo yaliyochochea kuzuka kwa Tapo hili
o   Maendeleo ya sayansi na teknolojia
o   Kuwepo kwa silaha kali na mapigano
o Mivutano au migogoro kati ya matajiri na maskini duniani kote
o  Vuguvugu la nchi nyingine kudai uhuru
Vigezo vya Tapo la Uhalisia
o   Demokrasia katika uumbaji wa fani na maudhui ya kazi ya fasihi
o  Usawiri mwanana wa mambo yanayotokea kila siku katika maisha ya watu.
o   Kuijua kwa kina dhana ya MWIGO. Mwanauhalisia lazima ajue jinsi ya kuiga na akijue akiigacho. Kwa kufanya hivyo, itasaidia nafasi kati ya kiingwacho na mwigo kutokuwa kubwa.
o Kutofungwa na ulazima wa kuwa na mpangilio wala muundo maalum katika kazi za sanaa. Hii ni kwa sababu maisha hayana muundo wala mpangilio maalum.
o Msanii azingatie athari za kazi yake katika hadhira yake.
o Athari hizo zaweza kuletwa na mambo kama vile urahisi (au usahili katika usanaji), umoja kwa moja katika kufafanua maudhui na usahihi wa mambo.
o Kazi yoyote ya fasihi lazima iwe na jukumu la kuadilisha na kufunza.
Aina za uhalisia
1.     Uhalisia wa Kibwanyenye
2.     Uhalisia wa Kihakiki
3.     Uhalisia wa Kijamaa
4.     Uhalisia Ajabu
Uhalisia wa Kibwanyenye
Waandishi wake huandika na kusawiri uozo wakati wa ubwanyenye. Hata hivyo, hawatoi masuluhisho ya kisayansi kuhusu migogoro iliyomo katika jamii.
Uhalisia wa Kihakiki
Mawanda yake hayaivuki jamii husika. Huihakiki jamii hiyo husika tu. Huchambua mambo ya jamii kwa namna moja, kwandani tu au kwa nje tu.
Uhalisia wa Kijamaa
Huchambua mambo ya jamii kutoka ndani na nje ya jamii. Humchambua mhusika kwa kumhusisha na nguvu mbalimbali za kijamii, kiuchumi, kiutamaduni na kisiasa.
Uhalisia Ajabu
Wengine huuita uhalisia mazingaombwe. Huchanganya uhalisia na mambo ya ajabuajabu. Uajabu―ajabu hapa unarejelea matumizi ya wahusika, mandhari na hata vitushi vilivyo nje ya hali ya kawaida. Mfano mmojawapo wa kazi iliyo katika kijitapo hiki ni Baba alipofufuka, utata wa 9/12, Nagona n.k.
]]>
DARASA LA RIWAYA YA KISWAHILI 
Kozi hii itajumuisha saa 3 za kujifunza kwa juma, ambapo saa 2 ni za mhadhara na saa 1 ya semina. Majuma 15 ya ufundishaji pamoja na majuma 2 ya mitihani ya chuo yatatumika kukamilisha ujifunzaji na ufundishaji wa kozi hii.
Maelezo ya msingi juu ya kozi hii
Kozi hii inalenga kutoa taaluma kunt‘u juu ya riwaya ya kiswahili kwa kuangazia chanzo na maendeleo ya riwaya sambamba na ufafanuzi wa vipera vyake. Vilevile inajadili athari zitokanazo na kuwepo kwa riwaya ndani ya jamii, mwisho, inaangazia vijenzi muhimu katika masimulizi ya kubuni.
Malengo ya kozi
Kozi hii itawawezesha wanafunzi kuuchunguza na kuutathmini muundo wa nje na wa ndani wa taaluma nzima ya riwaya ya kiswahili na riwaya zenyewe za kiswahili. 
 MUHTASARI WA KOZI
1.   Nadharia ya riwaya:
· Dhana ya riwaya
· Historia ya chimbuko la riwaya
o   Riwaya na matapo ya fasihi
o   Dhana ya ubunilizi katika riwaya
o   Muundo wa riwaya
o   Mikondo (aina) kuu za riwaya
2.   Riwaya ya kiswahili
·        Maana ya riwaya ya Kiswahili
·        Historia ya riwaya ya Kiswahilio   Kabla ya uhuruo   Baada ya uhuru
o   Kipindi cha kuanzia miaka ya 1980
o   Baada ya kutamalaki kwa zama za sayansi ya teknolojia
·        Maendeleo ya riwaya ya Kiswahili (Sababu za kuibuka, kukua na keenea ama kudumaa kwa riwaya ya Kiswahili).
·        Wanariwaya maarufu wa riwaya ya Kiswahili
3. Mbinu za kifani zinazotumika katika ujenzi wa riwaya za Kiswahili
o   Naratolojia (Usimulizi, mwendo)
o   Msuko wa vitushi na motifu zake
o   Uhusika na wahusika
o   Mtagusano wa kifasihi
o   Matumizi ya lugha
o   Mianzo na miisho ya kifomula
4. Mitazamo na mielekeo inayojichomoza katika riwaya za Kiswahili
o   Dhana ya usomaji wa riwaya za Kiswahili (maana, hadhi matatizo)o   Uhai au ufu wa riwaya za Kiswahilio   Mawazo yaliyotamalaki katika riwaya ya Kiswahili katika mapito yakeo   Masuala mtambuka katika riwaya za Kiswahilio   Tathmini ya mchango wa riwaya ya Kiswahili kwa ustawi wa waswahili
5.  Uhakiki wa riwaya Teule za Kiswahili
o   Dhana ya uhakiki na nadharia za kuhakikia kazi za fasihi
o   Kuchambua riwaya teule za Kiswahili
o   Ulinganuzi na ulinganishi wa vipengele muhimu vya kiuhakiki vijitokezavyo katika       riwaya za Kiswahili
      Riwaya Teule zitakazoshughulikiwa:
o   Nagona
o   Kusadikika
o   Kasiri ya Mwinyi Fuad
o   Mfadhili
o   Barua Ndefu kama hiio   Mirathi ya Hatari
o   Bwana Myombekele na Bibi Bugonoka
o   Hofuo   Pesa zako zinanuka
o   Mzimu wa watu wakale
         Namna ya Ufundishaji: 
Mihadhara na Mijadala.
         Saa za Ufundishaji: 
Jumla ya saa 45, saa 30 za Mihadhara na 15 za  Mijadala.
         Upimaji: 
Alama za Tamrini 40% na Mitihani ya mwisho 60%.
       
MATINI ILIYOTUMIKA 
Nadharia ya Riwaya
Kumekuwa na misuguano kadhaa kutoka kwa wanazuoni waliothubutu kutoa fasili ya riwaya. Imeonekana wazi kuwa kunakukubaliana kwa baadhi ya masuala na kutofautiana pia katika kutoa fasili hii. Miongoni mwa masuala yaliyopelekea misuguano katika utoaji wa fasili hii ni pamoja na:o   Dhima / maudhui ya riwayao   Mipaka ya riwaya pindi inapohusishwa na hadithi fupi au novelao   Ukubwa / urefu wa riwayao   Aina za riwaya
Kuna wengine huchanganya utanzu wa riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari (yaani, vile vitumiavyo lugha ya mjazo) kama vile Hadithi fupi, Novela, Tawasifu na Wasifu.
Hadithi fupi
Tofauti yake na riwaya hujikita katika upeo na uchangamani. Hii inamaana kuwa hadithi fupi huwa sahili sana ilihali riwaya huwa imetanza zaidi.
Novela
Hii huwa ni changamani zaidi kuliko hadithi fupi. Huweza kuwa na visa vingi kiasi kulinganisha na hadithi fupi.
Tawasifu
Ni utungo utumiao lugha ya mjazo ukisimulia habari za mtunzi mwenyewe.
Wasifu
Ni utungo utumiao lugha ya mjazo ambapo mtunzi husimulia habari za mtu mwingine.
Ukichunguza kwa makini vijitanzu hivyo utaona kuwa vinatofautiana na riwaya katika vigezo vya: urefu, uchangamani, idadi ya wahusika, lugha, vitushi, U―Kina, dhamira n.k.
Hivyo, mtu anayetaka kuifasili dhana ya riwaya hupaswa kumakinika katika vipengele hivyo.
Maswali ya msingi
1.  Wanazuoni mbalimbali wametoa fasili ya riwaya. Eleza fasili hizo.
2.   Kwa nini fasili zao zimetofautiana?
3.   Je, wewe unadhani riwaya ni nini?
4.   Eleza tofauti ya riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari.
5. Unadhani tofauti hizo kati ya riwaya na vijitanzu vingine vya kinathari zinasababishwa na nini?
Sifa bainifu za riwaya
Ilinganishwapo na tanzu nyingine, riwaya huwa nasifa bainifu zifuatazo:
o   Kutokufungwa na sheria nyingi (kinyume na makumbo mengine ya tamthiliya na ushairi).
o   Matumizi ya lugha ya kinathari.
o   Kuwa na mawanda mapana katika urefu na kina.o   Ni zao halisi la kibepari.
o   Kuwa na uhalisi kwa kiasi kikubwa.
o   Mahitaji ya kusoma na kuandika.
o   Kuwepo kwa maisha na makazi yenye utulivu.
o   Kuwa na uwezo wa kugusia hadi vitu vionekanavyo kama vidogo (kwa maelezo       zaidi, tazama. Madumulla, 2009).
Miega ya Riwaya
Mwega ni nguzo au kiunzi kitumikacho kushikilia jambo / kitu. Kama ilivyo kwa kila kazi ya fasihi, riwaya yoyote lazima ijiegemeze katika miega au nguzo tatu muhimu za muktadha, fani na maudhui. Miega hiyo huishikilia vema riwaya katika uundwaji pamoja na utumiwaji (usomaji na uhakiki) wake. Miega yenyewe ni hii ifuatayo:
Muktadha                                                      
Muktadha ni kitu cha lazima katika kila riwaya kwasababu ndiyo huipa uhai riwaya yoyote. Riwaya yoyote hutokana na muktadha fulani au mseto wa miktadha kadhaa. Aghalabu, miega mingi ya fani na maudhui hujengwa kutoka katika nguzo hii. Hivyo, ni lazima riwaya iiakisi miktadha hiyo. Aghalabu, ni nadra sana kukuta riwaya imejikita katika muktadha wa namna moja pekee. Kwa hiyo, riwaya nyingi ni zao la mseto wa miktadha ambayo mtunzi huipitia.
Tanbihi: dhana hii ya muktadha ni vema ikachukuliwa kwa upana wake. Wengi huifinya kwa kuinasibisha na mazingira ya kijiografia (mandhari) pekee! Miktadha yaweza kuwa ya:o   Taarifa za msingi zinazomuhusu mtunzi (kuzaliwa, kazi, elimu n.k)o   Jografia (mandhari) ya maisha na mapitoo   Historia ya mapito yake / jamii yake (matukio muhimu yaliyomgusa yeye au jamii yake)o   Utamadunio   Uchumi n.k.
MAUDHUI
Nayo ni nguzo muhimu sana. Bila maudhui, hakuna riwaya. Hivyo, kila riwaya iliyosanwa vema lazima iwe na mwega huu. Ndani ya maudhui kuna mambo muhimu matatu ambayo ni: ujumbe, dhamira na vipopo vya fikra.
Dhamira
Baadhi ya wataalamu hudai kuwa dhamira muhimu zipo 4: nazo ni: kuburudisha, kuhifadhi amali na historia, kuelimisha na kupambana na maovu / madhila yaikumbayo au yatakayoikumba jamii.
Vipopo vya Fikra
Vipopo vya fikra au vitumba vya mawazo ni mawazo yajengekayo katika akili ya msomaji au mhakiki kutokana na vitushi vya riwaya, aghalabu, hutokana na utambuzi wake binafsi kuhusu mambo mbalimbali au tajiriba. Wengine huviita dhamira ndogo ndogo. Mara nyingine, vipopo vya fikra siyo lazima vijioneshe moja kwa moja riwayani. Bali, msomaji au mhakiki huweza kujiwa navyo tu kadri asomavyo riwaya huku akihusisha na utambuzi wake binafsi au tajiriba.
Ujumbe
Haya ni mavuno ayapatayo msomaji kutokana na dhamira au vipopo vya fikra. Pia, si lazima ujumbe aupatao msomaji au mhakiki ulandane na kile alichokikusudia msanii. Hii ni kwasababu, msomaji au mhakiki huweza kujenga maana ya akisomacho kutokana na kuhusisha na mazoea na utambuzi wake binafsi.
FANI
Huhusisha vipengele vitengenezavyo umbo na sura ya riwaya (mjengeko na ladha ya riwaya). Vipengele hivyo viko katika makundi mawili ya: Muundo na Ubunilizi.
Dhana ya Muundo katika Riwaya
Hii hurejelea mjengo wa kazi yenyewe. Hujumuisha vipengele mbalimbali ambavyo huiweka kazi katika umbo na muundo husika. Muundo wa kazi ya mwandishi wategemea zaidi kanuni asilia za kazi husika pamoja na jamii aiandikiayo. Ili kupata mjengeko autakao katika kazi yake, msanii hutumia mbinu mbalimbali. Mbinu hizo huhusisha vipengele kama vile:
i.      Mtindo                                  
ii.   Lugha
iii.    Vitushi                                  
vi. Migogoro
v.  Udhamira                            
vi. Muwalai
vi.     Wahusika                            
vii Mandhariv.                 
Ushikamani                                                      
Mitindo mbalimbali ya utunzi na uandishi hutokana na athari malimbali za jamii ambayo mtunzi amekulia au vionjo binafsi vya mtunzi.Kipengele kingine katika suala la mtindo ni matumizi ya nafsi. Dhana hii ya matumizi ya nafsi hurejelea matumizi ya midomo ya wahusika katika kufikisha mwazo yake. Waandishi wengi hupendelea nafsi I na ya III. Nafsi II haitumiki kwa sababu humrejelea msomaji. Hivyo, waandishi huepuka kumchoma na kumchusha msomaji. Nafsi I na III zina uhuru wa kuzitumia kwa sababu hujiweka mbali na athari zozote zimwelekeazo msomaji. Suala la nafsi ni muhimu sana katika uandishi. Kwa jumla, mbinu za kimuundo ni kipengele cha lazima cha mwega huu wa fani. Kamwe, hakiwezi kukosekana katika kazi husika na kazi hiyo ikabaki kuwa katika utanzu husika. Kipengele hiki ni tofauti na kipengele cha mbinu za kibunilizi.
Dhana ya Ubunilizi katika RiwayaRiwaya, pamoja na kazi za tanzu nyingine kama vile nudhumu na tamthiliya ni kazi za kibunilizi. Neno Ubunilizi au Ubunifu linatokana na kitenzi buni. Kubuni ni kuunda jambo. Aghalabu, jambo hilo huwa katika hali ya kidhahania kabla halijaonekana au halijadhihirika kwa hadhira kupitia ogani za fahamu. Hivyo, kwa jumla, twaweza kusema kuwa ubunilizi ni uwazaji na uundaji wa wazo katika hali inayohalisika. Dhana ya ubunilizi hutusaidia kutofautisha fasihi na matukio halisi maishani. Fasihi si maisha halisi bali ni tokeo la ubunifu wa mtunzi yaani, mtunzi ana uwezo wa kubuni visa na wahusika wake kwa njia ambayo haikanganyi hali halisi ya maisha. Mambo muhimu yamwezeshayo mtu kutunga kazi bunilizi ni:
o   Silika / karama / kipawa
o   Uwezo wa kiutafiti
o   Uzoefu
o   Mawazo au fikra (taaluma)
o   Nia, lengo au azma
Misingi hii yatudokezea na kutusaidia kujibu swali la msingi tupaswalo kujiuliza tuifikiriapo kazi fulani ya kibunilizi na kuichukulia kuwa bora/nzuri ni: je, kazi hiyo ni tokeo/zao la msingi ya kitaaluma? Au silika (kipawa/karama)? Au tajiriba (uzoefu wa kimaisha)? Au ni tokeo la mseto wa vipengele hivyo vyote? Au ni tokeo la mseto wa baadhi ya vipengele hivyo?
Ubunifu wa riwaya na bunilizi za tanzu nyingine lazima uongozwe na kaida mbalimbali za hali halisi ya maisha. Mtunzi anapaswa kuufanya ulimwengu wake wa kubuni kuwa picha halisi ya maisha katika ukamilifu na ukweli wake. Uhalisia ni ukweli wa jambo kama lilivyo au linavyofahamika. Kuna ukweli wa aina 2 ambazo ni:
o   Ukweli katika hali halisi (uhalisi na uasilia wa jambo/kitu).
o   Ukweli wa kisanaa (husawiri mambo yaliyobuniwa na mtunzi).Hivyo, ubunilizi ni utengenezaji wa ukweli wa jambo kadri afikiriavyo na akusudiavyo msanii. Kwa jumla, msanii hufanya ubunilizi kwa kuzingatia vigezo muhimu vinne. Hivi ni:
o   Kaida za jamii (yake au anayoiandikia)
o   Uwezekano wa utokeaji wa jambo husika
o   Azma au lengo (hisia? ufunuo? kujibu?)
o   Hadhira 
Yafaa ubunilizi usipitilize, kwani ni rahisi kwenda mbali na jamii halisi inayoandikiwa. Hata hivyo, ifahamike kuwa kumtaka mtunzi afuate kaida fulani si kumnyima uhuru wa ubunifu. Kama mtunzi atakanganya hali halisi ya maisha kama mbinu yake ya kutunga, basi na tumpe uhuru huo ilimradi kazi yake twaielewa kwa mtizamo huo. Kazi yoyote ya kisanaa lazima iwe na vipengele muhimu vya aina/makundi mawili. Haya ni: vipengele vya kimuundo na vipengele vya kibunilizi.
Vipengele vya kimuundoHivi ni vile vinavyoifanya kazi husika iwe katika utanzu au kumbo husika. Kila utanzu una aina na namna zake za vipengele vya kimuundo. Vipengele hivyo ndivyo huwa nguzo―msingi zishikiliazo tanzu husika. Kazi fulani hujulikana kuwa ni aina ama shairi, utenzi, utendi, hadithi, fupi, riwaya au tamthiliya kutokana na vipengele hivi. Vipengele vya kimuundo hutegemeana na utanzu husika. Hata hivyo, aghalabu, huhusisha vipengele kama vile: vitushi, uhusika na wahusika, ushikamani, lugha, muwala na mandhari.
Vipengele vya kibuniliziNi jumla ya mambo ambayo mtunzi huyabuni na kuyaingiza au kuyatumia katika kazi zake ili ilete mvuto na mnato kwa hadhira. Mbinu hizi huakisi kipawa cha utunzi alichonacho mtunzi na kumtofautisha na watunzi wengine. Hii ni kwa sababu, kupitia mbinu hizo, kazi hubeba vionjo tofauti (hata kama kazi hizo tofauti zinazungumzia jambo au mada inayofanana, lazima zitatofautiana kutokana na matumizi ya mbinu tofauti za kibunilizi). Vipengele vya kibunilizi vitumiwavyo sana na watunzi wa riwaya za Kiswahili ni:
i.    Taharuki                         
ii. Kisengerenyuma
iii.  Utomeleaji                    
vi.Ufumbaji
v. Ritifaa                           
vi.Usawiri wa wahusikai
vii.  Dayolojia                      
 viii. Utanzia
xi.  Ujadi                                
x.  Ufutuhi
Taharuki Ni hali ya kuwa na dukuduku la kutaka kujua juu ya nini kitafuatia katika usimulizi wa kazi ya fasihi. Mtunzi huijengea hamu hadhira yake ya kutaka kujua zaidi. Mbinu hii hutumiwa sana/hujitokeza sana katika kazi za fasihi pendwa. Hujitokeza pia katika fasihi nenwa. Taharuki, katika kazi za fasihi simulizi hujengwa kwa kutumia:
o   Mabadiliko ya lugha―uso/sura
o   Vipashio vya fonolojia arudhi
o   MatendoNa, katika fasihi andishi, taharuki hujengwa kwa kutumia:
o   Mbinu nyingine za kibunilizi k.v. kisengerenyuma
o   Utumizi wa wahusika wa ajabu―ajabu
o   Mandhari ya ajabuajabu
Kisengerenyuma Ni namna ya kupangilia vitushi au kusimulia kwa kuanza na tukio―tokeo kisha kufuatia tukio―chanzi. Watunzi huitumia kwa namna tofautitofauti. Mbinu hii pia husaidia sana kuboresha hamu ya hadhira kutaka kujua muundo wa vitushi vya kazi husika.
UtomeleajiHujulikana pia kama mwingiliano wa tanzu. Ni kitendo cha kuchopeka/kuingiza vipande vya utanzu mwingine (ulio tofauti na utanzu ushughulikiwao) na katika utanzu mkuu ambao mtunzi anautunga. Kwa mfano, mtunzi wa hadithi fupi huweza kuchopeka mashairi/tenzi au barua katika kazi yake kuu. Utanzu wa nathari huongoza kwa uhuru wa kufanya utomelezi ulinganishwapo na tanzu nyingine. Mbinu hii huwa na tija zifuatazo:
o   Kuonesha umbuji wa tanzu hizo
o   Kuimarisha maudhui
o Kuondoa uchovu kwa wasomaji
o   Kuweka msisitizo
o   Kujikaribisha na uhalisi (senkoro, 2011:70―71).
UfumbajiNi utumiaji wa kauli zenye maana fiche. Kauli hizo huwa na maana iliyo kinyume au tofauti na umbo la nje la kazi au matini husika. Ufumbaji huweza kujitokeza katika: Anuani/mada/kichwa cha habari, majina ya wahusika, Aya, Sura ya kazi, kazi nzima n.k. tija zake ni:
o   Kuonesha umbuji wa kisanaao   Kuishirikisha hadhira kwa karibu
o   Kujitanibu na ghasia za kufuatwa―fuatwa na mkono wa dola.
UjadiHuu ni utumiaji wa kauli, matendo au mazingira ya asili yanayofungamana sana na jamii inayoandikiwa. Aghalabu, ujadi hujumuisha:o   Kauli kama vile methali, nahau, vipengele mbalimbali vya kimazungumzo ambavyo hutumiwa sana na jamii husika.o   Matambikoo   Vyakula asiliao   Watunzi hufanya hivyo ili kujiweka karibu na hadhira yao.o   Yaani, hadhira hujiona iko karibu sana na kazi husika waonapo baadhi ya vipengele vya usimulizi na kiutendaji vya kijadi wavitumiavyo kila siku vimetumiwa katika kazi fulani ya fasihi.
o   Pengine, husaidia kuongeza au kupanua hadhira.
DayalojiaHii ni mbinu ambayo mtunzi hutumia kauli za majibizano katika kuwasilisha mawazo yake. Hutumia vinywa vya wahusika wake kudokeza maudhui ayalengayo. Katika baadhi ya tanzu, dayalojia huwa ni kipengele cha kimuundo (kwa mfano, tamthiliya dayalojia ndiyo kijenzi cha msingi cha utanzu huu husika). Na kwa tanzu nyingine hujitokeza kama kipengele cha kibunilizi. Tija zake ni:
o Huondoa uchovu kwa wasomaji
o Huonesha ufundi wa mtunzi katika matendo, maneno na hadhi ya                                    wahusika.
o Husaidia kuwasilisha mawazo kwa hali ya uasili (mtunzi huwa mbali na                       uwasilishaji, hadhira hupata ladha ya maudhui kutoka kinywa asilia).
Usawiri wa wahusikaNi kitendo cha kuwachora, kuwafafanua, kuwatambulisha na kuwajenga wahusika huku wakipewa maneno, matendo, hadhi na uwezo unaolandana au unaowiana na uhusika wao. Wahusika hutumia mbinu nyingi sana katika kuwasawiri wahusika katika kazi zao. Mbinu hizo ni:
o   Majazi: utoaji wa majina kulingana na sifa, tabia au dhima. Kwa mfano,             Rosa Mistika (katika Rosa Mistika) na Sulubu (katika Nyota ya Rehema).
o   Uzungumzaji nafsi
o   Kuzungumza na hadhirao   Kuwatumia wahusika wengine (Mhusika 1                 kumfafanua mwingine).
o   Ulinganifu wa usambamba
o   Maelezo (mtunzi kumwelezea mhusika)
RitifaaNi hali ambayo mtu mmoja hufanya mawasiliano na mtu aliye mbali naye (umbali huo huweza kuwa wa kijiografia au kufariki). Aghalabu, mawazo yasawiriwayo kupitia mbinu ya ritifaa huwa na vionjo vya kihisia sana. (kila mmoja kwa wakati wake achunguze ujitokeaji wa ritifaa katika riwaya zilizoteuliwa kama zilivyoainishwa kweye muktasari wa kozi hii).
UfutuhiNi mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele mbalimbali vizuavyo ucheshi, raha, kicheko au furaha kwa hadhira yake. Vipengele hivyo huweza kujengwa na kejeli, utani, dhihaka, ubeuzi na mizaha. Miongozi mwa tija zake ni:o   Kufurahisha hadhirao   Kuwaondolea uchovuo   Kujikwepesha na nguvu za dolao   Kulainisha uwasilishaji wa maudhui yanayochoma au yenye hisia kali (utasifida).
UtanziaMbinu hii ni kinyume cha ufutuhi. Ni mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele mbalimbali vizuavyo huzuni, masikitiko, jitimai na mateso kwa hadhira yake. Vipengele hivyo huweza kujengwa na: mateso, ugumu wa maisha, vifungo, mabaa kama vile njaa, gharika, kimbunga, magonjwa na ulemavu (wa viungo au michakato ya mwili kama vile ugumba na utasa).
HISTORIA YA RIWAYA
Riwaya na Matapo ya Fasihi
Matapo ni vipindi mbalimbali vya kihistoria ambavyo fasihi au sanaa kwa jumla imevipitia. Matapo pia huweza kutafsiriwa kuwa ni mkondo au makundi makuu ya kinadharia ambayo yametawala katika fasihi/sanaa katika nyakati maalumu. sanaa/fasihi imepitia katika mikondo mingi sana. Bali ile mikuu ni minne. Nayo ni:
o   Tapo la Urasimi Mkongwe (850 ― 325 K. Y. M)
o   Tapo la Urasimi Mpya (1680 ― 1780 B. Y. M)
o   Tapo la Ulimbwende (1790 ― 1870 B. Y. M)
o   Tapo la Uhalisia (Baada ya utawala wa Malkia Viktoria na Mapinduzi ya viwanda hadi sasa).
Matapo haya yaliingiliana na kukamilisha kwa kiwango kikubwa katika muda wa kuwapo kwake. Hivyo, yawezekana kuwa matapo mawili au zaidi yakatamalaki kwa wakati mmoja.
TAPO LA URASIMI MKONGWE
Dhana ya Urasimi humaanisha mkusanyo wa mikondo ya kifikra au kimtazamo ambayo chanzo chake ni sanaa na utamaduni wa Wayunani na Warumi. Dhana hii ilijiegemeza sana katika usimikwaji wa sheria na taratibu mbalimbali za kuongoza utendekaji wa sanaa/fasihi. Sehemu kubwa ya mawazo yao katika sanaa ilimezwa na nadharia ya MWIGO. waasisi/wadau wakuu wa Urasimi mkongwe ni: Plato na Aristotle
Muhtasari wa Mawazo ya Plato Kuhusu Sanaa
o Uhusiano baina ya uwezo wa mshairi na nguvu za Mungu. Anaamini kuwa msanii ni kiumbe kitakatifu ambach
o hupokea mawazo maalumu/ufunuo kutoka kwa Mungu ili afikishe ujumbe kwa hadhira.
o Uwezo wa msanii hautokani na hekima zake, bali jazba na mpagao utokao kwa Mungu.
o Muigo si chochote, kwani msanii huigiza uhalisia wa maisha ambao hata yeye mwenyewe haujui.
o Alitoa sheria muhimu zilizopaswa kuimiliki sanaa ya utungaji mashairi (wasanii wote walipaswa kuzifuata). Sheria hizo ni:
o Kazi yoyote ya ushairi lazima ipitiwe na kamati maalumu ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 50.
o Watunga mashairi wote lazima watimize miaka 50.
o Ushairi lazima ueleze mazuri tu (kama vile juu ya mashujaa na watawala wa nchi).
o Washairi wasitunge chochote kilicho kinyume cha sheria za Jamhuri. (Rejea kitabu chake, The Laws)
Muhtasari wa Mawazo ya Aristotle juu ya Sanaa
o Kuhusu Ushairi na Tamthiliya (sanaa): Mwigo/uwakilishi ni nadharia bora. Kulingana na Aristotle, mwigo ni kiwakilishi cha maisha (uhalisi), maisha yenyewe halisi. Mwigo hupunguza au kuondoa madhara yatokanayo na woga au hasira.
o Kuhusu Hadhira: Sanaa iwe na hadhira mbili ambazo ni: Hadhira ya watu wa nasaba bora (Tanzia) na Hadhira ya watu wa nasaba duni (Futui). Tanzia: kwa mujibu wa Aristotle, ni masuala tata yenye kusikitisha na kufikirisha. Futuhi: ni masuala mepesi na yanayochekesha. Watu duni wapewe haya kwa vile akili yao haiwezi kuchambua mambo.
o Kuhusu Muundo mahususi: Sehemu za kazi ya sanaa sharti zioane/ziwiane. Kazi ya sanaa iwe na sehemu 3 ambazo ni kichwa, kiwiliwili na miguu. Miundo hii itofautiane kulingana na aina ya kazi (kama ni tanzia au futuhi). Alisisitiza kuwapo kwa nguzo muhimu katika sanaa (tamthiliya). 
Nazo ni:
ü Muundo/msuko
ü Wahusika
ü Nyimbo
ü Wazo kuu (maudhui)
ü Hadhira
ü Lugha bora kulingana na hadhira
oKuhusu Historian na ukweli katika sanaa: Sanaa ni mwigo au kiwakilisho cha ukweli na uhalisia wa maisha ya jamii. Hivyo, mwanasanaa huelezea historia kupitia sanaa. Huweza kuweka mipaka ya historia iliyopita na iliyopo. Pia huweza kuvuka mawanda ya uhalisia uliopita na uliopo. Hivyo akasema Sanaa ni halisi kuliko uhalisi wenyewe. Na ina ukweli zaidi kuliko ukweli wenyewe.
Vigezo vya Jumla vya Tapo la Urasimi
o   Kuwapo kwa fani mahsusi
o   Kuoana kwa fani na lengo/maudhui ya kazi ya sanaa (ulinganifu)
o   Kueleweka kwa kazi ya sanaa (urahisi)
o   Kutiliwa maanani kwa muundo na mpango mahususi
o   Mtindo mahsusio   Kuheshimu jadi
o   Kutotawaliwa na jazba (msanii aitawale jazba).
TAPO LA URASIMI MPYABaadhi ya wadau wake ni: Donne, Market, Herrick, Hrbvert, Cowley, Vongham, Crasha na wengine wengi.
Mambo ya Msingi Kuhusu Tapo hili ni:
o   Lilizingatia kigezo cha Mantiki na Mjadala katika kazi za sanaa (mashairi)
o   Kazi za sanaa lazima ziwe na fumbo litakalomfikirisha msomaji (hadhira)
o   Sanaa lazima iwe kwa ajili ya watu. 
