MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
JIFUNZE KISWAHILI - MAISHA YA SHAABAN ROBERT NA MAWAZO YAKE (M.A. Maganga) – 1

JIFUNZE KISWAHILI

Full Version: MAISHA YA SHAABAN ROBERT NA MAWAZO YAKE (M.A. Maganga) – 1
You're currently viewing a stripped down version of our content. View the full version with proper formatting.
[Image: shaabanrobert.jpg]
Makala haya yamegawika sehemu
mbili. Sehemu ya kwanza inachungua mawazo ya Shaaban Robert aliyoyatoa katika
vitabu vyake viwili: Adili na Nduguze
na Wasifu wa Siti Binti Saad. Sehemu ya
pili yatumia mawazo hayo kupimia vitendo na maisha ya Shaaban kama
alivyotueleza yeye mwenyewe katika vitabu viwili vingine vilivyokusanywa
pamoja: Maisha Yangu na Baada ya Miaka
Hamsini.
Nionavyo mimi, Shaaban Robert
amechukua nafasi ya kuandika vitabu vyake hivi viwili vya mwanzo ili aweze
kutoa mawazo na maoni yake kuhusu mambo mabaya na mazuri, yapi ya kufuata na
yapi ya kuepuka katika dunia yenye maisha mbalimbali. Baada ya kuvisoma vitabu
hivyo kwa makini, nimekatikiwa kuwa Shaaban alikuwa na mawazo yasiyo tafauti na
siasa ya Ujamaa na Kujitegemea. Amefikiria kuishi kwa ujamaa katika kitabu
chake cha Adili na Nduguze na katika Wasifu wa Siti Binti Saad ametoa mawazo
yake kuhusu maisha ya kujitegemea; na bila shaka ana lengo halisi katika kutoa
mawazo hayo. Pengine alipenda kueleza na kufafanua, au kupanua zaidi, yasemwayo
katika Injili Takatifu, yaani ‘umpende jirani yako kama nafsi yako’, na mapenzi
hayo ndiyo msingi wa wema, matendo safi, na juhudi ya kazi ziletazo faida kwa
watu wote.
Kwa kuwa vitabu viwili hivi
vimetumiwa kama vyombo vya kuelezea aina mbili za mawazo na maoni ya mtungaji,
naona ni vema nisivichanganye katika uchambuzi huu bali nivichukue kimoja
kimoja. Ebu nianze na kile kilichotangulia kutoka. Kimoja kilitoka mara ya
kwanza katika jarida la 1958 (Nambari 28/1) la Kamati ya Kiswahili ya Afrika
Mashariki, na kingine kilitoka mara ya kwanza kama kitabu kamili mnamo 1952,
nacho ni Adili na Ndiguze ambacho
ndicho tutakachoanzia.
Nimesema kwamba mawazo ya Shaaban
Robert yana lengo au kiini fulani. Katika Adili
na Nduguze lengo lake ni upendo, yaani watu wapendane na kuishi kiujamaa-na
upendo huo ndio alioufungulia kitabu chenyewe alipoandika mwanzoni:
‘Kwa marafiki zangu
Wazawa wa Afrika
Pamoja na Wazungu
Wapendao afrika’.
Shaaban Robert amekianza kitabu
chake kwa maelezo juu ya Mfalme Rai. Mawazo yenyewe, nionavyo mimi, ni sawa nay
ale yasemwayo na Azimio la Arusha kwamba, ili kuleta mafanikio na maendeleo ya
nchi, vihitajiwavyo ni ardhi, watu, uongozi bora na siasa safi.
Kiini cha kumuanzia Rain i kutaka
kueleza kwamba, hata kama ardhi na watu wapo, jambo la kwanza linalotakiwa ni
uongozi bora wenye msingi ufananao na tabia ya Rai. Pengine ardhi na watu wa
Ughaibuni walifanikiwa na kuendelea kwa sababu ya uongozi mzuri wa Rai. Mawazo ya
Shaaban ni kuwa uongozi mzuri wa nchi ni kama ule wa Rai ambao kiini chake
kilikuwa upendo. Alikuwa na mapenzi na wanaadamu, nao wakampenda;alifuata
msingi wa kidini wa zamani ambapo Daudi aliwapenda wanyama na Sulemani akatiiwa
na majini.
