MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
JIFUNZE KISWAHILI - UHAKIKI WA RIWAYA YA KUFIKIRIKA

JIFUNZE KISWAHILI

Full Version: UHAKIKI WA RIWAYA YA KUFIKIRIKA
You're currently viewing a stripped down version of our content. View the full version with proper formatting.
KITABU: KUFIKIRIKA
MWANDISHI : S. ROBERT
MCHAPISHAJI : OXFORD UNIVERSITY PRESS
MWAKA : 1967
Riwaya ya kufikirika ni riwaya iliyotungwa na mwandishi mashughuli Shaabani Robert, katika riwaya hii mwandishi anaeleza juu ya mila na desturi zilizopitwa na wakati kuwa hazina nafasi katika kipindi cha sasa. Mwandishi anaeleza kuwa jamii ya watu wakufikirika ilikuwa inaamini juu ya uganga na mambo ya kijadi. Hivyo kupitia mhusika utu busara ambaye alikuwa anaelimu kubwa ya dunia. Utu Busara alijiingiza katika kundi la utabiri ili aweze kuleta mabadiliko katika nchi ya kufikirika. Kutokana na utabiri wake Mfalme na Malkia wanafanikiwa kupata mtoto na baadae Utu Busara tena anakuwa mwalimu wa mtoto wa mfalme na kuanza kumfundisha elimu ya dunia ambayo ni kinyume na matakwa ya mfalme, baada ya kufukuzwa na mfalme, Utu Busara anaamua kujiingiza katika kilimo ambapo ikapelekea kukamatwa kwa kudhaniwa kuwa ni mjinga. Kutokana na elimu na weledi alionao utu busara anafanikiwa kujiokoa kutoka gerezani na kufanikiwa kumponya mtoto wa mfalme kwa kutoa ushauri kuwa apelekwe hospitali. Mwisho mtoto wa mfalme anapona na kufanya utu busara kufanikiwa katika nia yake ya kuleta mabadiliko katika nchi ya kufikirika.
Katika kuhakiki na kuchambua riwaya hii ya Kufikirika tutazingatia vipengele vya fani na maudhui. Hivyo tutaanza kwa kuchambua vipengele vya maudhui ambavyo hujumuisha dhamira, ujumbe, migogoro, mtazamo, na falsafa na kisha tutatalii kwa kina juu ya fani na vipengele vyake..
Dhamira, Katika riwaya hii ya Kufikirika mwandishi shaaban Robert ameonesha dhamira kuu ni ukombozi wa kiutamaduni. Kiujumla riwaya ya kufikirika inajdili harakati zinazofanywa na Utu Busara za kupambana na tamaduni zilizopitwa na wakati. Kupitia mhusika Utu Busara mwandishi anaonesha kuwa mila na tamaduni zilizopitwa na wakati hazina budi kutupiliwa mbali hasa katika kipindi hiki cha sayansi na teknolojia.
Licha ya dhamira kuu, pia mwandishi amejadili dhamira ndogondogo kupitia wahusika lukuki ambao amewatumia katika riwaya hii, Dhamira hizo ni kama zifuatazo:
Suala la uongozi, Mwandishi Shaban Robert hakupuuzia suala la uongozi katika riwaya hii, anaonesha kuwa viongozi wa nchi ni lazima wawe mstari wa mbele katika kuhakikisha maslahi ya nchi yanalindwa na wananchi wanaishi kwa amani. Mwandishi anabainisha suala hili kwa kumtumia mhusika mfalme (uk 1-2)
“Nimejaliwa kupata ufalme kuliko wafalme wengine walio majirani zangu. Binafsi yangu nimepigana vita nyingi kulinda nchi isitekwe adui. Ushindi wa kila vita umenipa utukufu wa namna ya peke yake. Milki yangu pana imeenea kaskazini, kusini, mashariki na magharibi.”
