MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
VYOMBO VYA UKUZAJI NA UENEZAJI WA KISWAHILI

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
VYOMBO VYA UKUZAJI NA UENEZAJI WA KISWAHILI
#1
Vyombo vya ukuzaji na uenezaji wa Kiswahili
Ili kuimarisha matumizi ya lugha ya Kiswahili serikali iliamua kuanzisha vyombo mbalimbali vya ukuzaji wa Kiswahili. Katika mada hii utaweza kujua vyombo mbalimbali vya kitaifa na kimataifa vinavyojishughulisha na ukuaji na uenezaji wa Kiswahili. Pia utaweza kujua majukumu ya kila chombo kataka ukuaji na uenezaji wa Kiswahili.
Tangu Tanzania ipate uhuru hadi sasa kuna vyombo kadha wa kadha vilivyoanzishwa kwa ajili ya kukuza na kueneza Kiswahili baadhi ya vyombo hivyo ni hivi vifuatavyo:
BAKITA
Hii ni taasisi ya serikali iliyoundwa kwa sheria ya Bunge Na.27 ya mwaka 1967 kwa madhumuni ya kukuza Kiswahili. Kutokana na sheria hii Baraza ndilo mratibu wa kusimamia asasi zote na mawakala wote wanaokuza Kiswahili katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
BAKITA imekuwa na mchango mkubwa sana katika ukuzaji na uenezaji wa lugha ya Kiswahili kupitia majukumu yake. Majukumu ya Baraza kama yalivyofafanuliwa katika sheria hiyo ni haya yfuatayo:
  • Kuratibu na kusimamia maendeleo na matumizi ya Kiswahili nchini kote. Katika kufanya hivi Baraza lina jukumu la kuhakikisha Kiswahili kinaendelea na kuhakikisha kuwa matumizi ya Kiswahili yanakuwa sahihi.
  • Kushirikiana na vyombo vingine nchini vinavyojihusisha na maendeleo ya Kiswahili na kuratibu shughuli zao. Vyama vya Kiswahili kama vile CHAKAMA, CHAWAKAMA vina mchango mkubwa wa kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili kwa kushirikiana na BAKITA. Ushirikiano wa BAKITA na vyama hivi waweza kuwa ni wa kuto ushauri, au msaada wa kifedha, kwa mfano BAKITA imekuwa ikiwasaidia CHAWAKAMA pale wanapokuwa wanataka kufanya makongamano nap engine wanahitaji msaada wa kifedha, kwa hiyo BAKITA imekuwa ikiwasaidia kifedha.
  • Kuhimiza matumizi ya Kiswahili katika shughuli rasmi na za kawaida. BAKITA imekuwa ikiandaa vipindi mbalimbli redioni ili kuhimiza matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili.
  • Kushirikiana na mamlaka zinazohusika kuthibitisha tafsiri sanifu za istilahi. Katiaka uundaji wa istilahi, BAKITA imekuwa ikichapisha vitabu mbalimbali ikionesha istilahi sanifu zilizoingizwa katika lugha ya Kiswahili. kwa hiyo kupitia jukumu hili Kiswahili kimekuwa kinakua.
  • Kutoa huduma za tafsiri na ukalimani kwa serikali, mashirika ya serikali na yasiyo yaserikali na asasi nyingine. Kupitia tafsiri zinazofanywa na BAKITA Kiswahili kimekuwa kikikuwa na kuenea.
  • Kuchapisha jarida au toleo linalohusu lugha na fasihi ya Kiswahili. Machapisho haya ya BAKITA yanaendelea kukifanya Kiswahili kukua kwa kuongeza msamiati mpya na hivyo watu wanaposoma machapisho hayo wanajifunza msamiati mpya na hivyo kufanya Kiswahili kukua.
  • Kushirikiana na mashirika ya kitaifa, asasi na watu binafsi, kufuatilia, kushauri na kusimamia shughuli zinazolenga kukuza Kiswahili nchini Tanzania.
  • Kutoa ushauri kwa waandishi na wachapishaji ili watumie Kiswahili fasaha. Kwa kufanya hivi matumizi bora ya Kiswahili yanakuwa yanaimarika.
  • Kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuthibitisha vitabu vya Kiswahili vitakavyotumika shuleni na vyuoni kabla havijachapishwa. Hili pia ni jamabo linaloimarisha matumizi ya Kiswahili sanifu.
TAKILUKI
Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI) ilianzishwa mwaka 1979 kwa lengo la kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya Zanzibar, ili kutimiza lengo hilo TAKILUKI inajishughulisha na kazi zifuatazo:
  • Kuratibu na kuendesha mafunzo ya lugha ya Kiswahili visiwani Zanzibar, kuendesha mafunzo ya lugha ya Kiswahili kwa wazawa na wageni, kuhariri miswada mbalimbali ili kuthibitisha ufasaha wa Kiswahili na kufanya tafiti za Kiswahili katika Nyanja zake zote, hususani katika uwanja wa sarufi na fasihi.