Mawazo ya Shaaban juu ya kiongozi
bora wa nchi yoyote yameelezwa katika wasifu wa Rai, ukurasa wa pili. Hapo uongozi
bora unaonekana unahitajia uadilifu, wema, kufanya kazi ndogo na kubwa au kutoa
amri zifanywe, kusaidia na kushiriki katika maendeleo ya nchi, kutolazimisha
watu mambo bali kuwashawishi tu (kama uhitajivyo ujamaa wa kweli), kuvuta mioyo
ya watu ili kusiwe na wavivu, magoigoi wala waoga.
Kwa namna hii Shaaban Robert atoa
mawazo kwamba viumbe wote wangefurahia sifa ya kiongozi wa namna hiyo-tangu
malaika mbinguni hadi ndege angani, watu duniani, samaki majini, na hata majini
na mashetani popote pale wafikiriwapo wapo. Upendo na ujamaa wa kweli ni
kufanya urafiki na viumbe mbalimbali pamoja na kuwajali watu wote. Baada ya
upendo ni matendo. Na hapa ndipo Shaaban aliposema: ‘Tendo hukidhi haja
maridhawa kuliko neno.’ Yaani, tendo huleta haja upesi lakini neno huichelesha;
na neno tu si njia ya kuleta mapinduzi kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
Katika kuhukumu mwandishi
aonekane ana machache ya kueleza. Itolewapo hukumu inatakikana kiongozi awe
imara, asipendelee bali watu wote wawe sawa mbele ya sheria. Hiyo ndiyo
demokrasi halisi-demokrasia ya kiujamaa. Uongozi bora ni ule ufuatao haki ya
watu na wanyama pia, na ule ufanyao uchunguzi wa matukio yote-mazuri na
mabaya-kwa raia. Na, katika uchunguzi wa Rai kuhusu kasoro iliyotokea Janibu,
ndimo Shaaban Robert anamoeleza mawazo yake kuhusu tabaka kwa tabaka za maisha
ya kiujamaa nay ale yasiyo ya kiujamaa. Na juu ya huo uchunguzi Shaaban
anasema, ‘Mambo katika maisha yambo katika mwnedo huu siku zote. Hayajulikani mpaka
yamechunguzwa na kuthibitishwa kwanza.’ Kiongozi bora kama Rai huwa mtu arifu
wa mwendo huu!
Tunaambiwa vile vile kuwa si
kiongozi tu atakikanaye kuwa mtu wa kufaa bali watu wote walio na wajibu na
mamlaka chini yake, kama vile Rai alivyokuwa na Maarifa (Waziri Mkuu) na
Ikibali (Mshauri). Na kazi lazima ipokezanwe kwani kiongozi hawezi kufanya kazi
zote peke yake. Juu ya Ikibali, ambaye alikuwa na wajibu wa kwenda Janibu
kuchungua mambo ya kodi, tunayaona mawazo mengi ya mwandishi kuhusu njia nzuri
ya mtu kuiweza kazi yake kwa urahisi. Zaidi ya kuwa na maarifa mengi, kuchuana
na watu kwahitaji tabia njema ambayo
ndiyo inayomkamilisha mtu. Tabia njema kwa viongozi wa nchi ndiyo alama ya ‘jembe’
au ‘nyumba’ ambayo Shaaban anataka watu waiangalie wanapoteua viongozi wao, na
ndiyo sifa inayowapa watu kuwaamini na kuwapenda.
