MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
ODC : MUHADHARA WA KUMI NA NANE : FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
ODC : MUHADHARA WA KUMI NA NANE : FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI
#1
MUHADHARA WA KUMI NA NANE
FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI
18.1 Utangulizi
Katika muhadhara huu utasoma vipengele vya fani na maudhui na jinsi vinavyohusiana.
Madhumuni ya Muhadhara
Baada ya kumaliza kusoma muhadhara huu, utaweza :
  • Kufafanua vipengele vya fani na maudhui.
  • Kuhusianisha vipengele vya fani na maudhui
18.2 Fani na Maudhui
Fani katika kazi za fasihi ni ule ufundi wa kisanaa anaoutumia mwandishi kufikisha ujumbe kwa jamii aliyokusudia. Fani inahusisha mambo yafuatayo; Muundo, Mtindo, Matumizi ya lugha, Wahusika naMandhari. Maudhui katika fasihi ni yale mawazo yanayozungumzwa pamoja na mtazamo wa mwandishi juu mawazo hayo. Nayo,yaliyomsukuma mtunzi kutunga na kusana kazi fulani ya sanaa. Pia katika maudhui kuna falsafa ya mwandishi.
Kuna mitazamo miwili inayojadili uhusiano wa fani na maudhui. Mitazamo hiyo ni mtazamo wa kidhanifu na mtazamo wa kiyakinifu.
Mtazamo wa kidhanifu ni ule unaoona kuwa fani na maudhui ni vipengele ambavyo havina uhusiano wowote, kwamba vinaweza kutenganishwa. Wataalamu kadhaa wanalinganisha fani na maudhui na kikombe cha chai. Kikombe kinachukuliwa kama ndiyo fani na upande mwingine chai iliyomo ndiyo maudhui. Mnywaji wa chai hiyo analinganishwa na wasomaji wa kazi ya fasihi.
Vilevile wanafafanua kuwa fani na maudhui hulinganishwa na chungwa ambalo lina sehemu ya nje na ndani. Maudhui ya kazi ya fasihi yanalinganishwa na nyamanyama za chungwa na fani ni sehemu ya nje (ganda). Kwa ufupi hawa wanaona kuwa fani ni umbo la nje la kazi ya fasihi na maudhui ni umbo la ndani.
Mtazamo huu una udhaifu wake (mkubwa) na unaweza kuwachanganya wasomaji. Kwa sababu hauonyeshi ama kuwakilisha ukweli wa mambo juu ya uhusiano uliopo kati ya fani na maudhui katika kazi ya fasihi.
Mtazamo wa kiyakinifu unaeleza vizuri ukweli wa mambo ulivyo. Ni kwamba vitu hivi viwili hutegemeana na kuathiriana na wala havitazamwi katika utengano.
Wanafasihi wenye mtazamo huu, wanalinganisha fani na maudhui na sura mbili za sarafu moja, na si rahisi wala sahihi huzitenga na kuzieleza katika upweke, bila kuhusisha upande mmoja na nyingine. Sura moja ya sarafu ikikosekana, basi sarafu hiyo haiwezi kuwa na hadhi ya kisarafu. Jambo la muhimu ni kuona jinsi kitu kimoja (fani) kinavyoweza kukikamilisha kingine (maudhui).
Wanafasihi hawa wanaonesha kuwa kila kimoja cha kigezo cha fani na maudhui kimo ndani ya chenziwe, kushirikiana na kuathiriana katika ama kijenga vizuri au kubomoa kazi ya sanaa.
Kama kazi ya fasihi itakuwa na fani duni, lakini maudhui yake ni mazuri basi hata maudhui yaliyokusudiwa hayatatoa ujumbe unaokusudiwa ipasavyo. Mfano mzuri ni riwaya ya kikasuku   zilizoandikwa baada ya Azimio la Arusha zinazojadili dhamira ya ujenzi wa jamii mpya kama vile Shida, Mtu ni Utu, Ufunguo Wenye Hazina, Njozi za Usiku, Ndoto za Ndaria n.k. zilisisitiza zaidi maiudhui na kuupuzia kipengele cha fani.
Vile vile kama maudhui ni duni na fani ni bora, pia jamii itapata hasara ya kufikiwa na maudhui yasiyo na maana. Mfano mzuri ni riwaya pendwa zote zimeweka msisitizo kwenye fani na kusahau kipengele cha maudhui. Katika riwaya pendwa kama vile riwaya za upelelezi , mapenzi na uhalifu, zina wahusika ambao hawaaminiki kwani wanapewa sifa ambazo si rahisi kuziona kwa binadamu wa kawaida. (Toa mifano ya riwaya hizo).
Fani na maudhui ni vitu viwili ambavyo huwiana, hutegemeana hatimaye kuathiriana. Uhusiano huo ndio unaojenga kazi bora ya fasihi. Msanii hutumia vipengele mbalimbali vya maudhui katika kuijenga fani na hutumia vipengele mbalimbali vya fani katika kujenga maudhui.
18.3  Vipengele muhimu vya fani na maudhui vijengavyo kazi ya fasihi andishi.
Katika fasihi andishi, fani hujumuisha vipengele vifuatavyo:
Kwanza ni muundo ambao  ni mpangilio na mtiririko wa matukio toka mwanzo hadi mwisho. Hapa tunaangalia jinsi msanii alivyounda na alivyounganisha tukio moja na linguine, kitendo  kimoja na  lingine sura na sura, ubeti na ubeti n.k.  Katika  hadithi na Tamthiliya  muundo unaweza kuwa wa moja kwa moja (Msago), wa Kioo (Rejeshi) au wa rukia. Katika ushairi muundo unaweza kuwa wa  Tathnia, Tathlitha, Tarbia au Sabilia.
Pili, Mtindo, ambao ni upangaji wa fani na maudhui katika kazi ya fasihi andishi kwa njia ambayo hatimaye huonesha nafsi au labda upekee wa mtungaji wa kazi hiyo. Katika riwaya, mtindo unaweza kuwa na masimulizi, monolojia au doyolojia na katika tamthiliya mtindo wake ni dayolojia (majibizano). Katika ushairi mtindo unaweza kuwa wa kimapokeo au wa kisasa.
 
