MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
MyBB Internal: One or more warnings occurred. Please contact your administrator for assistance.
UHAKIKI WA SERA YA LUGHA KATIKA ELIMU YA TANZANIA

Thread Rating:
  • 0 Vote(s) - 0 Average
  • 1
  • 2
  • 3
  • 4
  • 5
UHAKIKI WA SERA YA LUGHA KATIKA ELIMU YA TANZANIA
#1
ELIMU AU MAIGIZO?
Uhakiki wa Sera ya Lugha Katika Elimu Tanzania
Z.S.M. Mochiwa katika Kioo cha Lugha 2,1996/97:41-58
Z.S.M.Mochiwa katika kuhakiki sera ya elimu katika Tanzania anaeleza yafuatayo:
Utangulizi
Katika wimbo wa Taifa la Tanzania, hekima, umoja na amani hutamkwa kuwa ngao za Watanzania. Aidha, nembo ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam imesogeza falsafa hii hatua moja mbele kwa kutangaza kuwa: Hekima ni uhuru. Hainipitii akilini mwangu kuwa kuna mtu-hadhiri wa nafsi yake anayeweza kusema matamko haya ni mufilisi. Mimi, binafsi yangu, ninayahesabu kuwa miongoni mwa vito vichache tulivyo navyo katika taifa hili.
Kwa bahati mbaya, sijapata kusikia majadiliano yanayomulika jinsi vito hivi vinavyorutubishwa ndani ya jamii. Penyenye peke yake niliyoona ni ile inayotokana na matumizi ya kito kimoja ndani ya nembo ya Chuo Kikuu. Kwa kuwa Chuo Kikuu ni taaisis ya elimu, hapana shaka kuwa nemno ile inahusisha elimu na hekima. Kwa maana hiyo, ndani ya elimu, hekima hukua na inapokua, hekima humpa aliye nayo uhuru.
Tukiyaondoa hayo yote, bado taifa halielekei kujiuliza kwa dhati kabisa, hekima, umoja na amani hukuzwa na kuendelezwa vipi. Hata wataalamu wa Chuo Kikuu, pamoja na kudai kuwa hekima ni uhuru, hawaelekei kuionesha imani hii kwa vitendo kwa kubainisha na kutumia mbinu zinazokuza hekima. Aidha, mtu anapohakiki safari ya taifa hili tangu lizaliwe hadi hivi leo, na hususan miaka kumi hivi iliyopita, inadhihirika wazi kuwa kuna kupuuzwa kwa virutubisho vya vito hivi.
Inawezekana kuwa mwenendo wa kupuuzwa kwa virutubisho hivi si wa makusudi. Linaloelekea kuwa dhahiri kwangu, ni kule kutotambua vizuri virutubisho hivyo ni vipi na vina umuhimu gani. Mathalan, baada ya uhuru, Tanzania ilianzisha wizara ya Utamaduni-kirutubisho cha kwanza cha hizo ngao za taifa-lakini wizara hii haikuweza kudumu na nafsi yake. Kisa cha kupachikwa pachikwa kwa wizara hii kila mahali-mara utamaduni ni sehemu ya Wizara ya kazi, mara vijana, ningethubutu kusema, ni taswira yake yenye uvumilivu mbele ya wahandisi wanaoanzisha wizara katika Jamhuri. Hali hii ya uvumilivu wa taswira ya wizara huakisika pia katika mgao wa mafungu ya fedha. Hali hii hujirudia kwenye taasisi za wizara hii, kama vile, BAKITA. Kwa ufupi taifa halijapambaukiwa kwamba utamaduni ndiyo nyenzo pekee ya kurutubishia vito vya taifa.
Katika makala haya ninakusudia kudai kuwa Tanzania haikupiga hatua kubwa kielimu na kimaendeleo kwa ujumla kwa sababu ya kuweka kipaumbele chake katika mambo ambayo, kwa maoni ya makala haya, si ya msingi. Kuitelekeza lugha ya Kiswahili ikabaki kuwa lugha ya kuuzia nyanya sokoni, kumeleta maafa makubwa kielimu, kijamii na kiuchumi, ima kwa neno moja kiutamaduni. Ikisemwa vinginevyo, kwa kupuuza lugha ya Kiswahili na kuikumbatia ya Kiingereza, Tanzania imekubali kujiweka katika hali ya kutojitegemea. Matokeo ya mwenendo huu ni kwamba kila kinachofanyika ni maigizo tu. Hali hii hailiruhusu taifa kuishi kwa nafsi yake isipokuwa kwa nafsi ya kuazima. Kabla ya kuanza mjadala huo hapana budi kuelekeza makini yetu kwenye dhana muhimu, nazo ni taifa, utamaduni, maendeleo ya kijamii, elimu na lugha.
 