Sura ya kwanza ni fupi; lakini
mwandishi ameitumia kutolea mawazo mengi kuhusu uongozi bora wa watu na utumiaji
bora wa ardhi, kuhusu raia, serikali, mawaziri, siasa safi na mifano bora ya
viongozi. Sehemu yote iliyosalia-na ni kubwa-anaitumia kutolea mawazo yake
kuhusu umma na jinsi ya kuishi kwa mapenzi na ujamaa. Na sura zote kumi na nne
zifuatazo, hadi kufikia mwisho, ni maoni juu ya ‘machimbo na hazina zake’, ‘biashara
na faida yake’, ‘safari na manufaa yake’, ‘utajiri na Baraka yake’, ‘hali na
heshima yake’ na juu ya ndugu, watu, jamaa na matendo yao-mambo yahsuyo dunia
nzima. Kwanza kabisa amekwisha kutoa maoni yake kuhusu ardhi na mimea yake na
mifugo na mazao yake, kwamba ni hazina za urithi wa watu wote. Hebu basi
tuangalie ni nini awazacho mtungaji huyu juu ya ujamaa na upendo kati ya watu.
Katika sura ya pili, mwandishi
anatoa maoni yake kuhusu mgeni Ikibali aliyekuwa na hulka ya kuwapendeza watu
waliokutana naye na ambaye usoni aling’aa kwa kicheko; na aliyekuwa na fadhila
na shukrani. Katika kwenda kwake Janibu, Ikibali anakutana na Adili, Liwali wa
mji huo ambaye mtungaji anamtumia kuelezea mawazo yake kuhusu namna nzuri na
mbaya ya kuishi na ndugu na watu mbalimbali. Ikibali alipotaka kurudi
Ughaibuni, Adili alimwomba akae Janibu kwa muda wa siku tatu zaidi ili wazidi
kutafaraji pamoja. Ikibali akakubali, kwani ‘waungwana hawanyimani neno’. Kwa hiyo
tunaona vile vile kuwa penye upendo pana kujitolea na subira pia.
Twafahamu kwamba subira mara
nyingi huvuta heri, basi Ikibali naye katika kusubiri kwake alivuna heri-na heri
yenyewe ilikuwa ni kule kuona kuwa kuna kitu fulani kibaya ambacho ilimlazimu
Adili kukitenda bila furaha. Juu ya habari hii ya Adili, Shaaban
anatutanabahisha tusimchukulie mtu kwa hali yake ya nje tu, tukafikiri yakuwa
mtu kama Adili-Liwali mzima-ati hana jambo linalomuondolea furaha. Mtu kama
huyo, tunapogundua ana tatizo, inafaa tumsaidie-si katika mambo ya kikazi tu
bali hata mambo yake mwenyewe binafsi. Hii ndiyo sababu Ikibali akaazimia
kumsaidia mwenziwe ingawa hilo jambo la kusaidiwa lilikuwa ni la siri: siri ambayo
ilibidi ifichuliwe ili msaada upatikane. Ndipo Ikibali akaitoboa siri hiyo, ya
Adili na manyani wake, na baadaye akenda naye mbele ya Rai, si kwa ajili ya
kumuaibisha bali kumfanya Rai ayasikilize maelezo ambayo huenda yakawa ndio
ufunguo wa furaha. ‘Aonae kosa akitoa hana lawama’, ndivyo asemavyo mwandishi. Na
kusaidiana ni dalili ya upendo nan i ujamaa.
Katika sura ya tatu, mawazo ya
mwandishi ni kuwa vitendo ni mapinduzi. Tunaambiwa kwamba busara nyingi humjia
mtu baada ya jambo kufanyika. Hivyo, Adili hakumkasirikia Ikibali kwa kumtolea
siri yake kwa Rai. Inaonekana kwamba wazo la mtungaji ni kusema kuwa itukiapo
ajabu, au jambo la kushangaza, huenda kukawa na sababu maalumu na kwamba, jambo
lenyewe likichunguzwa, huenda sababu yenyewe ikaonekana. Ajabu ya wale manyani
waliopanda farasi na kumfanyia mfalme ishara inapochunguliwa ndipo sababu yake
inapofahamika. Katika kusikiliza shauri la Adili na manyani kuna wazo kwamba ‘waungwana
hawasemi uongo’. Kwa hivyo ingawa Adili ameshtakiwa kwamba anawatesa manyani,
tunaona anawageukia manyani wale wale na kuwataka wayathibitishe ayasemayo.
