MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
JIFUNZE KISWAHILI - SIMULIZI: MKEO AMEFARIKI

JIFUNZE KISWAHILI

Full Version: SIMULIZI: MKEO AMEFARIKI
You're currently viewing a stripped down version of our content. View the full version with proper formatting.
MKEO AMEFARIKI.
“Mkeo amefariki Msiba uko hapa nyumbani?” Denis alipokea ujumbe mfupi kwenye simu yake, kuangalia ulitoka kwa Mama yake mzazi. Nguvu zilimuishia, alikua akiongea na mteja ofisini kwake lakini sauti ilikauka.
Bila kujijua alijikuta ananyanyuka na kuanza kutembeatembea ofisini kwake akiwa hajitambui. Wafanyakazi wake walimuuliza bosi vipi lakini hakuwa na jibu la maana la kuwapa.
Akili yake ilikumbuka maneno ambayo alimuambia mkewe asubuhi wakati anaondoka, mkewe alimuambia sukari imeisha na kwa dharau alimjibu “Sasa unaniambia mimi ili nini? Kwani ni lazima unywe chai huko kwenu mlikua mnakunywa chai kila siku??”
Alikumbuka namna usiku wake alivyompiga makofi baada tu ya mboga kuungua alipochelewa kuepua kwani alikua ananyonyesha mtoto wao wa mwisho ambaye yeye mwenyewe ndiyo alimuita amnyonyeshe kwani alikua analia sana.
Alikumbuka namna siku mbili kabla mkewe alisema amechoka kupigwa na kunyanyaswa, anakumbuka namna alivyomjibu kwa dharau kuwa kama amechoka aondoke amuachie watoto wake.
“Ameniachia wanangu!” Alijikuta anaropoka na machozi yalianza kumtoka. Alishindwa hata kutembea hivyo alikaa chini kabisa sakafuni. Wafanyakazi wake walikuja na kumnyanyua na baada ya kumuuliza ndipo alipowaambia mkewe amefariki.
Walimchukua mpaka kwenye gari na safari ya kurejea nyumbani ilianza, walifika nyumbani, kila kitu kilikua kimya, nyumba ilikua imefungwa na hakukua na mtu.
Denis alizidi kuchanganyikiwa zaidi asijue nini cha kufanya ndipo alipokumbuka kuwa Mama yake alimuambia msiba uko nyumbani hivyo alidhani kuwa ni nyumbani kwao.
*****
Safari nyingine ilianza, Denis alikua na mawazo, hayakuwa mawazo tu ya kufiwa bali ya aibu. Pamoja na kumiliki kampuni kubwa akiajiri watu ziadi ya kumi lakini mkewe alimnyanyasa na kumtesa kama kinyago, mbali na kumpiga lakini alikua hamhudumii vizuri.
“Atakua amefia kwa Mama wakati amenda kuomba hela ya matumizi…” Aliwaza kwani mara nyingi alipokuwa akimnyima pesa Mama yake mzazi ndiyo alikua akimsaidia na ndiyo alizuia mara nyingi mkewe asiondoke.
Alifika mpaka nyumbani kwao, kweli kulikua na msiba, maturubai yalishawekwa, watu walishaanza kupika na watu walishaanza kujaa taratibu. Alijitahidi kushuka kwenye gari na kuanza kutembea kuelekea nyumbani.
Watu walikua wakimsalimia na kumpa pole, aliipokea kwa aibu huku akiwaza ni kitu gani kiliwasukuma wazazi wake kufanyia msiba pale na ni nini kilikua kimesababisha mauti ya mkewe.
“Ameumwa sana muacheni apumzike..” Ilikua ni sauti ya Baba yake ikimuambia jirani yao mmoja. Hapo ndipo alichanganyikiwa zaidi akiwaza ni kwa namna gani mkewe alikua anaumwa bila yeye kujua.
Lakini alikumbuka ni mara kibao mkewe alimuambia anaumwa lakini alidharau na ni mara nyingi Mama yake alimsema kuhusu kutokumsikiliza mkewe na mara nyingi tu Mama yake aliongozana na mkewe hospitalini.
Yeye kwake yote hayo hakujali, kila mke alipomuambia anaumwa yeye alidai haki yake ya ndoa, alizidi kumpiga na alianza kukumbuka namna ambavyo alimpiga mpaka kulazwa lakini bado hakujali.