Wadau wa tapo hili walimchukulia binadamu kuwa ni kiumbe mwenye kasoro asotimia; ambaye alitakiwa arekebishwe na kazi za fasihi/sanaa. Hivyo, kufaulu au kushindwa kwa kazi ya fasihi/sanaa kupimwe kulingana na kufaulu au kushindwa kwake kumzingatia/kumtumikia mtu. Yaani, sanaa lazima imfurahishe, imsahihishe na imwelimishe mtu katika maisha yake.
o   Kuwapo kwa Mpango mahsusi katika kazi ya sanaa.
o   Kuzingatiwa kwa sheria za utungaji kulingana na aina ya utanzu.
Athari za Tapo la Urasimi Mpya katika Sanaa ya sasa
o   Uteuzi mahsusi wa maneno na tungo/mishororoo   Umuhimu wa taswira katika ushairio   Matumizi ya akili kuliko jazba (hasa wakati wa utungaji wa kazi za fasihi)
TAPO LA ULIMBWENDELilishamiri barani Ulaya mnamo karne ya 18 hadi 19. Lilitokana na msisimko wa kifasihi, kifalsafa, kidini, kisiasa  na kisanaa kutokana na Urasimi mpya. Wadau maarufu wa Tapo hili ni:
o Uingereza, walikuwa: William Wordsmith na George Grabbe
o Ujerumani, walikuwa: Goethe, Holderline na Schiller
o Ufaransa: Victor Hugo
o Italia: Novalis
Mambo ya Msingi kuhusu Tapo hili:
o  Sifa yake kuu ni uhuru wa msanii. Msanii alipata uhuru wa kuchagua mada, hadhira na lugha kwa matakwa yake. Mambo ya kufikirika kama vile mambo ya ndoto/ruya yalianza kuandikwa.
o Pia wahusika wa ajabuajabu walianza kutumika kwa mfano, shetani na jangili.o   Lilizingatia hisia za ndani pamoja na mazingira ya mzungukayo mtu huyo.
o Tapo hili lilielezea maisha jinsi wao (watunzi) walivyotaka yawe.Kuzuka kwa tapo hili kulichangizwa na kuwapo kwa mambo kadhaa ambayo yalisababisha msisimko na athari za maisha ya wakati huo. Mambo hayo ni:
o  Safari za kuvumbua ulimwengu
o   Harakati za USA kudai uhuru wakati huo
o   Kuzuka kwa miji na viwanda kwa haraka
o   Ulinganishi wa nguvu za kisilaha na kisiasa baina ya mataifa mbalimbali
o   Mivutano na harakati za kitabaka.
Vigezo vya Jumla vya wana―Ulimbwende ni:
o   Kutilia mkazo mazingira na asili
o   Kuandika/kusana kazi mbalimbali zilizowazungumzia wahusika kuanzia utoto waoo   Matumizi ya wahusika wa ajabuajabu kama vile shetani, jangili, wavunja sheria, Malaya n.k.
o Kuruhusu matumizi ya ndoto zilizovuka mipaka ya uhalisi wa maisha. Hii iliruhusiwa ili kurekebisha matumizi ya fani na maudhui katika utunzi.
o Kupinga sheria zilizowekwa na Wanaurasimi: kama vile: Kutenga hadhira, kutenga mitindo ya lugha kulingana na matabaka ya hadhira na kutenga baadhi ya wahusika kulingana na nasaba.
TAPO LA UHALISIA
Uhalisia ni sawa kabisa na udodosi―mambo ambapo huwa na uzingatiaji mkubwa wa uhalisi katika kuwasilisha uhalisi huo katika fasihi. Lilielezea maisha kwa jinsi yalivyo, yaani jambo lilielezwa kwa undani na kweli. Miongoni mwa waasisi wake ni Hegel. Mazingira na wahusika walisawiri kikwelikweli kuyaakisi maisha ya kila siku (kwa kuzingatia furaha, huzuni, matumaini, matazamio na matatizo)Lilishamiri katika karne ya 20. Tapo hili lilijihusisha sana na riwaya. 
Mambo yaliyochochea kuzuka kwa Tapo hili
o   Maendeleo ya sayansi na teknolojia
o   Kuwepo kwa silaha kali na mapigano
o Mivutano au migogoro kati ya matajiri na maskini duniani kote
o  Vuguvugu la nchi nyingine kudai uhuru
Vigezo vya Tapo la Uhalisia
o   Demokrasia katika uumbaji wa fani na maudhui ya kazi ya fasihi
o  Usawiri mwanana wa mambo yanayotokea kila siku katika maisha ya watu.
o   Kuijua kwa kina dhana ya MWIGO. Mwanauhalisia lazima ajue jinsi ya kuiga na akijue akiigacho. Kwa kufanya hivyo, itasaidia nafasi kati ya kiingwacho na mwigo kutokuwa kubwa.
o Kutofungwa na ulazima wa kuwa na mpangilio wala muundo maalum katika kazi za sanaa. Hii ni kwa sababu maisha hayana muundo wala mpangilio maalum.
o Msanii azingatie athari za kazi yake katika hadhira yake.
o Athari hizo zaweza kuletwa na mambo kama vile urahisi (au usahili katika usanaji), umoja kwa moja katika kufafanua maudhui na usahihi wa mambo.
o Kazi yoyote ya fasihi lazima iwe na jukumu la kuadilisha na kufunza.
Aina za uhalisia
1.     Uhalisia wa Kibwanyenye
2.     Uhalisia wa Kihakiki
3.     Uhalisia wa Kijamaa
4.     Uhalisia Ajabu
Uhalisia wa Kibwanyenye
Waandishi wake huandika na kusawiri uozo wakati wa ubwanyenye. Hata hivyo, hawatoi masuluhisho ya kisayansi kuhusu migogoro iliyomo katika jamii.
Uhalisia wa Kihakiki
Mawanda yake hayaivuki jamii husika. Huihakiki jamii hiyo husika tu. Huchambua mambo ya jamii kwa namna moja, kwandani tu au kwa nje tu.
Uhalisia wa Kijamaa
Huchambua mambo ya jamii kutoka ndani na nje ya jamii. Humchambua mhusika kwa kumhusisha na nguvu mbalimbali za kijamii, kiuchumi, kiutamaduni na kisiasa.
Uhalisia Ajabu
Wengine huuita uhalisia mazingaombwe. Huchanganya uhalisia na mambo ya ajabuajabu. Uajabu―ajabu hapa unarejelea matumizi ya wahusika, mandhari na hata vitushi vilivyo nje ya hali ya kawaida. Mfano mmojawapo wa kazi iliyo katika kijitapo hiki ni Baba alipofufuka, utata wa 9/12, Nagona n.k.
]]>
<![CDATA[NAFASI YA FASIHI KATIKA KUSAWIRI SUALA LA DINI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1209 Thu, 09 Sep 2021 05:00:47 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1209
.pdf   Nafasi-ya-Fasihi-katika-Kusawiri-suala-la-Dini.pdf (Size: 395.24 KB / Downloads: 2) ]]>

.pdf   Nafasi-ya-Fasihi-katika-Kusawiri-suala-la-Dini.pdf (Size: 395.24 KB / Downloads: 2) ]]>
<![CDATA[Miongozo ya Lugha na Fasihi]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1208 Thu, 09 Sep 2021 04:54:22 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1208 MIONGOZO ya Lugha na Fasihi ni mfululizo uliokusudiwa wanafunzi na wapenzi wa lugha na fasihi ya Kiswahili. Mfululizo huu umebuniwa kutokana na lengo la kuwasaidia wanafunzi wa lugha na fasihi katika ngazi mbalimbali za taaluma zao, hasa wale wanaojiandaa kwa mitihani ya Taifa. Mfululizo huu utatoa vijitabu ambaVyo vitakuwa vinasaidia kuchambua vitabu vya lugha na fasihi ambavyo vimeteuliwa na Wizara ya Elimu vitumike kuwatahini wanafunzi katika vyuo na sekondari nchini. Kwa hali hiyo, mfululizo huu utajumuisha uchambuzi wa vitabu vilivyochapishwa na Dar es Salaam Umvereity Press (DUP) na vile ambavyo vitakuwa vimechapishwa na mashirika raengine.
Uchambuzi wa kila kitabu utazingatia fani na maudhui yanayojitokeza katika kazi hiyo, na mwishoni kuna maswali ambayo yanamwongoza mwanafunzi. Miongozo hii imeandaliwa kwa kuzingatia utaalamu wa hali ya juu ili kurahisisha usomaji wa kitabu kinachohusika. Wanafunzi na wapenzi wa lugha na fasihi watafaidika mno na mfululizo huu. Mhariri mwanzilishi wa mfululizo huu anawatakia usomaji mwema.
Namna ya Kuitumia
Miongozo ya Lugha na Fasihi inaweza kuwa ya manufaa kwa wanafunzi; lakini pia inaweza kuhatarisha juhudi za welewa kwa baadhi ya wanafunzi. Miongozo ya aina hii inapasa iwe kichocheo kwa wanafunzi katika kushiriki hisia na mihemko ya mwandishi iliyoko katika kazi ya fasihi inayohusika. Kutokana na hoja hii, msomaji anatakiwa aione miongozo hii kama kitu kinachosaidia kuimarisha stadi na welewa wake na sio kibadala cha kitabu kinaohohusika.
Wakati wa kusoma miongozo hii mambo muhimu yanayotakiwa kuzingatiwa nipamoja na haya yafuatayo:
Quote:
· Kabla ya kusoma mwongozo wowote ule, inampasa mwanafasihi asome kwanza kazi ya fasihi inayohusika.
· Kilichoandikwa katika mwongozo wowote kisichukuliwe kuwa ni sawa na maandiko matakatifu kama vile Quran Tukufu na Biblia Takatifu. Msomaji una nafasi ya kukubali au kukataa maoni yaliyomo katika mwongozo unaohusika.
· Msomaji una nafasi ya kutoa uchambuzi na uhakiki mpana zaidi kuhusu kitabu kilichohakikiwa.
· Msomaji ihusishe kazi ya fasihi na mazingira ambamo watu walioandikiwa wanayaishi. Jifanye kama yanakukuta utayatatuajie?
Mwishoni mwa mwongozo wowote kuna maswali ambayo yanasaidia kupanua welewa zaidi kwa mwanafunzi na msomaji wa kawaida. Msomaji aghalabu yuko huru kujadili kwa mapana zaidi kazi inayohusika.
I Mwandishi
Penina Muhando ni Profesa na Afisa Mkuu Taaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mchango wake katika fasihi na taaluma ya Kiswahili ni mkubwa – hasa kwa upande watamthiliya.
Katika tamthiliya, ‘mwandishi huyo amepata kutunga Hatia (EAPH), Tambueni Haki Zetu (EAPH), Pambo (F. Books), Nguzo Mama (DUP), Harakati za Ukombozi (na wenzake) (TPH) na huu wa Lina Ubani (DUP). Kazi zote hizo zinajishughulisha sana na maisha ya watanzania kwa ujumla; kuanzia enzi za ukoloni hadi kipindi tulichonacho. Aidha, Lina Vbani ni tamthiliya inayoangalia matatizo yanayomkabili mtanzania wa leo kama tutakavyoangalia katika uchambuzi/uhakiki ufuatao.
II Dhamira Kuu
Maudhui ya Lina Ubani yanaweza kuangaliwa katika nyanja mbali mbali za maisha ya jamii ya kitanzania. Maudhui hayo yanazungukia dhamira muhimu ya ujenzi wa jamii tnpya, artbamo ndani mwake kuna vidhamira vingine vidogo vidogo. Tutazichambua dhamira hizo hapo ehini.
III Maelezo ya Awali na Dhamira Zenyewe
Kwa kipindi cha ‘miaka kadhaa nchi ya Tanzania imekumbwa na msukosuko wa kiuchumi. Kuyumba huko kunatokana na hali halisi kwamba bidhaa zake zimekuwa zile ambazo hupangiwa bei kutoka kwa wanunuzi wake ambao ni mataifa makubwa ya dunia ya kwanza.
Pamoja na hali hiyo, nchi ya Tanzania yenyewe ilipopata uhuru ilidhamiria kujengajamii nlpya anlbayo itakuwa na uhuruwa kweli, haki kwa watu wake, usawa wa binadamu, uchumi kuwa mikononi mwa umma na mengineyo ya aina hiyo. Hali hiyo ilianza kutekelezwa, lakini haikufikia hali nzuri kabisa. Hii ilitokana na kutotekelezwa kwa misingi thabiti iliyotangazwa katika “Azimio la Arusha” ambalo lilikusudiwa lirekebishe hali mbaya iliyokuwepo nchini. Kama kwamba hili halikutosha, hali iliongezewa uduni baada ya nchi hii kushiriki katika vita vya kumng’oa Idi Amini aliyekuwa ameivamia. Tamthiliya ya Lina Ubani inaisimulia vita hiyo kwa kutumia mbinu za kifasihi simulizi na za kisasa, kwani mwandishi anatumia masimulizi ya ngano kuhuSu dude lililowavamia ndege na wanyama katika makazi yao msituni. Baada ya kuvamiwa na dude liitwalo Dyamini, ndege na wanyama hawa walikimbilia kijiji cha jirarii walikowakuta binadamu, nao wakawapokea vizuri. Baadaye binadamu na ndege na wanyama wanashirikiana kupambana na kumfukuza Dyamini, lakini kwa sadaka kubwa ya uchumi na niaisha ya watu. Tunaweza kuchambua mambo yanayojitokeza katika tainthiliya hiyo kania ifuatavyo:
(a) Dhana ya Ukale na Usasa
Tamthiliya hii inatumia mbinu za aina mbili katika usimulizi wake. Kwanza, mwandishi anamtumia mhusica Bibi, ambaye hutamba hadithi ya Dynamini kwa mtoto Mota – ambaye ni mjukuu wake. Kwa kutamba hadithi, mwandishi ameonyesha, mbinu za kifasihi simulizi (ukale), na hivyo kufanya kwa mara ya kwanza pawcpo na jaribio la matumizi ya mbinu za kifasihi simulizi naza kisasa katika tamthiliya moja. Mhusika Bibi anaonyesha dhana yake ya ukale katika masuala mbalimbali; yakiwemo:
(i) Suala la Ndoa
Quote:
Bibi anasema kwamba suala la kuoa bila kufuata ushauri wa wazazi na mababu ni kosa. Mashauri na maelekezo ya wakongwe ni kuwa wanamchagulia mchumba kijana wao, na mara zote wanakuwa wa kabila moja. Bibi analaumu kuwa mtoto wake Huila hakumsikiliza alipomchagulia mchumba na kujiamulia kuoa mwanamke wa Kichusa. Kwa maono ya Bibi, mwanatnke huyu hafai, na mkatili kwa kila hali. Jambo la mtu kujiamulia kuoa anavyopenda linakiuka matakwa ya wazazi katika kabila la Bibi.
(ii) Chakula na Neema Nyingine
Quote:
Bibi anaonyesha pia kuwa neema ya chakula ilikuwa hapo zamani; siyo sasa ambapo anaona mambo yamebadilika. Bibi anamwelezea mjukuu wake Mota kuhusu kijijini kwao Malolo; kabla ya kuhujumiwa na mwanamke Lijino.
…mwanamke yule katufanya kitendo. Wenyewe tulistarehe kule kwetu Malolo. Chakula kila aina. Wewe ulikuwa mdogo sana mlipokuja na mama yako, Malolo, Ndizi! Viazi!! Miwa! mmoja humalizi (uk. 17).
Yawezekana lawama nyingine za Bibi kuhusu chakula kwa Huila na Sara zinatokana na imani ya hali ya maisha aliyoizoea ya kijijini na siyo ile ya mjini.
(iii) Elimu ya Zamani
Quote:
Bibi anaona pia hapo zamani mambo yalikuwa mazuri kwa upande wa elimu. Watoto wake, akiwa Daudi na Huila, walipokuwa wakisoma zamani walikuwa wanaimba na kufurahi sana, siyo kama hawa wa sasa, akina Mota. Nyimbo za sasa, Bibi anazionani kelele tu zisizo na msingi. Anaziona shule za siku hizi kuwa duni, kwani zimejaa kelele za ujamaa! ujamaa! tu.
(iv) Mabadiliko ya Kihistoria
Quote:
Katika hali isiyo ya kawaida tunamwona Bibi akiulizia mabadiliko ya jamii; jambo ambalo katika hali ya kawaida ya ukale wa Bibi tusingelitegemea, Katikatamko hilitunamsikia akisema:
Quote:
…niambiebasi. Zamani sanaulikuwepo utumwa – nasikia walikuwa wanapita kijijini kwetu wanapelekwa pwani. Utumwaukaisha. Ukaja ukoloni, wazungu wakaja kukaa pale kwetu. Halafu ukoloni ukaisha wazungu wakahama. Halafu ukaja uhuru, wakaondoka machifu. Babu Wa baba yako, huyo Daudi akaambiwa yeye si chifu tena. Halafu Uhuru ukaisha. Halafu ndiyo tukasikia Ujamaa! Ujamaa! Huuujamaa Mwalimu anasema utakwisha lini (uk. 27).
Mawazo ya Bibi katika dondoo hili yanaonyesha anatambua nguvu za mabadiliko katika jamii. Lakini pamoja na kutambua mabadiliko hayo, inaelekea Bibi huyo amechanganyikiwa, kwani kuna mawazo ya kukubali mabadiliko na kuna mawazo yanayopinga mabadiliko ya jamii kama tulivyokwishadokeza.
(v) Fasihi Simulizi
Quote:
Jambo jingine linalojitokeza ni lile linalohusu Fasihi Simulizi na imani za utambaji wake. Kuna imani miongoni mwa jamii mbalimbali kuwa utambaji wa hadithi unafanywa usiku na siyo mchana. Jamii hizo zilisisitiza jambo hili kufanyika usiku badala ya mchana kwa sababu muda wa mchana watu walilazimika kujishughulisha na kazi kama vile kilimo na usiku wakati wa mapumziko watambe hadithi. Dhana hii inajitokeza pia katika tamthiliya hiyo.
(b) Ukombozi wa Jamii
Dhamira hii muhimu inajadiliwa pia na mwandishi katika tamthiliya hii. Ukombozi huo tunaweza kuujadili kwa kuzingatia hatua mbili; kwanza, kwa kutumia ngano ya Dynamini aliyeivamia Tanzania, kuna mapambano ya kumwondoa adui huyo. Pili, kuna ukombozi wa Watanzania wenyewe na sualala kuijenga jamii mpya.
(i) Mapambano ya Kumwondoa Mvamizi
Ingawa katika ngano inayojadiliwa, Dyamini ndiye dude vamizi, lakini katika hali halisi, Idi Amini ndiye aliyeivamia Tanzania mwaka 1978. Uvamizi huo wa Amini ulifanywa kwa madai kwamba alikuwa akiwasaka wapinzani “Guerrillas” ambao ilidaiwa walitokea Tanzania. Baada ya uvamizi huo wa Amini, kulifuatiwa na mapambano makali yaliyofanywa kwa hatua.
– Hatua ya Kwanza
Hii ilihusu kupambana ili kupata nafasi ya kujenga daraja ya Kyaka katika mto Nile upya. Baada ya ujenzi huo wa daraja, kulikuwa na kuvuka kwa majeshi na vifaa vya kivita.
– Hatua ya Pili
Kupambana ili kumwondoa kabisa Idi Amini kutoka ardhi ya Tanzania. Hii ilifanyika kwa muda usiopungua majuma mawili.
– Hatua ya Tatu
Mapigano kuhamia Uganda. Haya yalidumu hadi kukombolewa kwa Uganda na Amini kukimbia kabisa.
Pamoja na kuikimbia Uganda, na pamoja na kuwa Tanzania ilikuwa imeshinda vita, kulikuwa na madhara ambayo yalitokana na vita hiyo.
– Upotevu wa Maisha ya Watu
Kulikuwa na vifo vya watu wengi, askari nawananchi. Kulikuwanawengi waliopata vilema vya maisha.’Katika tamthiliya hii tunaambiwa kuwa Daudi, mtoto wa Bibi alikufa vitani, kitendo ambacho yaelekea kiliwehusha akili yake.
– Kutetereka kwa Uchumi
Uchumi wa Tanzania ulitetereka kwa kiasi kikubwa. Inasemekana vita hiyo ilikuwa inatumia T.Shs.7,000,000.00 kwa siku moja na hivyo kudhoofisha kabisa uchumi wa Tanzania ambao ulikuwa tayari umeanza kuimarika kwa wakati huo. Aidha, tatizo la uchumi nchini linatokana pia na hali ya uchumi duniani.
– Wizi wa Fedha za Umma
Kuna methali inayosema “Kufa Kufaana!” Vita hivyo vimeleta tabia ya wizi kwa baadhi ya maofisa wajeshi na hata wa kawaida.
Kwaupandewa maofisawajeshi, baadhi yaowalikuwaamawanaiba fedha, au wanazitumia vibaya fedha walizokuwa wamepewa kwa ajili ya vita.
Pensheni ya wanajeshi waliofia vitani kama vile Daudi wa tamthiliya haikuwafikia, wamekula “wakubwa”. Waliopoteza viungo vyao wakati wa mapigano pia hawakulipwa.
Maofisini, watu mbalimbali walikuwa wameiba fedha kwa kisingizio cha vita.
Kuliibuka matatizo mengi ya kijamii na kiuchumi na kila tatizo ilisemwa ni kwa sababu ya hali ngumu ya kiuchumi iliyokuwa imetokana na vita vya kumwondoa Amini. Kimsingi, hivyo vilikuwa visingizio tu. Kutokana na hali ilivyokuwa, kuna baadhi ya watu wanaona ni afadhali kama Tanzania isingeingia vitani – kwani imeleta hasara zaidi kuliko faida. Lakini Amini angekaa hapa hadi lini?
(ii) Ujemi wa Jamii Mpya
Dhamira hii imekuwa ikijitokeza katika kazi nyingi za kifasihi toka kutangazwa kwa “Azimio la Arusha” ambalo ndilo lilikuwa nguzo ya ujenzi wa jarnii mpya iliyokusudiwa. Jamii mpya kimsingi ilipasa kuzingatia mambo kama vile usawa wa binadamu, haki miongoni mwa watu wajamii, uongozi safi, niakazi bora na chakula cha kutosha. Mwandishi wa tamthiliya ya Lina Ubani amechambua matendo ya wanajumuia na kuyatafiti kwa undani.
– Suala la Haki
Mwandishi anaiona jamii kukosa kuWatendea haki watu kama wanavyostahili. Katika kuilalamikia jamii, mwandishi anatumia mifano mbalimbali, lakini ya msingi hii inayotajwa hapa chini:
I. Kuhamia Vijijini
Miaka ya 1970…; Tanzania iliamua kuwahamishia watu katika vijiji vya maefndeleo. Mipango ya kuwahamishia watu katika vijiji haikutekelezwa vyema. Watu walihamishwa kutoka sehemu nzuri na kuwekwa nyikani kama mhusika Bibi anavyosema; na kulalamikia uamuzi wa Lijino hivi:
Quote:
Basi kaja huyo Lijino huyo! Mfflh! Mwanamke yule! Nasikia ana watoto lakini utafikiri hakuzaa. Mtahama! Amri moja! Kwa hiyari mmekataa. Sasa amri moja. Mmh! Basi kwenda kutuweka nyikani….
Huu ni mfano mmoja wa kunyimwa haki kwa bitiadamu.
II. Kunyimwa Vitu/Vyeo Wasomi
Jambo jingine muhitnu linaloonyesha kukosekana kwa haki kwa watu m kule kuwapa vyeo wasiosoma, na wasomi kuwatUmikia wasiosoma. Imeelezwa kuwa wale waliosoma wanakosa hata gari la kutembelea wakati wale wasibsoma ndio wenye kustarehe. Tazama Bibi anavyosema kuhusu suala hilo:
Quote:
…. Kumbe vyeo wanakuja kupata wasiosoma. Baba yako kasoma, kasoma miaka na miaka. Sasa mie namuuliza, ‘hivyo mwanangu kusoma kote kule hata gari unashindwa kununua?’ Akaniambia eti magari hayaruhusiwi. Mbona barabarani yamejaa?. Eti hayo ni ya wakubwa. Hao wasiosoma hao! Ningejua wanangu wasingesoma. Wamesoma nimepata faida gani? (uk. 33 – 34).
Mwandishi anaichambua jamii ya Tanzania katika uhalisi wakc. Kwa muda mrefu sasa watu ambao elimu yao si ya juu sana, au hata wale wasiosoma kabisa, wamekuwa ndio wanaoteuliwa kuwa viongozi. Wamekuwa wakitembelea magari, na wameruhusiwa kununua magari. Hali hii imekuwa ikikatisha tamaa watu wengi, na hivyo wakati mwinginp kuathiri utendaji kazi wa wasomi mbalimbali.
Katika utendaji kazi, tumeona kuwa wakati mwingine kumekuwa na chuki kati ya wasomi na wasiosoma, na kwa sababu hii; wasiosoma wamekataa kushauriwa nawasomi. Mfano mzuri hapa niwa Zoersi na Huila.
Huila ni mtaalamu na ni msomi wa kiwango chajuu. Kila mara amekuwa akijitahidi kutoa ushauri kwa mwanasiasa mashuhuri, lakini aliyekosa busara na welewa Bwana Zoeni. Zoeni, kama zilivyo tabia za baadhi ya wanasiasa, amekuwa akidharau kabisa mawazo ya mtaalamu Huila. Kisingizio kikubwa cha Zoeni ni kuwa SERA ya CHAMA haiwezi kujadiliwa na wataalamu. Matokeo ya dharau ya watu wa aina hii ni kuanguka kwa uchumi wa nchi na kufanya mikataba ya kuifilisi nchi. Iko mifano kadhaa katika tamthiliya hiyo.
– Zoeni anagongana kimawazo na Huila wakati anapotoa ushauri wa kitaalamu. Zoeni anaona Huila anamfundisha kazi, na hivyc anamfokea:
Quote:
…sihitaji ushauri wako. Kazi yako ni kutekeleza. Sera siyo kazi yako. Ondoka ofisini kwangu… (uk. 25).
– Zoeni anafanya mikataba kwa niaba ya nchi ambayo inahatarisha kabisa uchumi wa nchi. Kwa mfano kuna mikataba inayohusu nishati katika nchi nzima. Kwa sababu ya kutokuwa na upeo mkubwa vva kitaalamu, tunaambiwa Zoeni aliwekeana mikataba na nchi zilizoendei ‘a ili kupata mitambo ya nuklia ambayo haikutakiwa kwa wakati huo nchini. Zoeni anamkebehi mtaalamu na kumdharau, kwa mfano anasema;
Quote:
…. Tujadili sera? Unazungumza nini bwana mtaalamu? Sera inajadiliwa?
…. Ulipokuwa unasomea huo utaalamu hawakukufundisha kuva sera ikishapitishwa haijadiliwi?
…. Ninyiwataalamukwaninimnapendakuchezeaakilizawatu. Pesa zote tunapoteza kusomesha watu, utaalamu wenyewe ndiyo huu… (uk. 24 – 25).
Iko pia miradi mbalimbali inayotekelezwa bila mpango maalumu kama vile kuanzishwa kwa “windmills” katika kila kijiji (jambo ambalo haliwezekani), kushughulikia mti wa ‘Hanga’ unaotoa mafuta ambao Zoeni amepata habari kuwa Philippines kuna mti huo ambao yawezekana upo pia nchini. Bila kufanya tathmini, inaamriwa rnradi uanze mara moja! Hili ni jambo la hatari na linaonyesha hali halisi ambayo imekuwa ikitokea nchini. Miradi mingi imeanzishwa na kufa bila mafanikio kutokana na kutosikiliza maoni na ushauri wa wataalamu wetu. Muda umefika wa kubadilisha hali hii.
– Suala la Makazi Bora
Jamii ya Tanzania ilikusudia kujenga makazi bora kwa wananchi wake, hasa baada ya kutangazwa kwa “Azimio la Arusha”. Ingawa wazo lilikuwa zuri, utekelezaji wake haukuridhisha kwa kiwango kikubwa. Yaelekea vyombo vya dola vilitumia vibaya madaraka yake na hivyo kuwatesa wananchi bila sababu za msingi. Kuna watu waliobomolewa nyumba zao eti kwa sababu zilikuwa nje ya kiwanja kilichopimwa, lakini ilikuwa katika eneo lililotakiwa; kama Bibi anavyolalamika:
Quote:
…Mh! Tuna taabu. Huyo Kibwana Kata! Mmh! Shoga yangu Mama Senga nyumba yake maskini: ‘Bomoa! Haiko kwenye kiwanja’. Tumetutika maji sie! Tukasema: hela Senga kaleta, maji tutashindwa kuteka nyumba ijengwe? Hata! Basi kila kukicha ndoo kichwani. Halafu Kibwana Kata anakuja: ‘Bomoa!’ Tukadhani anatania. Wakabomoa… (uk.12)
Hali hii inaonyesha kwamba watu wengi waliathiriwa na “Operesheni Vijiji” ya miaka ya mapema ya sabini. Wananchi wengi waliteseka. Kuonyesha kwamba kulikuwa na utekelezaji mbaya wa Operesheni hiyo hivi sasa baadhi ya watu waliohamishwa wakati huo wameruhusiwa kurudi kwenye vijiji vyao vya zamani.
– Mipango Mibaya ya Maendeleo
Tumeidokeza dhamira hii pale awali. Lakini pengine hapa tungezungumzia tatizo la mipango mibaya ya maendeleo na utekelezaji wake. Mfano wa maelezo ya jambo hili nl ule wa Talafa aliyegeuzwa shingo “uso ukawa nyuma”. Inasemekana aliwalazimisha wananchi walime pamba ambayo haikuchukuliwa/kununuliwa na serikali kwa vile hapakuwa na daraja la mto uliokitenga kijiji hicho. Mwaka uliofuata inasemekana wananchi waliamua kulima fiwi badala ya pamba. Jambo hili linaonyesha pia mpango mbaya wa utekelezaji wa sera za kiuchumi nchini na kusema kweli matukio ya aina hii nimengimno.
Kuna Ubani
Huo wote ni mvundo ambao si sawa na ule wa “La kuvunda halina ubani”, bali “La kuvunda lina ubani!” Hakuna tatizo hata moja kati ya yaliyosemwa ambayo hayawezi kutatuliwa. Kuna ubani…. Matatizo haya yana dawa. Ni suala la kuamua tu. Mifano michache imeanza kuonekana katika baadhi ya taasisi zetu: Kwa mfano, hivi sasa Waziri wa Mambo ya Ndani anajitahidi kuisafisha jamii. Rais na Waziri Mkuu wamemwunga mkono. Ili kufanikisha jambo hili, ni lazima watanzania wote tumwunge au tuunge mkono juhudi hizo za kuleta “ubani” utakaoondoa “mvundo” kama vile uzembe, wizi, uvivu na ufujaji wa mali ya umma na pia unyimaji wa haki kwa watu.
© Dhamira Nyingine
Pamoja na dhamira hizo tulizoziona, kuna dhamira kadhaa ambazo ingefaa zijadiliwe hapa. Tuziangalie dhamira hizo.
(i) Imani ya Ushirikina na Uchawi
Jamii nyingi zina imani hizo za uchawi na ushirikina. Nchini Tanzania imani hizo pia zipo; na kimsingi zilipata kujitokeza wakati wa “Operesheni Vijiji” ambapo inasemekana baadhi ya watendaji wake walikumbana na matatizo mengi. Uchawi na ushirikina wakati mwingine vimetumika kama nguzo ya wanyonge ya kujitetea dhidi ya tabaka tawala. Hatuna ushahidi wa kufanikiwa kwake, lakini kuendelea kutumiwa kama nguzo na baadhi ya jamii ni dalili kuwa huenda kuna mafanikio.