Suala la ugumba na utasa,mwandishi shaban robert hakusita kulielezea suala la ugumba na utasa katika riwaya hii ambalo ndio lilipelekea kuibua dhamira mbalimbali. Mwandishi anamtumia mhusika mfalme na malkia katika kuonesha tatizo hili. Mwandishi anaonesha kuwa licha ya ujasili, uzalendo na furaha yote aliyokua nayo mfalme na malkia lakini walijiona sio kitu kutokana na kukosa mtoto, ambaye angekuja kurithi madaraka mara baada ya kufa kwa mfalme.(uk 3)
“…………….jina lake litachorwa kwa majohari, wa watu hawa na pia nashukuru kwa kuwa bwana juu ya vitu vya faraja visivyokwisha, lakini nina sikitiko kubwa kwa kukosa mtoto. Maskini mwenye mtoto namuona kuwa bora kuliko mimi………….”
Kutokana na tatizo hili mfalme akatafuta kila njia ili aweze kupata mtoto. Hapa ndipo mfalme alipoamua kuweka bayana tatizo lake hili aweze kuaidiwa.
Suala la imani potofu, mwandishi anaonesha juu ya dhana potofu zilizojengeka katika vichwa vya watu wa kufikilika juu ya mtu mwerevu na mjinga. Wanaona kuwa mjinga na mwelevu hujulikana kutokana na kazi anayoifanya mtu, utu busara alionekana kama mtu mjinga kutokana na shughuli ya kilimo aliyokuwa anaifanya halikadhalika mfanyabiashara alionekana mwelevu kutokana na kazi yake (uk 39)
”…………mtu wa kwanza alikuwa na umbo kuza. Kazi yake ilikuwa ni biashara mjini. Ajali ya kukamatwa ilikua amekaa kitako dukani pake. Yeye alihesabiwa kuwa ni mwerevu. Mtu wa pili alikua na umbo la wastani. Amali yake ilikuwa ni ukulima. Ajali ya kufanywa mahabusi wa kafara ilimkuta shambani pake analima. Huyu alidhaniwa kuwa ni mjinga……..”
Kutokana na mtazamo huu, hatimaye mwelevu aliweza kujinasua na kifo hicho, hivyo mwandishi shaban robert anajaribu kutoa mwanga kwa jamii juu ya dhana potofu na kuitaka jamii kubadilika ili kuendana na wakati.
Halikadhalika imani potofu imekisili katika jamii ya watu wa kufikirika kwani wanaamini juu ya mambo ya jadi hasa uganga na kupuuzia huduma za kisasa kama vile hospitali. Hivyo mwandishi shaban robert kupitia mhusika wake Utubusara anaitaka jamii kuachana na mila na tamaduni zilizopitwa na wakati kwani huweza kusababisha hasara kubwa kwa jamii husika kama ilivyowapata watu wa kufikirika ambao walipoteza vitu vingi kwa ajili ya uganga (Uk 8-14)
Nafasi ya mwanamke, mwandishi shaaban robert hakupuuza nafasi ya mwanamke katika riwaya yake. Katika riwaya hii mwandishi amemchora mwanamke kama mtu muhimu katika jamii mwenye kutoa ushauri na ukakubalika. Mfalme analithibitisha hili katika ( uk 1) anasema
“………alikuwa tayari kupokea msaada uliotolewa kwa hiyari na mwanamke lakini kulazimisha kutendewa msaada hakupenda. Aliona kazi na faraju zitendwazo na wanawake katika maisha zilitosha kuwa mzigo mzito juu yao…..”
Hivyo mwandishi anaonesha jinsi mwanamke anavyofanya mambo makubwa katika jamii, hivyo anapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa.
Pia mwanamke amechorwa kama mtu mvumilivu, mwandishi Shaaban Robert amemuonesha mwanamke kama mtu mwenye kuvumilia matatizo mbalimbali yanayomkabili. Malkia licha ya kukumbwa na tatizo la kukosa mtoto hakuvunjika moyo aliendeleza upendo wake kwa mfalme mpaka pale mungu alipowajalia kupata mtoto.
