MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
ETIMOLOJIA YA MANENO ' ADA' na 'ADAA' - Printable Version
JIFUNZE KISWAHILI
ETIMOLOJIA YA MANENO ' ADA' na 'ADAA' - Printable Version

+- JIFUNZE KISWAHILI (https://jifunzekiswahili.co.tz)
+-- Forum: My Category (https://jifunzekiswahili.co.tz/forumdisplay.php?fid=1)
+--- Forum: Majadiliano ya Wadau wa Kiswahili (https://jifunzekiswahili.co.tz/forumdisplay.php?fid=16)
+--- Thread: ETIMOLOJIA YA MANENO ' ADA' na 'ADAA' (/showthread.php?tid=1791)



ETIMOLOJIA YA MANENO ' ADA' na 'ADAA' - MwlMaeda - 12-22-2021

HII NDIYO ETIMOLOJIA YA MANENO ' ADA' na 'ADAA'

Neno *ada* katika lugha ya Kiswahili lina maana zifuatazo:

1. *Nomino* : Gharama au karo anayolipa mtu ili apatiwe huduma fulani kwa mfano katika elimu, burudani au kupata uanachama katika chama.

2. *Nomino:* Mila na desturi za jamii fulani. (Mfano: Kila kabila lina ada zake za maziko.)

3. Kawaida katika kufanya jambo. (Kwa mfano: Kunywa chai kila jioni ni ada yake.)

Kuna methali: *Ada ya mja hunena, muungwana ni kitendo.*

Katika lugha ya Kiarabu, neno hili *ada* (soma: *aadatun/aadatan/aadatin عادة* ) lina maana zifuatazo:

1. *Nomino* : Jambo ambalo mtu amezoea kulifanya na kulikariri.

2. *Nomino* : Kulitekeleza jambo ipasavyo na ndani ya wakati.

3. *Nomino* : Kutimiza wajibu na kuukamisha.

4. Jambo linalokariri kutokea kila mwezi; ada ya mwezi.

Kinachodhihiri ni kuwa neno hili ( *aadatun/aadatan/aadatin عادة*) lilipoingia katika lugha ya Kiswahili na kutoholewa kuwa neno *ada*  maana yake katika Kiarabu haikubadilika na lilichukua dhana mpya ya *gharama au karo anayolipa mtu ili apatiwe huduma fulani a*  dhana ambayo  Kiarabu huitwa *rasmun/rusuumun*  *رسم/رسوم* .

Neno *adaa* katika lugha ya Kiswahili lina maana ya 'ulazima unaompasa mtu kuutekeleza kwa mujibu wa maamrisho ya dini kwa mfano kuswali, kufunga na kutoa Zaka.

Neno hili *adaa* (soma: *adaa-un/adaa-an/adaa-in أداء* ) katika lugha ya  Kiarabu lina maana ya:

1. Kulifikisha jambo na kulitimiza au kulitekeleza kwa namna inavyopasa.

2. Kuzitamka herufi za lugha kwa namna inayopasa.

Kinachodhihiri ni kuwa neno hili *adaa*(soma: *adaa-un/adaa-an,/adaa-in أداء*) lilipoingia katika Kiswahili maana yake katika Kiarabu haikubadilika ingawa lilijifunga katika wajibu wa kutekeleza maamrisho ya dini.

*Shukran sana.*

*Khamis S.M. Mataka.*