MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
JIFUNZE KISWAHILI - MIAKA 30 YA UJERUMANI KUFUNDISHA KISWAHILI

JIFUNZE KISWAHILI

Full Version: MIAKA 30 YA UJERUMANI KUFUNDISHA KISWAHILI
You're currently viewing a stripped down version of our content. View the full version with proper formatting.
MBALAMWEZI YA KISWAHILI: Miaka 130 ya Ujerumani kufundisha Kiswahili

Kwa ufupi
  • Mtazamo wa wengi wetu umejikita katika kuvibeza vilivyo vyetu na kuvitukuza vya wenzetu.
Na. Erasto Duwe
Hivi karibuni Profesa Clarisa Vierke wa kutoka Chuo Kikuu cha Bayreuth, Ujerumani aliyeshiriki katika Kongamano la Chama cha Kiswahili cha Afrika Mashariki lililofanyika jijini Dar es Salaam, aliwashtua wengi alipopewa nafasi ya kutoa neno katika kongamano hilo.
Akiongea kwa Kiswahili, katika maelezo yake alisema kwamba mwaka 2017 Chuo Kikuu cha Bayreuth, kinataraji kusherehekea miaka 130 ya ufundishaji wa Kiswahili.
Kauli hiyo ya kusherekea miaka 130 ya ufundishji wa Kiswahili Ujerumani na umahiri wa profesa huyo katika kutumia Kiswahili, vilionekana kuibua picha ya aina yake akilini mwa baadhi ya washiriki.
Mbalamwezi ya Kiswahili ilisikia sauti za minong’ono kutoka kwa washiriki waliokuwa wameketi karibu, “Daa aise, kumbe Kiswahili si mchezo! Miaka 130 …Kiswahili… Ujerumani!…” Jambo hilo lilionekana geni kwa wahusika hao.
 Yumkini kauli hizo za kuonyesha mshangao uliochanganyika na furaha ya aina yake, zilitolewa kutokana na mazoea na mitazamo ya baadhi ya Waswahili wazawa ambao hukichukulia Kiswahili katika mtazamo dufu badala yake huzishadidia zaidi lugha za kigeni.
Profesa Vierke aliendelea kusema, “Lugha ni ufunguo wa utamaduni. Ajuaye lugha ni tajiri. Tukuze Kiswahili na kukisherehekea… Kuna wazungumzaji wengi zaidi wa Kiswahili duniani ukilinganisha na wazungumzaji wa Kijerumani…
‘‘Tutambue pia kuwa kila lugha ni bora kwa watumiaji wake. Lakini pia tusisahau kwamba aliye na lugha moja ni maskini…”  Kwa ujumbe huu wa Profesa Vierke tunayo mengi ya kujifunza na kuyafanyia tafakuri.
Mintarafu ufundishwaji wa Kiswahili duniani, vipo vyuo vikuu vingi vinavyofundisha Kiswahili. Katika vyuo hivyo kuna idara na taasisi za masomo ya Kiafrika kama ilivyo katika Chuo Kikuu cha Bayreuth ambako Profesa Vierke ni mhadhiri. Miongoni mwa masomo hayo ya Kiafrika ni somo la Kiswahili ambacho kitovu chake ni Afrika Mashariki.
Mtazamo wa wengi wetu umejikita katika kuvibeza vilivyo vyetu na kuvitukuza vya wenzetu. Ni kinyume cha mambo, wenzetu kila jambo hulipa umuhimu, huvienzi vyao na kuvishikilia vya wengine kwa kuangalia umuhimu ya thamani yake.
Nchini Ujerumani pekee, vipo vyuo vingi vifundishavyo Kiswahili. Miongoni mwa hivyo ni Chuo Kikuu cha Kolon, Leipzig, Bayreuth, Humbolt, Berlin na Hamburg. Kwa nini vyuo vikuu vyote hivyo? Ni kutokana na dhima na thamani waionayo katika lugha hii adhimu ya Kiswahili.
Sherehe hiyo ya maadhimisho ya miaka 130 ya ufundishaji wa Kiswahili ni ya Ujerumani nzima. Tunaweza kujiuliza walianza lini kufundisha Kiswahili hata washerehekee miaka yote hiyo?
Tukiirejelea historia ya Kiswahili na wageni waliopata kukita guu nchini mwetu, yaani wamisionari, wakoloni na wafanyabiashara, tutapata majibu.
 Kiswahili kilianza kufundishwa huko Ujerumani katika karne ya 19 kwa ajili ya kuwaandaa wale ambao walipaswa kuja kufanya kazi nchini Tanganyika. Kituo kikuu cha ufundishaji wa Kiswahili kwa wakati huo kilikuwa  katika mji ujulikanao kwa jina la Kolon.
Ikiwa wenzetu wanakienzi Kiswahili kwa namna hiyo kiasi cha baadhi yetu kuwashangaa, basi sisi wenye lugha tunawiwa mengi na lugha hii. Tunapaswa kufanya hivyo maradufu, kwa kuwa Kiswahili ni lugha yetu na ndiyo ufunguo wa utamaduni wetu.
Mbalamwezi ya Kiswahili, katu haipingi watu kujifunza lugha nyingine na chambilecho Profesa Virke, kujua lugha nyingi ni utajiri. Kinachosisitizwa na makala haya ni mtu kukipenda na kukithamini kilicho chake.
Kiswahili ni chetu Watanzania, kabla ya kuthamini wa nje ya mipaka ya nchi, tuanze sisi kukithamini.