Dhamira nyingine ni dharau na majivuno, dhamira hii imejitokeza pale ambapo mhusika Mfanyabiashara alipokuwa gerezani alikuwa anamdharau utu busara. Kutokana na kazi aliyokuwanayo mfanyabiashara alijiona kuwa ni bora kuliko mkulima( uk 40)
………….Huwaje, wewe mvaa koja la ushanga shingoni kama mwanamke kupata njia! Una sifa zaidi ya ujinga. Nashangaa kwanini hawakutakiwa wajinga wawili kwa kafara hii! Ujinga ni ila ya kustahili upanga wa chakali.
Umuhimu wa elimu ni dhamira nyingine ambayo mwandishi Shaaban Robert ameijadili katika kazi yake. Mwandishi anaonesha kuwa watu wa Kufikirika walikuwa hawana elimu ya dunia walijiegemeza zaidi katika mambo ya uganga, hivyo utu busara alijaribu kuleta mabadiliko katika nchi ya kufikirika kwa kuwapatia elimu ya dunia ambayo baadae ilisaidia kuikomboa nchi ya kufikirika.
Pia dhamira nyingine ni matumizi mabaya ya mali, kutokana na mfalme kukosa mtoto, waganga walitumia sehemu kubwa ya mali ya nchi ya kufikirika hadi ikapelekea matatizo katika nchi ya kufikirika( uk 14)
Nchi ambayo zamani ilikuwa ya shibe, utajili, nguo, tafrija na neema zote sasa ilikuwa imegeuka nchi ya njaa, umaskini, uchi, uzito na uhitaji wa kila namna ulikuwa mbele ya watu………
Kipengele kingine ni ujumbe. katika riwaya ya kufikirika kupitia dhamira mbalimbali zimeweza kutuibulia ujumbe ufuatao.
· Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Mfano wananchi wa kufikirika walikuwa na umoja katika kufanikisha ustawi wa nchi yao hali kadhalika watu wa kufikirika walikuwa na umoja na ushirikiano katika kufanikisha mfalme wao anapata mtoto.
· Kwenye upendo, umoja na ushirikiano hakuna vurugu na matatizo mbalimbali.ustawi wa nchi ya Kufikirika umetokana na umoja na ushirikiano waliokuwa nao.
· Jamii isijiegemeze katika imani za kimila na kitamaduni tu bali iangalie upande mwingine. Hii inatokana na ukweli kwamba wanakufikirika walikuwa hawaamini masuala ya hospitali badala yake walikuwa wanaamini mambo ya kimila na kitamaduni.
· Ujinga na werevu wa mtu hupimwa kwa matendo na sio kazi anayoifanya. Hii inatokana na watu wa kufikirika ambayo walikuwa wanapima werevu na ujinga wa mtu kutokana na kazi zao.
· Ujumbe mwingine ni kwamba viongozi lazima wadumishe sheria za nchi ili kuleta usawa na amani katika nchi.
Hivyo Shaaban Robert anaitaka jamii ibadilike kwa kuzingatia maonyo na maadili yapatikanayo katika riwaya ya kufikirika.
Kipengele kingine ni migogoro, mgogoro ni mvutano kati ya pande mbili au zaidi.mwandishi Shaaban Robert katika riwaya hii ya kufikirika ameonyesha migogoro mbalimbali kama vile mgogoro wa kiuchumi,kijamii,kisiasa,utamaduni na mgogoro wa nafsi.
Tukianza na mgogoro wa kiuchumi, Mwandishi ameonyesha jinsi nchi ya kufikirika ilvyoyumba kiuchumi kutokana na mali zote za nchi zilivyotumika katika kumtibu mfalme na malkia na mwishowe shughuli za nchi zilisimama.uk (8-12).
Pia kuna mgogoro wa kijamii, mwandishi ameonyesha mgogoro wa mfalme na malkia kwa kukosa mtoto,kwakua walijiona hawana umuhimu katika jamii ingawa walikua na mali nyingi. Uk(1-6).
Pia mgogoro mwingine wa kijamii ni kati ya mfalme na waganga kwamba makundi matano ya waganga waliokusudiwa kumtibu mfalme na malkia walishindwa kuwatibu.uk(8-13).