Taifa
Inaposemwa kwamba Tanzania ni taifa, ina maana ni kundi la watu ambao wana nduni mahususi. Kwanza kundi hilo lina kipande cha ardhi ambacho wote kwa pamoja wanadai kuwa ni chao; ni nchi yao. Watanzania, kwa mfano, huishi Tanzania, na Wakenya huishi Kenya. Pili, ili wawe taifa, ni lazima watu hao wawe na mambo kadhaa yanayofanana. Miongoni mwa mambo hayo ni historia, mila na desturi. Tunaposema, mila na desturi, tunasema taifa haliwezi kuwa taifa bila ya kuwa na utamaduni wake. Nduni hizi ndizo zinzorutubisha umoja wao.

Watu wenye mila na desturi au, kwa neno moja, utamaduni unaofanana wana kongamano kubwa la rai, mtazamo na hisia. Hukumu zao kuhusu masuala na matukio mbalimbali hufanana. Kwa misingi hii watu wa namna hii wana umoja wa aina fulani katika mienendo na hukumu kuhusu vilivyo na visivyo. Pamoja na kuzikubali nduni hizi, Gerth na Mills (1954:197) wanaongeza kuwa kundi hilo lina uwezo wa kujiundia chombo cha uongozi kikawa serikali yao. Kwa kuwa moja ya nduni za taifa ni utamaduni wake, tujipe wasaa wa kuifasili dhana hii.

Utamaduni
Kwa watu wa kawaida, utamaduni unafasiliwa kwa namna nyingi kwa kutegemea muktadha. Utamaduni unanasibishwa na uganga au mazingaombwe, uchawi, michezo au ngoma au mambo yote ambayo, kwa macho ya sasa, yamepitwa na wakati. Mifano halisi ya mikanganyiko hiyo ni pamoja na jina la wizara yenyewe inayosimamia masuala ya utamaduni nchini ambayo inaitwa Wizara ya Elimu na Utamaduni. Kutenganisha Elimu na Utamaduni ni kudai kuwa Elimu huweza kuangaliwa pekee bila ya kuhusisha Utamaduni. Jina la Wizara halidokezi kuwa Utamaduni ni elimu na elimu ni utamaduni. Aidha, inapotokea kuwa watu huiita Wizara hii kuwa ya michezo, kwa sababu tu wao ni washabiki wa michezo, hii ni dalili ya ufahamu nusu nusu wa dhana nzima ya utamaduni. Hali hii, kwa maoni yangu, inatia hofu kwa sababu utamaduni, kwa sehemu kubwa, unaonekana kuwa mambo ya jana na si ya leo. Ni mambo ambayo hayana mchango wa moja kwa moja katika uhai wa jamii hivi leo. Aidha, fasili hizi zinaelekea kudokeza uwezekano wa utamaduni kuwa kikwazo katika maendeleo ya jamii badala ya kuwa suluhu au mashine yenyewe ya maendeleo hayo.