Aliwaza labda ndiyo ilikua sababu ya kifo chake. “Au alikua anaumwa kimyakimya hasemi akaja kusema nyumbani..” Alitembea mpaka kufika ndani, alikaa na kusalimiana na ndugu wengine ambao nao walikua wanampa pole kwa msiba.
Alizipokea huku akijaribu kujizuia machozi yasitoke. Mara mtoto wake wapili wa miaka minne alikuja. Alikua akilia akimtaka Mama yake watu wakimuambia asubiri Mama yake anakuja.
Mtoto alimkimbilia Dennis na kuanza kulia namtaka Mama namtaka Mama. Denis alichaganyikiwa kwani hakuwa na jibu la kumpa, hakujua amumbie nini kuhusu Mama yake.
Mara mtoto mwingine mkubwa kidogo wa miaka saba alikuja, alikua amembeba mtoto wao mdogo mchanga wa miezi sita. Alimfuata Baba yake na kumuuliza Baba Mama yuko wapi Jack anataka kunyonya.
Hapo ndipo aliishiwa nguvu kabisa, maneno yake ya “Ondoka niachie wanangu yalizunguka kichwani kwake” Aliwaangalia wanae na kusema kweli nimeachiwa, umeniweza Juddy mke wangu.
Alijikuta anaanza kulia kama mtoto kitu ambacho kiliwafanya na wanae wote kulilia. Denis alichanganyikiwa, kila mtu aliyekua anakuja alienda kumpa pole, nguvu zilimuishia alikata tamaa, na majuto ya hali ya juu, kila tendo baya alilokua akimfanyia mkewe lilimjia kichwani.
****
“Mama Jose njoo umnyonyeshe mtoto analia muda mrefu..” Ilikua ni sauti ya Mama yake, Denis alistuka na kunyanyuka kuangalia, Mama Jose ni mkewe na hakujua ni kwanini Mama yake alikua anamuambia aje kumnyonyesha mtoto wakati alishafariki dunia.
Kabla hajasema chochote Mama yake aliingia “Ohhh umekuja, nikajua utakuja baadaye kazi zimekubana, mkeo alisema hupatikani kwenye simu.”
Denis alizidi kuchanganyikiwa, alibaki na mshangao. Mara mkewe aliingia, hapo ndipo alichanganyikiwa zaidi, alistuka kama vile ameona mzimu, kidogo amdondoshe mtoto aliyekua amempakata.
“Vipi Baba Jose…” Mkewe alimuuliza, namna alivyokua akimuangalia haikua kawaida. “Uko hai mke wangu?” Alijikuta anauliza. “Ndiyo kwani vipi ulitaka nife?” Mkewe alijibu kwa kebehi kidogo kwani alijua ni madharau ya mumewe.
“Lakini Mama..” Denis aliongea kwa kushangaa huku akimuangalia Mama yake. Mama yake alitabasamua na kumuambia, aliyekufa ni Bibi yako si ndiyo anakuitaga mume wangu.
Wewe mbona kila siku ukipiga simu unaulizia mke wangu hajambo. Denis alipumua kwa nguvu huku akikaa chini, mkewe alichukua mtoto kwenda kumnyonyesha. Denis alimfuata huko huko chumbani, alipiga magoti mbele yake na kusema.
“Samahani mke wangu nilikua sijajua thamani yako mpaka leo. Yaani leo ndiyo nilichanganyikiwa, nilijua umekufa na tayari nilishaona maisha hayawezekani bila wewe. Naahidi nitabadilika nitakua mume mwema na kamwe sikunyanyasi tena.
Mama yake ambaye alisimama mlangoni alitingisha kichwa na kucheka. Huku akisema “Unavyoringa uachiwe watoto kila siku unajua uchungu wa kulea wewe au unataka uachiwe ili uje kunitupia wanao hapa nianze kulea wajukuu!”
Hakusubiri hata jibu aliondoka akimuacha mwanae akiendelea kuomba msamaha akiwa haamini kuwa mkewe yuko hai. Siku ile ndiyo ilikua siku ya Mabadiliko ya Denis hakuwahi kumpiga wala kumnyanyasa tena mkewe.
****MWISHO.