Katika tamthiliya ya Lina Ubani tunaambiwa kuwa Talafa aliyekuwa msumbufu kwa wanakijiji walioktiwa wamelima fiwi badala ya pamba aligeuzwa shingo, uso umetazama mgongoni! Jambo hili ni la kutisha. Linaweza kubadilisha nia ya afisa yeyote mtendaji ambaye atakwenda kijijini hapo.
(ii) Elimu na Nafasi Yake
Tumetaja hapo awali kuwa Bibi alisifia elimu ya zamani. Lakini hakujadili mchango ama nafasi yake katikajamii.
Tamthiliya hii inaonyesha umuhimu wa elimu katika jamii na hasara zinazoweza kutokea kama elimu haithaminiwi. Kutothaminiwa kwa wasomi wetu kunaweza kuleta madhara makubwa.
Elimu ya jadi pia imedokezwa kwa namna fulani katika tamthiliya hii. Elimu hii inatolewa kwa kizazi kipya kupitia hadithi kama vile Bibi anavyofanya kwa Mota. Elimu zote zinaweza kuwa za manufaa katika jamii zikitumiwa vyema.
(iii) Nafasi ya Mwanamke katika Jamii
Mwanamke katika tamthiliya hii ana nafasi za msingi mbili: mwanamke mzazi na mwanamke mfanyakazi.
– Mwanamke Mzazi
Mwanamke katika kipengele hiki amejengwa akiwa na nafasi yake kama mama watoto. Hapa tunawaona akina mama wawili: Sara akiwa na mtoto wake Mota. Pili kuna Bibi ambaye ana watoto Daudi na Huila. Seti mbili za akina mama na watoto hao zinakamilishwa kwa dhana muhimu ya malezi. Mama, inakubalika na kueleweka kuwa ni mwalimu wa kwanza wa mtoto. Kwa hiyo nafasi yake kama mlezi ni muhimu sana katikajamii. Malezi mema huzaa chema. Malezi mabaya huzaa kibaya. Tumeonyeshwa katika tamthiliya hii mbinu na watu mbalimbali walio muhimu katika malezi, msingi wa kwanza akiwa ni mama.
– Mwanamke Mfanyakazi
Mwanamke huyu ni msomi. Hapa tuna mfano wa Sara na Lijino. Hakuna tatizo kubwa linalojitokeza kwa Sara, lakini tunaambiwa na Bibi juu ya mwanamke Lijino kuwa alikuwa mkatili, kama kwamba hakuzaa. Usemi huu unasisitiza ukatili wa Lijino.
Kutokana na hali hii, tunaweza kusema kuwa tabia haitegemei jinsi-nafsi. Mwanamke ana uwezo sawa tu na mwanaume kama akipewa nafasi inavyotakiwa.
(iv) Mjadala Kuhusu Ushairi
Suala la ushairi wa vina na mizani (kimapokeo) na ule wa masivina linaelekea kujitokeza katika tamthiliya hii. Mota katika tamthiliya hiyo anatunga “ngonjera” ambayo “haina” vina na mizani.
Katika ngonjera yake anawakashifu Madyamini ambao yeye anawaona wako hata sasa:…hapa hapa shuleni, kama yulefulani anakaa deski la mbele, kachukua machungwa ya wenzake… (uk. 55). Hapa dhana ya Madyamini imepanuliwa na kuwa wabaya wote.
(v) Ulevi na Ukweli wa Maisha
Mwanahego ni mtu aliyechorwa kuwa ni mlevi ambaye anaonekana kuwa na akili zake zenye ukweli mtupu. Maneno anayoyasema Mwanahego si ya mlevi, bali ni mtu ambaye ameamua kuserna ukweli, lakini baada ya kujifanya mlevi. Kwa upande mwingine, tukubaliane na hali hii ya ulevi, je, Mwanahego anaelewa juu ya suala la umoja? Anaelewa umuhimu wa fedha za kigeni? Kuna utata.
Ni vyema kuelewa kwamba mlevi mara nyingi hakumbuki anayosema. Mlevi ni tofauti na mnywaji. Tunafikiri Mwanahego ni kipaza sauti cha mwandishi ambaye amedhamiria kuihakiki jamii yake.
Mwisho, tunaweza kusema kuwa hizo ni baadhi tu ya dhamira za Lina Ubani. Wasomaji wana nafasi ya kufanya utafiti zaidi na kugundua dhamira zaidi.
IV Vipengele vya Fani
Fani na maudhui ni pande mbili za sarafu moja. Lazima vitu hivyo viangaliwe katika mchangamano. Lakini hapa tumetenganisha kwa ajili ya majadiliano tu. Majadiliano yatazingatia muundo na mtindo, ujenzi wa wahusika, mazingira au mandhari, na hatimaye matumizi ya lugha.
(a) Muundo na Mtimdo
Tamthiliya hii inatumia mbinu za aina mbili za kimuundo. Mbinu hizo ni za kifasihi simulizi na zile za kidrama ambazo ndizo wasanii wengi wa tamthiliya huzitumia hivi sasa.
Katika kuineemesha, mwandishi anatumia (viingizi vya) nyimbo na maombolezo, ambavyo au huletwa na watambaji wanaounda sehemu ya wahusika na wahusika wengine kama vile Bibi.
Kimtindo, tamthiliya hii inatumia masimulizi ya ngano katika kuelezea ukweli wa namna fulani wa kifasihi. Aidha, kuna mbinu za kisasa za kidrama pia. Hali hii huunda michezo miwili katika mmoja.
Wachezaji muhimu wa mchezo ule wa kifasihi simulizi ni Bibi na Mota, wakisaidiwa na watambaji. Wale wanaotumika katika mchezo wa kidrama ambao ni wa kisasa ni pamoja na Zoeni, Huila na wale watu wa mataifa ya kigeni.
Michezo yote miwili huenda sambamba na kuunganishwa na watambaji. Watambaji katika tamthiliya hii ni muhimu kwani wao wanasaidia kupambanua zaidi dhana muhimu ya ukale na usasa.
Maombolezo katika tamthiliya hii yanaletwa na Bibi (ambaye kwa kweli kwa namna fulani analeta kero). Maombolezo hayo ni mengi, na tunadiriki kusema kuwa hii ni tamthiliya ya kwanza ya aina yake. Haijawahi kutokea tamthiliya ya aina hii, na Profesa Muhando anastahili pongezi.
Suala la matumizi ya nyimbo na ngoma limejitokeza katika tamthiliya hiyo. Wasomaji hufurahia kuisoma lakini wakati huo huo kuwa makini katika kutoa uhakiki wake.
(b) Wahusika
Kama tulivyodokeza sehemu nyingine hapo awali, wahusika ni watu, wanyama, vitu na mahali. Vitu hivi pamoja na viumbe hai vinaweza kutumika katika kazi ya fasihi kwa pamoja, au vinaweza visitumike vyote kwa mara moja. Hapa tutachambua wahusika muhimu tu – wakiwemo Mtambaji, Bibi, Huila, Zoeni, Mota, Daudi, Mwanahego, Lijino, Dyamini na wengineo.
(i) Bibi
Miongoni mwa wahusika muhimu wa tamthiliya hii ni Bibi. Kupitia Bibi, mwandishi anatoa dhamira mbalimbali ambazo zinaihusu jamii nzima. Bibi mwenyewe aghalabu anaonyesha tabia za aina yake pia.
– Ni mlalamishi. Ana uchungu wa kufiwa na mtoto wake kipenzi Daudi.
– Kiungo muhimu katika dhamira ya ukale na usasa. Msisitizo wake wa kutaka mtoto wake achaguliwe mchumba wa kabila lake, kusifia kwa nyimbo za zamani, kutamba hadithi ni miongoni mwa vitu vinavyothibitisha dhana ya ukale na usasa.
– Amechanganyikiwa. Tabia zake katika hadithi ya tamthiliya hii inashindwa kueleweka. Je, ni nini hicho anachodai kiteremke toka, mawinguni? Kuna nyakati tunafikiri labda ni utawala/viongozi u(wa)lio juu na wanalazimishwa kuteremka. Aidha, kuna wakati inajionyesha tabiayawehu.
– Ni mtu asiye na shukrani.
Haridhiki kwa huduma anayopewa na mke wa Huila. Hampendi Sara – anamwita mchawi.
– Ili kuonyesha uzee wake, Bibi amepewa sifa zote za kizee.
– Mhakiki muhimu wa jamii, kwani anazungumzia matatizo ya kuhamia vijijini yaliyotokana na utekelezaji mbaya, matatizo ya ndoa za mseto wa makabila na kadhalika.
(ii) Zoeni
Huyu ni mwanasiasa ambaye kimsingi amepewa tabia nyingi zinazoudhi. Tabia hizo ni kama zifuatazo:
– Ana dharau na hajasoma elimu ya kisasa. Haambiliki.
– Ana kiburi. Yeye ni mhusika muhimu ambaye anakuwa nguzo ya mchezo katika tamthiliya hiyo yenye mbinu za kidrama.
– Mwanasiasa asiye makini. Hajali utaalamu wa wasomi kama vile Huila.
– Ni mpenda rushwa na hongo. Aidha, ni mzembe! Hali hii inajitokeza wakati anapokwenda mkutanoni kuiwakilisha nchi naye analala katika chumba cha mkutano.
– Ni mbadhirifu wa mali ya umma kwa shughuli zake za binafei.
– Hana adabu kwa wafanyakazi wengine. Anawatukana na kuwaaibisha mbelezawatu.
(iii) Huila
Tofauti na mhusika kama Zoeni, Huila ni msomi, ambaye ana tabia zifuatazo:
– Ni mtulivu namvumilivu mkubwa.
– Nimchapa kazi, na ana juhudi kubwa.
– Hakatitamaa upesi.
– Ni mtetezi wahakiza binadamu.
– Ana ushirikiano mkubwanawafanyakaziwenzake.
– Anajalifamilia yake wakati wote.
(iv) Mwanahego
Miongoni mwa wahusika airibao wamechprwa kuwa wazembe, lakini ni muhimu sanani Mwanahego.
– Ni msema ukweli
– Nimcheshi
– Anawahakiki viongozi wazembe katika J’amii.
(v) Sara
Ni mke wa Huila. Anamsaidia sana mume wake katikakumfariji anapokuwa namatatizo.
(vi) Mota
Huyu ni mtoto wa Huila na Sara. Anakuwa kiungo muhimu cha rtiaelezo kuhusu malezi ya kizazi kipya.
– Mota anatumika kuelezea migogoro kati ya ushairi wa mapokeo na masivina.
– Ni mwelezaji wa hali ya ubaya miongoni mwa watu: Kwamba kila mahali kuna wabaya (Madyamini).
– Ni msikivu. Ni mtulivu. Ana akili bora.
(vii) Daudi
Kakake Huila ambaye alifia vitani; wakati wa kumfukuza Dyamini.
(viii) Dyamini
– Mvamizi.
(ix) Watambaji
Wanaisimulia hadithi na kuiunga kati ya hadithi ya kingano na ile ya kisasa.
(x) Wahusika wengine
Lijino, Katibu Kata, Katibu Tarafa na wengine wanasiasa.
© Mazingira/Mandhari
Mazingira ya tamthiliya hii ni ya kitanzania. Ni mazingira ya baada ya Azimio la Arusha na vita ya kumwondoa Idi Amini. Japokuwa hadithi (sehemu kubwa) inasimuliwa kingano, hadithi hiyo inaihusu Tanzania.
(d) Matumizi ya Lugha
Lugha ni chombo cha mawasiliano miongoni mwa jamii. Matumizi ya lugha hutofautisha kazi – kazi ya kisanaa na isiyo ya kisanaa.
Katika tamthiliya hiyo, mwandishi ametumia lugha vyema katika kuwajenga wahusika wake. Tuchambue matumizi yake.
(i) Lugha ya Kikabila
Mwandishi amemjenga mhusika muhimu sana, Bibi, kwa kutumia lugha za aina mbili: lugha ya Kiswahili fasaha na lugha ya kikabila – Kikaguru. Jambo hili limesaidia kwa namna moja katika kuumba hali halisi aliyokuwa nayo Bibi. Lakini pia, tahadhari ni kuwa baadhi ya mambo ambayo hayakutafsiriwa kwa Kiswahili yatashindwa kufikisha ujumbe ipasavyo.
(ii) Lugha za Kigeni
Yako matumizi ya lugha za kigeni, zikiwemo Kifaransa, Kiingereza, Kijerumani n.k. katika kuwajenga wahusika wanaohudhuria mkutano wa kimataifa. Hali hii inaweka mazingira ya tamthiliya iwe karibu na uhalisia wa mambo yanayozungumzwa.
(iii) Kiswahili Fasaha
Lugha hii imetumiwa na msanii pia. Pamoja na lugha hii, kuna pia matumizi ya lugha iliyo sanifu.
(iv) Matumizi yu Methali, Misemo na Nahau,
Mwandishi ametumia misemo na nahau, pamoja na methali pia katika kuimarisha kazi hii. Angalia kwa mfano;
– Penye wema(…) ubaya huzengea (uk. 36)
– La kuvunda lina ubani (uk. 58).
(v) Tamathali za usemi.
Mwandishi ametumia tamathali mbalimbali za usemi. Tamathali hizo ni pamoja na sitiari, tamathali ambayo hulinganisha mambo/vitu viwili au zaidi vyenye sifa tofauti, lakini haitumii maneno ya viungo kama tashbiha. Mfano wasifa tofauti ni huu ambao ni kilio cha Bibi.
Quote:
“Aliyeua Daudi (Kaua jembe langu)”
………
(Kaua kuni zangu)
………
(Kaua nguozangu) (uk.2)
Kwa upande wa tashibiha, hizo nazo zimetumiwa katika tamthiliya hii. Tunamsikia Bibi akisema:
Quote:
….Basi kupaka tu wacha iniwashe. Inachonyota kama upupu Kaja Talafa, Mkali kama pilipili
Tunaweza kupata picha ya sabuni hiyo inayosemekana inachonyota kama upupu. Lazitna iwe sabuni mbaya! Halafu tunamfikiria huyu Katibu Tarafa aliye mkali kama pilipili. Hapana shaka huyu ni mtu mkatili na hana utu wala ubinadamu.
Matumizi ya tamathali za tabaini yapo pia. Tabaini ni mtindo wa uneni wa fasaha ambao kwayo msemaji husisitiza kauli kwa kutumia maneno yenye ukinzani, aghalabu neno si. Tunamsikia Bibi akimlalamikia au kumsema mtoto wake aliyeamua kuolewa na Mchusa aliyemwelezea ukatili wake kuwa alikuwa, “Mbogo si mbogo, Kifaru si kifaru”. Matokeo yake? Inasemekana Melina “akakonda akawa mifupa mitupu”. Kwa mara nyingine tena tabaini hapa imeimarishwa na tamathali ya sitiari.
Kumekuwa na matumizi pia ya tamathali ya kiritifaa. Ritifaa ni mbinu ya aina ya semi ambazo kwazo (i) mtu aliyekufa huombolezwa na kuliliwa kama vile angali hai. (ii) vitu visivyokuwa ulimwenguni kwa sasa, husimuliwa au husifiwa kama viumbe katika hali ya maisha ya duniani. Katika tamthiliya ya Lina Ubani Bibi analia na kaomboleza mara kwa mara kuhusu mtoto wake Daudi. Tena pia tunamsikia akimlaumu Dyamini na kumkashifu kutokana na ubaya wake. Pamoja na tamathali hizo, kuna matumizi machache ya dhihaka na kejeli.
Licha ya tamathali tulizozisema, mwandishi artietumia pia mbinu nyingine za kisanaa. Mbinu hizo kwa mfano ni takriri mbalimbali. Takriri ni mbinu ambayo husisitiza jambo kwa kulirudiarudia. Ziko takriri za aina mbalimbali: takriri-imundo, takriri-neno na kadhalika. Katika tamthiliya hii takriri zinazojitokeza mara nyingi ni zile za maneno. Angalia kWa mfano Mota anavyoyalalamikia Madyamini – ambayo anayaona kuwapo: “Madyamini shule, Madyantini vijijini, Madyamini mijini”. Neno Madyamini limerudiwa ili kusisitiza dhana anayoitaka msanii. Hakika mbinu hizi ni nyingi mno na zinasaidia sana kuimarisha kazi hii. Matumizi ya mdokezo yapo pia kwa wingi. Hii ni tobinu ambayo kwayo mwandishi husema na kukatiza maneno na kumwachia msomaji au msikilizaji ahisi yeye binafsi mwisho wa maneno hayo. Kwa mfano Huila anasikika kwenye simu: “Haloo… Oh! Dr. Matayo…eeee… ndiyo…mama…ee?Vipitena…?eeh? (uk. 57). Maneno hayo yanaonyesha hamu ya kujua nini kipo upande wa pili. Mbinu ya mjalizo imetumika pia. Mbinu hii huunga vifungu vya’maneno kwa kutumia mikato, kwa mfano, kama Huila anavyolalamika kuwa…. “Nimekwenda kote huko! Ugawaji, Usagishaji, Biashara” (uk. 36). Tashtiti, hali ya kuuliza na kushangaa mambo yanayofahamika imetumiwa vyema na mwandishi wa Lina Ubani. Mifano iko mingi. Pamoja na tashtiti kuna pia matumizi ya nidaa. Nidaa m aina au namna ya msemo wa msisimuo au sauti ya mshangao atoayo mtu kudhihirisha maono yake ya ndani au kilio cha moyo wakati apatwapo na mgutusho ghafla wa furaha, hasira, huzuni, chuki na kadhalika. Nidaa imetumiwa sana na mwandishi wa Lina Ubani. Sara, kwa mfano anapomwona Bibi analia na kuendelea kuwa mlalamishi anasema: “Ee Mungu wangu!” (Anatoka) (uk. 32). Msemo huu unaonyesha nidaa. Tamathali na mbinu za kisanaa zimesaidia katika kuijenga taswira pia.
Hizo ni baadhi tu ya mbinu za kisanaa katika tamthiliya hii ya Lina Ubani. Utafiti zaidi unaweza kuzifafanua nyingine.
V Mwisho
Profesa Penina Muhando anlefanya jaribio ambalo halijawahi kufanywa katika uandishi wa tamthiliya za Kiswahili. Jambo hili limefanya tamthiliya hii kuwa na hadhi ya aina yake rta ya kipekee kuliko zile alizopata kuziandika mwenyewe. Aidha, kwa rtsomaji wa kawaida anaweza kujikuta katika matatizo ya kushindwa kuufuatilia vema mchezo huu kutoka mwanzo hadi mwisho. Vinginevyo, hiini kazi bora, tunampongeza Profesa kwa kazi nzuri hii.
VI Maswali
1. Ni kwa vipi dhamira ya kisiasa imejitokeza katika Lina Ubani.
2. Eleza maana ya muundo na mtindo katika kazi ya fasihi. Je, Lina Ubani ina muundo na mtindo gani?
3. Chambua dhamira za Lina Ubani, kishajadili kufanikiwa au kutofanikiwa kwa mwandishi.
4. Jadili wasifu wa wahusika Zoeni, Bibi, Sara na Huila.
]]>
MIONGOZO ya Lugha na Fasihi ni mfululizo uliokusudiwa wanafunzi na wapenzi wa lugha na fasihi ya Kiswahili. Mfululizo huu umebuniwa kutokana na lengo la kuwasaidia wanafunzi wa lugha na fasihi katika ngazi mbalimbali za taaluma zao, hasa wale wanaojiandaa kwa mitihani ya Taifa. Mfululizo huu utatoa vijitabu ambaVyo vitakuwa vinasaidia kuchambua vitabu vya lugha na fasihi ambavyo vimeteuliwa na Wizara ya Elimu vitumike kuwatahini wanafunzi katika vyuo na sekondari nchini. Kwa hali hiyo, mfululizo huu utajumuisha uchambuzi wa vitabu vilivyochapishwa na Dar es Salaam Umvereity Press (DUP) na vile ambavyo vitakuwa vimechapishwa na mashirika raengine.
Uchambuzi wa kila kitabu utazingatia fani na maudhui yanayojitokeza katika kazi hiyo, na mwishoni kuna maswali ambayo yanamwongoza mwanafunzi. Miongozo hii imeandaliwa kwa kuzingatia utaalamu wa hali ya juu ili kurahisisha usomaji wa kitabu kinachohusika. Wanafunzi na wapenzi wa lugha na fasihi watafaidika mno na mfululizo huu. Mhariri mwanzilishi wa mfululizo huu anawatakia usomaji mwema.
Namna ya Kuitumia
Miongozo ya Lugha na Fasihi inaweza kuwa ya manufaa kwa wanafunzi; lakini pia inaweza kuhatarisha juhudi za welewa kwa baadhi ya wanafunzi. Miongozo ya aina hii inapasa iwe kichocheo kwa wanafunzi katika kushiriki hisia na mihemko ya mwandishi iliyoko katika kazi ya fasihi inayohusika. Kutokana na hoja hii, msomaji anatakiwa aione miongozo hii kama kitu kinachosaidia kuimarisha stadi na welewa wake na sio kibadala cha kitabu kinaohohusika.
Wakati wa kusoma miongozo hii mambo muhimu yanayotakiwa kuzingatiwa nipamoja na haya yafuatayo:
Quote:
· Kabla ya kusoma mwongozo wowote ule, inampasa mwanafasihi asome kwanza kazi ya fasihi inayohusika.
· Kilichoandikwa katika mwongozo wowote kisichukuliwe kuwa ni sawa na maandiko matakatifu kama vile Quran Tukufu na Biblia Takatifu. Msomaji una nafasi ya kukubali au kukataa maoni yaliyomo katika mwongozo unaohusika.
· Msomaji una nafasi ya kutoa uchambuzi na uhakiki mpana zaidi kuhusu kitabu kilichohakikiwa.
· Msomaji ihusishe kazi ya fasihi na mazingira ambamo watu walioandikiwa wanayaishi. Jifanye kama yanakukuta utayatatuajie?
Mwishoni mwa mwongozo wowote kuna maswali ambayo yanasaidia kupanua welewa zaidi kwa mwanafunzi na msomaji wa kawaida. Msomaji aghalabu yuko huru kujadili kwa mapana zaidi kazi inayohusika.
I Mwandishi
Penina Muhando ni Profesa na Afisa Mkuu Taaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mchango wake katika fasihi na taaluma ya Kiswahili ni mkubwa – hasa kwa upande watamthiliya.
Katika tamthiliya, ‘mwandishi huyo amepata kutunga Hatia (EAPH), Tambueni Haki Zetu (EAPH), Pambo (F. Books), Nguzo Mama (DUP), Harakati za Ukombozi (na wenzake) (TPH) na huu wa Lina Ubani (DUP). Kazi zote hizo zinajishughulisha sana na maisha ya watanzania kwa ujumla; kuanzia enzi za ukoloni hadi kipindi tulichonacho. Aidha, Lina Vbani ni tamthiliya inayoangalia matatizo yanayomkabili mtanzania wa leo kama tutakavyoangalia katika uchambuzi/uhakiki ufuatao.
II Dhamira Kuu
Maudhui ya Lina Ubani yanaweza kuangaliwa katika nyanja mbali mbali za maisha ya jamii ya kitanzania. Maudhui hayo yanazungukia dhamira muhimu ya ujenzi wa jamii tnpya, artbamo ndani mwake kuna vidhamira vingine vidogo vidogo. Tutazichambua dhamira hizo hapo ehini.
III Maelezo ya Awali na Dhamira Zenyewe
Kwa kipindi cha ‘miaka kadhaa nchi ya Tanzania imekumbwa na msukosuko wa kiuchumi. Kuyumba huko kunatokana na hali halisi kwamba bidhaa zake zimekuwa zile ambazo hupangiwa bei kutoka kwa wanunuzi wake ambao ni mataifa makubwa ya dunia ya kwanza.
Pamoja na hali hiyo, nchi ya Tanzania yenyewe ilipopata uhuru ilidhamiria kujengajamii nlpya anlbayo itakuwa na uhuruwa kweli, haki kwa watu wake, usawa wa binadamu, uchumi kuwa mikononi mwa umma na mengineyo ya aina hiyo. Hali hiyo ilianza kutekelezwa, lakini haikufikia hali nzuri kabisa. Hii ilitokana na kutotekelezwa kwa misingi thabiti iliyotangazwa katika “Azimio la Arusha” ambalo lilikusudiwa lirekebishe hali mbaya iliyokuwepo nchini. Kama kwamba hili halikutosha, hali iliongezewa uduni baada ya nchi hii kushiriki katika vita vya kumng’oa Idi Amini aliyekuwa ameivamia. Tamthiliya ya Lina Ubani inaisimulia vita hiyo kwa kutumia mbinu za kifasihi simulizi na za kisasa, kwani mwandishi anatumia masimulizi ya ngano kuhuSu dude lililowavamia ndege na wanyama katika makazi yao msituni. Baada ya kuvamiwa na dude liitwalo Dyamini, ndege na wanyama hawa walikimbilia kijiji cha jirarii walikowakuta binadamu, nao wakawapokea vizuri. Baadaye binadamu na ndege na wanyama wanashirikiana kupambana na kumfukuza Dyamini, lakini kwa sadaka kubwa ya uchumi na niaisha ya watu. Tunaweza kuchambua mambo yanayojitokeza katika tainthiliya hiyo kania ifuatavyo:
(a) Dhana ya Ukale na Usasa
Tamthiliya hii inatumia mbinu za aina mbili katika usimulizi wake. Kwanza, mwandishi anamtumia mhusica Bibi, ambaye hutamba hadithi ya Dynamini kwa mtoto Mota – ambaye ni mjukuu wake. Kwa kutamba hadithi, mwandishi ameonyesha, mbinu za kifasihi simulizi (ukale), na hivyo kufanya kwa mara ya kwanza pawcpo na jaribio la matumizi ya mbinu za kifasihi simulizi naza kisasa katika tamthiliya moja. Mhusika Bibi anaonyesha dhana yake ya ukale katika masuala mbalimbali; yakiwemo:
(i) Suala la Ndoa
Quote:
Bibi anasema kwamba suala la kuoa bila kufuata ushauri wa wazazi na mababu ni kosa. Mashauri na maelekezo ya wakongwe ni kuwa wanamchagulia mchumba kijana wao, na mara zote wanakuwa wa kabila moja. Bibi analaumu kuwa mtoto wake Huila hakumsikiliza alipomchagulia mchumba na kujiamulia kuoa mwanamke wa Kichusa. Kwa maono ya Bibi, mwanatnke huyu hafai, na mkatili kwa kila hali. Jambo la mtu kujiamulia kuoa anavyopenda linakiuka matakwa ya wazazi katika kabila la Bibi.
(ii) Chakula na Neema Nyingine
Quote:
Bibi anaonyesha pia kuwa neema ya chakula ilikuwa hapo zamani; siyo sasa ambapo anaona mambo yamebadilika. Bibi anamwelezea mjukuu wake Mota kuhusu kijijini kwao Malolo; kabla ya kuhujumiwa na mwanamke Lijino.
…mwanamke yule katufanya kitendo. Wenyewe tulistarehe kule kwetu Malolo. Chakula kila aina. Wewe ulikuwa mdogo sana mlipokuja na mama yako, Malolo, Ndizi! Viazi!! Miwa! mmoja humalizi (uk. 17).
Yawezekana lawama nyingine za Bibi kuhusu chakula kwa Huila na Sara zinatokana na imani ya hali ya maisha aliyoizoea ya kijijini na siyo ile ya mjini.
(iii) Elimu ya Zamani
Quote:
Bibi anaona pia hapo zamani mambo yalikuwa mazuri kwa upande wa elimu. Watoto wake, akiwa Daudi na Huila, walipokuwa wakisoma zamani walikuwa wanaimba na kufurahi sana, siyo kama hawa wa sasa, akina Mota. Nyimbo za sasa, Bibi anazionani kelele tu zisizo na msingi. Anaziona shule za siku hizi kuwa duni, kwani zimejaa kelele za ujamaa! ujamaa! tu.
(iv) Mabadiliko ya Kihistoria
Quote:
Katika hali isiyo ya kawaida tunamwona Bibi akiulizia mabadiliko ya jamii; jambo ambalo katika hali ya kawaida ya ukale wa Bibi tusingelitegemea, Katikatamko hilitunamsikia akisema:
Quote:
…niambiebasi. Zamani sanaulikuwepo utumwa – nasikia walikuwa wanapita kijijini kwetu wanapelekwa pwani. Utumwaukaisha. Ukaja ukoloni, wazungu wakaja kukaa pale kwetu. Halafu ukoloni ukaisha wazungu wakahama. Halafu ukaja uhuru, wakaondoka machifu. Babu Wa baba yako, huyo Daudi akaambiwa yeye si chifu tena. Halafu Uhuru ukaisha. Halafu ndiyo tukasikia Ujamaa! Ujamaa! Huuujamaa Mwalimu anasema utakwisha lini (uk. 27).
Mawazo ya Bibi katika dondoo hili yanaonyesha anatambua nguvu za mabadiliko katika jamii. Lakini pamoja na kutambua mabadiliko hayo, inaelekea Bibi huyo amechanganyikiwa, kwani kuna mawazo ya kukubali mabadiliko na kuna mawazo yanayopinga mabadiliko ya jamii kama tulivyokwishadokeza.
(v) Fasihi Simulizi
Quote:
Jambo jingine linalojitokeza ni lile linalohusu Fasihi Simulizi na imani za utambaji wake. Kuna imani miongoni mwa jamii mbalimbali kuwa utambaji wa hadithi unafanywa usiku na siyo mchana. Jamii hizo zilisisitiza jambo hili kufanyika usiku badala ya mchana kwa sababu muda wa mchana watu walilazimika kujishughulisha na kazi kama vile kilimo na usiku wakati wa mapumziko watambe hadithi. Dhana hii inajitokeza pia katika tamthiliya hiyo.
(b) Ukombozi wa Jamii
Dhamira hii muhimu inajadiliwa pia na mwandishi katika tamthiliya hii. Ukombozi huo tunaweza kuujadili kwa kuzingatia hatua mbili; kwanza, kwa kutumia ngano ya Dynamini aliyeivamia Tanzania, kuna mapambano ya kumwondoa adui huyo. Pili, kuna ukombozi wa Watanzania wenyewe na sualala kuijenga jamii mpya.
(i) Mapambano ya Kumwondoa Mvamizi
Ingawa katika ngano inayojadiliwa, Dyamini ndiye dude vamizi, lakini katika hali halisi, Idi Amini ndiye aliyeivamia Tanzania mwaka 1978. Uvamizi huo wa Amini ulifanywa kwa madai kwamba alikuwa akiwasaka wapinzani “Guerrillas” ambao ilidaiwa walitokea Tanzania. Baada ya uvamizi huo wa Amini, kulifuatiwa na mapambano makali yaliyofanywa kwa hatua.
– Hatua ya Kwanza
Hii ilihusu kupambana ili kupata nafasi ya kujenga daraja ya Kyaka katika mto Nile upya. Baada ya ujenzi huo wa daraja, kulikuwa na kuvuka kwa majeshi na vifaa vya kivita.
– Hatua ya Pili
Kupambana ili kumwondoa kabisa Idi Amini kutoka ardhi ya Tanzania. Hii ilifanyika kwa muda usiopungua majuma mawili.
– Hatua ya Tatu
Mapigano kuhamia Uganda. Haya yalidumu hadi kukombolewa kwa Uganda na Amini kukimbia kabisa.