  • Pia TAKILUKI wana kazi ya kuandaa istilahi za taaluma mbalimbali, kutoa huduma za taaluma mbalimbali, kutoa huduma za tafsiri na ukalimani kwa lugha mabalimbali kwa mashirika, idara, wizara, taasisi, kampuni na watu binafsi, kufundisha lugha za kigeni na kuandika vitabu mbalimbali vya Kiswahili.
  • Pia hujishughulisha na utoaji wa ushauri wa kitaaluma kwa watunzi wa vitabu ili waweze kuandika kazi zenye ubora, na kushirikiana na wadau wengine wa Kiswahili kama vile, mashirika, wizara, taasisi, vyuo na watu binafsi katika kuendesha shuguli za ukuzaji wa Kiswahili, mathalani kuandaa na kuendesha semina, warsha na kozi fupifupi za Kiswahili.
  • Vilevile hujishugulisha na usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili katika vyombo vya habari na katika shughuli mbalimbali za serikali na za kawaida.
TUKI/TATAKI
Majukumu ya TUKI ni pamoja na kuunda sera muafaka za kustawisha Kiswahili na pia kufanya utafiti katika lugha ya Kiswahili.
Majukumu mengine ya TUKI ni kuhariri, kuchapisha vitabu na kutawanya vitabu na majarida ya kitaaluma katika Kiswahili.
Kwa sasa TATAKI inatoa shahada ya awali na uzamili katika lugha ya Kiswahili, kwa njia hii inawaandaa wataalamu wa lugha ya Kiswahili ambao watatumika sehemu mbalimbali za ulimwengu kufundisha lugha ya Kiswahili.
CHAUKIDU
CHAUKIDU ni kifupi cha Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani, makao makuu ya chama hiki kwa sasa yapo chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani.
Madhumuni makuu ya CHAUKIDU ni: Kuwajumuisha pamoja wakuzaji wa Kiswahili duniani kote kwa lengo la kuchochea kasi ya malengo mahususi yafuatayo:
  • Kukuza Kiswahili katika nyanja zote ambamo lugha hii inatumika au inaweza kutumika na kuongeza ufanisi wa mawasiliano katika ufundishaji na utafiti wa maarifa ya aina zote, uandishi/utangazaji wa habari, uandishi wa vitabu, uchapishaji vitabu na majarida, utayarishaji wa safari za mafunzo katika Afrika ya Mashariki na Kati, n.k.
  • Kusambaza habari na matokeo ya utafiti kwa kutumia machapisho mbalimbali na teknolojia ya mtandao wa kompyuta juu ya vipengele mbalimbali vya Kiswahili na masuala yanayohusiana na Kiswahili.
  • Kuwajumuisha wanachama kwa ajili ya kubadilishana mawazo na tajiriba zao katika masuala mbalimbali yanayohusu Kiswahili (k.v. uboreshaji wa ufundishaji, utangazaji, utafiti, uandishi, nk.) kwa njia ya mkutano wa kila mwaka, warsha au semina au kongamano maalumu, na hata kwa njia ya mtandao.
  • Kuelimisha umma juu ya umuhimu wa kujivunia, kuendeleza, na kuheshimu Kiswahili.
  • Kushauri ama kushinikiza serikali za nchi ambamo Kiswahili kinazungumzwa kutambua thamani iliyobebwa na maliasili hii ili kuunda sera muafaka za kukiendeleza kadri ya uwezo wake kwa manufaa ya maendeleo ya serikali na watu wake kijamii, kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, kielimu, n.k.
CHAWAKAMA
CHAWAKAMA husimama badala ya Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili vyuo vikuu Afrika Mashariki. Chama hiki kilianzishwa mwaka 2004 kwa lengo la kukuza na kueneza Kiswahili katika eneo lote la Afrika Mashariki kupitia wanafunzi wanaosoma Kiswahili vyuoni. Wanachama wa chama hiki ni wale wanosoma Kiswahili na hata wale wenye mapenzi ya lugha ya Kiswahili pia wanaweza kujiunga na chama hiki.
Chama hiki kina utaratibu wa kuandaa makongamano ambapo wanachama wake kutoka nchi zote za Afrika Mashariki hupata fursa ya kukutana mara moja kila mwaka. Pamoja na utaratibu wa chama kuandaa makongamano pia uanzishwaji wake umeambatana na malengo kadhaa ambayo ndiyo dira inayoiongoza chama kwa mujibu wa katiba, malengo hayo ni haya yafuatayo:
  • Kuwapa wanachama nafasi ya kujadili, kuimarisha, kuendeleza na kukuza vipawa vyao vya lugha na fasihi ya Kiswahili.
  • Kuamsha ari ya mapinduzi ya utamaduni wa lugha ya kiswahili.
  • Kueneza lugha ya kiswahili ndani na nje ya nchi.
  • Kushirikiana na vyama vingine katika juhudi za kuendeleza na kuimarisha lugha ya kiswahili ndani na nje ya nchi wanachama.
  • Kuwaunganisha wanafunzi wa kiswahili Afrika Mashariki na kati katika kukikuza kiswahili.