Mgogoro mwingine wa kijamii ni kati ya mfalme na waliotakiwa kutolewa kafara,kwamba katika nchi ya kufikirika suala la mtu kutolewa kafara ni suala ambalo haliendani na sheria za nchi ya kufikirika.
Vilevile kuna mgogoro wa nafsi uliojitokeza kwa mfalme,jinsi mfalme alivyokua akiumia juu ya kukosa mtoto kwa muda mrefu takribani miaka kumi baada kuoana na malkia.
Pia malkia alikua na mgogoro na nafsi yake juu ya kukosa mtoto kwa muda mrefu tangu kuoana kwao.
Hali kadhalika kuna mgogoro kati ya waziri mkuu na wajumbe juu ya kubadili mfumo wa uongozi.
Pia kuna mgogoro kati ya ukale na usasa,kwamba wananchi wa kufikirika waliamini sana mambo ya kishirikina wakati Utubusara alikua akijaribu kuwaelimisha juu ya mambo ya sayansi na teknolojia na waachane na mambo ya zamani.
Pia kuna mgogoro wa kisiasa, mwandishi ameonyesha jinsi mfalme alivyokua ameegemea kuongoza nchi yake kupitia mila na desturi, lakini tunaona jinsi Utubusara alivyokua akijaribu kuishauri jamii ya kufikirika kuepukana na mila zilizopitwa na wakati na waegemee katika sayansi na teknolojia ili waweze kuleta mabadiliko.
Falsafa, kiujumla falsafa ni mchujo wa welekeo wa mawazo muhimu yajitokezayo kila mara katika kazi mbalimbali za msanii ( Senkoro 2011). Katika kazi hii shabaan Robert anaonekana kutawaliwa na falsafa kuwa mila na tamaduni zilizopitwa na wakati hazina nafasi katika nkipindi hiki cha sayansi na teknolojia.
Msimamo, msimamo ndio uwezao kuwatofautisha wasanii wawili wanaotunga kazi za fasihi zilizo na kiini na chimbuko moja ( senkoro 2011). Katika kazi hii mwandishi shaaban Robert anaonekana kuwa na msimamo wa kiyakinifu. Kwa mujibu wa mwandishi anaona katika kipindi cha sayansi na teknolojia mila na tamaduni za zamani zisipewe nafasi.
Mtazamo, mwandishi shaaban robert anaonekana kuwa na mtazamo wa kimapinduzi, mwandishi anaona kuwa ili jamii isiangalie mila na tamaduni tu bali iangalie mambo ya sayansi na teknolojia.
Baada ya kuchambua vipengele vya maudhui sasa tugeukie vipengele vya kifani.kiujumla fani katika fasihi ni ule ufundi wa kisanaa anaotumia msanii katika kazi yake(Senkoro 2011). Katika kuchambua vipengele vya fani tutajikita katika muundo, mtindo, wahusika, mandhari na matumizi ya lugha.
Wahusika, hawa ni watu, ama viumbe, waliokusudiwa wawakilishe dhana, mawazo au tabia za watu, katika kazi za fasihi. Katika riwaya ya kufikirika mwandishi Shaaban Robert amepambanisha wahusika mbalimbali katika kuibua au kusindikiza dhamira zake. Baadhi ya wahusika aliowatumia ni kama wafuatao
Mfalme, huyu alikuwa ndiye kiongozi au mfalme wa nchi ya kufikirika ambaye aliongoza vema na alikuwa mtu mwenye huruma na upendo na watu wake. Hali kadhalika mfalme alikuwa ni jasiri na mzalendo aliyepigania haki za raia wake na kuzilinda sheria za nchi ya kufikirika. Licha ya mali na furaha yote aliyonayo mfalme lakini kwa kipindi kirefu cha maisha yake mfalme amekuwa akisumbuliwa na tatizo la kukosa mtoto. Kupitia uhusika alioubeba mfalme ameibua dhamira mbalimbali kama vile suala la uongozi, ujasiri na uzalendo, umuhimu wa kuwajali wanawake na imani potofu.