Pamoja na kuikimbia Uganda, na pamoja na kuwa Tanzania ilikuwa imeshinda vita, kulikuwa na madhara ambayo yalitokana na vita hiyo.
– Upotevu wa Maisha ya Watu
Kulikuwa na vifo vya watu wengi, askari nawananchi. Kulikuwanawengi waliopata vilema vya maisha.’Katika tamthiliya hii tunaambiwa kuwa Daudi, mtoto wa Bibi alikufa vitani, kitendo ambacho yaelekea kiliwehusha akili yake.
– Kutetereka kwa Uchumi
Uchumi wa Tanzania ulitetereka kwa kiasi kikubwa. Inasemekana vita hiyo ilikuwa inatumia T.Shs.7,000,000.00 kwa siku moja na hivyo kudhoofisha kabisa uchumi wa Tanzania ambao ulikuwa tayari umeanza kuimarika kwa wakati huo. Aidha, tatizo la uchumi nchini linatokana pia na hali ya uchumi duniani.
– Wizi wa Fedha za Umma
Kuna methali inayosema “Kufa Kufaana!” Vita hivyo vimeleta tabia ya wizi kwa baadhi ya maofisa wajeshi na hata wa kawaida.
Kwaupandewa maofisawajeshi, baadhi yaowalikuwaamawanaiba fedha, au wanazitumia vibaya fedha walizokuwa wamepewa kwa ajili ya vita.
Pensheni ya wanajeshi waliofia vitani kama vile Daudi wa tamthiliya haikuwafikia, wamekula “wakubwa”. Waliopoteza viungo vyao wakati wa mapigano pia hawakulipwa.
Maofisini, watu mbalimbali walikuwa wameiba fedha kwa kisingizio cha vita.
Kuliibuka matatizo mengi ya kijamii na kiuchumi na kila tatizo ilisemwa ni kwa sababu ya hali ngumu ya kiuchumi iliyokuwa imetokana na vita vya kumwondoa Amini. Kimsingi, hivyo vilikuwa visingizio tu. Kutokana na hali ilivyokuwa, kuna baadhi ya watu wanaona ni afadhali kama Tanzania isingeingia vitani – kwani imeleta hasara zaidi kuliko faida. Lakini Amini angekaa hapa hadi lini?
(ii) Ujemi wa Jamii Mpya
Dhamira hii imekuwa ikijitokeza katika kazi nyingi za kifasihi toka kutangazwa kwa “Azimio la Arusha” ambalo ndilo lilikuwa nguzo ya ujenzi wa jarnii mpya iliyokusudiwa. Jamii mpya kimsingi ilipasa kuzingatia mambo kama vile usawa wa binadamu, haki miongoni mwa watu wajamii, uongozi safi, niakazi bora na chakula cha kutosha. Mwandishi wa tamthiliya ya Lina Ubani amechambua matendo ya wanajumuia na kuyatafiti kwa undani.
– Suala la Haki
Mwandishi anaiona jamii kukosa kuWatendea haki watu kama wanavyostahili. Katika kuilalamikia jamii, mwandishi anatumia mifano mbalimbali, lakini ya msingi hii inayotajwa hapa chini:
I. Kuhamia Vijijini
Miaka ya 1970…; Tanzania iliamua kuwahamishia watu katika vijiji vya maefndeleo. Mipango ya kuwahamishia watu katika vijiji haikutekelezwa vyema. Watu walihamishwa kutoka sehemu nzuri na kuwekwa nyikani kama mhusika Bibi anavyosema; na kulalamikia uamuzi wa Lijino hivi:
Quote:
Basi kaja huyo Lijino huyo! Mfflh! Mwanamke yule! Nasikia ana watoto lakini utafikiri hakuzaa. Mtahama! Amri moja! Kwa hiyari mmekataa. Sasa amri moja. Mmh! Basi kwenda kutuweka nyikani….
Huu ni mfano mmoja wa kunyimwa haki kwa bitiadamu.
II. Kunyimwa Vitu/Vyeo Wasomi
Jambo jingine muhitnu linaloonyesha kukosekana kwa haki kwa watu m kule kuwapa vyeo wasiosoma, na wasomi kuwatUmikia wasiosoma. Imeelezwa kuwa wale waliosoma wanakosa hata gari la kutembelea wakati wale wasibsoma ndio wenye kustarehe. Tazama Bibi anavyosema kuhusu suala hilo:
Quote:
…. Kumbe vyeo wanakuja kupata wasiosoma. Baba yako kasoma, kasoma miaka na miaka. Sasa mie namuuliza, ‘hivyo mwanangu kusoma kote kule hata gari unashindwa kununua?’ Akaniambia eti magari hayaruhusiwi. Mbona barabarani yamejaa?. Eti hayo ni ya wakubwa. Hao wasiosoma hao! Ningejua wanangu wasingesoma. Wamesoma nimepata faida gani? (uk. 33 – 34).
Mwandishi anaichambua jamii ya Tanzania katika uhalisi wakc. Kwa muda mrefu sasa watu ambao elimu yao si ya juu sana, au hata wale wasiosoma kabisa, wamekuwa ndio wanaoteuliwa kuwa viongozi. Wamekuwa wakitembelea magari, na wameruhusiwa kununua magari. Hali hii imekuwa ikikatisha tamaa watu wengi, na hivyo wakati mwinginp kuathiri utendaji kazi wa wasomi mbalimbali.
Katika utendaji kazi, tumeona kuwa wakati mwingine kumekuwa na chuki kati ya wasomi na wasiosoma, na kwa sababu hii; wasiosoma wamekataa kushauriwa nawasomi. Mfano mzuri hapa niwa Zoersi na Huila.
Huila ni mtaalamu na ni msomi wa kiwango chajuu. Kila mara amekuwa akijitahidi kutoa ushauri kwa mwanasiasa mashuhuri, lakini aliyekosa busara na welewa Bwana Zoeni. Zoeni, kama zilivyo tabia za baadhi ya wanasiasa, amekuwa akidharau kabisa mawazo ya mtaalamu Huila. Kisingizio kikubwa cha Zoeni ni kuwa SERA ya CHAMA haiwezi kujadiliwa na wataalamu. Matokeo ya dharau ya watu wa aina hii ni kuanguka kwa uchumi wa nchi na kufanya mikataba ya kuifilisi nchi. Iko mifano kadhaa katika tamthiliya hiyo.
– Zoeni anagongana kimawazo na Huila wakati anapotoa ushauri wa kitaalamu. Zoeni anaona Huila anamfundisha kazi, na hivyc anamfokea:
Quote:
…sihitaji ushauri wako. Kazi yako ni kutekeleza. Sera siyo kazi yako. Ondoka ofisini kwangu… (uk. 25).
– Zoeni anafanya mikataba kwa niaba ya nchi ambayo inahatarisha kabisa uchumi wa nchi. Kwa mfano kuna mikataba inayohusu nishati katika nchi nzima. Kwa sababu ya kutokuwa na upeo mkubwa vva kitaalamu, tunaambiwa Zoeni aliwekeana mikataba na nchi zilizoendei ‘a ili kupata mitambo ya nuklia ambayo haikutakiwa kwa wakati huo nchini. Zoeni anamkebehi mtaalamu na kumdharau, kwa mfano anasema;
Quote:
…. Tujadili sera? Unazungumza nini bwana mtaalamu? Sera inajadiliwa?
…. Ulipokuwa unasomea huo utaalamu hawakukufundisha kuva sera ikishapitishwa haijadiliwi?
…. Ninyiwataalamukwaninimnapendakuchezeaakilizawatu. Pesa zote tunapoteza kusomesha watu, utaalamu wenyewe ndiyo huu… (uk. 24 – 25).
Iko pia miradi mbalimbali inayotekelezwa bila mpango maalumu kama vile kuanzishwa kwa “windmills” katika kila kijiji (jambo ambalo haliwezekani), kushughulikia mti wa ‘Hanga’ unaotoa mafuta ambao Zoeni amepata habari kuwa Philippines kuna mti huo ambao yawezekana upo pia nchini. Bila kufanya tathmini, inaamriwa rnradi uanze mara moja! Hili ni jambo la hatari na linaonyesha hali halisi ambayo imekuwa ikitokea nchini. Miradi mingi imeanzishwa na kufa bila mafanikio kutokana na kutosikiliza maoni na ushauri wa wataalamu wetu. Muda umefika wa kubadilisha hali hii.
– Suala la Makazi Bora
Jamii ya Tanzania ilikusudia kujenga makazi bora kwa wananchi wake, hasa baada ya kutangazwa kwa “Azimio la Arusha”. Ingawa wazo lilikuwa zuri, utekelezaji wake haukuridhisha kwa kiwango kikubwa. Yaelekea vyombo vya dola vilitumia vibaya madaraka yake na hivyo kuwatesa wananchi bila sababu za msingi. Kuna watu waliobomolewa nyumba zao eti kwa sababu zilikuwa nje ya kiwanja kilichopimwa, lakini ilikuwa katika eneo lililotakiwa; kama Bibi anavyolalamika:
Quote:
…Mh! Tuna taabu. Huyo Kibwana Kata! Mmh! Shoga yangu Mama Senga nyumba yake maskini: ‘Bomoa! Haiko kwenye kiwanja’. Tumetutika maji sie! Tukasema: hela Senga kaleta, maji tutashindwa kuteka nyumba ijengwe? Hata! Basi kila kukicha ndoo kichwani. Halafu Kibwana Kata anakuja: ‘Bomoa!’ Tukadhani anatania. Wakabomoa… (uk.12)
Hali hii inaonyesha kwamba watu wengi waliathiriwa na “Operesheni Vijiji” ya miaka ya mapema ya sabini. Wananchi wengi waliteseka. Kuonyesha kwamba kulikuwa na utekelezaji mbaya wa Operesheni hiyo hivi sasa baadhi ya watu waliohamishwa wakati huo wameruhusiwa kurudi kwenye vijiji vyao vya zamani.
– Mipango Mibaya ya Maendeleo
Tumeidokeza dhamira hii pale awali. Lakini pengine hapa tungezungumzia tatizo la mipango mibaya ya maendeleo na utekelezaji wake. Mfano wa maelezo ya jambo hili nl ule wa Talafa aliyegeuzwa shingo “uso ukawa nyuma”. Inasemekana aliwalazimisha wananchi walime pamba ambayo haikuchukuliwa/kununuliwa na serikali kwa vile hapakuwa na daraja la mto uliokitenga kijiji hicho. Mwaka uliofuata inasemekana wananchi waliamua kulima fiwi badala ya pamba. Jambo hili linaonyesha pia mpango mbaya wa utekelezaji wa sera za kiuchumi nchini na kusema kweli matukio ya aina hii nimengimno.
Kuna Ubani
Huo wote ni mvundo ambao si sawa na ule wa “La kuvunda halina ubani”, bali “La kuvunda lina ubani!” Hakuna tatizo hata moja kati ya yaliyosemwa ambayo hayawezi kutatuliwa. Kuna ubani…. Matatizo haya yana dawa. Ni suala la kuamua tu. Mifano michache imeanza kuonekana katika baadhi ya taasisi zetu: Kwa mfano, hivi sasa Waziri wa Mambo ya Ndani anajitahidi kuisafisha jamii. Rais na Waziri Mkuu wamemwunga mkono. Ili kufanikisha jambo hili, ni lazima watanzania wote tumwunge au tuunge mkono juhudi hizo za kuleta “ubani” utakaoondoa “mvundo” kama vile uzembe, wizi, uvivu na ufujaji wa mali ya umma na pia unyimaji wa haki kwa watu.
© Dhamira Nyingine
Pamoja na dhamira hizo tulizoziona, kuna dhamira kadhaa ambazo ingefaa zijadiliwe hapa. Tuziangalie dhamira hizo.
(i) Imani ya Ushirikina na Uchawi
Jamii nyingi zina imani hizo za uchawi na ushirikina. Nchini Tanzania imani hizo pia zipo; na kimsingi zilipata kujitokeza wakati wa “Operesheni Vijiji” ambapo inasemekana baadhi ya watendaji wake walikumbana na matatizo mengi. Uchawi na ushirikina wakati mwingine vimetumika kama nguzo ya wanyonge ya kujitetea dhidi ya tabaka tawala. Hatuna ushahidi wa kufanikiwa kwake, lakini kuendelea kutumiwa kama nguzo na baadhi ya jamii ni dalili kuwa huenda kuna mafanikio.
Katika tamthiliya ya Lina Ubani tunaambiwa kuwa Talafa aliyekuwa msumbufu kwa wanakijiji walioktiwa wamelima fiwi badala ya pamba aligeuzwa shingo, uso umetazama mgongoni! Jambo hili ni la kutisha. Linaweza kubadilisha nia ya afisa yeyote mtendaji ambaye atakwenda kijijini hapo.
(ii) Elimu na Nafasi Yake
Tumetaja hapo awali kuwa Bibi alisifia elimu ya zamani. Lakini hakujadili mchango ama nafasi yake katikajamii.
Tamthiliya hii inaonyesha umuhimu wa elimu katika jamii na hasara zinazoweza kutokea kama elimu haithaminiwi. Kutothaminiwa kwa wasomi wetu kunaweza kuleta madhara makubwa.
Elimu ya jadi pia imedokezwa kwa namna fulani katika tamthiliya hii. Elimu hii inatolewa kwa kizazi kipya kupitia hadithi kama vile Bibi anavyofanya kwa Mota. Elimu zote zinaweza kuwa za manufaa katika jamii zikitumiwa vyema.
(iii) Nafasi ya Mwanamke katika Jamii
Mwanamke katika tamthiliya hii ana nafasi za msingi mbili: mwanamke mzazi na mwanamke mfanyakazi.
– Mwanamke Mzazi
Mwanamke katika kipengele hiki amejengwa akiwa na nafasi yake kama mama watoto. Hapa tunawaona akina mama wawili: Sara akiwa na mtoto wake Mota. Pili kuna Bibi ambaye ana watoto Daudi na Huila. Seti mbili za akina mama na watoto hao zinakamilishwa kwa dhana muhimu ya malezi. Mama, inakubalika na kueleweka kuwa ni mwalimu wa kwanza wa mtoto. Kwa hiyo nafasi yake kama mlezi ni muhimu sana katikajamii. Malezi mema huzaa chema. Malezi mabaya huzaa kibaya. Tumeonyeshwa katika tamthiliya hii mbinu na watu mbalimbali walio muhimu katika malezi, msingi wa kwanza akiwa ni mama.
– Mwanamke Mfanyakazi
Mwanamke huyu ni msomi. Hapa tuna mfano wa Sara na Lijino. Hakuna tatizo kubwa linalojitokeza kwa Sara, lakini tunaambiwa na Bibi juu ya mwanamke Lijino kuwa alikuwa mkatili, kama kwamba hakuzaa. Usemi huu unasisitiza ukatili wa Lijino.
Kutokana na hali hii, tunaweza kusema kuwa tabia haitegemei jinsi-nafsi. Mwanamke ana uwezo sawa tu na mwanaume kama akipewa nafasi inavyotakiwa.
(iv) Mjadala Kuhusu Ushairi
Suala la ushairi wa vina na mizani (kimapokeo) na ule wa masivina linaelekea kujitokeza katika tamthiliya hii. Mota katika tamthiliya hiyo anatunga “ngonjera” ambayo “haina” vina na mizani.
Katika ngonjera yake anawakashifu Madyamini ambao yeye anawaona wako hata sasa:…hapa hapa shuleni, kama yulefulani anakaa deski la mbele, kachukua machungwa ya wenzake… (uk. 55). Hapa dhana ya Madyamini imepanuliwa na kuwa wabaya wote.
(v) Ulevi na Ukweli wa Maisha
Mwanahego ni mtu aliyechorwa kuwa ni mlevi ambaye anaonekana kuwa na akili zake zenye ukweli mtupu. Maneno anayoyasema Mwanahego si ya mlevi, bali ni mtu ambaye ameamua kuserna ukweli, lakini baada ya kujifanya mlevi. Kwa upande mwingine, tukubaliane na hali hii ya ulevi, je, Mwanahego anaelewa juu ya suala la umoja? Anaelewa umuhimu wa fedha za kigeni? Kuna utata.
Ni vyema kuelewa kwamba mlevi mara nyingi hakumbuki anayosema. Mlevi ni tofauti na mnywaji. Tunafikiri Mwanahego ni kipaza sauti cha mwandishi ambaye amedhamiria kuihakiki jamii yake.
Mwisho, tunaweza kusema kuwa hizo ni baadhi tu ya dhamira za Lina Ubani. Wasomaji wana nafasi ya kufanya utafiti zaidi na kugundua dhamira zaidi.
IV Vipengele vya Fani
Fani na maudhui ni pande mbili za sarafu moja. Lazima vitu hivyo viangaliwe katika mchangamano. Lakini hapa tumetenganisha kwa ajili ya majadiliano tu. Majadiliano yatazingatia muundo na mtindo, ujenzi wa wahusika, mazingira au mandhari, na hatimaye matumizi ya lugha.
(a) Muundo na Mtimdo
Tamthiliya hii inatumia mbinu za aina mbili za kimuundo. Mbinu hizo ni za kifasihi simulizi na zile za kidrama ambazo ndizo wasanii wengi wa tamthiliya huzitumia hivi sasa.
Katika kuineemesha, mwandishi anatumia (viingizi vya) nyimbo na maombolezo, ambavyo au huletwa na watambaji wanaounda sehemu ya wahusika na wahusika wengine kama vile Bibi.
Kimtindo, tamthiliya hii inatumia masimulizi ya ngano katika kuelezea ukweli wa namna fulani wa kifasihi. Aidha, kuna mbinu za kisasa za kidrama pia. Hali hii huunda michezo miwili katika mmoja.
Wachezaji muhimu wa mchezo ule wa kifasihi simulizi ni Bibi na Mota, wakisaidiwa na watambaji. Wale wanaotumika katika mchezo wa kidrama ambao ni wa kisasa ni pamoja na Zoeni, Huila na wale watu wa mataifa ya kigeni.
Michezo yote miwili huenda sambamba na kuunganishwa na watambaji. Watambaji katika tamthiliya hii ni muhimu kwani wao wanasaidia kupambanua zaidi dhana muhimu ya ukale na usasa.
Maombolezo katika tamthiliya hii yanaletwa na Bibi (ambaye kwa kweli kwa namna fulani analeta kero). Maombolezo hayo ni mengi, na tunadiriki kusema kuwa hii ni tamthiliya ya kwanza ya aina yake. Haijawahi kutokea tamthiliya ya aina hii, na Profesa Muhando anastahili pongezi.
Suala la matumizi ya nyimbo na ngoma limejitokeza katika tamthiliya hiyo. Wasomaji hufurahia kuisoma lakini wakati huo huo kuwa makini katika kutoa uhakiki wake.
(b) Wahusika
Kama tulivyodokeza sehemu nyingine hapo awali, wahusika ni watu, wanyama, vitu na mahali. Vitu hivi pamoja na viumbe hai vinaweza kutumika katika kazi ya fasihi kwa pamoja, au vinaweza visitumike vyote kwa mara moja. Hapa tutachambua wahusika muhimu tu – wakiwemo Mtambaji, Bibi, Huila, Zoeni, Mota, Daudi, Mwanahego, Lijino, Dyamini na wengineo.
(i) Bibi
Miongoni mwa wahusika muhimu wa tamthiliya hii ni Bibi. Kupitia Bibi, mwandishi anatoa dhamira mbalimbali ambazo zinaihusu jamii nzima. Bibi mwenyewe aghalabu anaonyesha tabia za aina yake pia.
– Ni mlalamishi. Ana uchungu wa kufiwa na mtoto wake kipenzi Daudi.
– Kiungo muhimu katika dhamira ya ukale na usasa. Msisitizo wake wa kutaka mtoto wake achaguliwe mchumba wa kabila lake, kusifia kwa nyimbo za zamani, kutamba hadithi ni miongoni mwa vitu vinavyothibitisha dhana ya ukale na usasa.
– Amechanganyikiwa. Tabia zake katika hadithi ya tamthiliya hii inashindwa kueleweka. Je, ni nini hicho anachodai kiteremke toka, mawinguni? Kuna nyakati tunafikiri labda ni utawala/viongozi u(wa)lio juu na wanalazimishwa kuteremka. Aidha, kuna wakati inajionyesha tabiayawehu.
– Ni mtu asiye na shukrani.
Haridhiki kwa huduma anayopewa na mke wa Huila. Hampendi Sara – anamwita mchawi.
– Ili kuonyesha uzee wake, Bibi amepewa sifa zote za kizee.
– Mhakiki muhimu wa jamii, kwani anazungumzia matatizo ya kuhamia vijijini yaliyotokana na utekelezaji mbaya, matatizo ya ndoa za mseto wa makabila na kadhalika.
(ii) Zoeni
Huyu ni mwanasiasa ambaye kimsingi amepewa tabia nyingi zinazoudhi. Tabia hizo ni kama zifuatazo:
– Ana dharau na hajasoma elimu ya kisasa. Haambiliki.
– Ana kiburi. Yeye ni mhusika muhimu ambaye anakuwa nguzo ya mchezo katika tamthiliya hiyo yenye mbinu za kidrama.
– Mwanasiasa asiye makini. Hajali utaalamu wa wasomi kama vile Huila.
– Ni mpenda rushwa na hongo. Aidha, ni mzembe! Hali hii inajitokeza wakati anapokwenda mkutanoni kuiwakilisha nchi naye analala katika chumba cha mkutano.
– Ni mbadhirifu wa mali ya umma kwa shughuli zake za binafei.
– Hana adabu kwa wafanyakazi wengine. Anawatukana na kuwaaibisha mbelezawatu.
(iii) Huila
Tofauti na mhusika kama Zoeni, Huila ni msomi, ambaye ana tabia zifuatazo:
– Ni mtulivu namvumilivu mkubwa.
– Nimchapa kazi, na ana juhudi kubwa.
– Hakatitamaa upesi.
– Ni mtetezi wahakiza binadamu.
– Ana ushirikiano mkubwanawafanyakaziwenzake.
– Anajalifamilia yake wakati wote.
(iv) Mwanahego
Miongoni mwa wahusika airibao wamechprwa kuwa wazembe, lakini ni muhimu sanani Mwanahego.
– Ni msema ukweli
– Nimcheshi
– Anawahakiki viongozi wazembe katika J’amii.
(v) Sara
Ni mke wa Huila. Anamsaidia sana mume wake katikakumfariji anapokuwa namatatizo.
(vi) Mota
Huyu ni mtoto wa Huila na Sara. Anakuwa kiungo muhimu cha rtiaelezo kuhusu malezi ya kizazi kipya.
– Mota anatumika kuelezea migogoro kati ya ushairi wa mapokeo na masivina.
– Ni mwelezaji wa hali ya ubaya miongoni mwa watu: Kwamba kila mahali kuna wabaya (Madyamini).
– Ni msikivu. Ni mtulivu. Ana akili bora.
(vii) Daudi
Kakake Huila ambaye alifia vitani; wakati wa kumfukuza Dyamini.
(viii) Dyamini
– Mvamizi.
(ix) Watambaji
Wanaisimulia hadithi na kuiunga kati ya hadithi ya kingano na ile ya kisasa.
(x) Wahusika wengine
Lijino, Katibu Kata, Katibu Tarafa na wengine wanasiasa.
© Mazingira/Mandhari
Mazingira ya tamthiliya hii ni ya kitanzania. Ni mazingira ya baada ya Azimio la Arusha na vita ya kumwondoa Idi Amini. Japokuwa hadithi (sehemu kubwa) inasimuliwa kingano, hadithi hiyo inaihusu Tanzania.
(d) Matumizi ya Lugha
Lugha ni chombo cha mawasiliano miongoni mwa jamii. Matumizi ya lugha hutofautisha kazi – kazi ya kisanaa na isiyo ya kisanaa.
Katika tamthiliya hiyo, mwandishi ametumia lugha vyema katika kuwajenga wahusika wake. Tuchambue matumizi yake.
(i) Lugha ya Kikabila
Mwandishi amemjenga mhusika muhimu sana, Bibi, kwa kutumia lugha za aina mbili: lugha ya Kiswahili fasaha na lugha ya kikabila – Kikaguru. Jambo hili limesaidia kwa namna moja katika kuumba hali halisi aliyokuwa nayo Bibi. Lakini pia, tahadhari ni kuwa baadhi ya mambo ambayo hayakutafsiriwa kwa Kiswahili yatashindwa kufikisha ujumbe ipasavyo.
(ii) Lugha za Kigeni
Yako matumizi ya lugha za kigeni, zikiwemo Kifaransa, Kiingereza, Kijerumani n.k. katika kuwajenga wahusika wanaohudhuria mkutano wa kimataifa. Hali hii inaweka mazingira ya tamthiliya iwe karibu na uhalisia wa mambo yanayozungumzwa.
(iii) Kiswahili Fasaha
Lugha hii imetumiwa na msanii pia. Pamoja na lugha hii, kuna pia matumizi ya lugha iliyo sanifu.
(iv) Matumizi yu Methali, Misemo na Nahau,
Mwandishi ametumia misemo na nahau, pamoja na methali pia katika kuimarisha kazi hii. Angalia kwa mfano;
– Penye wema(…) ubaya huzengea (uk. 36)
– La kuvunda lina ubani (uk. 58).
(v) Tamathali za usemi.
Mwandishi ametumia tamathali mbalimbali za usemi. Tamathali hizo ni pamoja na sitiari, tamathali ambayo hulinganisha mambo/vitu viwili au zaidi vyenye sifa tofauti, lakini haitumii maneno ya viungo kama tashbiha. Mfano wasifa tofauti ni huu ambao ni kilio cha Bibi.
Quote:
“Aliyeua Daudi (Kaua jembe langu)”
………
(Kaua kuni zangu)
………
(Kaua nguozangu) (uk.2)
Kwa upande wa tashibiha, hizo nazo zimetumiwa katika tamthiliya hii. Tunamsikia Bibi akisema:
Quote:
….Basi kupaka tu wacha iniwashe. Inachonyota kama upupu Kaja Talafa, Mkali kama pilipili
Tunaweza kupata picha ya sabuni hiyo inayosemekana inachonyota kama upupu. Lazitna iwe sabuni mbaya! Halafu tunamfikiria huyu Katibu Tarafa aliye mkali kama pilipili. Hapana shaka huyu ni mtu mkatili na hana utu wala ubinadamu.
Matumizi ya tamathali za tabaini yapo pia. Tabaini ni mtindo wa uneni wa fasaha ambao kwayo msemaji husisitiza kauli kwa kutumia maneno yenye ukinzani, aghalabu neno si. Tunamsikia Bibi akimlalamikia au kumsema mtoto wake aliyeamua kuolewa na Mchusa aliyemwelezea ukatili wake kuwa alikuwa, “Mbogo si mbogo, Kifaru si kifaru”. Matokeo yake? Inasemekana Melina “akakonda akawa mifupa mitupu”. Kwa mara nyingine tena tabaini hapa imeimarishwa na tamathali ya sitiari.
Kumekuwa na matumizi pia ya tamathali ya kiritifaa. Ritifaa ni mbinu ya aina ya semi ambazo kwazo (i) mtu aliyekufa huombolezwa na kuliliwa kama vile angali hai. (ii) vitu visivyokuwa ulimwenguni kwa sasa, husimuliwa au husifiwa kama viumbe katika hali ya maisha ya duniani. Katika tamthiliya ya Lina Ubani Bibi analia na kaomboleza mara kwa mara kuhusu mtoto wake Daudi. Tena pia tunamsikia akimlaumu Dyamini na kumkashifu kutokana na ubaya wake. Pamoja na tamathali hizo, kuna matumizi machache ya dhihaka na kejeli.
Licha ya tamathali tulizozisema, mwandishi artietumia pia mbinu nyingine za kisanaa. Mbinu hizo kwa mfano ni takriri mbalimbali. Takriri ni mbinu ambayo husisitiza jambo kwa kulirudiarudia. Ziko takriri za aina mbalimbali: takriri-imundo, takriri-neno na kadhalika. Katika tamthiliya hii takriri zinazojitokeza mara nyingi ni zile za maneno. Angalia kWa mfano Mota anavyoyalalamikia Madyamini – ambayo anayaona kuwapo: “Madyamini shule, Madyantini vijijini, Madyamini mijini”. Neno Madyamini limerudiwa ili kusisitiza dhana anayoitaka msanii. Hakika mbinu hizi ni nyingi mno na zinasaidia sana kuimarisha kazi hii. Matumizi ya mdokezo yapo pia kwa wingi. Hii ni tobinu ambayo kwayo mwandishi husema na kukatiza maneno na kumwachia msomaji au msikilizaji ahisi yeye binafsi mwisho wa maneno hayo. Kwa mfano Huila anasikika kwenye simu: “Haloo… Oh! Dr. Matayo…eeee… ndiyo…mama…ee?Vipitena…?eeh? (uk. 57). Maneno hayo yanaonyesha hamu ya kujua nini kipo upande wa pili. Mbinu ya mjalizo imetumika pia. Mbinu hii huunga vifungu vya’maneno kwa kutumia mikato, kwa mfano, kama Huila anavyolalamika kuwa…. “Nimekwenda kote huko! Ugawaji, Usagishaji, Biashara” (uk. 36). Tashtiti, hali ya kuuliza na kushangaa mambo yanayofahamika imetumiwa vyema na mwandishi wa Lina Ubani. Mifano iko mingi. Pamoja na tashtiti kuna pia matumizi ya nidaa. Nidaa m aina au namna ya msemo wa msisimuo au sauti ya mshangao atoayo mtu kudhihirisha maono yake ya ndani au kilio cha moyo wakati apatwapo na mgutusho ghafla wa furaha, hasira, huzuni, chuki na kadhalika. Nidaa imetumiwa sana na mwandishi wa Lina Ubani. Sara, kwa mfano anapomwona Bibi analia na kuendelea kuwa mlalamishi anasema: “Ee Mungu wangu!” (Anatoka) (uk. 32). Msemo huu unaonyesha nidaa. Tamathali na mbinu za kisanaa zimesaidia katika kuijenga taswira pia.
Hizo ni baadhi tu ya mbinu za kisanaa katika tamthiliya hii ya Lina Ubani. Utafiti zaidi unaweza kuzifafanua nyingine.
V Mwisho
Profesa Penina Muhando anlefanya jaribio ambalo halijawahi kufanywa katika uandishi wa tamthiliya za Kiswahili. Jambo hili limefanya tamthiliya hii kuwa na hadhi ya aina yake rta ya kipekee kuliko zile alizopata kuziandika mwenyewe. Aidha, kwa rtsomaji wa kawaida anaweza kujikuta katika matatizo ya kushindwa kuufuatilia vema mchezo huu kutoka mwanzo hadi mwisho. Vinginevyo, hiini kazi bora, tunampongeza Profesa kwa kazi nzuri hii.
