MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
SHAIRI : ETI SIYE TULIKUWA, WASHENZI HAPO ZAMANI - Printable Version
JIFUNZE KISWAHILI
SHAIRI : ETI SIYE TULIKUWA, WASHENZI HAPO ZAMANI - Printable Version

+- JIFUNZE KISWAHILI (https://jifunzekiswahili.co.tz)
+-- Forum: My Category (https://jifunzekiswahili.co.tz/forumdisplay.php?fid=1)
+--- Forum: Fasihi simulizi (https://jifunzekiswahili.co.tz/forumdisplay.php?fid=6)
+---- Forum: Ushairi (https://jifunzekiswahili.co.tz/forumdisplay.php?fid=50)
+---- Thread: SHAIRI : ETI SIYE TULIKUWA, WASHENZI HAPO ZAMANI (/showthread.php?tid=1947)



SHAIRI : ETI SIYE TULIKUWA, WASHENZI HAPO ZAMANI - MwlMaeda - 01-03-2022

SHAIRI : ETI SIYE TULIKUWA, WASHENZI HAPO ZAMANI
**************

Jameni ninaumia, sana ninahangaika,
mno nikifikiria, imepita mingi miaka,
tangu zama n’kisikia, n’kisoma wanoandika,
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani.

****
Vitabu waliandika, Waasia na Wazungu,
hata ndugu Wafirika, waliofundwa kizungu,
‘ti hatukuthamanika, mbele ya kuja Wazungu,
eti siye tulikuwa , washenzi hapo zamani.

*****
“Babu zetu walikuwa, wapo totoro gizani”,
haya nilifundishiwa, karibu miaka sitini,
‘mi bado sijaelewa, na staki kwelewa hini,
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani !!?

*****
Huku yote waliponda, eti ya kishenzi yetu,
vyema tulivyoviunda, hawakuthamini katu,
vya chuma tulipounda, waka’amba vina kutu,
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani.

*****
Wajameni fikiria, tafakari n’nayowaza,
Ziwa la Vikitoria, si li’kuwa Ziwa Nyanza?
kila walichopitia, walikibatiza kwanza,
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani.

*****
Mlima wa Eligoni, hauna la jadi jina?
Wakenya nipulikeni, mnambie na maana,
Babu wana jina gani, la mlima walinena?
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani.

*****
Leo napata simanzi, kasumba walotutia,
tukakubali ushenzi, hadi leo nawambia,
tunalo soko mshenzi, na la kizungu sikia,
eti siye tulikuwa, washenzi hapo zamani.

****^
Haya ya Nyerere mambo, kuusaili uzungu,
kauliza hili jambo,la kasumba ya kizungu,
vitu vyenye kubwa umbo, mwaviita vya kizungu,
nzi mwenye kubwa umbo, hamusemi wa kizungu?

*****
Ushenzi haswa yakini, na ma’na ye halisia,
siye huo wa zamani, waliotupakazia,
ni uno wa enzi hini, kasumba kukumbatia,
yetu kutoyathamini, tukaona ya kishenzi,

*********
Rwaka rwa Kagarama,,( Mshairi Mnyarwanda)
Jimbo la Mashariki, Wilaya ya Nyagatare,
R W A N D A..