Kipengele cha tatu ni wahusika ambao hutumiwa na msanii kufikisha ujumbe kwa jamii yake. Katika hadithi na Tamthiliya kuna wahusika wakuu, wadodo (wasaidizi) na wajenzi. Wahusika wakuu na wadogo wanaweza kuwa wahusika bapa, mviringo (duara) au shinda (wafoili).
Kipengele kingine ni matumizi ya lugha, ambayo mwandishi hutumia kuyaibusha mawazo yake katika kazi hiyo. Vipengele vya lugha wanavyotumia sana ni:
  • Matumizi ya semi – Misemo, Nahau, Methali, Misimu, Mafumbo n.k.
  • Matumizi ya tamathali za semi
  • Matumizi ya mbinu nyingine za kisanaa
  • Matumizi ya taswira
  • Matumizi ya ucheshi
 
 Pia kuna Kipengele cha Mandhari hii ni sehemu ambapo matukio muhimu ya kazi ya fasihi hutokea. Mandhari inaweza kuwa ya kubuni au ya kweli. Katika masimulizi mengi ya kihistoria mandhari yake ni ya kweli na kazi za kubuni mandhari yake ni ya kubuni.
Kipengele kingine ni jarada kazi za fasihi huwa na michoro au picha na hata rangi kwenye majarada yake.Inawezekana majarada hayo yakawa na uhusiano na dhamira au maudhui ya kazi zinazohusika.Picha hizi huweza kuwa kielekezi muhimu cha fani kwenye uchambuzi wa kazi ya kifasihi.mfano picha za majarada ya Nyota ya Rehema ya M.S.Mohamed,Kufa Kuzikana ya K.Walibora,Babu alipofufuka ya M.S.Mohamed na Bina-Adamu ya K.W.Wamitila na nyingi nyinginezo Hata hivyo ni muhimu kutambua kuwa sio kazi zote za kifasihi ambazo zinaonesha uwiano kati ya majarada yake na yaliyomo.
 
Vipengele vya maudhui, kipengele cha kwanza ni dhamira.
Dhamira ni wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika kazi ya fasihi andishi. Dhamira hutokana na jamii. Katika dhamira, kuna dhamira kuu na dhamira ndogo ndogo.
 
Kipengele cha pili ni mtazamo wa mwandishi. Hapa ni hali ya kuyaona mambo katika maisha kwa kuzingatia mazingira aliyonayo msanii mwenyewe. Mtazamo wa msanii unaweza kuwa wa kiyakinifu au wa kidhanifu.
 
Kipengele kingine ni msimamo wa mwandishi ambayo ili  hali ya mwandishi kuamua kufuata na kushikilia jambo fulani. Jambo hili linaweza kuwa halikubaliki na wengi, lakini yeye atalishikilia tu.
Msimamo wa msanii ndio unaosababisha kazi ya sanaa iwe na  mwelekeo maalum na hata kutofautiana na kazi za wasanii wengine.
Kipengele cha nne ni falsafa ya mwandishi. Ambao huu ni mwelekeo wa imani ya msanii. Msanii anaweza kuamini kwa mfano “Mungu hayupo”.
Maadili na ujumbe ni kipengele kingine cha maudhui.Katika fasihi andishi, ujumbe ni mafunzo mbalimbali ambayo hupatikana baada ya kusoma kazi Fulani ya fasihi andishi.
 