VI Maswali
1. Ni kwa vipi dhamira ya kisiasa imejitokeza katika Lina Ubani.
2. Eleza maana ya muundo na mtindo katika kazi ya fasihi. Je, Lina Ubani ina muundo na mtindo gani?
3. Chambua dhamira za Lina Ubani, kishajadili kufanikiwa au kutofanikiwa kwa mwandishi.
4. Jadili wasifu wa wahusika Zoeni, Bibi, Sara na Huila.
]]>
<![CDATA[UHUSIANO WA FASIHI NA SANAA NYINGINE]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1206 Thu, 09 Sep 2021 04:37:31 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1206 Fasihi ni taaluma inayotumia sanaa maalum ya lugha. Nayo SANAA ni uzuri unaojitokeza katika umbo lililosanifiwa, umbo ambalo mtu hulitumia kueleza hisi zinazomgusa kwa kutoakielelezo au vielelezo vyenye dhana maalum. Ukiachilia mbali fasihi, baadhi ya tanzu nyingine za sanaa ni: Ususi, utarizi, sanaa za maonyesho, ufinyanzi, uchoraji na uchongaji. Upo uhusiano wa fasihi na tanzu hizi za sanaa kama inavyoelezwa:
Zote ni kazi za sanaa. Kama ufinyanzi, uchoraji na uchongaji ulivyo, yaani uzuri unaojitokeza katika umbo lililosanifiwa, umbo ambalo mtu hulitumia kueleza hisi zinazomgusa kwa kutoa kielelezo au vielelezo vyenye dhana maalum.
Fasihi na tanzu nyingine za sanaa hutoa mafunzo fulani. kwa mfano, katika kazi ya fasihi andishi ya WATOTO WA MAMAN’TILIE, tunapata mafunzo kuwa, ulevi si suluhisho la matatizo. Pia, katika sanaa nyingine kama sanaa za maonyesho, kuna mafunzo ambayo watazamaji huyapata.
Fasihi na tanzu nyingine za sanaa hutegemea watu. Riwaya, tamthiliya na ushairi hutegemea watunzi na wasomaji. Fasihi simulizi hutegemea fanani na hadhira. Ususi hutegemea mtu mjuvi wa huo ususi, katika ununuzi hutegemea wateja. Uchongaji nao vivyo hivyo, pasi na mchonga vinyago na mnunuzi wa sanaa hiyo, hakuna kitakachoendelea.
Yapo mengi sana yanayofanya fasihi na tanzu nyingine za sanaa zihusiane. Hata hivyo, hii haina maana kuwa fasihi na tanzu nyingine za sanaa hazina tofauti.
]]>
Fasihi ni taaluma inayotumia sanaa maalum ya lugha. Nayo SANAA ni uzuri unaojitokeza katika umbo lililosanifiwa, umbo ambalo mtu hulitumia kueleza hisi zinazomgusa kwa kutoakielelezo au vielelezo vyenye dhana maalum. Ukiachilia mbali fasihi, baadhi ya tanzu nyingine za sanaa ni: Ususi, utarizi, sanaa za maonyesho, ufinyanzi, uchoraji na uchongaji. Upo uhusiano wa fasihi na tanzu hizi za sanaa kama inavyoelezwa:
Zote ni kazi za sanaa. Kama ufinyanzi, uchoraji na uchongaji ulivyo, yaani uzuri unaojitokeza katika umbo lililosanifiwa, umbo ambalo mtu hulitumia kueleza hisi zinazomgusa kwa kutoa kielelezo au vielelezo vyenye dhana maalum.
Fasihi na tanzu nyingine za sanaa hutoa mafunzo fulani. kwa mfano, katika kazi ya fasihi andishi ya WATOTO WA MAMAN’TILIE, tunapata mafunzo kuwa, ulevi si suluhisho la matatizo. Pia, katika sanaa nyingine kama sanaa za maonyesho, kuna mafunzo ambayo watazamaji huyapata.
Fasihi na tanzu nyingine za sanaa hutegemea watu. Riwaya, tamthiliya na ushairi hutegemea watunzi na wasomaji. Fasihi simulizi hutegemea fanani na hadhira. Ususi hutegemea mtu mjuvi wa huo ususi, katika ununuzi hutegemea wateja. Uchongaji nao vivyo hivyo, pasi na mchonga vinyago na mnunuzi wa sanaa hiyo, hakuna kitakachoendelea.
Yapo mengi sana yanayofanya fasihi na tanzu nyingine za sanaa zihusiane. Hata hivyo, hii haina maana kuwa fasihi na tanzu nyingine za sanaa hazina tofauti.
]]>
<![CDATA[‘Babu Alipofufuka’, riwaya inayoakisi uhalisia]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1049 Sat, 28 Aug 2021 04:06:44 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1049 Riwaya ya ‘Babu Alipofufuka’ imeandikwa na mwandishi maarufu wa kazi za fasihi na mtaalamu wa lugha ya Kiswahili, Profesa Said Ahmed Mohammed, na kuchapishwa na Jomo Kenyatta Foundation mwaka 2001. Katika gamba lake la mbele, pameandikwa: “pengine ni riwaya ya ujasiri mno kupita zote Said A. Mohammed alizowaji kuandika.” Na hivyo hasa ndivyo ilivyo – hii ni riwaya ya kijasiri, ya kimapinduzi.
Hii ni riwaya iliyoandikwa kwa mtindo wa kejeli, lakini yenye mchomo mkali kwa wale wanaoelekezewa kejeli hiyo – yaani watawala waovu – na pia inayoibua hisia nzito kwa wale wanaoathirika na uovu wa watawala – yaani raia wa kawaida.
Uovu wenyewe unadhihirishwa katika riwaya hii kwa namna ya tashnina na inda, lakini katika hali inayowiana sana na ukweli halisi uliomo katika maisha ya kila siku kwenye mataifa yetu ya dunia inayoambiwa inaendelea. Hadithi nzima inasimuliwa kupitia mazingira yasiyo ya kawaida. Huyo Babu mwenyewe Aliyefufuka anatujia kwa umbo la ajabuajabu kupitia kichwani mwa mjukuu wake, K, ambaye ndiye muhusika mkuu. K mwenyewe ni sehemu ya hao watawala ambao kwao kijembe cha riwaya nzima kinaelekezwa. Kwa ustadi wa hali ya juu, mwandishi anampa Babu nguvu za kuziunganisha dunia zetu mbili – baina ya ile tuionayo kwa macho ya nje na ile ionekanayo kwa jicho la ndani tu.
Baina ya dunia hizi mbili, ndipo msomaji anapopewa taswira halisi ya tafauti za waziwazi na za kificho walizonazo wanaoishi ndani yao. Upande mmoja ni maisha ya starehe na anasa za watawala, kule kujilabu na kujitapa kwao, ule uroho na tamaa zao zisizokwisha. Upande wa pili ni maisha magumu ya watawaliwa, kule kutumai na kutamauka kwako, kule kuinuka na kuanguka kwao, na kule kupambana na kujipapatuwa kwao kutoka makucha ya “wenye dunia yao”.
Katika ukurasa wa 14 hadi 15, kwa mfano, tunakutaka na maelezo kuhusu K ambayo yanawasilisha hisia zake za kuutaka na kuupenda ufakhari kama ilivyo kawaida ya watawala wa aina yake:
“Mbali na gari, kulikuwa pia na kasri la kuonewa fahari. Na fahari ndiyo madhumuni yenyewe. Na kasri lake K linamstahiki kwa kila hali, kwa kile cheo cha kiungo. Kama chumvi na chakula alikuwa. Bila ya yeye, mengi ya wakubwa na wadogo hayachapuki… Mjengo wa kasri lake ni wa aina ya zile husuni za tasnifa tunazoziona kwenye snema za filamu za sayansi ya kubuni.”
Wakati akina K wakiishi maisha hayo ya ukwasi na kujitanua, akina Kali ndio muhanga wa anasa hizo za watawala. Kwao maisha ni msegemnege na hali zao ni ngumu kupindukia. Huko ndiko kwenye ‘maitikwenenda’ kama wanavyoitwa na mwandishi na walivyowahi kuitwa na Sembene Ousmane kwenye God’s Bits of Wood au Ayi Kwei Armah kwenye The Beautiful Ones Are Not Yet Born.
Katika ukurasa wa 115 hadi 116, kwa mfano, tunasimuliwa maisha ya watu kula togonya na mboga ya kikwayakwaya sio kwa kupenda, bali kwa kuwa hawana namna nyengine. Huku ndiko ambako mtu anakwenda hospitalini kusaka matibabu, lakini anaondoka akiwa ameongezwa maradhi mengine zaidi kwa kuwa serikali imezitelekeza zahanati zake:
“Walipofika zahanati, mlango ulikuwa wazi, lakini mwuguzi aliyekuwa zamuni hayupo. Ilichukuwa saa nzima mpaka alipopatikana. Alikuwa kenda kumpiga mtu sindano kwa pesa. Alipofika alimkagua Kali, alisema anahitajia wembe wa kumnyoa nywele. Kisha uzi wa kushonea anao lakini anahitajia sindano au shazia ambayo hanayo. Alisema japo ya kushonea nguo inafaa. Zaidi ya hayo hana vidonge vya kuondolea maumivu. Plasta pia hakuna… Kali akanyolewa bila maji, akashonwa bila ya sindano ya ganzi, akatiwa plasta na kupewa vidonge viwili vya asprini kubwia…. alipoondoka, juso na jichwa lake zima lilikuwa limemvimba.” (Uk. 121-22)
Huko kunaitwa Kataa na K anaamini kisa cha kuitwa hivyo ni kwa kuwa watu wa huko ni wakaidi na hawakubaliani hata kidogo na watawala wao. Ndiko hasa alikotokea K, lakini ambako mwenyewe amekutupa na kukusahau kwa miaka yote hiyo. Kwa ujumla, hali ya maisha ya watu wa huko ni duni sana, nyumba zao ni dhaifu na hawana pesa za kununulia hata mahitaji ya lazima:
“Mbele zaidi waliposonga wakipasua kiini cha miti na mimea iliyokuwa mali kubwa hapo zamani, maisha na uhali yalianza kujiliza. Vibanda viwili vilivyolalia yombo. Kitambo,,, vibanda vyengine vitano vikirukuu. Hatua… vibanda vyengine vikisujudu…. ghafla walitokeza mahala ambapo ungeweza kupapagaza jina la sokoni. Watu walionekana… wamesogelea chanja zilizowekwa biashara… wote wametumbua macho, bila ya kuweza kununua chochote. Wengine wanavitumbulia macho vidaka vya nazi. Wengine vichungwa, vilimau, viembe na vipapai… kwenye soko la samaki, mafungu ya dangaauronga na dagaaupapa yakishindana kutumbuliana macho na watu…” (Uk. 95)
Kwa hivyo, riwaya ya Babu Alipofufuka ni kielelezo cha usimulizi unaoakisi uhalisia wa dunia mbili zinazoishi ndani ya jamii moja kwenye mataifa yetu. Mwandishi anampa Babu nguvu za kumfanya mjukuu wake, muhusika mkuu K, azidurusu dunia hizo ambazo kwa kila hali zimekuwa sehemu yake – moja aliyotokea na akaikimbia na kuitelekeza na nyengine aliyokimbilia, kuipenda na kuitukuza. Babu yake alipofufuka na kumjia kwenye maisha yake ya ndani, ndipo anatoa wasaa kwa msomaji kuyaona yaliyomo kwenye nafsi za madhalimu na madhulumu na zinavyosawirika dunia zao.
Baada ya kuziona dunia hizo, mwandishi anamfanya msomaji wake ahitimishe kwa mambo matatu haya:
Kwanza, watu wa aina ya K, ambao wameendeleza dhuluma kubwa kwa kutumia vyeo na majina yao, huwa wanaishi na khofu ya milele ya kuporomoka. Matokeo yake, kila siku hutamani na kupigania kwenda juu na juu zaidi kusudi wasifikwe na walio chini, ambao wanadhani kuwa endapo mikono yao itawafikia tu, basi watawashika miguu na shingo zao na kuwaporomosha chini kwa kishindo kikubwa. Kwa hivyo, ishara yoyote ya kuporomoshwa huwatia jaka moyo kubwa na kuwatetemesha hadi machango. Katika ukurasa wa 92, mathalan, mwandishi anatuonesha namna K anavyogwaya akiliogopa anguko lake:
“Ghafla alijihisi anachukuliwa na lepe jengine lililomdidimiza katka singizi zito la ajabu. Alitumbukia kwenye singizi huku akienda. Lilikuja tu kwa hakika hilo singizi ama upepo wa ghafla. Lilikuja kumvaa na kumdidimiza kwenye maweko ya chini ya kiini cha dunia. Alihisi anazama kwenye dimbwi refu lisilo ukomo… di, di, di… alididimia mpaka akajihisi ameibuka pahala penye mwangaza wa maisha. Akajihisi kama katupwa hapo. Katupwa kama gunia. Moyo ukaanza kupiga beni alipogundua hivyo. Aa, kubwagwa kila siku yeye alikuwa akikuogopa. Kuanguka alikuchelea. Akihofu kutupwa, hasa namna hiyo.”
Pili, msomaji anahitimisha kuwa watawala wa aina ya K wanakuwa wanajijuwa hasa kwamba wamewakosea raia. Kwa hivyo, kila wanapokaa huwa wanajitia wasiwasi kuwa wanaandamwa au wanafuatwafuatwa na watu hao wenye hasira na wakati wowote wanaweza kulipiziwa kisasi kwa maovu yao. Hayo ndiyo matokeo ya kuishi kwa dhuluma. Siku zote huwa unakhofu kuwa madhulumu wako watakurudi kwa yale uliyowatenda. Huwa huko huru. Angalia vile wanavyopita barabarani kwenye magari yaliyofungwa vioo vyote, tena vyeusi visivyopenya risasi na bado mbele yao ving’ora mita kadhaa ili wapishwe njia peke yao na bado maaskari kibao na bunduki. Hawa hawafanyi yale kwa kupenda, bali kutokana na khofu waliyonayo kwa umma walioukosea (Uk.24-7). Wakati Babu anamzukia K kwa mara ya kwanza kwenye ndoto-macho zake, alijitambulisha kwa namna hii:
“Nikwambie tena, mimi ni babu yako; kisha niongeze kuwa mimi ni dhahiri kwa kisia kikubwa kuliko hata wewe, kwa sababu sina farakano na watu. Wala sina makiwa na utawa kama ulionao wewe. Sina hofu wala siogopi kama uogopavyo wewe. Nakwenda nipendapo. Nakutana na nimpendaye. Ufunguo wa kasi yangu ninao mwenyewe. Hakuna niliyemdhulumu.” (Uk. 21-2)
Tatu, msomaji anahitimisha kuwa khofu hizi za watawala zina uhalali wake na ni za kweli. Ni kweli kuwa wananchi walioonewa na kudhulumiwa kwa miaka mingi hufika pahala pa kusema “hapana” kwa watawala wao. Miongoni mwao huwa wanasema hivyo kwa maneno, wengine kwa vitendo, wengine wakiwa na akili zao na wengine tayari wameshachanganyikiwa kwa mateso ya muda mrefu. La muhimu ni kuwa wananchi hufika mahala wakasema “liwalo na liwe” lakini hawatakubali tena dhuluma nyengine dhidi yao. Katika ukurasa wa 92, K alimkuta Mussa katika eneo la Kataa akijisemea peke yake njiani:
“La, hatutaki, hata ikiwaje hatutali tena…. La, hatutaki, hata iwaje hatutali tena…. La, hatutaki, hata ikawaje, hatutali tena..”
Lakini madhulumu wengine huamua kwenda mbali zaidi ya kupita mitaani wakijisemea peke yao tu. Wao huamua kuwarudi madhalimu wao kwa namna yoyote ile wanayoiona inawafalia na wanaimudu. Mno yachosha eti! Na ni hiki ndicho ambacho kinadhihirika mwishoni, pale umma uliokwishachoshwa na udhalimu wa watawala wao, unapoingia barabarani na kuukabili mkono wa utawala.
“Nje aliwakuta wale mahasimu zake wamejipanga upande huu na huu wa njia. Sasa walikuwa mamia kwa mamia… Kuna waliochukuwa marungu na wengine mabango yaliyoandikwa maneno mengi…M’MEZIFISIDI NAFSI ZETU…. MMEVUNJA HESHIMA ZETU…. VIJANA WETU WANAPOTEA… VIFO NA NJAA NA MARADHI SABABU SI SISI… HATUNA NAFASI PANAPOSTAHIKI NAFASI ZETU… ARDHI INACHUKULIWA HIVI HIVI TUNAONA…. KESHO YETU IMO KATIKA GIZA…TUNAANGAMIA…TUMESHAKWENDA KAPA…na zaidi na zaidi…Mlio ule wa bunduki K aliusikia ndani apokuwa tayari ameshakua kitini ofisini mwake. Alitetemeka kwa muda. Lakini alipojishika, aligunduwa kwamba hata ofisini mambo yalikuwa yamegeuka pia.” (Uk. 154-56)
Riwaya inamalizika kwa kumuonesha K akipoteza kila kitu – ulwa, nyumba, gari na, zaidi kuliko yote, hata ile heshima aliyojidhani alikuwa nayo. Na mwisho anakufa kifo cha kidhalilifu kama alivyosababisha maelfu ya wengine kufa katika udhalilifu kwenye zama za madaraka yake.
“Alfajiri ya siku ya pili, watu wa kijiji kile waliamshwa na sauti ya jibwa kubwa, Biye aliloliita Doggy. Ilikuwa si kawaida jibwa kubwa kama lile kubweka kwa muda mrefu namna ile hapo kijijini. Walipoufuata mbweko wa jibwa, walimkuta K ananing’inia kwenye kigogo cha mti uliokuwa umeota katikati ya kaburi la Babu. Alikuwa mkavu keshang’ang’anaa.”(Uk.165)
Naam, hapa ndipo hasira ya umma ilipomfikisha K. Hapa, kwa hakika, ndipo kiuhalisia wafikishwapo watawala madhalimu wa aina yake. Hivyo ndivyo umma unavyomuhukumu mkosaji wake. Umma ukikosewa kiasi kikubwa kama hiki, ni wenyewe ndio ambao hushitaki, na wenyewe ukahukumu. Na hivi ndivyo Babu Alipofufuka na kumtahadharisha mjukuu wake, K:
“…Pia unashitakiwa na wakati ulioutumia vibaya…Unashitakiwa vile vile na matendo yako mwenyewe…matendo ya upotofu…Maovu yako mwenyewe….Hakuna uchaguzi. Huna njia. Wakati ukifika, utakwenda tu; utakwenda tu…” (Uk. 137)   Chanzo >>>>>>>
]]>
Riwaya ya ‘Babu Alipofufuka’ imeandikwa na mwandishi maarufu wa kazi za fasihi na mtaalamu wa lugha ya Kiswahili, Profesa Said Ahmed Mohammed, na kuchapishwa na Jomo Kenyatta Foundation mwaka 2001. Katika gamba lake la mbele, pameandikwa: “pengine ni riwaya ya ujasiri mno kupita zote Said A. Mohammed alizowaji kuandika.” Na hivyo hasa ndivyo ilivyo – hii ni riwaya ya kijasiri, ya kimapinduzi.
Hii ni riwaya iliyoandikwa kwa mtindo wa kejeli, lakini yenye mchomo mkali kwa wale wanaoelekezewa kejeli hiyo – yaani watawala waovu – na pia inayoibua hisia nzito kwa wale wanaoathirika na uovu wa watawala – yaani raia wa kawaida.
Uovu wenyewe unadhihirishwa katika riwaya hii kwa namna ya tashnina na inda, lakini katika hali inayowiana sana na ukweli halisi uliomo katika maisha ya kila siku kwenye mataifa yetu ya dunia inayoambiwa inaendelea. Hadithi nzima inasimuliwa kupitia mazingira yasiyo ya kawaida. Huyo Babu mwenyewe Aliyefufuka anatujia kwa umbo la ajabuajabu kupitia kichwani mwa mjukuu wake, K, ambaye ndiye muhusika mkuu. K mwenyewe ni sehemu ya hao watawala ambao kwao kijembe cha riwaya nzima kinaelekezwa. Kwa ustadi wa hali ya juu, mwandishi anampa Babu nguvu za kuziunganisha dunia zetu mbili – baina ya ile tuionayo kwa macho ya nje na ile ionekanayo kwa jicho la ndani tu.
Baina ya dunia hizi mbili, ndipo msomaji anapopewa taswira halisi ya tafauti za waziwazi na za kificho walizonazo wanaoishi ndani yao. Upande mmoja ni maisha ya starehe na anasa za watawala, kule kujilabu na kujitapa kwao, ule uroho na tamaa zao zisizokwisha. Upande wa pili ni maisha magumu ya watawaliwa, kule kutumai na kutamauka kwako, kule kuinuka na kuanguka kwao, na kule kupambana na kujipapatuwa kwao kutoka makucha ya “wenye dunia yao”.
Katika ukurasa wa 14 hadi 15, kwa mfano, tunakutaka na maelezo kuhusu K ambayo yanawasilisha hisia zake za kuutaka na kuupenda ufakhari kama ilivyo kawaida ya watawala wa aina yake:
“Mbali na gari, kulikuwa pia na kasri la kuonewa fahari. Na fahari ndiyo madhumuni yenyewe. Na kasri lake K linamstahiki kwa kila hali, kwa kile cheo cha kiungo. Kama chumvi na chakula alikuwa. Bila ya yeye, mengi ya wakubwa na wadogo hayachapuki… Mjengo wa kasri lake ni wa aina ya zile husuni za tasnifa tunazoziona kwenye snema za filamu za sayansi ya kubuni.”
Wakati akina K wakiishi maisha hayo ya ukwasi na kujitanua, akina Kali ndio muhanga wa anasa hizo za watawala. Kwao maisha ni msegemnege na hali zao ni ngumu kupindukia. Huko ndiko kwenye ‘maitikwenenda’ kama wanavyoitwa na mwandishi na walivyowahi kuitwa na Sembene Ousmane kwenye God’s Bits of Wood au Ayi Kwei Armah kwenye The Beautiful Ones Are Not Yet Born.
Katika ukurasa wa 115 hadi 116, kwa mfano, tunasimuliwa maisha ya watu kula togonya na mboga ya kikwayakwaya sio kwa kupenda, bali kwa kuwa hawana namna nyengine. Huku ndiko ambako mtu anakwenda hospitalini kusaka matibabu, lakini anaondoka akiwa ameongezwa maradhi mengine zaidi kwa kuwa serikali imezitelekeza zahanati zake:
“Walipofika zahanati, mlango ulikuwa wazi, lakini mwuguzi aliyekuwa zamuni hayupo. Ilichukuwa saa nzima mpaka alipopatikana. Alikuwa kenda kumpiga mtu sindano kwa pesa. Alipofika alimkagua Kali, alisema anahitajia wembe wa kumnyoa nywele. Kisha uzi wa kushonea anao lakini anahitajia sindano au shazia ambayo hanayo. Alisema japo ya kushonea nguo inafaa. Zaidi ya hayo hana vidonge vya kuondolea maumivu. Plasta pia hakuna… Kali akanyolewa bila maji, akashonwa bila ya sindano ya ganzi, akatiwa plasta na kupewa vidonge viwili vya asprini kubwia…. alipoondoka, juso na jichwa lake zima lilikuwa limemvimba.” (Uk. 121-22)
Huko kunaitwa Kataa na K anaamini kisa cha kuitwa hivyo ni kwa kuwa watu wa huko ni wakaidi na hawakubaliani hata kidogo na watawala wao. Ndiko hasa alikotokea K, lakini ambako mwenyewe amekutupa na kukusahau kwa miaka yote hiyo. Kwa ujumla, hali ya maisha ya watu wa huko ni duni sana, nyumba zao ni dhaifu na hawana pesa za kununulia hata mahitaji ya lazima:
“Mbele zaidi waliposonga wakipasua kiini cha miti na mimea iliyokuwa mali kubwa hapo zamani, maisha na uhali yalianza kujiliza. Vibanda viwili vilivyolalia yombo. Kitambo,,, vibanda vyengine vitano vikirukuu. Hatua… vibanda vyengine vikisujudu…. ghafla walitokeza mahala ambapo ungeweza kupapagaza jina la sokoni. Watu walionekana… wamesogelea chanja zilizowekwa biashara… wote wametumbua macho, bila ya kuweza kununua chochote. Wengine wanavitumbulia macho vidaka vya nazi. Wengine vichungwa, vilimau, viembe na vipapai… kwenye soko la samaki, mafungu ya dangaauronga na dagaaupapa yakishindana kutumbuliana macho na watu…” (Uk. 95)
Kwa hivyo, riwaya ya Babu Alipofufuka ni kielelezo cha usimulizi unaoakisi uhalisia wa dunia mbili zinazoishi ndani ya jamii moja kwenye mataifa yetu. Mwandishi anampa Babu nguvu za kumfanya mjukuu wake, muhusika mkuu K, azidurusu dunia hizo ambazo kwa kila hali zimekuwa sehemu yake – moja aliyotokea na akaikimbia na kuitelekeza na nyengine aliyokimbilia, kuipenda na kuitukuza. Babu yake alipofufuka na kumjia kwenye maisha yake ya ndani, ndipo anatoa wasaa kwa msomaji kuyaona yaliyomo kwenye nafsi za madhalimu na madhulumu na zinavyosawirika dunia zao.
Baada ya kuziona dunia hizo, mwandishi anamfanya msomaji wake ahitimishe kwa mambo matatu haya:
Kwanza, watu wa aina ya K, ambao wameendeleza dhuluma kubwa kwa kutumia vyeo na majina yao, huwa wanaishi na khofu ya milele ya kuporomoka. Matokeo yake, kila siku hutamani na kupigania kwenda juu na juu zaidi kusudi wasifikwe na walio chini, ambao wanadhani kuwa endapo mikono yao itawafikia tu, basi watawashika miguu na shingo zao na kuwaporomosha chini kwa kishindo kikubwa. Kwa hivyo, ishara yoyote ya kuporomoshwa huwatia jaka moyo kubwa na kuwatetemesha hadi machango. Katika ukurasa wa 92, mathalan, mwandishi anatuonesha namna K anavyogwaya akiliogopa anguko lake:
“Ghafla alijihisi anachukuliwa na lepe jengine lililomdidimiza katka singizi zito la ajabu. Alitumbukia kwenye singizi huku akienda. Lilikuja tu kwa hakika hilo singizi ama upepo wa ghafla. Lilikuja kumvaa na kumdidimiza kwenye maweko ya chini ya kiini cha dunia. Alihisi anazama kwenye dimbwi refu lisilo ukomo… di, di, di… alididimia mpaka akajihisi ameibuka pahala penye mwangaza wa maisha. Akajihisi kama katupwa hapo. Katupwa kama gunia. Moyo ukaanza kupiga beni alipogundua hivyo. Aa, kubwagwa kila siku yeye alikuwa akikuogopa. Kuanguka alikuchelea. Akihofu kutupwa, hasa namna hiyo.”
Pili, msomaji anahitimisha kuwa watawala wa aina ya K wanakuwa wanajijuwa hasa kwamba wamewakosea raia. Kwa hivyo, kila wanapokaa huwa wanajitia wasiwasi kuwa wanaandamwa au wanafuatwafuatwa na watu hao wenye hasira na wakati wowote wanaweza kulipiziwa kisasi kwa maovu yao. Hayo ndiyo matokeo ya kuishi kwa dhuluma. Siku zote huwa unakhofu kuwa madhulumu wako watakurudi kwa yale uliyowatenda. Huwa huko huru. Angalia vile wanavyopita barabarani kwenye magari yaliyofungwa vioo vyote, tena vyeusi visivyopenya risasi na bado mbele yao ving’ora mita kadhaa ili wapishwe njia peke yao na bado maaskari kibao na bunduki. Hawa hawafanyi yale kwa kupenda, bali kutokana na khofu waliyonayo kwa umma walioukosea (Uk.24-7). Wakati Babu anamzukia K kwa mara ya kwanza kwenye ndoto-macho zake, alijitambulisha kwa namna hii:
“Nikwambie tena, mimi ni babu yako; kisha niongeze kuwa mimi ni dhahiri kwa kisia kikubwa kuliko hata wewe, kwa sababu sina farakano na watu. Wala sina makiwa na utawa kama ulionao wewe. Sina hofu wala siogopi kama uogopavyo wewe. Nakwenda nipendapo. Nakutana na nimpendaye. Ufunguo wa kasi yangu ninao mwenyewe. Hakuna niliyemdhulumu.” (Uk. 21-2)
Tatu, msomaji anahitimisha kuwa khofu hizi za watawala zina uhalali wake na ni za kweli. Ni kweli kuwa wananchi walioonewa na kudhulumiwa kwa miaka mingi hufika pahala pa kusema “hapana” kwa watawala wao. Miongoni mwao huwa wanasema hivyo kwa maneno, wengine kwa vitendo, wengine wakiwa na akili zao na wengine tayari wameshachanganyikiwa kwa mateso ya muda mrefu. La muhimu ni kuwa wananchi hufika mahala wakasema “liwalo na liwe” lakini hawatakubali tena dhuluma nyengine dhidi yao. Katika ukurasa wa 92, K alimkuta Mussa katika eneo la Kataa akijisemea peke yake njiani:
“La, hatutaki, hata ikiwaje hatutali tena…. La, hatutaki, hata iwaje hatutali tena…. La, hatutaki, hata ikawaje, hatutali tena..”
Lakini madhulumu wengine huamua kwenda mbali zaidi ya kupita mitaani wakijisemea peke yao tu. Wao huamua kuwarudi madhalimu wao kwa namna yoyote ile wanayoiona inawafalia na wanaimudu. Mno yachosha eti! Na ni hiki ndicho ambacho kinadhihirika mwishoni, pale umma uliokwishachoshwa na udhalimu wa watawala wao, unapoingia barabarani na kuukabili mkono wa utawala.
“Nje aliwakuta wale mahasimu zake wamejipanga upande huu na huu wa njia. Sasa walikuwa mamia kwa mamia… Kuna waliochukuwa marungu na wengine mabango yaliyoandikwa maneno mengi…M’MEZIFISIDI NAFSI ZETU…. MMEVUNJA HESHIMA ZETU…. VIJANA WETU WANAPOTEA… VIFO NA NJAA NA MARADHI SABABU SI SISI… HATUNA NAFASI PANAPOSTAHIKI NAFASI ZETU… ARDHI INACHUKULIWA HIVI HIVI TUNAONA…. KESHO YETU IMO KATIKA GIZA…TUNAANGAMIA…TUMESHAKWENDA KAPA…na zaidi na zaidi…Mlio ule wa bunduki K aliusikia ndani apokuwa tayari ameshakua kitini ofisini mwake. Alitetemeka kwa muda. Lakini alipojishika, aligunduwa kwamba hata ofisini mambo yalikuwa yamegeuka pia.” (Uk. 154-56)
Riwaya inamalizika kwa kumuonesha K akipoteza kila kitu – ulwa, nyumba, gari na, zaidi kuliko yote, hata ile heshima aliyojidhani alikuwa nayo. Na mwisho anakufa kifo cha kidhalilifu kama alivyosababisha maelfu ya wengine kufa katika udhalilifu kwenye zama za madaraka yake.