Malkia, huyu alikuwa ni mke wa mfalme ambaye pia alikuwa anasumbuliwa na tatizo la utasa. Ni mwanamke mvumilivu na mwenye subira hivyo anafaa kuigwa na jamii. Mwandishi kwa kumtumia mhusika malkia ameibua dhana ya utasa na uvumilivu.
Utu busara ujinga hasara, ni mhusika aliyeibua dhamira nyingi katika riwaya hii ya kufikirika, alikuwa ni mtu makini na mwenye upeo mkubwa katika kufikiria mambo. Huyu ndiye aliyetabiri kuzaliwa kwa mtoto wa mfalme, baadae akawa mwalimu wa mtoto wa mfalme na baadae akajiingiza katika ukulima( uk 49). Hekima na uelewa aliokuwa nao ulikuwa ngao tosha iliyomsaidia kujikomboa kutoka katika vikwazo vyote alivyokumbana navyo, hakika ni mtu anayefaa kuigwa katika jamii.
Mwerevu, huyu alikuwa ni mfanyabiashara ambaye alionekana ni mwerevu kutokana na kazi yake. Ama hakika ni mtu aliyajaa dharau na majivuno( uk 40) anasema,
………….Huwaje, wewe mvaa koja la ushanga shingoni kama mwanamke kupata njia! Una sifa zaidi ya ujinga. Nashangaa kwanini hawakutakiwa wajinga wawili kwa kafara hii! Ujinga ni ila ya kustahili upanga wa chakali.
Kwa hakika utu busara alileta mwanga katika nchi ya kufikirika juu ya imani na tamaduni zilizopitwa na wakati.
Waziri mkuu, huyu uwakilisha viongozi wanaopindisha sheria kwa manufaa ya watu wachache. Mwandishi anamchora mhusika huyu kama mtu ambaye aliyetumia vitisho na nguvu katika kushawishi wajumbe kukubaliana na ubadilishaji wa sheria. Hakika hafai kuigwa na jamii hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko.
Muundo, Katika kazi ya fasihi muundo ni mpango na mtiririko wa kazi hiyo kwa upande wa visa na matukio( Senkoro 2011). Hivyo katika riwaya hii ya Kufikirika mwandishi Shaaban Robert ametumia muundo wa moja kwa moja ambapo amesimulia kitabu mwanzo hadi mwisho. Katika kuipamba kazi yake mwandishi Shaaban Robert ameigawa riwaya yake katika sehemu ndogondogo , Kila sura ina kichwa cha habari. Sura hizo ni kama vile Mfalme, Waganga, Matokeo ya utabiri, Mtoto wa mfalme na Kafara. Pia sura ya tano ameigawa katika sehemu kuu mbili na kuipa jina la Baraza na Gereza.
Mtindo, katika kazi ya fasihi ni ile nama mbayo msanii hutunga kazi hiyo na huipa sura ambayo kifani na kimaudhui huainisha kanuni au kawaida zilizofuatwa kama ni zilizopo( za kimapokeo) au ni za kipekee( senkoro 2011). Mwandishi shaaban Robert katika kazi yake hii ametumia mtindo wa masimulizi yaani amesimulia matukio yote katika mtiririko unaofaa.pia nafsi zote zimetumika, hali kadhalika katika kuipamba kazi yake mwandishi ametumia ushairi ( uk 18-19) anasema.
Jina lipewe wana
Kulikariri kwa moyo
Waelezewe maana
Wakuze wayatendayo
Kama milivyoona
Matendo ya mtu huyo
Katenda bora sana
Kwa tuzo apewayo
Pia katika riwaya hii, mwandishi ametumia mtindo wa kutoa maana ya meneno magumu mwishoni ili kufanya kazi yake ieleweke kwa urahisi.