Kuhusu malezi ya Hasidi, Mwivu na
Adili, mtungaji atoa wazo kwamba kumlea mtoto ni kumtunza mwili, kumfundisha
mawaidha na kuzipanua fikra zake, na zaidi ya yote ni kumfundisha ‘wema’ wa
moyoni. Moyo ndio makao ya upendo ambao ndio msingi wa ujamaa.
Kuhusu madeni inaonekana kwamba,
ili kutengeneza maisha ya upendo na kujitegemea, kukopa si jambo zuri na
kwamba, kama imekuwa lazima kulipa kabla ya kudaiwa. Na yule anayekukopesha
naye asiwe na lazima ya kudai kwa kero au inda.
Shaaban anamtumia Adili kueleza
kuwa, ingawa yeye alikuwa kitinda mimba, aliweza kuwa na busara na subira zaidi
ya wakubwaze. Busara yake ilimfanya afaulu katika biashara kwani aliweka
daftari ya mapato, kwa hivyo mali yake haikupotea bila ya kuelewa vile
ilivyopotea. Wazo la mtungaji ni kuwa biashara au shamba lahitaji mpango ambao
usipokuwepo patapatikana hasara. Kwa kuwa ndugu zake Adili hawakuwa na mpango
walifilisika baada ya mwaka mmoja tu. Na hivi ndivyo watu wengi duniani
wafanyavyo: hupata mali wakafanyia pupa kwa kutaka kuchuma zaidi bila mpango,
mara wakapata hasara. Lakini mtu kuvumilia na kusamehe ndugu zake ndilo jambo
linalohitajia, na hapa mtungaji anazidisha sana wazo lake la ukarimu. Kwa ajili
ya upendo, Adili aliwagawia tena mali nduguze ili wafanye tena biashara na
wajitegemee, wasimnyonye. Katika safari waliyoifanya wote watatu, Shaaban
anachukua nafasi ya kueleza faida za safari kwa kusema kuwa safari huleta ‘kufarijika
kkatika hamu, kujua namna ya kuendesha maisha, kupata elimu mpya, kuelewa tabia
za watu mbalimbali, kukutana na marafiki wa kweli kushinda ndugu, na mtu mwenye
bahati mbaya kwao huweza kupata bahati njema ugenini.’
Katika sura ya sita mwandishi
aeleza tena kwamba upendo ndiyo jambo muhimu duniani, kwani Adili ‘aliwapenda
ndugu zake kama pumzi ya maisha yake mwenyewe’. Pendo huleta huruma, na huruma
hii ndiyo iliyomwezesha Adili kumwokoa yule tandu aliyetaka kuangamizwa na
nyoka. Jambo la kukumbuka hapa ni kwamba jema hulipwa na jema. Yule tandu,
ambaye alijigeuza msichana, aliahidi kumlipa wema Adili na akamwombea dua
njema. Sura hii inaonesha kwamba ujasiri unatakiwa sana katika kufanya mambo
yaonekanayo kuwa magumu. Kwa ujasiri wake, Adili alipata maji, na safari ya
pili akajitolea peke yake kwenda mji wa Mawe kutafuta tena maji ya kunywa.
Sura ya saba haina mawazo mengi
ya mtungaji ila kusema kwamba duniani kuna mali nyingi lakini ni vigumu mtu
kuipata ikiwa amejificha. Watakaoipata ni wale wajasiri tu wenye nia ya
kuipata. Sura ifuatayo yasema hivyo hivyo: bahati ya turufu humwendea mchezaji,
na ndivyo ilivyokuwa bahati ya Adili, hata sasa akawa na bahati ya kukaribishwa
humo mjini na msichana mrembo.