“Alfajiri ya siku ya pili, watu wa kijiji kile waliamshwa na sauti ya jibwa kubwa, Biye aliloliita Doggy. Ilikuwa si kawaida jibwa kubwa kama lile kubweka kwa muda mrefu namna ile hapo kijijini. Walipoufuata mbweko wa jibwa, walimkuta K ananing’inia kwenye kigogo cha mti uliokuwa umeota katikati ya kaburi la Babu. Alikuwa mkavu keshang’ang’anaa.”(Uk.165)
Naam, hapa ndipo hasira ya umma ilipomfikisha K. Hapa, kwa hakika, ndipo kiuhalisia wafikishwapo watawala madhalimu wa aina yake. Hivyo ndivyo umma unavyomuhukumu mkosaji wake. Umma ukikosewa kiasi kikubwa kama hiki, ni wenyewe ndio ambao hushitaki, na wenyewe ukahukumu. Na hivi ndivyo Babu Alipofufuka na kumtahadharisha mjukuu wake, K:
“…Pia unashitakiwa na wakati ulioutumia vibaya…Unashitakiwa vile vile na matendo yako mwenyewe…matendo ya upotofu…Maovu yako mwenyewe….Hakuna uchaguzi. Huna njia. Wakati ukifika, utakwenda tu; utakwenda tu…” (Uk. 137)   Chanzo >>>>>>>
]]>
<![CDATA[VUTA N’KUVUTE YA SHAFI ADAM SHAFI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1048 Sat, 28 Aug 2021 03:58:22 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1048
Kwa miongo mingi sasa, wahakiki wa kazi za fasihi wamezisifu kazi za waandishi wa Kizanzibari kwa sifa tele. Kwa mfano, akirejea riwaya za Mohamed Suleiman Mohamed, Said Ahmed Mohamed na Shafi Adam Shafi, M. M. Mulokozi aliandika mwaka 1985: “Maendeleo muhimu kabisa, na pengine ya kufurahisha sana, katika kazi za fasihi za Kiswahili katika miaka ya 1970 na 1980, ni kuibuka kwa Zanzibar kama mtoaji bora kabisa wa kazi za Kiswahili kuwahi kutokea hadi sasa, na kiongozi wa wazi wa riwaya za Kiswahili katika siku zijazo.”
Hisia kama hizi zinaelezewa pia na R. Ohly ambaye, baada ya kukumbana na riwaya zilizoandikwa na waandishi wa Kizanzibari na wale wa Kitanzania na Kikenya baina ya mwaka 1975 na 1981, amezielezea riwaya za Kizanzibari kama changamoto kubwa kwa uwezo wa kisanaa kwa waandishi wengine wa Kiswahili.
Ingawa mnasaba uliotumiwa na Ohly unaweza kujadilika kwa kujikita kwake na kazi zilizotolewa Bara hasa hadithi fupi fupi na kuwaacha waandishi wenye vipaji kama vile Euphrase Kezilahabi au Claude Mung’ong’o, uhakiki wake bado umezungumzia sifa kuu za riwaya za Kizanzibari, yaani kujikita sana kwenye masuala ya kihistoria na kijamii, pamoja na utajiri wa lugha mwanana na kutokufanya mzaha kwenye masuala ya fani.
Sifa hizi za fani zinashabihiana sana na riwaya ya ‘Vuta N’kuvute’ iliyoandikwa na Shafi Adam Shafi na kuchapishwa mwaka 1999, ambayo ndiyo shughuliko la uhakiki huu.
Waandishi wa Kizanzibari mara kadhaa wameandika riwaya za kihistoria, wakizikita simulizi zao katika zama za ukoloni ama za kabla ya Mapinduzi visiwani humo. Kufuatia hali hiyo, matukio kwenye ‘Vuta N’kuvute’ nayo yanazungumzia siku za mwisho mwisho za ukoloni visiwani Zanzibar.
Mandhari ya riwaya hii ni changamano sana, maisha ya dhiki ya wahusika wakuu yanachorwa kupitia matukio kadhaa, wahusika wadogo, matendo ya kuchangamsha, yote yanaunganishwa na mapenzi ya uhuru na kujitawala katika viwango tafauti vya maisha ya kibinafsi, kijamii na kisiasa, na hivyo kuusafirisha ule moyo wa Ujamaa katika muonekano wa kilimwengu zaidi.
Hadithi yenyewe inaanza kwa kumtambulisha msomaji kwa msichana wa Kihindi, Yasmin, ambaye kutokana na mila ya ndoa za kupangwa na wazazi, anakwenda Mombasa na mume wake, mfanyabiashara mzee, Bwana Raza. Lakini Yasmin anaoneshwa kuwa mtu asiye na furaha na mpweke na hatimaye anaasi na kurudi nyumbani, Zanzibar.
Kutabiri matokeo ya makuzi mabaya ni jambo maarufu kwenye riwaya za Kiswahili, ambapo kawaida waandishi huchora mashaka yale yale yanayoathiri maisha ya vijana, hasa wa kike, ama kushindwa hadi kufikia mauti yao au mateso ya kiakili na kimwili kama vile Rosa Mistika au Asumini, au kukimbia mazingira kandamizi kama vile Maimuna na Yasmin, ambapo mote hupelekea maisha mapya kabisa.
Mara tu baada ya kurudi Zanzibar, Yasmin anakataliwa na mjomba wake na anaomba msaada wa shoga yake wa pekee, Mwajumba, msichana wa Kiswahili anayeishi kwenye mitaa ya masikini ya Ng’ambo, ambaye anampokea kwa moyo wote.
Licha ya ukarimu wa Mwajuma, mama yake Yasmin anakataa kumsamehe bintiye sio tu kwa kuiabisha familia kwa kumuasi mumewe, bali pia kwa kujichanganya na Waswahili na hivyo kuvunja khulka ya jamii yake na tafauti za kijamii na kitamaduni zilizojikita sana kwenye unyanyapaa wa sera za kikoloni linapohusika suala la mahusiano kati ya makabila yanayounda jamii kubwa ya Kizanzibari.
Baada ya kukandamizwa kwenye misuguano na ubaguzi wa kijamii huko alikokulia, Yasmin anapata ladha ya maisha mapya wakati akiishi kwa Mwajuma, ambako anagundua maisha yenye wasaa zaidi, mukiwemo ulevi, klabu za usiku na, zaidi ya yote, anapendana na kijana aitwaye Denge.
Denge ni kijana msomi aliyerejea nyumbani akitokea Ulaya akiwa hana chochote zaidi ya digrii yake ya Kirusi na dhamira madhubuti ya kuikomboa nchi yake kutoka kwenye Himaya ya Mwingereza. Yeye na marafiki zake wanaandamwa na polisi kwa kufanya propaganda ya kisiasa na kuingiza kwenye nchi vitabu na magazeti yaliyopigwa marufuku na wakoloni.
Yasmin anajikuta akihusika moja kwa moja katika mapambano kati ya kundi la Denge na polisi, ambao wanajaribu kumlazimisha amsaliti mpenzi wake “mkomunisti” na “kafiri”, lakini anaamua kuwasaidia wanaharakati hao, akiamini wanaandamwa kwa sababu tu wanapigania uhuru.
Kama inavyoelezwa na Denge katika ukurasa wa 68 wa riwaya hii, serikali ya Kiingereza ilijaribu kuwatenganisha wapigania uhuru na wafuasi wao kwa kutumia sera ya wagawe uwatawale:
“Sikiliza Sista, hawa wakoloni na vijibwa vyao ni watu wapumbavu kabisa, kwao kila mtu ni koministi Ukidai haki yako wewe koministi Ukisema kweli wewe koministi Ukipinga kutawaliwa wewe koministi. Kila anayedai haki kwao ni koministi, na sumu yao kubwa wanayoitumia ya kutaka kutenganisha watu kama hao na wananchi wenziwao ni kusema kwamba watu hao wanaowaita makoministl hawaamini Mungu.”
Mapambano ya daima kati ya maafisa wa kikoloni na wapigania uhuru yanaipeleka riwaya hii kwenye upeo wa hadithi ya kusisimua, kurusha roho na hekaya za kijasusi, mtindo ambao uliletwa kwa mara ya kwanza kwenye riwaya za Kiswahili na Mohamed Said Abdulla (Bwana MSA), ingawa kwenye riwaya hii polisi wamekuwa wahusika wabaya, wanaotumikia maslahi ya kikoloni kibubusa.
Kama inavyoelezewa na Pazi katika ukurasa wa 113, katika mapambano ya kuwania uhuru, ni muhimu kutumia hata njia zisizo za halali kisheria:
“Wakati tunapambana na adui lazima tutumie mbinu zote tunazoweza kuzitumia. Pale inapoyumkinika kutumia mbinu za dhahiri basi tuzitumie kwa kadiri ya uwezo wetu.. Pale ambapo hapana budi ila kutumia njia ya siri kwani mapambano yetu ni ya vuta n’kuvute. Wao wanavutia kule na sisi tunavutia huku na katika mvutano huo hapana suluhisho linaloweza kupatikana isipokuwa kuwa huru. Uhuru ndiyo suluhisho, kwa hivyo lazima tutumie mbinu mbalimbali katika kutafuta suluhisho hilo.”
Jambo la kufurahisha ni kuwa upinzani na mapambano kwenye riwaya hii hayajumuishi vitendo vya kutumia nguvu dhidi ya binaadamu wengine, bali maandamano na mashambulizi dhidi ya alama ya nguvu za kikoloni (kama vile mikahawa iliyotengewa watu wa matabaka fulani tu), kusambaza kazi ambazo zinachukuliwa na serikali kuwa ni haramu na uanzishaji wa gazeti liitwalo Kimbunga.
Mambo yote haya yanaelezewa kwenye Vuta n’kuvute kama kipimo cha majaribu ya mapambano ya kusaka uhuru.
Hapa pia, kama ilivyo kwenye kazi nyingi za Kizanzibari, tunaona uhusiano wa wazi baina ya jina na maudhi, ambao ishara yake inajidhihirisha wazi  kwenye mtiririko wa visa unaomsaidia msomaji kuitafsiri riwaya katika muktadha wa kihistoria.
Katika Vuta n’kuvute, uhuru wa mawazo na kujieleza ni sehemu muhimu ya mapambano ya jumla, lakini baadhi ya wakati pande hizo mbili hukinzana. Kwa mfano, wakati mwengine mtu kusimamia haki yake kwenye mapenzi ni jambo la anasa linapolinganishwa na suala la ulinzi wa nchi, kama anavyoungama Denge katika ukurasa wa 145:
“Yasmin mimi najua kama unanipenda, na mimi nakupenda vile vile, lakini kuna kitu kimoja napenda uelewe. Kuna mapenzi na wajibu wa mtu katika jamii. Kila mtu ana wajibu fulani katika jamii na mimi wajibu wangu mkubwa ni kufanya kila niwezalo kwa kushirikiana na wenzangu ambao wengine unawajua na wengine huwajui ili kuona kwamba nchi hii inakuwa huru. Hii ni kazi ngumu, ina matatizo mengi na inahitaji kujitolea muhanga na mimi ni miongoni mwa hao waliojitolea muhanga kufa, kupona, potelea mbali. Tupo wengi tuliojitolea namna hiyo, tena wengi sana, maelfu.”
Maisha ya Denge yametolewa muhanga kwa kile akiaminicho, ikiwemo kutengwa au kuishi uhamishoni, na Yasmin anapaswa kukubali majaaliwa yake ya upweke, na kushika njia akaenda zake.
Kwa mara nyengine, Yasmin anakabiliwa na upotoshaji wa kikabila. Makutano yake na Bukheti, aliyewahi kuwa jirani yake Mombasa, yanapingwa na familia zote mbili, zikionesha khofu na dharau zao kwake kama mkando.
Anadhalilishwa kwa kila aina ya maneno machafu, kama anavyoibuka na kutoa kauli kwenye ukurasa wa 254:
“Iko wapi heshima ya binadamu, ikiwa Muhindi anamwita Mswahili golo na Mswahili naye anamwita Muhindi ponjoro?”
Upatanishi uliofanywa na marafiki wa zamani wa kifamilia na ambao ni watu wenye mwamko, unasaidia kuzitenga kando dharau hizo; na riwaya hiyo inamalizia kwenye muunganiko wa furaha, unaofunikwa na ghamu ya Yasmin.
Tukio la mwisho lenye kumuacha msomaji na athari kubwa kutoka riwaya hiyo linaelezewa kwa nyimbo ya Kihindi ambayo Yasmin aliisikiliza Mombasa, na kudimka peke yake kutuliza roho yake na pia kuiimba kwenye kundi la taarab kisiwani Unguja.
Daima Yasmin anauchukulia muziki kama kimbilio binafsi na beti za nyimbo hizo zinamkumbusha utamu na ukali wa uhuru.
Fani
Sasa natuangalie baadhi ya vipengele vya usimulizi wa riwaya hii ya Vuta n’kuvute, tukichunguza zaidi muundo wa hadithi yenyewe, mitindo na matumizi ya lugha.
Kama zilivyo kazi nyingi za Kizanzibari, kazi hii ina kiwango kikubwa cha kisanii, ikiwa imejengwa kwa sura fupifupi kumi na nane, zinazokwendana na mjengeko wa matukio, mikasa, na mapigo yanayomfanya msomaji azidi kupata hamu ya kuisoma.
Kipengele cha wakati kwenye riwaya hii kwa jumla kimetumika vyema – ni nadra kukuta matukio yanayoelezewa kwa kurudi nyuma, kama lile la maisha ya Denge barani Ulaya.
Mtiririko wa visa unasimulia hadithi mbalimbali za maisha ya wahusika wakuu, wakati mwengine zinazopishana na wakati mwengine kuoana. Matukio mengi ni muhimu sana kwa mjengeko mzima wa riwaya.
Ufundi huu wa uandishi unaipa riwaya sifa ya kuwa “riwaya ya masimulizi” bila ya kuondosha mantiki ya matukio kama lile la mazingira ya Roger na Salum kumtembelea Mwajuma na ugomvi uliozuka baina ya wanaume hao wawili.
Mwandishi amefanikiwa kwa ustadi mkubwa kuweka mizani baina ya mbinu za kuonesha (ambapo matukio huwa yanasimuliwa na wahusika) na ile ya kuelezea (ambapo matukio yanasimuliwa na msimulizi, yaani mwandishi mwenyewe).
Uwasilishaji wa msimulizi aliye wazi na aliyejificha ni miongoni mwa vipengele vya ubora kwenye kazi za fasihi, na katika riwaya hii tangu awali kabisa msimulizi huyo huonekana kwa sura zote mbili na katika viwango tafauti.
Kwa mfano, riwaya hii imejengwa kwa majibizano – ambapo msimulizi anakuwa haonekani kabisa – sio tu kwenye mazungumzo mafupi mafupi, lakini zaidi kwenye mistari mirefu ya kujenga hoja, lakini wakati mwengine majibizano haya huchukua nafasi muhimu sana katika kutoa taarifa kuhusu wahusika na au ujumbe muhimu, ambao mwandishi anauwasilisha kwa hadhira yake, kama dondoo za Denge na Pazi zilizotajwa hapo juu.
Ndani ya riwaya hii, msomaji anagundua pia matumizi ya kauli zisizo za moja kwa moja, ambako maneno au mawazo yanasimuliwa na msimulizi lakini yakinasibishwa kwa ukaribu sana na mhusika, kama vile kwenye ukurasa wa 49 pale mwandishi anapoelezea namna Yasmin alivyomuona Denge kwa mara ya kwanza:
“Kwa Yasmin huyo alikuwa n’do Mwafrika wa kwanza kuambiwa ametoka Ulaya. Shilingi mbili za kununua ukanda wa kufungia suruali yake zinamshinda, na ile suruali isiyokuwa na pasi aliyovaa imezuiliwa kiunoni kwa tai labda aliyorudi nayo kutoka huko Ulaya, na hivyo viatu alivyovaa, karibu vidole vingine vinataka kuchungulia nje.”]]>
Kwa miongo mingi sasa, wahakiki wa kazi za fasihi wamezisifu kazi za waandishi wa Kizanzibari kwa sifa tele. Kwa mfano, akirejea riwaya za Mohamed Suleiman Mohamed, Said Ahmed Mohamed na Shafi Adam Shafi, M. M. Mulokozi aliandika mwaka 1985: “Maendeleo muhimu kabisa, na pengine ya kufurahisha sana, katika kazi za fasihi za Kiswahili katika miaka ya 1970 na 1980, ni kuibuka kwa Zanzibar kama mtoaji bora kabisa wa kazi za Kiswahili kuwahi kutokea hadi sasa, na kiongozi wa wazi wa riwaya za Kiswahili katika siku zijazo.”
Hisia kama hizi zinaelezewa pia na R. Ohly ambaye, baada ya kukumbana na riwaya zilizoandikwa na waandishi wa Kizanzibari na wale wa Kitanzania na Kikenya baina ya mwaka 1975 na 1981, amezielezea riwaya za Kizanzibari kama changamoto kubwa kwa uwezo wa kisanaa kwa waandishi wengine wa Kiswahili.
Ingawa mnasaba uliotumiwa na Ohly unaweza kujadilika kwa kujikita kwake na kazi zilizotolewa Bara hasa hadithi fupi fupi na kuwaacha waandishi wenye vipaji kama vile Euphrase Kezilahabi au Claude Mung’ong’o, uhakiki wake bado umezungumzia sifa kuu za riwaya za Kizanzibari, yaani kujikita sana kwenye masuala ya kihistoria na kijamii, pamoja na utajiri wa lugha mwanana na kutokufanya mzaha kwenye masuala ya fani.
Sifa hizi za fani zinashabihiana sana na riwaya ya ‘Vuta N’kuvute’ iliyoandikwa na Shafi Adam Shafi na kuchapishwa mwaka 1999, ambayo ndiyo shughuliko la uhakiki huu.
Waandishi wa Kizanzibari mara kadhaa wameandika riwaya za kihistoria, wakizikita simulizi zao katika zama za ukoloni ama za kabla ya Mapinduzi visiwani humo. Kufuatia hali hiyo, matukio kwenye ‘Vuta N’kuvute’ nayo yanazungumzia siku za mwisho mwisho za ukoloni visiwani Zanzibar.
Mandhari ya riwaya hii ni changamano sana, maisha ya dhiki ya wahusika wakuu yanachorwa kupitia matukio kadhaa, wahusika wadogo, matendo ya kuchangamsha, yote yanaunganishwa na mapenzi ya uhuru na kujitawala katika viwango tafauti vya maisha ya kibinafsi, kijamii na kisiasa, na hivyo kuusafirisha ule moyo wa Ujamaa katika muonekano wa kilimwengu zaidi.
Hadithi yenyewe inaanza kwa kumtambulisha msomaji kwa msichana wa Kihindi, Yasmin, ambaye kutokana na mila ya ndoa za kupangwa na wazazi, anakwenda Mombasa na mume wake, mfanyabiashara mzee, Bwana Raza. Lakini Yasmin anaoneshwa kuwa mtu asiye na furaha na mpweke na hatimaye anaasi na kurudi nyumbani, Zanzibar.
Kutabiri matokeo ya makuzi mabaya ni jambo maarufu kwenye riwaya za Kiswahili, ambapo kawaida waandishi huchora mashaka yale yale yanayoathiri maisha ya vijana, hasa wa kike, ama kushindwa hadi kufikia mauti yao au mateso ya kiakili na kimwili kama vile Rosa Mistika au Asumini, au kukimbia mazingira kandamizi kama vile Maimuna na Yasmin, ambapo mote hupelekea maisha mapya kabisa.
Mara tu baada ya kurudi Zanzibar, Yasmin anakataliwa na mjomba wake na anaomba msaada wa shoga yake wa pekee, Mwajumba, msichana wa Kiswahili anayeishi kwenye mitaa ya masikini ya Ng’ambo, ambaye anampokea kwa moyo wote.
Licha ya ukarimu wa Mwajuma, mama yake Yasmin anakataa kumsamehe bintiye sio tu kwa kuiabisha familia kwa kumuasi mumewe, bali pia kwa kujichanganya na Waswahili na hivyo kuvunja khulka ya jamii yake na tafauti za kijamii na kitamaduni zilizojikita sana kwenye unyanyapaa wa sera za kikoloni linapohusika suala la mahusiano kati ya makabila yanayounda jamii kubwa ya Kizanzibari.
Baada ya kukandamizwa kwenye misuguano na ubaguzi wa kijamii huko alikokulia, Yasmin anapata ladha ya maisha mapya wakati akiishi kwa Mwajuma, ambako anagundua maisha yenye wasaa zaidi, mukiwemo ulevi, klabu za usiku na, zaidi ya yote, anapendana na kijana aitwaye Denge.
Denge ni kijana msomi aliyerejea nyumbani akitokea Ulaya akiwa hana chochote zaidi ya digrii yake ya Kirusi na dhamira madhubuti ya kuikomboa nchi yake kutoka kwenye Himaya ya Mwingereza. Yeye na marafiki zake wanaandamwa na polisi kwa kufanya propaganda ya kisiasa na kuingiza kwenye nchi vitabu na magazeti yaliyopigwa marufuku na wakoloni.
Yasmin anajikuta akihusika moja kwa moja katika mapambano kati ya kundi la Denge na polisi, ambao wanajaribu kumlazimisha amsaliti mpenzi wake “mkomunisti” na “kafiri”, lakini anaamua kuwasaidia wanaharakati hao, akiamini wanaandamwa kwa sababu tu wanapigania uhuru.
Kama inavyoelezwa na Denge katika ukurasa wa 68 wa riwaya hii, serikali ya Kiingereza ilijaribu kuwatenganisha wapigania uhuru na wafuasi wao kwa kutumia sera ya wagawe uwatawale:
“Sikiliza Sista, hawa wakoloni na vijibwa vyao ni watu wapumbavu kabisa, kwao kila mtu ni koministi Ukidai haki yako wewe koministi Ukisema kweli wewe koministi Ukipinga kutawaliwa wewe koministi. Kila anayedai haki kwao ni koministi, na sumu yao kubwa wanayoitumia ya kutaka kutenganisha watu kama hao na wananchi wenziwao ni kusema kwamba watu hao wanaowaita makoministl hawaamini Mungu.”
Mapambano ya daima kati ya maafisa wa kikoloni na wapigania uhuru yanaipeleka riwaya hii kwenye upeo wa hadithi ya kusisimua, kurusha roho na hekaya za kijasusi, mtindo ambao uliletwa kwa mara ya kwanza kwenye riwaya za Kiswahili na Mohamed Said Abdulla (Bwana MSA), ingawa kwenye riwaya hii polisi wamekuwa wahusika wabaya, wanaotumikia maslahi ya kikoloni kibubusa.
Kama inavyoelezewa na Pazi katika ukurasa wa 113, katika mapambano ya kuwania uhuru, ni muhimu kutumia hata njia zisizo za halali kisheria:
“Wakati tunapambana na adui lazima tutumie mbinu zote tunazoweza kuzitumia. Pale inapoyumkinika kutumia mbinu za dhahiri basi tuzitumie kwa kadiri ya uwezo wetu.. Pale ambapo hapana budi ila kutumia njia ya siri kwani mapambano yetu ni ya vuta n’kuvute. Wao wanavutia kule na sisi tunavutia huku na katika mvutano huo hapana suluhisho linaloweza kupatikana isipokuwa kuwa huru. Uhuru ndiyo suluhisho, kwa hivyo lazima tutumie mbinu mbalimbali katika kutafuta suluhisho hilo.”
Jambo la kufurahisha ni kuwa upinzani na mapambano kwenye riwaya hii hayajumuishi vitendo vya kutumia nguvu dhidi ya binaadamu wengine, bali maandamano na mashambulizi dhidi ya alama ya nguvu za kikoloni (kama vile mikahawa iliyotengewa watu wa matabaka fulani tu), kusambaza kazi ambazo zinachukuliwa na serikali kuwa ni haramu na uanzishaji wa gazeti liitwalo Kimbunga.
Mambo yote haya yanaelezewa kwenye Vuta n’kuvute kama kipimo cha majaribu ya mapambano ya kusaka uhuru.
Hapa pia, kama ilivyo kwenye kazi nyingi za Kizanzibari, tunaona uhusiano wa wazi baina ya jina na maudhi, ambao ishara yake inajidhihirisha wazi  kwenye mtiririko wa visa unaomsaidia msomaji kuitafsiri riwaya katika muktadha wa kihistoria.
Katika Vuta n’kuvute, uhuru wa mawazo na kujieleza ni sehemu muhimu ya mapambano ya jumla, lakini baadhi ya wakati pande hizo mbili hukinzana. Kwa mfano, wakati mwengine mtu kusimamia haki yake kwenye mapenzi ni jambo la anasa linapolinganishwa na suala la ulinzi wa nchi, kama anavyoungama Denge katika ukurasa wa 145:
“Yasmin mimi najua kama unanipenda, na mimi nakupenda vile vile, lakini kuna kitu kimoja napenda uelewe. Kuna mapenzi na wajibu wa mtu katika jamii. Kila mtu ana wajibu fulani katika jamii na mimi wajibu wangu mkubwa ni kufanya kila niwezalo kwa kushirikiana na wenzangu ambao wengine unawajua na wengine huwajui ili kuona kwamba nchi hii inakuwa huru. Hii ni kazi ngumu, ina matatizo mengi na inahitaji kujitolea muhanga na mimi ni miongoni mwa hao waliojitolea muhanga kufa, kupona, potelea mbali. Tupo wengi tuliojitolea namna hiyo, tena wengi sana, maelfu.”
Maisha ya Denge yametolewa muhanga kwa kile akiaminicho, ikiwemo kutengwa au kuishi uhamishoni, na Yasmin anapaswa kukubali majaaliwa yake ya upweke, na kushika njia akaenda zake.
Kwa mara nyengine, Yasmin anakabiliwa na upotoshaji wa kikabila. Makutano yake na Bukheti, aliyewahi kuwa jirani yake Mombasa, yanapingwa na familia zote mbili, zikionesha khofu na dharau zao kwake kama mkando.
Anadhalilishwa kwa kila aina ya maneno machafu, kama anavyoibuka na kutoa kauli kwenye ukurasa wa 254:
“Iko wapi heshima ya binadamu, ikiwa Muhindi anamwita Mswahili golo na Mswahili naye anamwita Muhindi ponjoro?”
Upatanishi uliofanywa na marafiki wa zamani wa kifamilia na ambao ni watu wenye mwamko, unasaidia kuzitenga kando dharau hizo; na riwaya hiyo inamalizia kwenye muunganiko wa furaha, unaofunikwa na ghamu ya Yasmin.
Tukio la mwisho lenye kumuacha msomaji na athari kubwa kutoka riwaya hiyo linaelezewa kwa nyimbo ya Kihindi ambayo Yasmin aliisikiliza Mombasa, na kudimka peke yake kutuliza roho yake na pia kuiimba kwenye kundi la taarab kisiwani Unguja.
Daima Yasmin anauchukulia muziki kama kimbilio binafsi na beti za nyimbo hizo zinamkumbusha utamu na ukali wa uhuru.
Fani
Sasa natuangalie baadhi ya vipengele vya usimulizi wa riwaya hii ya Vuta n’kuvute, tukichunguza zaidi muundo wa hadithi yenyewe, mitindo na matumizi ya lugha.
Kama zilivyo kazi nyingi za Kizanzibari, kazi hii ina kiwango kikubwa cha kisanii, ikiwa imejengwa kwa sura fupifupi kumi na nane, zinazokwendana na mjengeko wa matukio, mikasa, na mapigo yanayomfanya msomaji azidi kupata hamu ya kuisoma.
Kipengele cha wakati kwenye riwaya hii kwa jumla kimetumika vyema – ni nadra kukuta matukio yanayoelezewa kwa kurudi nyuma, kama lile la maisha ya Denge barani Ulaya.
Mtiririko wa visa unasimulia hadithi mbalimbali za maisha ya wahusika wakuu, wakati mwengine zinazopishana na wakati mwengine kuoana. Matukio mengi ni muhimu sana kwa mjengeko mzima wa riwaya.
Ufundi huu wa uandishi unaipa riwaya sifa ya kuwa “riwaya ya masimulizi” bila ya kuondosha mantiki ya matukio kama lile la mazingira ya Roger na Salum kumtembelea Mwajuma na ugomvi uliozuka baina ya wanaume hao wawili.
Mwandishi amefanikiwa kwa ustadi mkubwa kuweka mizani baina ya mbinu za kuonesha (ambapo matukio huwa yanasimuliwa na wahusika) na ile ya kuelezea (ambapo matukio yanasimuliwa na msimulizi, yaani mwandishi mwenyewe).
Uwasilishaji wa msimulizi aliye wazi na aliyejificha ni miongoni mwa vipengele vya ubora kwenye kazi za fasihi, na katika riwaya hii tangu awali kabisa msimulizi huyo huonekana kwa sura zote mbili na katika viwango tafauti.
Kwa mfano, riwaya hii imejengwa kwa majibizano – ambapo msimulizi anakuwa haonekani kabisa – sio tu kwenye mazungumzo mafupi mafupi, lakini zaidi kwenye mistari mirefu ya kujenga hoja, lakini wakati mwengine majibizano haya huchukua nafasi muhimu sana katika kutoa taarifa kuhusu wahusika na au ujumbe muhimu, ambao mwandishi anauwasilisha kwa hadhira yake, kama dondoo za Denge na Pazi zilizotajwa hapo juu.
Ndani ya riwaya hii, msomaji anagundua pia matumizi ya kauli zisizo za moja kwa moja, ambako maneno au mawazo yanasimuliwa na msimulizi lakini yakinasibishwa kwa ukaribu sana na mhusika, kama vile kwenye ukurasa wa 49 pale mwandishi anapoelezea namna Yasmin alivyomuona Denge kwa mara ya kwanza:
“Kwa Yasmin huyo alikuwa n’do Mwafrika wa kwanza kuambiwa ametoka Ulaya. Shilingi mbili za kununua ukanda wa kufungia suruali yake zinamshinda, na ile suruali isiyokuwa na pasi aliyovaa imezuiliwa kiunoni kwa tai labda aliyorudi nayo kutoka huko Ulaya, na hivyo viatu alivyovaa, karibu vidole vingine vinataka kuchungulia nje.”]]>
<![CDATA[UDHANAISHI KATIKA RIWAYA YA KICHWAMAJI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1047 Sat, 28 Aug 2021 03:53:14 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1047
.pdf   MUKHTASARI NA UCHAMBUZI WA FASIHI.pdf (Size: 157.86 KB / Downloads: 3) ]]>

.pdf   MUKHTASARI NA UCHAMBUZI WA FASIHI.pdf (Size: 157.86 KB / Downloads: 3) ]]>
<![CDATA[FALSAFA YA KIAFRIKA NA RIWAYA YA KISWAHILI]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1046 Sat, 28 Aug 2021 03:36:31 +0000 MwlMaeda]]> https://jifunzekiswahili.co.tz/showthread.php?tid=1046
Huyu ni mwanafalsafa maarufu aliyezaliwa nchini Kenya, alitumikia waasifu wa uparoko katika kanisa la Roman Catholic (RC). Aliandika maandiko mawili yaliyotalii falsafa ya kiafrika “Africa Religious Philosophy (1966) and African concept of God (1970). Alizungumzia yafuatayo kuhusu falsafa ya kiafrika.
Dhana ya wakati; kwa waafrika hawaangalii wakati na hawana haraka na wakati, mwafrika katika kuangalia wakati, namba za saa ni kitu dhahania, kwa mwafrika wakati hauamui matendo kama ilivyo kwa mzungu, dhana hii imedhihirika katika riwaya ya “ Nagona” kwa muhusika babu alipokuwa akimweleza mjukuu mwaka wake wa kuzaliwa kwa kuyarejea matukio kama matukio ya “utupu” ajali gharika kupatwa kwa jua kama asemavyo mwandishi.
“……nataka kujua habari za kuzaliwa kwangu wazazi wangu hajapata kunieleza kikamilifu….. natakueleza. Hivi ndivyo ilivyokuwa…….hapakuwa na ujuzi wa jema na baya. Hapakuwa na fikra. Palikuwa na utupu katika kitovu cha undani na hapakuwa na nguvu zilizoweza kutoa uongozi…….. ajali hii ilitokea katika bonde la hisia……. Katika ukweli huu palitokea gharika katika mto wa bonde…..(uk 11)”.