Mwisho, migogoro, ambayo ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi ya fasihi. Katika migogoro tunapata migogoro kati ya wahusika ama vikundi vya wahusika, familia zao, matabaka yao n.k. na migogoro hii mara nyingi hujikita katika mahusiano ya jamii. Migogoro yaweza kuwa ya kiuchumi, kiutamaduni, kisiasa na kinafsia.
18.4 Wahusika katika Fasihi ya Kiswahili
Wahusika ni watu, ama viumbe waliokusudiwa wawakilishe tabia fulani za watu katika kazi za fasihi ..
 Mitazamo mbalimbali juu ya Mhusika ni nani?
Jonathan Culler katika kitabu chake  cha Structural Poetics anasema kuwa uhusika ni kipengele cha msingi katika riwaya, kwani kila tukio lipo ili kumfafanua mhusika na maendeleo yake. Naye Barthes katika kitabu hichohicho anasema kuwa mhusika ni kitu kilichochorwa kwa fikra (maneno) kwa msingi wa vielelezo vya kitamaduni, kwa maana kwamba mhusika wa fasihi ya jamii fulani ataeleweka vizuri na kwa urahisi zaidi na jamii hiyo husika.
Nao Kasper na Wuckel wanasema kuwa mhusika ni picha ambayo huchorwa na fasihi, na ni kiini cha vyote vipya, dhamira na mada za fasihi: Wanaendelea kudai kuwa katika mhusika kuna uwili: kwanza kuna usawiri wa kisanaa na mtu kwa upande mmoja, na sura ya mtu kwa upande mwingine. Yaani, katika mhusika kuna hali ya welekeo binafsi (subject) na uhalisi (object). Aidha, dunia ni ghala ya wahusika wa namna mbalimbali kwa fikra, hisia na utendaji, na hayo ndiyo yanayosababisha maendeleo tofauti.
Aristole akizungumzia mwigo katika utanzu mkuu wa zama zake, yaani tanzia, alisema kuwa mhusika hufunua uadilifu na kuonyesha lipi zuri baya, kwani tanzua tanzia ni mwigo wa watu.
Naye Hegel, alisema kuwa mhusika ni kitovu katika usawiri wa kisanaa, na anapaswa kutazamwa katika utatu huu:
  1. Kama mtu binafsi mkamilifu;
  2. Kama mtu katika upekee;
  3. Kama mtu mwenye tabia maalum iliiliyojijenga ndani yake.
Karl Marx na F rederick Engels, kwa kutumia upembuzi wa kiyakinifu, walikubaliana na Hegel kuhusu umuhimu wa mhusika, isipokuwa utatu wake usiangaliwe katika ombwe, bali katika mazingira yake kama ifuatavyo:
  1. Kama mtu binafsi, kwa sababu ni zao la upekee usioweza kujirudia;
  2. Kama mtu tabaka, kwa sababu ni kiwakilishi cha kijamii kinachosimamia tabaka, au kikundi maalum na maendeleo maalum ya kipindi cha historia;
  3. Kama mtu jamii, kwa sababu ni mtu mwenyewe sifa za mtu na za kijamii.
Sifa mbili ni bayana, kwani hujionyesha kupitia matendeo. Lakini sifa ya tatu ni ya kidhahania, au ya kufikirika.
Kutokana na ufafanuzi huu mhusika, tunaona kuwa wahusika ni watu au viumbe katika kazi ya fasihi waliokusudiwa kuwakilisha tabia za watu katika maisha halisi. Wahusika katika hadithi za mapokeo na baadhi ya hadithi fupi, kwa kawaida huwa ni wanyama, wadudu, mimea, mashetani, miungu, n.k. kama ndio wahusika wakuu. Kitabia, wahusika hawa hugawika katika makundi makubwa ya ubaya na wema. Katika riwaya, hasa zile za mwanzomwanzo (za akina Shaaban Robert, Mathias Mnyampala na Faraji Katalambullah), uundaji wa wahusika uliathiriwa na ule wa hadithi za kimapokeo. Lakini wahusika katika riwaya halisi huwa ni wahusika halisi wanaoendana kwa karibu sana na maisha ya kila siku kwa sura yao, mavazi yao, lugha yao, na hulka yao kwa ujumla. Na kitabia, hawagawanyiki kwa urahisi katika makundi mawili, bali huwa na tabia mchangamano: hawana sifa za uungu na kuwa wazuri moja kwa moja, wala hawana sifa za shetani wakawa wabaya mia kwa mia.
Je, ni jambo gani huwezesha mabadiliko ya mhusika? Sababu ya msingi ni kule kujitokeza kwa wajibu mpya wa fasihi kutoka kipindi kimoja hadi kingine unaotelekezwa na ukweli wa maisha, kwa njia ya mahusiano ya kijamii. Mhusika wa kipindi cha ukoloni hawezi kuwa na wajibu sawa na mhusika wa kipindi cha baada ya Azimio la Arusha; wala kamwe hawezi kuwa sawa na Yule wa baada ya kufia kwa uchumi huria.
AINA ZA WAHUSIKA KATIKA FASIHI
  • Wahusika Wakuu
Hawa ni wale ambao wanajitokeza kila mara katika kazi ya fasihi tangu mwanzo hadi mwisho. Wahusika hawa hubeba kiini cha dhamira kuu na maana ya hadithi yote. Vituko na matendo yote hujengwa kuwahusu ama kutokana nao. Mara nyingi jambo hili limewafanya wahusika wakuu wa kazi za fasihi wawe “midomo” ua wasanii. Wawe vipaza sauti vya Watungaji. Wahusika Wakuu hasa wa riwaya na tamthiliya huchorwa na Wasanii kwa mapana na marefu ya maisha na tabia zao ili kuukamilisha unafsi wao.
  • Wahusika wadogo/wasaidizi
Hawa hujitokeza hapa na pale katika kazi ya fasihi ili kuukamilisha ulimwengu wa kazi hizo. Hawa husaidia kujenga dhamira flani katika kazi ya fasihi, lakini mradi dhamira hiyo ni ndogo, basi hata wahusika hao tutawaita kama ni wadogo. Wakati mwingine husaidia kuijenga dhamira kuu ya kazi ya kazi ya fasihi, lakini, kwa sababu nafasi yao  ni ndogo sana katika kuutoa msaada huo, basi hawa tunawaita wahusika wadogo.
  • Wahusika wajenzi
Hawa ni wahusika ambao wamewekwe ili kuikamilisha dhamira na maudhui fulani, kuwajenga na kuwakamilisha. Wahusika hawa wawili; yaani wahusika wakuu na wahusika wasaidizi.
Wahusika wakuu na wadodo tunaweza kuwaweka katika makundi makuu matatu:
  • Wahusika Bapa
Hawa ni wale wasiobadilika kitabia au kimawazo kulingana na mazingira au matumio ya wakati wanayokutana nayo. Wahusika bapa tunaweza kuwagawanya kwenye makundi mawili:
Wahusika Bapa – Sugu – hawa wanakuwa sugu katika hali zote, kiasi amacho hata tunapowaona mahali pengine hali zao ni zilezile, hawahukumiwa bali wao huhukumu tu, hawashauriwi bali wao  hushauri tu, madikteta, mfano Bwana Msa katika riwaya za  M.S. Abdalla ni mmoja wa wahusika hawa.
 
