MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
JIFUNZE KISWAHILI - DHANA YA LAFUDHI

JIFUNZE KISWAHILI

Full Version: DHANA YA LAFUDHI
You're currently viewing a stripped down version of our content. View the full version with proper formatting.
DHANA YA LAFUDHI
Kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili sanifu (Toleo la pili 2004-2005) inaeleza kuwa lafudhi ni matamshi ya mzungumzaji yanayotokana na lugha yake ya mwanzo au lugha zinazomzunguka, au ni udhihirishaji wa sauti za lugha unaomtambulisha mtu mmoja au jamii ya watu.
Massamba na wenzake (2009) SAMAKISA, wanasema kuwa lafudhi ni matamshi ya msemaji wa lugha fulani ambayo yanayotokana na athari za kimazingira.Mazingira hayo yanaweza kuwa eneo atokalo mtu, mahali aliposomea, kiwango chake cha elimu na tabaka lake la jamii.
          Kimsingi tunaweza kuhitimisha kwa kusema kuwa lafudhi ni sifa ya masikizi ambayo humtambulisha mzungumzaji na jiografia yake, uzungumzaji huo huwatofautisha wazungumzaji wa lugha moja katika jamii au mazingira fulani.
Kwa mujibu wa wavuti wa www.shuledirect.co.tz/notes/views/195 wanadai kuwa lugha ya Kiswahili ni lugha ya pili kwa watumiaji wengi wa Afrika Mashariki kwa hiyo hii inafanya kuwatambua wazungumzaji wa Kiswahili kulingana na makabila yao au maeneo wanakotoka. Kwa mfano hapa Tanzania tunaweza kuwatambua watu wa Mwanza kwa lafudhi yao, pia watu wa Mtwara kwa lafudhi yao.
Kwa mfano;
  1. Usiniretee maswara ya ubaguzi wa kikabira hapa. (Wakurya).
  2. Ukikaa nchale, ukisimama nchale. (Wamakonde).
  3. Wewe unakamuaga mang’ombe tu. (Wasukuma).
  4. Mbona unakuwa kinganganizi, nilishakwambia sikupendi lakini wewe bado unaningangania tu. (Wahaya).
Katika mifano tajwa hapo juu kuanzia mfano wa kwanza mpaka wanne tunaona makosa yanayojitokeza katika baadhi ya tungo wanazozitumia. Kwa mfano katika mfano wa (a) tunaona namna jamii ya Wakurya inavyotumia herufi “r” badala ya “l”, vilevile katika mfano wa pili (b) tunaona namna jamii ya Wamakonde wanavyotumia herufi “n” na “ch” badala ya “m”na “sh”.
          Katika mfano wa tatu © tunaona namna jamii ya Wasukuma wanavyoongeza vitamkwa katika baadhi yamaneno, kwa mfano katika mfano wameongeza vitamkwa “ma” katika neno “ng’ombe” na kitamkwa “ga” katika neno “unakamua”. Pia katika mfano (d) tunaona jinsi jamii ya Wahaya wanavyoshindwa kutamka herufi (ng’) katika tungo zao.
          Lafudhi pia inaweza kujitokeza katika mazingira mbalimbali kama vile;
  1. Kushindwa kutamka baadhi ya herufi au vitamkwa.
  2. kwa mfano kabila la Wanyakyusa hushindwa kutamka herufi “v” na badala yake hutumia herufi “fy” katika tungo zao.
Kwa mfano; fyatu fyimechanika badala ya viatu vimechanika.
Pia Wanyakyusa hutamka “s” badala ya “z”, kwa mfano, mapindusi badala ya mapinduzi, vilevile hutamka herufi “ky” badala ya “ch” kwa mfano, kyiama kya mapindusi badala ya chama cha mapinduzi.
  1. Kabila la wapare hushindwa kutamka herufi “s” na badala yake hutamka herufi “th”. Kwa mfano, Thithi thote ni ndugu badala ya Sisi sote ni ndugu. Wapare pia hushindwa kutamka herufi “z” na badala yake hutamka “dh”. Kwa mfano, Nguo dhao dhote dhimeibiwa badala ya Nguo zao zote zimeibiwa.
  2. Kabila la Waha hushindwa kutamka herufi “n” hasa katika neno kama vile “nne”. Kwa mfano, Mwanafunzi amejibu maswali maine badala ya Mwanafunzi amejibu maswali manne.
  3. Lafudhi inayojitokeza katika mazingira ya kuongeza vitamkwa, kwa mfano,
  4. Katika kabila la Wasukuma hupenda kuongeza vitamkwa “ma” na “ga” katika baadhi ya maneno. Kwa mfano, Mang’ombe mengi badala ya Ng’ombe wengi, Watoto wanapendaga kula badala ya Watoto wanapenda kula.
  • Lafudhi inayojitokeza katika mazingira ya kupoteza au kudondosha baadhi ya vitamkwa. Kwa mfano katika kabila la Wachaga baadhi ya vitamkwa hudondoshwa wakati wa utamkaji wa baadhi ya maneno, kwa mfano Wachaga hudondosha kitamkwa “h” katika neno “hela” na “y” katika neno “yangu”. Kwa mfano, Mangi nipe ela angu aise!
  • Hali ya kupanda na kushuka kwa sauti, lafudhi pia huweza kujitokeza katika mazingira ya kupanda na kushuka kwa sauti hasa kwa wazungumzaji wageni wa lugha ya Kiswahili.
Kwa mfano, Habari zenu
                     Hamjambo wote
Hivyo basi pamoja na kuwa lafudhi inamtambulisha mzungumzaji fulani kuwa anatoka wapi (asili yake), lakini pia lafudhi huweza kuvuruga utaratibu wa lugha sanifu ambapo tunaona kuwa lafudhi inaweza kupoteza maana ya baadhi ya maneno kwa wazungumzaji wa lugha moja, kwa mfano neno “kura” na “kula” pia “mahali” na “mahari” ni maneno ambayo huweza kuleta utata hasa pale yanapotamkwa na jamii ya Wakurya.
MAREJEO
Crystal D, (2003) A Dictionary of Linguistics and Phonetics: Blackwell.
 Shengli F, (2003) A prosodic grammar of Chinese: University of Kansas.
Kihore Y.M na wenzake (2003) Sarufi maumbo ya Kiswahili sanifu sekondari na vyuo: Dar-es-Salaam
Kamusi ya Kiswahili sanifu (Toleo la pili 2004-2005). Dar es Salaam Tanzania
Massamba na wenzake (2004) Fonolojia ya Kiswahili sanifu (FOKISA) Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili Dar es Salaam Tz
Massamba na wenzake (2009) SARUFI MAUMBO YA KISWAHILI SANIFU (SAMAKISA) Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili: Dar es Salaam Tz
Samwel M. (2009) Kozi tangulizi ya fonolojia na sintaksia ya kiswahili: (DUCE) Dar es Salaam