Vilevile katika kitabu cha riwaya ya “Mirathi ya hatari”  wazo limethibitishwa na familia ya Mzee Kazembe alivyokuwa akijilimisha usiku na mchana bila hata ya kuangalia wakati.      “……si yule wa mji wa Kazembe ajilimishaye usiku na mchana..(uk 5)”.
Hata katika mazingira halisi ya waafrika mambo haya yanahalisika.
Dhana ya kifo, Mwafrika anapokaribia kufa huwa anatoa urithi mfano mali, uchawi, jina au maelekezo fulani kuhusu baraka au laana katika “Mirathi ya hatari”, Gusto, kijana wa Mzee Kazembe aliachiwa urithi wa pesa, Mirathi ya hatari (uchawi), mashamba pamoja na baraka anasema.
“….mwanangu nakuachia kazi kubwa. Ni urithi mkubwa ukitumia vema; bali pia ni mirathi ya hatari usipojihadhari nayo. Nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu ya sihiri…(uk 15-16)”.
vile vile, Dina alimuachia maagizo Gusto alisema
 “mali yangu yote isipokuwa kitabu kilicho sandukuni mwangu, uwape maskini” (uk 90).
Pia katika kitabu cha “Nagona” Babu anatoa maagizo au maelezo kwa mjukuu wake baada ya kukaribia kufa alisema
“…. Mjukuu jihadhari siku ya ngoma kuu usikanyagwe daima fuata duara na macho yako wakati wote watazame hapo katikati hicho kitovu kitakapo pasuka mengi yaliyofichika kwa karne nyingi yataonekana harafu kwa shida alisema Nag…..Nag….” (uk 45).
Dini, kwa mwafrika , dini ni chimbuko la mambo yote na kwa asili mwafrika alizaliwa na dini yake, si suala la kujifunza na kusilimishwa; katika “Mirathi ya hatari” ametumia familia ya Mzee  Kazembe, Madoda na Mavengi waliokuwa na dini yao ya asili ilivyokuwa ikifanyika mapangoni usiku pamoja na baadhi yao kuamini dini ya kujifunza na kusilimishwa lakini hawakuiacha kamwe, kama asemavyo mwandishi;
                        “enyi mahoka wa mababu;
                                Enyi wazee mliotangulia
                                Enyi wenzangu,
                                Sikiliza kiapo changu!
                                Sitasema wala kuwaza lolote,
                                La ndani ni la ndani!
                                Nishindwe mara tatu,
                                Pembe hili linichome moto…!(uk 22)
Haya ni maneno yanayoonesha utii wa dini za asili zenye kuamini miungu, mahoka, wazee na binadamu.
Pia katika riwaya ya “Nagona” mwandishi amemtumia mhusika Padri ambaye alikuwa anaamini dini ya kujifunza na kubatizwa (Ukristo) na Wazee walishikiria dini ya kipagani kama dini ya asili kama asemavyo;
“…Padri alikaa kimya, wazee wote walimtazama, Padri alitabasamu aliwatazama wazee halafu akafungua kinywa chake, hakuna mkristo miongoni mwenu?” wazee walitazamana “ Hakuna” babu alijibu. (uk 10).
Hii inadhibitisha kuwa waafrika wanaozithamini dini zao za asili na kuzitupilia mbali dini za wageni kama ukristo hii hata katika mazingira halisi ya kiafrika imetawala sana hususani maeneo ya vijijini.
Kuhusu ufahamu wa ulimwengu na uwapo, waafrika wanaamini kuwa ulimwengu uliumbwa na Mungu na Mungu ndiye muumba wa vyote. Mfano katika riwaya ya “Nagona” imejidhihirisha katika majibizano ya Padri na Mtubu dhambi kama asemayo mwandishi;
                        “…Mmh! Baba unazo dhambi zingine”
                                “kubwa moja na ndogo nyingi”
                                 Lakini unajibebesha mzingo mzito! Dhambi za karne mbili!”
                                “Mungu aliumba ulimwengu na vyote vilivyomo…….” (uk 51)
Pia katika kitabu “Mirathi ya hatari” mwandishi amemtumia Gusto kama mhusika aliyekabiliwa na changamoto nyingi kutoka kwa wanafunzi wenzake katika safari yake ya masomo ila kwa kuwa alimwamini Mungu ndiyo chanzo cha yote hapa duniani alijipa moyo atayashinda kama asemavyo;
“…. Kwani yaliyopita si ndwele tugange yajayo kwa uwezo wa mbingu natumaini nitafanikiwa, sijui nianzie wapi” (uk 4).
Hivyo basi nukuu hii inaonesha jinsi waafrika wanavyotumaini Mungu kuwa hata mambo yawe magumu ama mepesi kuwa ndiyo yeye pekee anayeyajua kwani ndiye aliyeyafanya yawepo hapa dunia au ulimwenguni.
Kwa ujumla John Mbiti anaona kuwa falsafa ya kiafrika ipo na inaendelea kuwepo, na uwepo huo unajidhihirisha katika mambo ya kiutamaduni, japo athari za kiutamaduni wa kigeni unaokweza na sababu za maendeleo ya sayansi na teknolojia na zile za kiutandawazi.
Kwasi Wiredu
Ni miongoni mwa wanafalsafa wa kiafrika, alizaliwa mwaka 1931 katika nchi ya Ghana yeye aliangalia dhana ya Ngano na hadithi. Na jinsi gani zinavyojidhihirisha katika falsafa ya kiafrika. Kwasi Wiredu alidai kuwa waafrika hawana falsafa yao wenyewe bali mawazo yao hujiegemeza katika mapokeo ya watu wa magharibi. Hivyo Kwasi Wiredu katika kulinda mtazamo wake ametoa baadhi ya hoja madhubuti kuhusu kutokuwepo kwa falsafa ya kiafrika.
Hoja zake zinaweza kuwa na ukweli fulani na zisiwe na ukweli fulani kulingana na uchunguzi uliofanyika kwa kutumia riwaya ya “Nagona” na ile ya “Mirathi ya Hatari” kama ifuatavyo:
Mawazo ya kiafrika ya kiutamaduni na kijamii huwa hayabadiliki kulingana na wakati. Suala hili la kutobadilika kwa utamaduni sio tu kwa Afrika bali ni duniani kote. Hii hutokana na waafrika kushikilia baadhi ya misimamo yao kiutamaduni bila kujali mabadiliko ya wakati kutokan na waafrika wenyewe kutoruhusu fikra mpya. Haya yanadhirishwa kwenye riwaya ya “Nagona” japokuwa utamaduni unabadilika lakini mawazo ya kiafrika yanabaki vilevile. Mfano suala la ndoa katika riwaya hii mhusika Mimi alipotaka kumkumbatia msichana ambaye alilkuwa bado hajaolewa ilikuwa ni kinyume na tamaduni za kiafrika mwandishi anasema;
“….nilipomkaribia niliinua tena mikono yangu kuukumbatia mwanga. Lakini aliishika mikono akaishusha tena mahali pake akisema.
“Mila”
“mila gani?”
Myeleka lazima kwanza tupige myeleka ukifanikiwa kunishika na kunitupa kitandani basi umeshinda. Sitakuwa na la kusema. Utaruhusiwa kucheza ngoma kati kati ya duara” (uk 67).
Hii inaonyesha kuwa pamoja na mabadiliko ya wakati lakini bado waafrika wana mawazo yao juu ya utamaduni kwani hata katika jamii zetu mawazo kama haya bado yapo. Mfano, wamasai na wasukuma ili uweze kuoa binti wa kimasai lazima ufuate utamaduni. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” mtunzi anaonyesha hayo pale mtunzi anaposema;
“majira ya wakati yanabadilika mzee wangu…..ukweli ni kwamba sisi wenyewe wazee ni wa kulaumiwa tumeshindwa kutambua kuwa dunia ya leo si dunia yetu….tumeshindwa kutambua kwamba ulimwengu wa leo ni ulimwengu unaobadilika kwa kasi tusiyoweza kuimudu…. Nani kati yenu angetegemea kufika hospitalini na kupimwa huku na mwanamke mwafrika ambaye pia huendesha gari lake mwenyewe (uk 56)”
Hii inaonyesha dhahiri kuwa mawazo ya waafrika hayabadiliki kwani wazee wanashangaa jinsi wanawake wanavyoweza kufanya kazi ambazo hapo awali zilikuwa zikifanywa na wanaume katika jamii zetu pia tuanona kuna wazee ambao bado wanalalamika kwa jinsi waonavyo ulimwengu ulivyobadilika. Kwani kuna mawaziri, wabunge na wakuu wa mikoa.
Afrika hakukuwa na falsafa kwa kuwa mawazo yao yanahusisha wahenga na haina uthibitisho tofauti na ile ya kimagharibi. Kwasi anaamini kuwa Afrika hakuna falsafa kwa kuwa haikuandikwa bali mawazo yao yalihusisha Wahenga tu. Haya yanadhirika kwa kutumia riwaya ya “Nagona” pale mtunzi anaposema;
“…sauti ya kiwiliwili ilisikika kutoka katika mwanga, kwa sasa mazungumzo na roho yako yanatosha utakapo jua kuzungumza na roho yako vizuri mambo yataenda kwa haraka kidogo…..huu si mwanzo mbaya meza roho  yako….”(sura ya tatu (3).
Hii inaonyesha kuwa waafrika wakipata matatizo hukimbilia kuwaomba wahenga ili waweze kuwasaidia katika matatizo hayo. Katika jamii yetu pia kukiwa na matatizo wazee wa jamii huenda kuzungumza na wahenga ili waweze kuwasaidia, mfano katika jamii ya Wangindo wakipata  matatizo huenda “Ngende”. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” kuna mawazo yanayohusishwa na wahenga pale watu wapatapo matatizo;
                        “enyi mahoka wa mababu;
                                Enyi wazee mliotangulia
                                Enyi wenzangu,
                                Sikiliza kiapo changu!
                                Sitasema wala kuwaza lolote,
                                La ndani ni la ndani!
                                Nishindwe mara tatu,
                                Pembe hili linichome moto…!(uk 22)
Lakini kutokana na Kwasi anadai kuwa mawazo hayo ya Wahenga hayawezi kuthibitishwa kwa sababu hayakuweza kuandikwa katika andiko lolote bali yalikuwa ya kurithishwa tu. Hivyo hakuna falsafa ya Kiafrika.
Kinachoitwa falsafa ya Kiafrika kinajumuisha hekima, elimu, mila na desturi ambapo kwa Kwasi Wiredu anasema; vitu hivi haviitwi falsafa lakini matendo au vitu hivyo vyote vilikuwa vikifanywa na waafrika, kwani vinajidhihirisha kama ifuatavyo; Kuhusu hekima, huangalia matendo mema na maneno ya busara yaliyokuwa yakifanywa na waafrika hasa wazee wa zamani na hivyo huweza kurithisha hekima hizi kwa vijana au vizazi vya sasa. Katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Mzee Mavengi alimshangaa Gusto alivyokuwa akitoa maneno ya hekima kwa wenzie kuliko vile alivyokuwa akidhania.
            “…hivyo nadhani kuna chembe fulani ya ukweli na hekima fulani katika maneno yako…” (uk 26- 27)
Hii ni dhahiri kuwa Gusto alikuwa kijana mwenye hekima ambaye ni moja kati ya viashiria vya mawazo ya kifalsafa.
Kuhusu elimu, huangalia elimu ya awali kwa waafrika ambayo ni jando na unyago ambayo humuandaa kijana katika kupambana na mazingira yake na jamii kwa ujumla katika kudhihirisha hili katika riwaya ya “Nagona” mwandishi nanaonyesha kuwa waafrika walikuwa na njia/ chombo chao cha kutolea elimu ambacho ni jando;
            “….hatutaki ajali nyingine. Bado hujaenda jandoni, ukivalishwa ushanga…”(uk 20)
Elimu hii pia bado inatolewa katika jamii tafautitofauti za kiafrika mfano kimakonde.
Kuhusu mila na desturi, waafrika wanamila na desturi zao kama vile namna ya kusalimia, maisha yao na kurithisha mali ni desturi ya waafrika. Mawazo haya ambayo yalisemwa na Kwasi Wiredu yanadhihirishwa katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” .
            “….mwanangu nakuachia kazi kubwa, ni urithi mkubwa ukiutumia vema…..” (uk 15)
Hapa baba Gusto anamrithisha mwanae mirathi ya hatari kama desturi ya waafrika wengi pale mzazi anapokaribia kuaga dunia anaendelea kusema;
            “….nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu na sihiri…(uk 16).
Hayo pia yanadhihilishwa katika riwaya ya “Nagona” ambayo wazazi wanadesturi ya kuachia urithi wanao. Mfano, babu alipokuwa anakaribia kufa lakini mimi nimeacha mali gani nyuma? Hakuna isiyopokuwa wewe, baba yako na mama yako. Hii inaonyesha hata kama mzazi hana mali basi hupenda hata kuacha wosia kwa wale wanaobaki.
Mawazo mengi na tamaduni za kiafrika ni za kishenzi, ushirikina, uchawi na kupitwa na wakati. Hata wasomi wa kiafrika wanaamini mawe, mizimwi, miti, mapepo, mahoka na Miungu Kwasi anadai, kuwa hata kama mwafrika akisoma lazima atakuwa na tamaduni za kishenzi, kichawi na kushirikina hayo yanadhihilishwa katika riwaya kama zifuatavyo;  kuhusu uchawi, mwandishi wa riwaya ya “Mirathi ya Hatari” imejishughulisha sana na suala hili la uchawi kuwa mawazo waliyonayo waafrika kwa kiasi kikubwa. Gusto kijana mdogo tu wa shule alirithishwa tunguli (uchawi) na baba yake baada ya baba yake kufa, waafrika wengi huamini mazingaombwe kwa kila kitu hayo yanaonekana pale baba Gusto anasema;
          “….ukipatwa na adha
                Sihiri hii ikutulize
                Ukiona na hasidi
                Fingo hii impumbaze
utende mambo kwa idhaa
Kago hii ikuongoze…” (uk 23)
Pia katika riwaya ya “Nagona” mawazo ya kiafrika yamejikita katika suala hili la uchawikwa mfano anaposema;
            “….ndege wa mawio walipoanza kuwaimbia wachawi….(uk 23).
 Inaonesha waafrika huamini kiasi cha kushindwa kulala; “….hata wachawi hubisha  hodi…(uk 16).
 Hii inajidhihirisha kuwa mawazo ya waafrika yapo kwenye utamaduni wa kichawi. Pia kuhusu ushirikina, mwandishi anajaribu kuonyesha imani ya kishirikina kwa jamii za kiafrika, katika riwaya ya “Nagona” yanadhihishwa hayo kama ifuatavyo;
            “…na huyo paka! Yeye ndiye mlinzi wa kifo..(uk 9)”,
Wanajamii hii huamini kuwa paka anaweza kuwalinda dhidi ya kifo. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Mzee malipula na wenzake wanajadili juu ya suala la safari ya kwenda Malawi kumpeleka Gusto wakajue nani aliyehusika na kifo cha Mzee kapedzile;
“…njia iliyobora ni kwenda Malawi kwa Chikanga yeye amejaaliwa na kipawa cha kujua yupi mcahwi yupi si mchawi…nilichanjwa kifuani nilichanjwa magotini na usoni na vidoleni chale zilipotoka damu nikapakazwa madawa ya aina aina….(uk 59).
Pia anaendelea kusema juu ya imani ya kishirikina;
 “…nilivishwa kitu kama hirizi…(uk 23)
hii imekuwa imani ya waafrika wakiamini kuwa hirizi inaweza kuwalinda dhidi ya magonjwa au wachawi. Hivyo Wiredu anashauri kuwa waafrika hawana budi kuachana na Mila hizi pamoja na imani hizi ambazo kwa sasa hazina nafasi tena.
Waafrika wanaamini uchawi miungu, uhalali wa utumwa na ukandamizaji wa mwanamke Kwasi Wiredu anashauri waafrika waachane na mambo hayo kwani hayana tija kwa maisha yao. Kuhusu Miungu, waafrika huamini katika miungu wanapopatwa na shida, shida hizo zilitatuliwa kutokana na imani hiyo ya Miungu. Haya yanadhihilishwa katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari”
“…shida ya mvua, homa, ukame na mengineyo mengi…. Mahoka ya mababu, …enyi wazee mliotangulia.., …pembe hili linichome moto…”(uk 22)
Pia katika Miungu wanasema
 “….Mahoka wamempokea vyema kwao…(uk 52)”.
Hii inaonyesha kuwa Miungu wamepokea maombi yao. Vilevile katika riwaya ya “Nagona” kuna Padri aliyekuwa akihubiri habari za Kristo.
“..mimi nahubiri habari za kristo wewe unahubiri upagani…”(uk 19).
Hii ni kwamba waafrika walikuwa wakiamini kwenye upagani. Hali kadharika kuhusu uhalali wa utumwa hupenda kutumikiwa utemi, kuwa juu ya wengine yaani kunyenyekewa na watu wa chini yao. Mfano katika “Mirathi ya Hatari”, Mzee mavengi, Mzee malipula na wengine  walikuwa ni watu wenye mamlaka katika kijiji chao. Mzee malipula alikuwa Balozi wa nyumba kumi alitumia madaraka yake kuwanyanyasa wengine;
            “…hivi unafahamu kuwa mimi ni Balozi wa nyumba kumi kumi hapa…” (uk 60).
Kuhusu ukandamizaji wa mwanamke, waafrika wengi waamini kuwa mwanamke si chochote ni mtu asiye na umuhimu mkubwa sana kuliko mwanaume katika jamii. Hapa ndipo mfumo dume hujidhihilisha, falsafa hii inapendelea mwanamke kunyimwa uhuru hasa katika elimu, kuchagua mume ampendae. Mfano katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” pale msanii anapobainisha haya yafuatavyo;
            “…kumsomesha mtoto wa kike ni kama kumpa bangi imvuruge akili….?(uk 56)
Inaonekana kuwa wanawake wa kiafrika hawaaminiki kabisa katika kufanya lolote huu ni mfumo dume kuonekana kuwa mwanaume ndiye kila kitu. Hivyo Wiredu anashauri kuwa waafrika hawana budi kuachana na fikra hizo kwani ni potofu badala ya kuendeleza kuwalinda kwa madai kuwa ni falsafa yao.
Kwasi Wiredu anaonekana kuamini sana falsafa ya kimagharibi na kupuuza falsafa ya kiafrika, lakini katika mitazamo yake inazua maswali yafuatayo; je ni kweli hakuna falsafa ya kiafrika? Kama haipo kuna nini? Kama ipo ipoje? Je uchawi na ushirikina ni falsafa ya kiafrika? Kama ndio kwa nini? Kwa vipi? Na kama sio kwa nini? Hivyo hayo ni maswali kadhaa ambayo amewaacha wasomaji wakiwa bado wanajiuliza na kutokupata jibu kwani hajaweka wazi mambo hayo yote.
Placide, J.W. Temples
Huyu pia ni mwanafalsafa ambaye alikuwa padri aliyeishi nchini Kongo mwenye asili ya ufaransa na aliishi 1906 hadi 1977 alifanya uchunguzi juu ya sayansi ya makabila. Hivyo aliangalia falsafa ya kiafrika na kutoa baadhi ya mambo aliyoyachunguza kama ifuatavyo;
Maisha na kifo, mwanadamu katika fikra zake zimetawaliwa na vitu viwili yaani uhai na kifo, hivyo kwa waafrika mtu anayeweza kupunguza maisha ni mchawi na anayeweza kuongeza maisha ya mwanadamu ni mganga, hivyo waafrika wakipata matatizo huzirudia imani zao za jadi na Wahenga au mizimu huachiwa suluhisho la matatizo na wahenga wananguvu kuliko waliohai na hakuna kifo kisicho na sababu na kinatokana na uchawi. Hivyo haya yote yanajidhihilisha katika Riwaya ya “Mirathi ya Hatari” hivyo mwanafasihi anasema;
            “.. waaidha nilipewa kisu nikaonyeshwa sehemu za kukata…..”(uk 43)
Kutokana na kifo cha Mzee kapedzile sababu zilitolewa na Mzee malipula na Mzee mavengi kuwa aliyehusika ni Gusto.
“…..unasemaje nini, Dina? Mlifanya nini jana usiku?” ..usinidanganye sasa Gusto nafahamu yote, jana mmekutana na wale wazee mkamuua Kapedzile…..(uk 51).
Ukweli ni kwamba hata katika jamii zetu yapo mfano katika kabila la wabena kama mtu amefariki kwa ajali, au kufa ghafla ama kwa homa bado huwa inasadikika kuwa anaweza akawa ameuawa na miongoni mwa ndugu zake ili wapate kufanikiwa, na hii haipo katika jamii ya kusini tu mwa Tanzani bali ni viwakilishi tu kwamba jamii yote ya kiafrika mambo haya yapo.
Dhana ya kuhusu Mungu, Mwafrika anaamini kwamba kuna ngazi tofauti tofauti za kumfikia Mungu mkuu ambaye ndiyo nguvu kuu, Mizimu, Wahenga (walio kufa), Wazee waliohai, binadamu (mtu wa kawaida). Hivyo dhana hii inajidhihirisha katika riwaya ya “Nagona” ambapo mizimu imeonyeshwa kupitia Jogoo ambaye ni mzimu wa kulinda kisima, Paka Mzimu wa kulinda nyumba na kisima hicho cha damu. Pia Wahenga wazee waliokuwa wawili waliobakia pale kijijini walikuwa na uwezo wa kuwasiliana na mizimu, ambapo mizimu hiyo hufikisha taarifa kwa Mungu Mkuu. Kwa mfano Mzee aliyekuwa akilinda kisimani pale alikuwa anapata taarifa kupitia kuongezeka kwa damu kuwa kuna mtu atakuja.
Pia dhana hii ya imejidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” ambapo Gusto alikuwa na nguvu za sihiri bado aliamini kuwa Mungu bado yupo alichukuliwa na Madoda kwa ajili ya kuapishwa kuwa ndiye mrithi wa cheo kile alichokuwa nacho baba yake, lakini baada ya kuamka siku ya jumapili bado alijiandaa kwa kwenda kanisani, mfano;
“….niliporudi niliingia chumbani nikavaa nguo zangu rasmi tayari kwa kwenda kanisani… (uk 29).
Hivyo hii inaonesha jinsi waafrika wanavyoamini Mungu kuwa hata mambo yawe magumu au mepesi kuwa yeye pekee anayeweza kuwafanikishia mambo yao. Japokuwa waafrika tangia awali tulikuwa na dini zetu.
Mwafrika anaamini kuwa kuna watu wenye nguvu ya kubariki na kutoa laana pamoja na viongozi au wazee au watu mashuhuri. Hivyo wazo hili ni mojawapo ya mawazo ya Temples amejaribu kuwaainisha waafrika na kuona kuwa waafrika wanaamini hivyo katika maisha yao hasa pale mtu anapokuwa anaishi ama anakaribia kufa. Hivyo basi wazo hili linajitokeza katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” mwandishi amemtumia Mzee kazembe alimwita Gusto ili ambariki ampe mirathi. Lakini vilevile Mzee kazembe hakutaka kusogeleana na Rafael aliyekuwa amejitenga na kupewa laana na wazazi wake.
“….mwanangu nakuachia kazi kubwa. Ni urithi mkubwa ukitumia vema; bali pia ni mirathi ya hatari usipojihadhari nayo. Nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu ya sihiri …(uk 15)”.
Pia Mzee malipula alimlaani binti yake Dina kuwa hawezi kufanikiwa baada ya kuonekana anataka kuolewa na Gusto ambaye alidaiwa kuwa mchawi hivyo Mzee Malipula hakupenda.
Hivyo jambo hili katika jamii zetu linajidhihirisha wazi pale wazazi waonapo mtoto anafanya vema, wanatumia fursa hii kuwabariki na kuwatakia mema katika maisha yao na siyo tu watoto hata jamii kwa ujumla ionapo mtu fulani anafanya vizuri basi humbariki.
Mwaafrika anaamini kuwa mchawi ana nafsi mbili yaani nafsi iliyotulia na nafsi inayotembea ambapo ipo katika makundi mawili kundi la ndoto (nafsi iliyotulia) na nafsi inayotembea ndiyo inayoweza kudhuru. Temples katika uchunguzi wa falsafa ya kiafrika amebaini hilo ambalo pia linajidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Gusto alipoguswa mikono akiwa usingizini na mtu asiyeonekana ambaye ni Madoda;
“..usiogope Gusto ndimi Madoda mtumishi wa baba yako katika milki yake nimetumwa nije nikuchukue na nikuongoze huko wenzangu waliko……” (uk 18).
“…. Kweli hakuwa mwingine bali Madoda sura yake ilikuwa haijanitoka bado tangu tulipochunga ng’ombe pamoja…” (uk 19).
 Hivyo Madoda ni nafsi inayotembea na ndiyo yenye kumchukua Gusto wakati akiwa nyumbani kwao. Pia jambo hili hili linajitokeza katika riwaya ya “Nagona” ambapo tunakutana na nafsi inayotembea ambayo hudhuru na inajidhihilisha kama ifuatavyo;
“….nilishitukia napigwa viboko matakoni na mgongoni …nilipigwa viboko mfululizo lakini sikuweza kujitingisha…..”(uk 1).
Hapa ni nafsi inayotembea ambapo mtu anapigwa kiboko kichawi bila mtu kumwona. Hali kadharika katika jamii zetu jambo hili lipo mfano katika kabila la wabena (Njombe) mtu anayedhaniwa kuwa ni mchawi ukienda kumuuangalia usiku wa manane hata ukimshitua kwa nguvu mtu yule huwa haamuki lakini baada ya muda mtu yule akiamka husema nilikuwa nimesafiri, hivyo hii wazi kuwa ipo nafsi inayotembea na nafsi tuli.
Mwaafrika anatawaliwa sana na suala la ukarimu na ushirikiano katika shida na raha, Temples anaamini kuwa waafrika wamekuwa na ukarimu na ushirikiano hasa pale jirani ama ndugu yake anapopatwa na tatizo kama vile (msiba, ajali) na mengine yamfanyayo mtu kuwa na huzuni au kama kuna tukio la furaha kama vile kufanikiwa kitu fulani, arusi, jando na unyago, sherehe za kuhitimu shule na sherehe nyinginezo ambazo bado zinamfanya mtu awe mwenye furaha. Katika mambo hayo yote waafrika wanakuwa wakarimu pia hata kushirikiana ili kuhakiki jambo lile linafanikiwa, hivyo jambo hili limejidhihilisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” kama ifuatavyo;
“…..msichana mdogo aliyekuwa anazungumza na mama “kamwene binti yangu… habari gani zikuletazo asubuhi hivi?….(uk 49).
                “…mimi nakwenda huko kwenye kilio labda nitarudi tu jioni kuchukua matandiko..” (uk 50).
Bado wazo hili linajidhihirisha katika riwaya ya “Nagona” ambapo Mzee wakati anamkaribisha msanii na hii ndiyo inayoendelea kuthibitisha kuwa waafrika wanaukarimu.
“….karibu karibu karibu uketi. Tumekuwa tukikusubiri,” sauti ilitoka katikati ya mwanaga wewe mwenyewe” ahsante…(uk 14)”.
Hivyo kama ambavyo yamedhihirishwa katika riwaya zote mbili yaani Mirathi ya hatari na Nagona inasawili katika jamii zetu za kiafrika kwani waafrika hushirikiana na kuwa wakarimu katika shida na raha pale litokeapo tukio la furaha ama la huzuni kwa ndugu au jirani.
Mwaafrika hasahau jadi au asili hata kama ana elimu ya kimagharibi na kimashariki. Utafiti huu wa Temples katika suala hili ni kweli kwani licha ya kuwa mtu ana elimu ya juu kabisa ya kimagharibi yaani katika shahada ya kwanza, shahada ya uzamili pia shahada ya uzamivu bado akilejea kule alikozaliwa hufuata mila na taratibu zilizopo katika jamii husika bila kwenda kinyume, mfano katika makabila kama ni msukuma akirudi alikozaliwa huongea kisukuma na kama mnyakyusa hali kadharika. Na pia licha ya mtu kuwa na elimu hiyo bado anaamini nguvu za sihiri na hii imejidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya hatari” ambapo mwandishi amemtumia mhusika Gusto ambaye alikuwa ana elimu hiyo lakini bado anaamini kuwa hirizi ndiyo yenye kumfanikisha kufaulu mitihani;
            “…baba yako ni mchawi na hiyo hirizi uliyoivaa ni ya madawa ya kufaulu mitihani…(uk 6).”
Pia jambo hili linajitokeza katika riwaya ya “Nagona” ambapo mwandishi amemtumia mhusika Mkombozi wa pili pamoja na kuwa msomi lakini aliwafuata wazee wa mila ili kuleta ukombozi mbali na elimu aliyokuwa nayo ya kimagharibi;
“…nilipomkaribia niliinua tena mikono yangu…(uk 37)”
Kwahiyo basi ni hili lipo hata kwa sisi japo tuna elimu ya kimagharibi lakini hatuzipuuzi mila na desturi za kule tulikotoka.
Kila mtu ana chembe za nguvu hai yaani inayomwezesha kutenda mambo yake na chembe hai ya kike ni kubwa zaidi kuliko ya kiume. Uchawi ni nguvu hai watu hutumia kupatia vyeo, ushindi na hata vita, lakini nguvu hai inaweza kuboresha au kufifiza katika utendaji wa mambo. Mfano, matumizi ya hirizi na kupiga lamri ni kuongeza nguvu hai. Hivyo jambo hili limejitokeza katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” ambapo Gusto amekuwa akitumia hirizi aliyopewa na mama yake ili kujikinga na maovu kijijini na hata wakati mwingine kuitumia ili kuweza kufanikisha kuyafanya masomo yake kwa ustadi wa hali ya juu, kwani utumiaji wa hirizi ndio umemfanya Gusto asidhurike na maovu ya kijijini;
“…ni kweli kwamba nilikuwa navaa hirizi; hirizi niliyopewa na mama kama kinga ya maovu kijijini.(uk 6).
“….wengine tulipochoka yeye alikuwa kama vile ndiyo kwanza anaanza. Hata leo bado nashangaa nguvu zile alizipata wapi….” (.Uk 5)
Pia katika riwaya ya “Nagona” ambapo mhusika Mimi anaonekana ana chembe nguvu hai zilizomwezesha kuyashinda mambo makubwa kama ya kishirikina na kichawi yaliyomkabili katika safari yake (uk 1-3).
 
Hivyo basi nukuu hizi inaonesha namna waafrika wanavyoamini nguvu za sihiri katika kuyashinda mambo hata yawe magumu ama mepesi hirizi na lamri ndiyo mshindi wao katika kuyatatua kwani ndio aliyeyafanya mambo hayo yawepo hapa dunia.
]]>
Huyu ni mwanafalsafa maarufu aliyezaliwa nchini Kenya, alitumikia waasifu wa uparoko katika kanisa la Roman Catholic (RC). Aliandika maandiko mawili yaliyotalii falsafa ya kiafrika “Africa Religious Philosophy (1966) and African concept of God (1970). Alizungumzia yafuatayo kuhusu falsafa ya kiafrika.
Dhana ya wakati; kwa waafrika hawaangalii wakati na hawana haraka na wakati, mwafrika katika kuangalia wakati, namba za saa ni kitu dhahania, kwa mwafrika wakati hauamui matendo kama ilivyo kwa mzungu, dhana hii imedhihirika katika riwaya ya “ Nagona” kwa muhusika babu alipokuwa akimweleza mjukuu mwaka wake wa kuzaliwa kwa kuyarejea matukio kama matukio ya “utupu” ajali gharika kupatwa kwa jua kama asemavyo mwandishi.