  • Kushirikiana na asasi mbalimbali zinazojihusisha na ukuzaji na uenezaji wa kiswahili ndani na nje ya nchi kama vile BAKITA, TATAKI, TAKILUKI, UWAVITA, CHAKAMA, BAKIZA n.k.
  • Kuchapisha kijarida cha chama na machapisho mengine ili kusaidia kueneza taaluma ya kiswahili.
  • Kuweka kumbukumbu ya wataalamu wa kiswahili kwa nia ya kuwatumia katika kufanikisha malengo ya chama na wadau wa Kiswahili.
  • Kuratibu makongamano na mijadala mbalimbali inayohusiana na taaluma ya kiswahili.
Pamoja na malengo hayo, lengo kuu la chama hiki ni kueneza Kiswahili lakini sasa wanakienezaje? Wanachama wa chama hiki ambao ni nchi wanachama wa jumuia ya Afrika mashariki wanakawaida ya kuandaa makongamano kwa ngazi ya kitaifa na ngazi ya kimataifa.
Kwa ngazi ya kitaifa kila nchi huandaa kongamano kila mwaka ambalo linawakutanisha wanachama wote kutoka vyuo mbalimbali katika nchi husika. Katika kongamano hilo mada mbalimbali zinazohusu lugha ya Kiswahili na mustakabali wake hujadiliwa lakini pia maazimio mbalimbali huchukuliwa juu ya maendeleo ya chama. Sasa katika mijadala kama hii inatoa nafasi ya Kiswahili kukua kwani makala mbalimbali huandikwa ambazo pia husomwa na watu mbalimbali. Makala hizi pia zimekuwa zikichapishwa katika majarida ya chuo husika na pia zimekua zikichapishwa mtandaoni ambapo hutoa fursa kubwa kwa watu wengi zaidi kuzifikia na kusoma, hivyo kwa njia hiyo Kiswahili kinakua kimeenea.
MAFANIKIO NA CHANGAMOTO ZINAZOVIKABILI VYOMBO VYA UKUZAJI WA KISWAHILI
Mafanikio
  • Vyombo vya ukuzaji wa Kiswahili vimejitahidi sana kukuza lugha ya Kiswahili, kwa hali ya Kiswahili ilivyo sasa ni matokeo ya juhudi za vyombo hivyo. Mafanikio ya vyombo hivyo ni pamoja na haya yafuatayo:
  • Machapisho ya lugha ya Kiswahili ni mengi sana nchini na nje ya nchi, kufanya mafunzo ya Kiswahili, kukua kwa matumizi ya Kiswahili na kuongezeka kwa idadi ya watumiaji wa Kiswahili nchini.
  • Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika sehemu rasmi hasa katika ofisi za serikali na ofisi za watu binafsi inadhihirisha mafanikio ya jitihada za vyombo hivi kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili.
  • Kufundshwa kwa lugha ya Kiswahili kama taaluma kwa ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu. Hizi ni jitihada za TATAKI katika kuhakikisha kunapatikana wataalamu wa lugha ya Kiswahili, hivi sasa TATAKI wanafundisha lugha ya Kiswahili kwa ngazi ya shahada ya awali, uzamili na uzamivu.
  • Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika vyombo mabalimbali vya kimataifa, matumizi ya lugha ya Kiswahili katika vikao vya Umoja wa Afrika na pia ufundishwaji wa lugha ya Kiswahili katika vyo mabalimbali Duniani ni ishara tosha ya kuonesha mafanikio ya jitihada za vyombo vya ukuzaji na uenezaji wa Kiswahili.
Changamoto
Licha ya mafanikio hayo lakini pia kuna changamoto zinazovikabili vyombo hivi vya ukuzaji wa Kiswahili.
  • Vyombo hivi vinakabiliwa na upungufu wa wataalam. Wataalamu wengi waliobobea katika taaluma za Kiswahili wanakimbilia nje ya nchi wakidhani huko ndiko kuna maslahi mazuri zaidi.
  • Upungufu wa fedha za kuendeshea shughuli za ukuzaji wa Kiswahili katika vyombo hivi pia limekuwa ni tatizo sugu. Kwa hiyo shughuli za ukuzaji wa Kiswahili zinakuwa zinakwenda taratibu.
  • Taasisi hizi pia zinashindwa kujitangaza vizuri kutokana na kwamba hazina vyombo vya habari binafsi ambavyo vingeweza kutumika kutangaza shughuli zao. Jambo hili limesababisha vyombo hivi kushindwa kutoa elimu ya Kiswahili kwa kutumia vyombo vya habari kutokana na kwamba gharama za kufanya hivyo ni kubwa.
  • Vyombo hivi baadhi havina ofisi za kudumu, na hivyo kuhamahama jambo ambalo linaathiri utendaji kazi wa vyombo hivyo.
Mwl Maeda
Reply


Messages In This Thread
VYOMBO VYA UKUZAJI NA UENEZAJI WA KISWAHILI - by MwlMaeda - 09-09-2021, 07:49 AM

Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)