Mawazo ya uongozi bora yarudiwa
tena katika sura ya tisa. Katika ukurasa wa 35, tunaelezwa jinsi kiongozi
ahitajiwavyo kuwa katika maingiliano yake na watu na vile vile na dini ya kweli
ya Mungu. Mrefu alimwangamiza Mfalme Tukufu na enzi yake yote (ila bintiye,
Mwelekevu) kwa sababu kiongozi huyo alimdharau Mungu akawa anaamini mizimu na
uimamu wa Kabwere. Rehema za Mungu huwafikia wanaomtii, na hivi ndivyo
Mwelekevu alivyojaaliwa kukipata kile kitabu kitakatifu pamoja na ule
mkomamanga. Mizimu na kutomjali Mungu ni kinyume cha ustawi wa moyo.
Maelezo yafuatayo yanahusu wivu. Mtungaji
anatwambia kwa njia hii hii ya hadithi kuwa wivu haufai. Mwenye kupata kitu kwa
jasho lake aachwe kufurahia mapato yake. Katika ukurasa wa 40, mtungaji
anahubiri juu ya mambo machafu na hila mbovu kama za wale ndugu zake Adili
ambao kila mmoja wao aling’ang’ania kutaka kumwoa Mwelekevu na baadaye
wakaonelea kuwa yule binti awe mke wa wote-jambo ambalo ni chafu sana. Na hapo
ndipo atoapo mawazo yake kuhusu ndoa yenye msingi kamili, kuwa ndoa si jambo la
watu wote; ni la watu wawili tu-mume na mke. ‘Mwanamume hakukusudiwa kuwa
fahali wa kila mtamba, wala mwanamke kuwatembe wa kila jogoo’. Mafanikio ya
Adili yaliwakata maini nduguze, kwa hivyo maoni ya Shaaban hapa ni kwamba watu
wafanikiwao ni lazima wawe macho, watahadhari na kijicho wanachoonewa, kwani si
watu wote wapendao au wanaofurahia mafanikio yao. Tena nduguze Adili, waliokuwa
hawapendi Adili, wakamtosa majini kwa wivu. Tunaoneshwa kuwa, kwa upande
mwingine, pendo likitoka upande mmoja tu katika maisha ya ujamaa basi huwa
halina msingi imara, na maisha yake huwa si marefu. Pendo lazima litoke pande
zote mbili sawa kwa sawa.
Adili alitoswa majini lakini ile
dua ya msichana-tandu ikamuokoa. Mtenda mema mara ntingi hulipwa mema, na
mtenda mabaya naye pia hupata kadiri ya ule ubaya wake. Basi Adili akapata mali
zaidi, na nduguze walio na wivu wakaadhibiwa wakageuzwa manyani na kupigwa
mijeledi kila siku.
Sura ya kumi na nne na ya mwisho
zaonesha mambo mawili hasa: wajibu wa kiongozi kuwaangalia wafuasi wake kwa
shida zao-kama vile Rai alivyojishughulisha kumpatia Adili ushahidi kutoka kwa
babake Huria, Kisasi-na mafundisho kuhusu hali ya binadamu na vitendo vyake. Mawazo
haya ya Shaaban yasemwa na Rai kuwaambia nduguze Adili: ‘Weavivu walijitahidi
kuwa hodari, ilikuwa kinyume hodari kuwa wavivu; kama waovu walitaka kuwa wema,
ilichukiza wema kuwa waovu; kama maskini walitafuta utajiri, ilikuwa ujinga
matajiri kufuja walichokuwa nacho; kama mbegu kidogo iliongezwa mchanga,
ilikuwa uharabu mtu kuua ndugu yake; pia ilikuwa aibu kubwa sana kwa wazuri
kutenda maovu.’