“……nataka kujua habari za kuzaliwa kwangu wazazi wangu hajapata kunieleza kikamilifu….. natakueleza. Hivi ndivyo ilivyokuwa…….hapakuwa na ujuzi wa jema na baya. Hapakuwa na fikra. Palikuwa na utupu katika kitovu cha undani na hapakuwa na nguvu zilizoweza kutoa uongozi…….. ajali hii ilitokea katika bonde la hisia……. Katika ukweli huu palitokea gharika katika mto wa bonde…..(uk 11)”.
Vilevile katika kitabu cha riwaya ya “Mirathi ya hatari”  wazo limethibitishwa na familia ya Mzee Kazembe alivyokuwa akijilimisha usiku na mchana bila hata ya kuangalia wakati.      “……si yule wa mji wa Kazembe ajilimishaye usiku na mchana..(uk 5)”.
Hata katika mazingira halisi ya waafrika mambo haya yanahalisika.
Dhana ya kifo, Mwafrika anapokaribia kufa huwa anatoa urithi mfano mali, uchawi, jina au maelekezo fulani kuhusu baraka au laana katika “Mirathi ya hatari”, Gusto, kijana wa Mzee Kazembe aliachiwa urithi wa pesa, Mirathi ya hatari (uchawi), mashamba pamoja na baraka anasema.
“….mwanangu nakuachia kazi kubwa. Ni urithi mkubwa ukitumia vema; bali pia ni mirathi ya hatari usipojihadhari nayo. Nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu ya sihiri…(uk 15-16)”.
vile vile, Dina alimuachia maagizo Gusto alisema
 “mali yangu yote isipokuwa kitabu kilicho sandukuni mwangu, uwape maskini” (uk 90).
Pia katika kitabu cha “Nagona” Babu anatoa maagizo au maelezo kwa mjukuu wake baada ya kukaribia kufa alisema
“…. Mjukuu jihadhari siku ya ngoma kuu usikanyagwe daima fuata duara na macho yako wakati wote watazame hapo katikati hicho kitovu kitakapo pasuka mengi yaliyofichika kwa karne nyingi yataonekana harafu kwa shida alisema Nag…..Nag….” (uk 45).
Dini, kwa mwafrika , dini ni chimbuko la mambo yote na kwa asili mwafrika alizaliwa na dini yake, si suala la kujifunza na kusilimishwa; katika “Mirathi ya hatari” ametumia familia ya Mzee  Kazembe, Madoda na Mavengi waliokuwa na dini yao ya asili ilivyokuwa ikifanyika mapangoni usiku pamoja na baadhi yao kuamini dini ya kujifunza na kusilimishwa lakini hawakuiacha kamwe, kama asemavyo mwandishi;
                        “enyi mahoka wa mababu;
                                Enyi wazee mliotangulia
                                Enyi wenzangu,
                                Sikiliza kiapo changu!
                                Sitasema wala kuwaza lolote,
                                La ndani ni la ndani!
                                Nishindwe mara tatu,
                                Pembe hili linichome moto…!(uk 22)
Haya ni maneno yanayoonesha utii wa dini za asili zenye kuamini miungu, mahoka, wazee na binadamu.
Pia katika riwaya ya “Nagona” mwandishi amemtumia mhusika Padri ambaye alikuwa anaamini dini ya kujifunza na kubatizwa (Ukristo) na Wazee walishikiria dini ya kipagani kama dini ya asili kama asemavyo;
“…Padri alikaa kimya, wazee wote walimtazama, Padri alitabasamu aliwatazama wazee halafu akafungua kinywa chake, hakuna mkristo miongoni mwenu?” wazee walitazamana “ Hakuna” babu alijibu. (uk 10).
Hii inadhibitisha kuwa waafrika wanaozithamini dini zao za asili na kuzitupilia mbali dini za wageni kama ukristo hii hata katika mazingira halisi ya kiafrika imetawala sana hususani maeneo ya vijijini.
Kuhusu ufahamu wa ulimwengu na uwapo, waafrika wanaamini kuwa ulimwengu uliumbwa na Mungu na Mungu ndiye muumba wa vyote. Mfano katika riwaya ya “Nagona” imejidhihirisha katika majibizano ya Padri na Mtubu dhambi kama asemayo mwandishi;
                        “…Mmh! Baba unazo dhambi zingine”
                                “kubwa moja na ndogo nyingi”
                                 Lakini unajibebesha mzingo mzito! Dhambi za karne mbili!”
                                “Mungu aliumba ulimwengu na vyote vilivyomo…….” (uk 51)
Pia katika kitabu “Mirathi ya hatari” mwandishi amemtumia Gusto kama mhusika aliyekabiliwa na changamoto nyingi kutoka kwa wanafunzi wenzake katika safari yake ya masomo ila kwa kuwa alimwamini Mungu ndiyo chanzo cha yote hapa duniani alijipa moyo atayashinda kama asemavyo;
“…. Kwani yaliyopita si ndwele tugange yajayo kwa uwezo wa mbingu natumaini nitafanikiwa, sijui nianzie wapi” (uk 4).
Hivyo basi nukuu hii inaonesha jinsi waafrika wanavyotumaini Mungu kuwa hata mambo yawe magumu ama mepesi kuwa ndiyo yeye pekee anayeyajua kwani ndiye aliyeyafanya yawepo hapa dunia au ulimwenguni.
Kwa ujumla John Mbiti anaona kuwa falsafa ya kiafrika ipo na inaendelea kuwepo, na uwepo huo unajidhihirisha katika mambo ya kiutamaduni, japo athari za kiutamaduni wa kigeni unaokweza na sababu za maendeleo ya sayansi na teknolojia na zile za kiutandawazi.
Kwasi Wiredu
Ni miongoni mwa wanafalsafa wa kiafrika, alizaliwa mwaka 1931 katika nchi ya Ghana yeye aliangalia dhana ya Ngano na hadithi. Na jinsi gani zinavyojidhihirisha katika falsafa ya kiafrika. Kwasi Wiredu alidai kuwa waafrika hawana falsafa yao wenyewe bali mawazo yao hujiegemeza katika mapokeo ya watu wa magharibi. Hivyo Kwasi Wiredu katika kulinda mtazamo wake ametoa baadhi ya hoja madhubuti kuhusu kutokuwepo kwa falsafa ya kiafrika.
Hoja zake zinaweza kuwa na ukweli fulani na zisiwe na ukweli fulani kulingana na uchunguzi uliofanyika kwa kutumia riwaya ya “Nagona” na ile ya “Mirathi ya Hatari” kama ifuatavyo:
Mawazo ya kiafrika ya kiutamaduni na kijamii huwa hayabadiliki kulingana na wakati. Suala hili la kutobadilika kwa utamaduni sio tu kwa Afrika bali ni duniani kote. Hii hutokana na waafrika kushikilia baadhi ya misimamo yao kiutamaduni bila kujali mabadiliko ya wakati kutokan na waafrika wenyewe kutoruhusu fikra mpya. Haya yanadhirishwa kwenye riwaya ya “Nagona” japokuwa utamaduni unabadilika lakini mawazo ya kiafrika yanabaki vilevile. Mfano suala la ndoa katika riwaya hii mhusika Mimi alipotaka kumkumbatia msichana ambaye alilkuwa bado hajaolewa ilikuwa ni kinyume na tamaduni za kiafrika mwandishi anasema;
“….nilipomkaribia niliinua tena mikono yangu kuukumbatia mwanga. Lakini aliishika mikono akaishusha tena mahali pake akisema.
“Mila”
“mila gani?”
Myeleka lazima kwanza tupige myeleka ukifanikiwa kunishika na kunitupa kitandani basi umeshinda. Sitakuwa na la kusema. Utaruhusiwa kucheza ngoma kati kati ya duara” (uk 67).
Hii inaonyesha kuwa pamoja na mabadiliko ya wakati lakini bado waafrika wana mawazo yao juu ya utamaduni kwani hata katika jamii zetu mawazo kama haya bado yapo. Mfano, wamasai na wasukuma ili uweze kuoa binti wa kimasai lazima ufuate utamaduni. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” mtunzi anaonyesha hayo pale mtunzi anaposema;
“majira ya wakati yanabadilika mzee wangu…..ukweli ni kwamba sisi wenyewe wazee ni wa kulaumiwa tumeshindwa kutambua kuwa dunia ya leo si dunia yetu….tumeshindwa kutambua kwamba ulimwengu wa leo ni ulimwengu unaobadilika kwa kasi tusiyoweza kuimudu…. Nani kati yenu angetegemea kufika hospitalini na kupimwa huku na mwanamke mwafrika ambaye pia huendesha gari lake mwenyewe (uk 56)”
Hii inaonyesha dhahiri kuwa mawazo ya waafrika hayabadiliki kwani wazee wanashangaa jinsi wanawake wanavyoweza kufanya kazi ambazo hapo awali zilikuwa zikifanywa na wanaume katika jamii zetu pia tuanona kuna wazee ambao bado wanalalamika kwa jinsi waonavyo ulimwengu ulivyobadilika. Kwani kuna mawaziri, wabunge na wakuu wa mikoa.
Afrika hakukuwa na falsafa kwa kuwa mawazo yao yanahusisha wahenga na haina uthibitisho tofauti na ile ya kimagharibi. Kwasi anaamini kuwa Afrika hakuna falsafa kwa kuwa haikuandikwa bali mawazo yao yalihusisha Wahenga tu. Haya yanadhirika kwa kutumia riwaya ya “Nagona” pale mtunzi anaposema;
“…sauti ya kiwiliwili ilisikika kutoka katika mwanga, kwa sasa mazungumzo na roho yako yanatosha utakapo jua kuzungumza na roho yako vizuri mambo yataenda kwa haraka kidogo…..huu si mwanzo mbaya meza roho  yako….”(sura ya tatu (3).
Hii inaonyesha kuwa waafrika wakipata matatizo hukimbilia kuwaomba wahenga ili waweze kuwasaidia katika matatizo hayo. Katika jamii yetu pia kukiwa na matatizo wazee wa jamii huenda kuzungumza na wahenga ili waweze kuwasaidia, mfano katika jamii ya Wangindo wakipata  matatizo huenda “Ngende”. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” kuna mawazo yanayohusishwa na wahenga pale watu wapatapo matatizo;
                        “enyi mahoka wa mababu;
                                Enyi wazee mliotangulia
                                Enyi wenzangu,
                                Sikiliza kiapo changu!
                                Sitasema wala kuwaza lolote,
                                La ndani ni la ndani!
                                Nishindwe mara tatu,
                                Pembe hili linichome moto…!(uk 22)
Lakini kutokana na Kwasi anadai kuwa mawazo hayo ya Wahenga hayawezi kuthibitishwa kwa sababu hayakuweza kuandikwa katika andiko lolote bali yalikuwa ya kurithishwa tu. Hivyo hakuna falsafa ya Kiafrika.
Kinachoitwa falsafa ya Kiafrika kinajumuisha hekima, elimu, mila na desturi ambapo kwa Kwasi Wiredu anasema; vitu hivi haviitwi falsafa lakini matendo au vitu hivyo vyote vilikuwa vikifanywa na waafrika, kwani vinajidhihirisha kama ifuatavyo; Kuhusu hekima, huangalia matendo mema na maneno ya busara yaliyokuwa yakifanywa na waafrika hasa wazee wa zamani na hivyo huweza kurithisha hekima hizi kwa vijana au vizazi vya sasa. Katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Mzee Mavengi alimshangaa Gusto alivyokuwa akitoa maneno ya hekima kwa wenzie kuliko vile alivyokuwa akidhania.
            “…hivyo nadhani kuna chembe fulani ya ukweli na hekima fulani katika maneno yako…” (uk 26- 27)
Hii ni dhahiri kuwa Gusto alikuwa kijana mwenye hekima ambaye ni moja kati ya viashiria vya mawazo ya kifalsafa.
Kuhusu elimu, huangalia elimu ya awali kwa waafrika ambayo ni jando na unyago ambayo humuandaa kijana katika kupambana na mazingira yake na jamii kwa ujumla katika kudhihirisha hili katika riwaya ya “Nagona” mwandishi nanaonyesha kuwa waafrika walikuwa na njia/ chombo chao cha kutolea elimu ambacho ni jando;
            “….hatutaki ajali nyingine. Bado hujaenda jandoni, ukivalishwa ushanga…”(uk 20)
Elimu hii pia bado inatolewa katika jamii tafautitofauti za kiafrika mfano kimakonde.
Kuhusu mila na desturi, waafrika wanamila na desturi zao kama vile namna ya kusalimia, maisha yao na kurithisha mali ni desturi ya waafrika. Mawazo haya ambayo yalisemwa na Kwasi Wiredu yanadhihirishwa katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” .
            “….mwanangu nakuachia kazi kubwa, ni urithi mkubwa ukiutumia vema…..” (uk 15)
Hapa baba Gusto anamrithisha mwanae mirathi ya hatari kama desturi ya waafrika wengi pale mzazi anapokaribia kuaga dunia anaendelea kusema;
            “….nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu na sihiri…(uk 16).
Hayo pia yanadhihilishwa katika riwaya ya “Nagona” ambayo wazazi wanadesturi ya kuachia urithi wanao. Mfano, babu alipokuwa anakaribia kufa lakini mimi nimeacha mali gani nyuma? Hakuna isiyopokuwa wewe, baba yako na mama yako. Hii inaonyesha hata kama mzazi hana mali basi hupenda hata kuacha wosia kwa wale wanaobaki.
Mawazo mengi na tamaduni za kiafrika ni za kishenzi, ushirikina, uchawi na kupitwa na wakati. Hata wasomi wa kiafrika wanaamini mawe, mizimwi, miti, mapepo, mahoka na Miungu Kwasi anadai, kuwa hata kama mwafrika akisoma lazima atakuwa na tamaduni za kishenzi, kichawi na kushirikina hayo yanadhihilishwa katika riwaya kama zifuatavyo;  kuhusu uchawi, mwandishi wa riwaya ya “Mirathi ya Hatari” imejishughulisha sana na suala hili la uchawi kuwa mawazo waliyonayo waafrika kwa kiasi kikubwa. Gusto kijana mdogo tu wa shule alirithishwa tunguli (uchawi) na baba yake baada ya baba yake kufa, waafrika wengi huamini mazingaombwe kwa kila kitu hayo yanaonekana pale baba Gusto anasema;
          “….ukipatwa na adha
                Sihiri hii ikutulize
                Ukiona na hasidi
                Fingo hii impumbaze
utende mambo kwa idhaa
Kago hii ikuongoze…” (uk 23)
Pia katika riwaya ya “Nagona” mawazo ya kiafrika yamejikita katika suala hili la uchawikwa mfano anaposema;
            “….ndege wa mawio walipoanza kuwaimbia wachawi….(uk 23).
 Inaonesha waafrika huamini kiasi cha kushindwa kulala; “….hata wachawi hubisha  hodi…(uk 16).
 Hii inajidhihirisha kuwa mawazo ya waafrika yapo kwenye utamaduni wa kichawi. Pia kuhusu ushirikina, mwandishi anajaribu kuonyesha imani ya kishirikina kwa jamii za kiafrika, katika riwaya ya “Nagona” yanadhihishwa hayo kama ifuatavyo;
            “…na huyo paka! Yeye ndiye mlinzi wa kifo..(uk 9)”,
Wanajamii hii huamini kuwa paka anaweza kuwalinda dhidi ya kifo. Pia katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Mzee malipula na wenzake wanajadili juu ya suala la safari ya kwenda Malawi kumpeleka Gusto wakajue nani aliyehusika na kifo cha Mzee kapedzile;
“…njia iliyobora ni kwenda Malawi kwa Chikanga yeye amejaaliwa na kipawa cha kujua yupi mcahwi yupi si mchawi…nilichanjwa kifuani nilichanjwa magotini na usoni na vidoleni chale zilipotoka damu nikapakazwa madawa ya aina aina….(uk 59).
Pia anaendelea kusema juu ya imani ya kishirikina;
 “…nilivishwa kitu kama hirizi…(uk 23)
hii imekuwa imani ya waafrika wakiamini kuwa hirizi inaweza kuwalinda dhidi ya magonjwa au wachawi. Hivyo Wiredu anashauri kuwa waafrika hawana budi kuachana na Mila hizi pamoja na imani hizi ambazo kwa sasa hazina nafasi tena.
Waafrika wanaamini uchawi miungu, uhalali wa utumwa na ukandamizaji wa mwanamke Kwasi Wiredu anashauri waafrika waachane na mambo hayo kwani hayana tija kwa maisha yao. Kuhusu Miungu, waafrika huamini katika miungu wanapopatwa na shida, shida hizo zilitatuliwa kutokana na imani hiyo ya Miungu. Haya yanadhihilishwa katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari”
“…shida ya mvua, homa, ukame na mengineyo mengi…. Mahoka ya mababu, …enyi wazee mliotangulia.., …pembe hili linichome moto…”(uk 22)
Pia katika Miungu wanasema
 “….Mahoka wamempokea vyema kwao…(uk 52)”.
Hii inaonyesha kuwa Miungu wamepokea maombi yao. Vilevile katika riwaya ya “Nagona” kuna Padri aliyekuwa akihubiri habari za Kristo.
“..mimi nahubiri habari za kristo wewe unahubiri upagani…”(uk 19).
Hii ni kwamba waafrika walikuwa wakiamini kwenye upagani. Hali kadharika kuhusu uhalali wa utumwa hupenda kutumikiwa utemi, kuwa juu ya wengine yaani kunyenyekewa na watu wa chini yao. Mfano katika “Mirathi ya Hatari”, Mzee mavengi, Mzee malipula na wengine  walikuwa ni watu wenye mamlaka katika kijiji chao. Mzee malipula alikuwa Balozi wa nyumba kumi alitumia madaraka yake kuwanyanyasa wengine;
            “…hivi unafahamu kuwa mimi ni Balozi wa nyumba kumi kumi hapa…” (uk 60).
Kuhusu ukandamizaji wa mwanamke, waafrika wengi waamini kuwa mwanamke si chochote ni mtu asiye na umuhimu mkubwa sana kuliko mwanaume katika jamii. Hapa ndipo mfumo dume hujidhihilisha, falsafa hii inapendelea mwanamke kunyimwa uhuru hasa katika elimu, kuchagua mume ampendae. Mfano katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” pale msanii anapobainisha haya yafuatavyo;
            “…kumsomesha mtoto wa kike ni kama kumpa bangi imvuruge akili….?(uk 56)
Inaonekana kuwa wanawake wa kiafrika hawaaminiki kabisa katika kufanya lolote huu ni mfumo dume kuonekana kuwa mwanaume ndiye kila kitu. Hivyo Wiredu anashauri kuwa waafrika hawana budi kuachana na fikra hizo kwani ni potofu badala ya kuendeleza kuwalinda kwa madai kuwa ni falsafa yao.
Kwasi Wiredu anaonekana kuamini sana falsafa ya kimagharibi na kupuuza falsafa ya kiafrika, lakini katika mitazamo yake inazua maswali yafuatayo; je ni kweli hakuna falsafa ya kiafrika? Kama haipo kuna nini? Kama ipo ipoje? Je uchawi na ushirikina ni falsafa ya kiafrika? Kama ndio kwa nini? Kwa vipi? Na kama sio kwa nini? Hivyo hayo ni maswali kadhaa ambayo amewaacha wasomaji wakiwa bado wanajiuliza na kutokupata jibu kwani hajaweka wazi mambo hayo yote.
Placide, J.W. Temples
Huyu pia ni mwanafalsafa ambaye alikuwa padri aliyeishi nchini Kongo mwenye asili ya ufaransa na aliishi 1906 hadi 1977 alifanya uchunguzi juu ya sayansi ya makabila. Hivyo aliangalia falsafa ya kiafrika na kutoa baadhi ya mambo aliyoyachunguza kama ifuatavyo;
Maisha na kifo, mwanadamu katika fikra zake zimetawaliwa na vitu viwili yaani uhai na kifo, hivyo kwa waafrika mtu anayeweza kupunguza maisha ni mchawi na anayeweza kuongeza maisha ya mwanadamu ni mganga, hivyo waafrika wakipata matatizo huzirudia imani zao za jadi na Wahenga au mizimu huachiwa suluhisho la matatizo na wahenga wananguvu kuliko waliohai na hakuna kifo kisicho na sababu na kinatokana na uchawi. Hivyo haya yote yanajidhihilisha katika Riwaya ya “Mirathi ya Hatari” hivyo mwanafasihi anasema;
            “.. waaidha nilipewa kisu nikaonyeshwa sehemu za kukata…..”(uk 43)
Kutokana na kifo cha Mzee kapedzile sababu zilitolewa na Mzee malipula na Mzee mavengi kuwa aliyehusika ni Gusto.
“…..unasemaje nini, Dina? Mlifanya nini jana usiku?” ..usinidanganye sasa Gusto nafahamu yote, jana mmekutana na wale wazee mkamuua Kapedzile…..(uk 51).
Ukweli ni kwamba hata katika jamii zetu yapo mfano katika kabila la wabena kama mtu amefariki kwa ajali, au kufa ghafla ama kwa homa bado huwa inasadikika kuwa anaweza akawa ameuawa na miongoni mwa ndugu zake ili wapate kufanikiwa, na hii haipo katika jamii ya kusini tu mwa Tanzani bali ni viwakilishi tu kwamba jamii yote ya kiafrika mambo haya yapo.
Dhana ya kuhusu Mungu, Mwafrika anaamini kwamba kuna ngazi tofauti tofauti za kumfikia Mungu mkuu ambaye ndiyo nguvu kuu, Mizimu, Wahenga (walio kufa), Wazee waliohai, binadamu (mtu wa kawaida). Hivyo dhana hii inajidhihirisha katika riwaya ya “Nagona” ambapo mizimu imeonyeshwa kupitia Jogoo ambaye ni mzimu wa kulinda kisima, Paka Mzimu wa kulinda nyumba na kisima hicho cha damu. Pia Wahenga wazee waliokuwa wawili waliobakia pale kijijini walikuwa na uwezo wa kuwasiliana na mizimu, ambapo mizimu hiyo hufikisha taarifa kwa Mungu Mkuu. Kwa mfano Mzee aliyekuwa akilinda kisimani pale alikuwa anapata taarifa kupitia kuongezeka kwa damu kuwa kuna mtu atakuja.
Pia dhana hii ya imejidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” ambapo Gusto alikuwa na nguvu za sihiri bado aliamini kuwa Mungu bado yupo alichukuliwa na Madoda kwa ajili ya kuapishwa kuwa ndiye mrithi wa cheo kile alichokuwa nacho baba yake, lakini baada ya kuamka siku ya jumapili bado alijiandaa kwa kwenda kanisani, mfano;
“….niliporudi niliingia chumbani nikavaa nguo zangu rasmi tayari kwa kwenda kanisani… (uk 29).
Hivyo hii inaonesha jinsi waafrika wanavyoamini Mungu kuwa hata mambo yawe magumu au mepesi kuwa yeye pekee anayeweza kuwafanikishia mambo yao. Japokuwa waafrika tangia awali tulikuwa na dini zetu.
Mwafrika anaamini kuwa kuna watu wenye nguvu ya kubariki na kutoa laana pamoja na viongozi au wazee au watu mashuhuri. Hivyo wazo hili ni mojawapo ya mawazo ya Temples amejaribu kuwaainisha waafrika na kuona kuwa waafrika wanaamini hivyo katika maisha yao hasa pale mtu anapokuwa anaishi ama anakaribia kufa. Hivyo basi wazo hili linajitokeza katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” mwandishi amemtumia Mzee kazembe alimwita Gusto ili ambariki ampe mirathi. Lakini vilevile Mzee kazembe hakutaka kusogeleana na Rafael aliyekuwa amejitenga na kupewa laana na wazazi wake.
“….mwanangu nakuachia kazi kubwa. Ni urithi mkubwa ukitumia vema; bali pia ni mirathi ya hatari usipojihadhari nayo. Nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu ya sihiri …(uk 15)”.
Pia Mzee malipula alimlaani binti yake Dina kuwa hawezi kufanikiwa baada ya kuonekana anataka kuolewa na Gusto ambaye alidaiwa kuwa mchawi hivyo Mzee Malipula hakupenda.
Hivyo jambo hili katika jamii zetu linajidhihirisha wazi pale wazazi waonapo mtoto anafanya vema, wanatumia fursa hii kuwabariki na kuwatakia mema katika maisha yao na siyo tu watoto hata jamii kwa ujumla ionapo mtu fulani anafanya vizuri basi humbariki.
Mwaafrika anaamini kuwa mchawi ana nafsi mbili yaani nafsi iliyotulia na nafsi inayotembea ambapo ipo katika makundi mawili kundi la ndoto (nafsi iliyotulia) na nafsi inayotembea ndiyo inayoweza kudhuru. Temples katika uchunguzi wa falsafa ya kiafrika amebaini hilo ambalo pia linajidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” Gusto alipoguswa mikono akiwa usingizini na mtu asiyeonekana ambaye ni Madoda;
“..usiogope Gusto ndimi Madoda mtumishi wa baba yako katika milki yake nimetumwa nije nikuchukue na nikuongoze huko wenzangu waliko……” (uk 18).
“…. Kweli hakuwa mwingine bali Madoda sura yake ilikuwa haijanitoka bado tangu tulipochunga ng’ombe pamoja…” (uk 19).
 Hivyo Madoda ni nafsi inayotembea na ndiyo yenye kumchukua Gusto wakati akiwa nyumbani kwao. Pia jambo hili hili linajitokeza katika riwaya ya “Nagona” ambapo tunakutana na nafsi inayotembea ambayo hudhuru na inajidhihilisha kama ifuatavyo;
“….nilishitukia napigwa viboko matakoni na mgongoni …nilipigwa viboko mfululizo lakini sikuweza kujitingisha…..”(uk 1).
Hapa ni nafsi inayotembea ambapo mtu anapigwa kiboko kichawi bila mtu kumwona. Hali kadharika katika jamii zetu jambo hili lipo mfano katika kabila la wabena (Njombe) mtu anayedhaniwa kuwa ni mchawi ukienda kumuuangalia usiku wa manane hata ukimshitua kwa nguvu mtu yule huwa haamuki lakini baada ya muda mtu yule akiamka husema nilikuwa nimesafiri, hivyo hii wazi kuwa ipo nafsi inayotembea na nafsi tuli.
Mwaafrika anatawaliwa sana na suala la ukarimu na ushirikiano katika shida na raha, Temples anaamini kuwa waafrika wamekuwa na ukarimu na ushirikiano hasa pale jirani ama ndugu yake anapopatwa na tatizo kama vile (msiba, ajali) na mengine yamfanyayo mtu kuwa na huzuni au kama kuna tukio la furaha kama vile kufanikiwa kitu fulani, arusi, jando na unyago, sherehe za kuhitimu shule na sherehe nyinginezo ambazo bado zinamfanya mtu awe mwenye furaha. Katika mambo hayo yote waafrika wanakuwa wakarimu pia hata kushirikiana ili kuhakiki jambo lile linafanikiwa, hivyo jambo hili limejidhihilisha katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” kama ifuatavyo;
“…..msichana mdogo aliyekuwa anazungumza na mama “kamwene binti yangu… habari gani zikuletazo asubuhi hivi?….(uk 49).
                “…mimi nakwenda huko kwenye kilio labda nitarudi tu jioni kuchukua matandiko..” (uk 50).
Bado wazo hili linajidhihirisha katika riwaya ya “Nagona” ambapo Mzee wakati anamkaribisha msanii na hii ndiyo inayoendelea kuthibitisha kuwa waafrika wanaukarimu.
“….karibu karibu karibu uketi. Tumekuwa tukikusubiri,” sauti ilitoka katikati ya mwanaga wewe mwenyewe” ahsante…(uk 14)”.
Hivyo kama ambavyo yamedhihirishwa katika riwaya zote mbili yaani Mirathi ya hatari na Nagona inasawili katika jamii zetu za kiafrika kwani waafrika hushirikiana na kuwa wakarimu katika shida na raha pale litokeapo tukio la furaha ama la huzuni kwa ndugu au jirani.
Mwaafrika hasahau jadi au asili hata kama ana elimu ya kimagharibi na kimashariki. Utafiti huu wa Temples katika suala hili ni kweli kwani licha ya kuwa mtu ana elimu ya juu kabisa ya kimagharibi yaani katika shahada ya kwanza, shahada ya uzamili pia shahada ya uzamivu bado akilejea kule alikozaliwa hufuata mila na taratibu zilizopo katika jamii husika bila kwenda kinyume, mfano katika makabila kama ni msukuma akirudi alikozaliwa huongea kisukuma na kama mnyakyusa hali kadharika. Na pia licha ya mtu kuwa na elimu hiyo bado anaamini nguvu za sihiri na hii imejidhihirisha katika riwaya ya “Mirathi ya hatari” ambapo mwandishi amemtumia mhusika Gusto ambaye alikuwa ana elimu hiyo lakini bado anaamini kuwa hirizi ndiyo yenye kumfanikisha kufaulu mitihani;
            “…baba yako ni mchawi na hiyo hirizi uliyoivaa ni ya madawa ya kufaulu mitihani…(uk 6).”
Pia jambo hili linajitokeza katika riwaya ya “Nagona” ambapo mwandishi amemtumia mhusika Mkombozi wa pili pamoja na kuwa msomi lakini aliwafuata wazee wa mila ili kuleta ukombozi mbali na elimu aliyokuwa nayo ya kimagharibi;
“…nilipomkaribia niliinua tena mikono yangu…(uk 37)”
Kwahiyo basi ni hili lipo hata kwa sisi japo tuna elimu ya kimagharibi lakini hatuzipuuzi mila na desturi za kule tulikotoka.
Kila mtu ana chembe za nguvu hai yaani inayomwezesha kutenda mambo yake na chembe hai ya kike ni kubwa zaidi kuliko ya kiume. Uchawi ni nguvu hai watu hutumia kupatia vyeo, ushindi na hata vita, lakini nguvu hai inaweza kuboresha au kufifiza katika utendaji wa mambo. Mfano, matumizi ya hirizi na kupiga lamri ni kuongeza nguvu hai. Hivyo jambo hili limejitokeza katika riwaya ya “Mirathi ya Hatari” ambapo Gusto amekuwa akitumia hirizi aliyopewa na mama yake ili kujikinga na maovu kijijini na hata wakati mwingine kuitumia ili kuweza kufanikisha kuyafanya masomo yake kwa ustadi wa hali ya juu, kwani utumiaji wa hirizi ndio umemfanya Gusto asidhurike na maovu ya kijijini;
“…ni kweli kwamba nilikuwa navaa hirizi; hirizi niliyopewa na mama kama kinga ya maovu kijijini.(uk 6).
“….wengine tulipochoka yeye alikuwa kama vile ndiyo kwanza anaanza. Hata leo bado nashangaa nguvu zile alizipata wapi….” (.Uk 5)
Pia katika riwaya ya “Nagona” ambapo mhusika Mimi anaonekana ana chembe nguvu hai zilizomwezesha kuyashinda mambo makubwa kama ya kishirikina na kichawi yaliyomkabili katika safari yake (uk 1-3).
 
Hivyo basi nukuu hizi inaonesha namna waafrika wanavyoamini nguvu za sihiri katika kuyashinda mambo hata yawe magumu ama mepesi hirizi na lamri ndiyo mshindi wao katika kuyatatua kwani ndio aliyeyafanya mambo hayo yawepo hapa dunia.
]]>