Wahusika Bapa – Vielelzo – Ni wale ambao pamoja na kutobadilika kwao, wamepewa majina ambayo humfanya msomaji aielewe tabia na matendo yao. Shaaban Robert alikuwa fundi sana katika kuwaumba wahusika wa aina hii, akina Majivuno, Adili, Utubusara n.k. Hapa msanii anatilia mkazo tabia moja inayotawala, kiasi ambacho anaondoa sehemu nyingine zote za sifa za mhusika huyo.
  • Wahusika Duara/Mviringo
Hawa ni wahusika ambao wana desturi ya kubadilika kitabia, mawazo au kisaikolojia. Maisha yao yanatawaliwa na hali halisi za maisha. Hivyo wanavutia zaidi kisanii, kwani wanasogeza hadithi ielekee kwenye hali ya kutendeka au kukubalika na jamii. Mfano ni: Rose (Rosa Mistika), Josina (Pepo ya Mabwege).
  • Wahusika Shinda/Wafoili
Hawa wako katikati ya Wahusika bapa na wahusika duara. Hawakuja kama wahusika duara, lakini ni hai zaidi kuliko wahusika bapa. Tofauti kubwa kati ya wao na wahusika wengine ni kwamba wahusika shinda wanawategemea wahusika duara au wahusika bapa zaidi ili waweze kujengeka. Wanaendeshwa na mawazo ya wahusika wengine. Kwa mfano, katika riwaya za M.S. Abdalla, Najum ni mhusika shinda.
Mwl Maeda
Reply


Messages In This Thread
ODC : MUHADHARA WA KUMI NA NANE : FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI - by MwlMaeda - 12-25-2021, 03:32 PM

Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)