Kwa hiyo, ni dhahiri yakuwa
katika Adili na Nduguze Shaaban
afundisha watu waishi kwa kupendana chini ya uongozi bora, na wajisaidie
kiujamaa badala ya kujiangamiza na kuoneana wivu ambao hauna faida-si kwa hao
wenye wivu tu, bali kwa nchi nzima. Vile vile anawaambia wale wenye busara na
werevu kwamba dunia ni kubwa na imejaa mali na vitu vizuri ambavyo vitakuwa ni
vya kila avitoleaye jasho na mwenye wema moyoni na akili kichwani.
Wasifu wa Siti Binti Saad zaidi unaonesha pendo kuliko ujamaa,
lakini kiini chake ni ‘kujitegemea’. Kama Bwana Waziri Juma asemavyo katika
dibaji ya kitabu hicho (uk. vii), ni sawa kama mwandishi awatia moyo wasichana
na wanawake wengi wa Kiafrika wanaojibidiisha kwa shughuli mbalimbali kwa ajili
ya maisha yao.
Shaaban Robert ana nia ya kueleza
kwamba ni lazima mtu ajitegemee kwanza ndipo atakapofanikiwa kupata yale
ayatakayo. kule kuwa mwanamke, au kutosoma, au kutokuwa na fedha, au kutozaliwa
na kukaa mjini, au kutokuwa na sura nzuri, hayo yote si kitu kwani kujiamini,
kuwa na nia, na kuwa na subira na juhudi kunaweza kuleta mafanikio mengine
makubwa yasiyoweza kufikiriwa hata kidogo hapo mwanzoni. karibu kitabu chote
kinazungumza habari za mtu mmoja tu, na hakisemi mengi juu ya watu wengine ila
kuonesha tu yakuwa wapo wengine waliomuonea wivu Siti wakastahili kupewa jibu
la kuwatia vidaka vya midomo. kwa hivyo inaonekana kwamba maelezo yaliyomo humu
ni kama safari ya barabara moja yenye vipingamizi, na mtungaji anaonesha vile
msafiri mmoja anavyoendelea na safari yenyewe. na hata huyu msafiri mwenyewe, Siti,
ametumiwa na mtungaji ili awe mfano kwa wanawake wengine wanaojidharau na kuona
kwamba hakuna lolote hapa duniani wawezalo kulifanya. Lakini hivyo sivyo;
ulimwenguni ni mpana.
Shaaban Robert anataka kuonesha
kuwa katikati ya vizuizi mtu anaweza kusimama na kufanya kazi kwa bidii hata
akajipatia sifa. Siti hakuwa na bahati njema ya kuviepuka ‘vipingamizi’ vile vilivyotajwa
hapo juu (kutokuwa na sura nzuri na kadhalika), lakini vivyo alianza safari
yake katika maisha. alijua kuwa wazazi wake ni maskini, kwa hivyo aliendelea na
biashara yao ya kuuza vyungu. hakuna mtu aliyepata vyote au aliyekosa vyote. Mtumwa-jina
la Siti la hapo mwanzo-alikosa sura nzuri, lakini alifadhiliwa sauti ya kuvutia
kweli kweli. Fimbo iliyo mkononi ndiyo iuayo nyoka; kwa hivyo Siti aliifanya
sauti yake ndiyo fimbo yake, na akaitumia vilivyo. Hapa Shaaban anachukua
nafasi ya kutueleza kuwa sura nzuri si kitu cha kukiangalia sana maishani mara
kwa mara, wala si kizima kiu cha mapenzi. Mawazo yake ni kuwa inambidi mtu aikubali
hali yake kwanza, kisha ndipo atakapoweza kuona ni wapi anapofaa ili aweze
kufanya jambo atakalo kwa kadiri ya uwezo wake. na haya yote yawezekana, si ya
ajabu.
