MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
ODC : MHADHARA WA TISA: Mawanda ya Sintaksia

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
ODC : MHADHARA WA TISA: Mawanda ya Sintaksia
#1
Muhadhara 9:
MHADHARA WA TISA: Mawanda ya Sintaksia
9 .1  Utangulizi
Katika taaluma inayochunguza lugha, ambayo hujulikana kama isimu, lugha hugawanywa katika Nyanja kuu nne ambazo ni fonolojia, mofolojia, sintaksia na semantiki. Hivyo, sintaksia ni nyanja mojawapo ya isimu ya lugha. Sintaksia ni nini?
9.2  Fasili ya Sintaksia
Kwa mujibu wa Harper (2001-2010) Online Etymology Dictionary, neno sintaksia liliibuka takribani miaka ya 1600 na linatokana na neno la Kifaransa syntaxé au la Kilatini au Kigiriki syntaxis ambalo maana yake ni kupanga au kuweka vitu pamoja katika mpango. Hata hivyo, wataalamu wengi wa masuala ya sintaksia wanakubaliana kuwa neno hili lina asili ya Kigiriki kwa kuwa Wagiriki ndio wakongwe katika taaluma mbalimbali hapa duniani, ikiwa ni pamoja na taaluma ya lugha. Hata hivyo historia ya isimu inaonesha kuwa, uchunguzi wa kwanza wa lugha ulianza na Wamisri mnamo karne ya 5 Kabla ya Kuzaliwa Kristo (KK), Wagiriki ndio walioweka msingi wa taaluma ya lugha tuijuavyo hivi leo (Khamis & Kiango, 2002: 1).
Katika taaluma za sayansi ya kompyuta, sintaksia ni kanuni zifafanuazo jinsi alama zitumikazo katika lugha ya kikompyuta zinavyounganishwa pamoja kwa mpangilio unaokubalika kuwa ni muundo sahihi katika lugha hiyo ya kikompyuta (Programming Language).
Katika kozi hii hatutahusika na mpango wa vitu kwa ujumla wake wala kanuni fafanuzi za matumizi ya maneno na virai katika lugha ya kikompyuta, bali tutajikita zaidi katika taaluma ya isimu. Kwa hiyo, sintaksia ni nini katika taaluma ya isimu?
Besha (1994: 84), sintaksia ni taaluma inayojihusisha na uchambuzi na ufafanuzi wa muundo wa sentensi za lugha; kwa mujibu wa O’Grady (1996: 181), sintaksia ni taaluma inayochunguza jinsi maneno yanavyounganishwa ili kuunda sentensi. Sintaksia kwa mujibu wa Massamba na wenzake (2009: 34) ni, “Utanzu wa sarufi unaojishughulisha na uchanganuzi wa mpangilio wa maneno katika sentensi na uhusiano wa vipashio vyake.” Wanaendelea kusema kuwa katika utanzu huu kinachochunguzwa ni zile sheria au kanuni ambazo hazina budi kufuatwa katika kuyapanga maneno ya lugha katika mfuatano (neno moja baada ya jingine) kwa namna ambayo itayafanya maneno hayo yalete maana inayokubalika na kueleweka katika lugha husika.
Fasili hizi chache tumezitoa kama mifano tu ya kushadidia hoja ya kwamba kuna fasili nyingi za sintaksia. Pamoja na kuwapo kwa fasili nyingi, mtu akichunguza atagundua kwamba fasili takriban zote zinabainisha kuwa sintaksia ni tawi la isimu linalojihusisha na uchunguzi wa:
(a) Jinsi maneno yanavyopangwa katika tungo
(b) Kanuni au taratibu za lugha zinazotumika na zinavyotumika katika kuyaweka maneno hayo pamoja
Kwa hiyo, sintaksia inaweza kufasiliwa kuwa ni taaluma inayochunguza miundo ya tungo na kanuni mbalimbali za lugha zinazotawala miundo hiyo. Katika uchunguzi huo, sintaksia huhusika na mpangilio wa maneno katika miundo mitatu iliyopangwa kidarajia, yaani jinsi maneno yanavyopangwa ili kuunda virai, vishazi na sentensi.
9.3 Malengo ya Ufafanuzi wa Kisintaksia
Lengo kuu la ufafanuzi wa kisintaksia ni kupata sarufi inayotosheleza kwa usahihi miundo ya lugha. Hivi ni kusema, wanasintaksia hufafanua miundo ya sintaksia wakiwa na shabaha ya kupata njia sahihi na toshelevu zitakazosaidia kupata miundo sahihi na kukataa miundo isiyo sahihi katika lugha.
Tangu awali taaluma ya lugha ilipoanzishwa, enzi za Wagiriki na Walatini, kumekuwa na mbinu mbalimbali za uchanganuzi wa mfuatano wa vipashio katika muundo wa mlalo. Kwa mfano, sentensi:
  1. Mtoto ana bahati
Ni sentensi sahili ambayo ni sahihi. Ni utungo ambao una maneno yaliyopangwa kimlalo kwa kufuata sulubu maalumu. Maneno hayohayo yaliyotumika katika sentensi (1) yanaweza kupangwa vinginevyo na kutupatia miundo mbalimbali sahihi na isiyo sahihi. Mathalan:
  1. Bahati ana mtoto
  2. Ana bahati mtoto
  3. *Mtoto bahati ana
  4. *Ana mtoto bahati
Vivyo hivyo, sentensi:
  1. Tukiwa tunakula, nitakwambia vitu
Kimsingi hii, ni sentensi changamano, ni utungo ambao una maneno yaliyopangwa kwa kufuata sulubu maalumu. Maneno hayohayo yaliyotumika katika sentensi (6) yanaweza kupangwa vinginevyo na kutupatia miundo mbalimbali sahihi na isiyo sahihi kama vile:
  1. Tukiwa tunakula vitu, nitakwambia
  2. Nitakwambia, tukiwa tunakula vitu
  3. *Tunakula vitu, nitakwambia tukiwa
  4. *Tukiwa nitakwambia vitu tunakula
Sentensi zisizo na alama ya kinyota zimefuata sulubu inayokubalika katika lugha ya Kiswahili na kwa hiyo ndizo sentensi sahihi na zile zenye alama hiyo hazikufuata sulubu hiyo na kwa hiyo si sahihi. Je, tunajuaje kuwa sentensi hizi sahihi ni sahihi na nyingine zisizo sahihi si sahihi?
Tukitaka kujua usahihi na utosahihi wa tungo hizo, tunahitaji njia za uchanganuzi zitakazotupatia mbinu ya kujua mfuatano fulani wa vipashio katika tungo sahihi na zisizo sahihi kuzikataa. Lengo la wanasintaksia, ambalo hasa ndilo lengo la ufafanuzi wa kisintaksia, siku zote limekuwa ni kutafuta njia hizo za kuzikubali sentensi sahihi na kuzikataa sentensi zisizo sahihi. Njia hizo za kufanyia uchanganuzi wa sentensi ndizo huitwa sarufi (kwa maana yake finyu). Je, mwanasintaksia anafikiaje hatua ya kupata sarufi ya lugha inayohusika?
Kwanza, mwanasintaksia huchambua na kueleza maarifa aliyo nayo mjua lugha kuhusu miundo ya lugha yake. Na pili, huunda nadharia kulingana na ugunduzi wake kuhusiana na maarifa hayo ya mjua lugha.
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)