Mandhari. Mandhari ni mahali au sehemu ambayo kazi ya fasihi inatendeka. Katika riwaya ya kufikirika mwandishi shabani robert ametumia mandhari ya Kufikirika, kwani hata nchi inayozungumziwa ni ya Kufikirika, pia nchi zilizopakana na nchi ya Kufikirika nazo ni za kufikirika. Pia mwandishi ametumia muktadha halisi kama vile Gerezani, Nyumbani kwa Mfalme, Bustanini ( uk 1) na Shambani. Kupitia mandhari hizi mwandishi Shabani Robert ameibua dhamira mbalimbali ambazo tumejadili hapo awali.
Matumizi ya lugha, hujumuisha jinsi mtunzi alivyotumia lugha katika kuwasilisha kazi yake. Matumizi ya lugha hujumuisha misemo, nahau, methali na tamathali za semi.
Methali, methali zilizotumika katika riwaya hii ni kama vile, nyumba ya mgumba haina matanga (uk 5),mwenye haya hazai (uk 6),
Misemo, katika riwaya ya kufikirika misemo iliyotumika ni kama ifuatayo. Dunia haifichi siri (uk 23), maisha ni kama kuwa katika bahari ( uk 24).
Tamathali za semi, haya ni maneno ambayo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo na hata sauti katika maandishi au kusema. Pia tamathali za semi hutumika ili kupamba lugha au mazungumzo. Katika riwaya ya kufikirika mwandishi Shaaban Robert ametumia tamathali mbalimbali kama ifuatavyo:
Tashibiha, katika tamathali hii watu ama vitu viwili au zaidi hulinganishwa na watu ama vitu vingine kwa kutumia maneno kama mithili, kama, n.k, katika riwaya hii tahibiha zilizojitokeza ni kama vile kichwa chake kilishindiliwa kama gunia (uk 29),sauti ya waafrika ni kali kama ile ya radi ( uk 6)waliweza kunusa kama mbwa mwitu( uk 8), akili yake kali kama wembe ( uk 38), maswali aliyamimina kama maji ( uk 29), mtu mdogo kama mbilikimo (uk 41)
Tashihisi, katika aina hii vitu visivyo na sifa walizonazo watu hupewa sifa hizo. Katika riwaya hii mwandishi Shaaban Robert anabainisha tashihisi zifuatazo,sauti ya ndege waliokuwa wakiimba matawini kwa kuagana na mchana ilikuwa na simanzi masikioni (uk 1)
Sitiari, hii ni tamathali ambayo hulinganisha vitu bila kutumia viunganishi, mwandishi wa riwaya hii ametumia sitiari zifuatazo, mjinga ni mnyama ( uk 41), wanawake ni malaika( uk 40).
Mubalagha, ni tamathali ya semi ambayo hutia chumvi au hukuza jambo. Katika riwaya ya Kufikirika mwandishi ametumia mbinu hii katika( uk 11) siku hiyo kuni, mkaa, na mafuta yote yalikwisha kwa kuchoma hirizi hizo, moshi mwingi uliruka juu ukatanda katika hewa kama wingu kubwa la mvua.
Jinala kitabu, Jina lakitabu kufikirika linasadifu yaliyomo .Kwanza nchi yenyewe ya kufikirika ni nchi ambayo haipo,mwandishi anaonyesha kwamba hata mfalme mwenyewe haijui mipaka ya nchi yake.Hata nchi zinazopakana nazo ni nchi za kufikirika tu.Nchi kama Anasa,Majaribu,Bahari ya kufaulu na safu ya milima ya Jitihada vyote ni vya kufikirika tu.
Kwa upande wa maudhui, mambo ya kafara ni ya kufikirika tu,kwani mambo hayo katika jamii zetu hayapo.Matibabu mengi siku hizi hufanywa hospitalini,ambako kuna wataalamu waliosomea taaluma hii ya uganga na sio miti shamba kama wananchi wa kufikirika.
Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kuwa mwandishi shaaban robert kwa kiasi kikubwa ameonesha matatizo mbalimbali yanayoikumba jamii na kuyatolewa ufumbuzi.
Marejeo
Robert, S (1991) Kufikirika.Dar es salaam. Mkuki na nyota publishers.
Senkoro, F.E.M.K (2011) Fasihi. Dar es salaam. KAUTTU.