Lakini, katika kukata shauri juu
ya jambo la kutekeleza, mtu mara nyingi humbidi kuyatoa mhanga mambo yake
fulani aliyokuwa nayo kama vile Siti ilivyombidi kukiacha kijiji chao Fumba,
mumewe, mtoto wake na maisha ya utulivu yasiyo na ghasia, akakata shauri
kukidhihirisha kipawa chake kwa kuimba katika taarab mjini Unguja. Alihitajia
sana subira, juhudi, kujiamini na kujitegemea katika maisha mapya ya mjini
yaliyokuwa na vipingamizi vingi. kimojawapo cha vipingamizi hivyo kilikuwa ni
kushindwa kuimba siku ya kwanza alipotokea hadharani. Alikuwa hajazoea. Lakini
baadaye alifaulu kwani ‘alishikilia kazi yake kwa bidii’, akawa na dhamira na
nia ya kufaulu.
Kipawa bila ya ujasiri, dhamira
na nia ni bure tu. Maisha ya mjini ni magumu na hasa kwa mwanamke ambaye ni
mgeni tena ni mtu mzima ambaye hapo alipokuwapo hakuwa na mume. Lakini Siti
hakuwa muhuni. Aliweza kukaa imara kwani alikwenda mjini kwa kusudi maalumu; na
palimfaa kwalo. Hakwenda mjini kutafuta fedha, kwani tunaambiwa yakuwa Siti
hakupenda fedha, lakini kazi yake ilikusudiwa kumletea sifa na umaarufu. Hakuwa
mnyang’anya watu fedha kwa sababu ‘alikuwa mcha Mungu wa sala na saumu. Alisali
vipindi vitano kila siku, akafunga faradhi na suna katika maisha yake yote’.
Maoni ya mwandishi hapa ni kuwa mtu awe wa ibada saa za ibada, na mlimwengu
wakati wa mambo ya kilimwengu.
Pia inaonekana mwandishi
anafikiri kwamba Siti alifanikiwa kwa sababu ya ukarimu wake na Baraka kuliko
kuwa ni kwa sababu ya masharti ya mikataba na mapatano katika kazi yake.
Mafanikio, kwa wale wajuao wayafanyayo ni kama moto wa mbugani. Mara watu
wakawa wanamfuatafuata Siti, watribu wakamzunguka kwa vinanda ili awaimbie,
wapiga picha na wapiga chapa nao wakamwendea, watu wa santuri pia wakawa
wanamfuata, na kwa njia hii sifa za mwanamke huyu zikatapakaa hata nje ya Afrika
Mashariki. Mafanikio mengi ya Siti, asema Shaaban, ni kwa sababu alikuwa
mtanashati, hana majivuno, mwenye adabu na mlahaka kwa watu wote.
Ni kweli kabisa kwamba ‘jina
kubwa lolote halipatikani duniani bila vizuizi kadha wa kadha’ kwa maana kuna
mfano wa Siti ambaye, mara tu alipoanza kupata sifa kwa kuimba, watu walianza
kumwonea wivu na kumdharau na hata kumtukana. Kuhusu mambo haya yote, maoni ya
mwandishi ni haya: mtu lazima awe na subira, bidii na uvumilivu katika kazi
yake; aende mbele bila ya kuangalia nyuma.
Safari ya Siti katika maisha
ilifanikiwa kwa ramani ya maneno. Mwenye busara hujiwekea maneno ya kumwongoza.
Katika kuwajibu waliokuwa wakimtia ila na kumtukana, Siti alisema:
Si hoja uzuri, na sura jamali
Kuwa mtukufu, na jadi kubeli
Hasara ya mtu, kukosa akili

Huu ndio wimbo uliowakomesha
wapinzani wake. Na yaonesha kwamba mtu yambidi kujitetea anaposhambuliwa na
binadamu wenziwe, lakini si kujitetea kishenzi kama mnyama wa porini.
Kama kawaida, mwandishi
anajiuliza kwa nini Siti alifanikiwa hivyo? Maoni yake ni kwamba, kwanza, Siti
alifahamu sana tabia za watu, alikuwa na adabu na alijua kuchukuana nao (wazo
lililomo katika kitabu cha Adili na
Nduguze pia); na pili aliwapenda sana wasikilizaji wake. Hapa upendo
waonekana kuwa ndio msingi wa mafanikio. Hata hivyo, Siti hakujisifu mwenyewe.
Baada ya kueleza kwamba Siti
alizidi kusonga mbele, na kuviruka vipingamizi vingi, mwandishi anatoa mawazo
yake kwamba hayo hayakuwa mambo ya ajabu; matendo yake yanaweza kuigwa. Siti
alikuwa ni mtu kama watu wengine. Katika ukurasa wa 49 yapo mawazo mazuri ya
Shaaban yanayosema:
‘Fikiri kama na wewe umepata
kutenda neno lolote la fadhili kwa watu au nchi yako. Kama hujalifanya bado,
lifanye sasa. Yamkini una marafiki. Wafurahishe kwa fadhili yoyote uwezayo
kutenda. Haikosi una washindani. Wape sababu ya kukuajabia kwa unyofu ulio nao….Maisha
yalikuwa matendo, sio usingizi’.
Tangu mwanzo mpaka mwisho wa sura
ya nane Shaaban ameacha kutuzungumzia mtu wake. Hapa anasimama na kutoa mawazo
yake juu ya jambo moja muhimu sana kwa wanaadamu. Nalo ni tabia njema. Anasema
tabia njema imo katika ukweli na mapenzi ya moyoni. Tabia njema haifuati elimu,
wala utajiri, wala kuwa na cheo. ‘Tabia ilikuwa kama njia panda kuu katika
maisha yaliyogawa watu kwenda pande mbalimbali za dunia.’ Watu hutengana kadiri
ya tabia. Hata Mungu anawagawa watu kwa kufuata tabia zao. Ni vizuri kuwa na
tabia nzuri ambayo Shaaban Robert anafikiri ina amani na upole, saburi na
unyenyekevu, uungwana na uaminifu kwa watu wote-hiyo ni johari. Mwandishi
anahubiri juu ya tabia njema itakiwayo, akitoa mfano wa Siti, na anamalizia
kitabu chake vizuri sana kwa kutaja waziwazi kiini hasa cha mawazo na maoni
yake juu ya maisha.
Kama nilivyosema hapo awali,
Shaaban Robert katika Wasifu wa Siti
Binti Saad anaonesha jinsi mtu, hata akiwa katika hali ya chini, awezavyo
kujitahidi hadi akaweza kustawi na kujitegemea. Sura ya mwisho inatilia mkazo
neno kuu la kitabu hiki, ‘kujitegemea’. ‘Kujikimu ni kujiruzuku. Kujiruzuku ni kujitegemea kwa chakula, nguo na
masurufu mengine katika maisha.’ Na hapa ndipo tutakapokomea kutoa mawazo ya
mtungaji wa kitabu hiki.
 
Baada ya kuhakiki Adili na Nduguze na Wasifu wa Siti Binti Saad, na pia nikiyapima mawazo ya marehemu
Shaaban Robert katika fasihi zake nyingine kama mashairi yake Masomo Yenye Adili, Kusadikika, na Kufikirika, naona vigumu sana kuuepa
ukweli kwamba marehemu aliandika vitabu vyake kwa nia ya kufundisha watu;
alitoa fasihi yake iwe kioo cha watu kujiangalia ili waone jinsi wanavyoishi na
wanavyotaka kusihi, na vile vile waone jinsi ambavyo yeye mwenyewe Shaaban
Robert angependelea watu waishi. Kwa sababu hii, maandishi yake yote yanang’aa
kwa ilani isemayo, ‘Maisha ya mtu ni msingi wa maendeleo ya nchi.’ Maneno haya
ndiyo ufunguo uliomo mwanzoni kabisa mwa Maisha
Yangu na Baada ya Miaka Hamsini-kitabu ambacho kwacho Shaaban ametueleza na
kutuonesha sehemu ya maisha yake.