Chanzo cha mikanganyiko hii ni upana wa dhana yenyewe. Karibu kila kitu katika jamii kinanasibika na utamaduni. Kutokana na mikanganyiko hii, hata wataalamu wameelekea kufasili dhana hii kwa kutaja ‘orodha’ ya vitendo, matukio na mienendo ya jamii. Goodenough (1957:167), kwa mfano, anasema:

Quote:Utamaduni wa jamii ni mkusanyiko wa yote ambayo mwanajamii ni lazima ajue au aamini kama sharti la kukubalika kwa mwenendo wake kwa wanajamii wenzake…..(tafsiri ya mwandishi).
Maneno ‘mkusanyiko wa yote’ katika fasili husisitiza kuwa dhana ya utamaduni ni ‘kapu’ la kubebea yote yaliyo ndani ya jamii. Pamoja na upana wake, fasili hii ni maarufu kwa wataalamu wengi kama Wardhaugh (1992) na Baker (1995). Baker, kwa mfano, zaidi ya kutumia mkusanyiko wa yote, anaorodhesha vipengee kama fasili yake inavyoonesha:
Quote:Utamaduni ni mwenendo mzima wa maisha ya jamii, maono ya jamii, mpangilio wao wa uzoevu, taratibu za matazamio, mahusiano ya kijamii, kaida za mienendo, sayansi na teknolojia, n.k (uk. 28) (tafsiri ya mwandishi)
Udhaifu wa fasili hizi ni kwamba unaifanya dhana hii iwe ngumu kufumbatika kiakili. Aidha fasili hii inashindwa kuhusisha channzo na matokeo na badala yake kushikilia matokeo. Mienendo ya jamii, mpangilio wa uzoevu, matazamio na mahusiano kati ya wanajamii, ngoma, michezo n.k. peke yake si utamaduni. Utamaduni ni muunganiko wa haja ya jamii kupata nusura na jitihada zao za vitendo vya kuipatia nusura hiyo. Yote yanayoorodheshwa yanatokana na haja iliyo ndani ya nafsi ya kila mwanajamii ya kutaka kunusurika. Nusura hii ndiyo inayofasilika kuwa mfumo wa maitikio yote ya wanajamii katika kukabiliana na changamoto zilizomo ndani ya mazingira ya jamii yenyewe. Mbinu za kujiruzuku, kujihami, kujifurahisha, kujenga mahusiano kati ya wanajamii ni mkusanyiko wa jitihada za wanajamii ambazo zinakidhi haja ya kupata nusura.
Fasili hii, inatuwezesha kuona nafsi ya kubadilikabadilika kwa michomozo ya nusura. Ingawa haja ya kunusurika haibadiliki lakini mbinu zinazotumika ili kuipata hubadilika kutokana na mabadiliko ya mazingira. Tuchukue mfano wa burudani. Kuburudika ni kipengee muhimu kinachodhihirisha utashi wa mwanajamii wa kujipatia nusura. Lakini kwa kadiri miaka inavyobadilika jamii imeshuhudia kuingia na kutoka kwa aina mbalimbali za burudani. Ni nani, kwa mfano anajua Mserego au beni ni nini hivi leo? Kutoweka kwa ngoma kama hizi hakuna maana ya kupotea kwa haja ya burudani. Kilichotokea ni kwamba wanajamii hupata burudani wanayohitaji kutokana na ngoma, michezo au shughuli nyingine mpya.
Fasili kama hii inatusaidia kuusawiri mwanzo wa utamaduni ndani ya heba ya mwanajamii badala ya kuuona kuwa nje ya heba hiyo. Aidha fasili hii itatuzuia kuuona utamaduni kuwa gwanda ambalo mtu anaweza kuvaa au kuvua. Ingawa mtu hazaliwi nao, lakini mbegu ya utamaduni imo ndani ya nafsi yake. Utamaduni kwa mtazamo huu ni mfungamano wa nafsi ya mwanadamu ya kutaka nusura na maitikio yake ya changamoto za mazingira yake. Kutokana na mfungamano huo, utamaduni huifumbata heba yake. Kwa vyovyote itakavyofasiliwa, hapana budi dhana ya utamaduni iungane na heba ya jamii. Utamaduni ndiyo nafsi; ni dhati ya jamii.
Mjadala huu unatufanya kuuona utamaduni kuwa na nyuso mbili. Uso mmoja ambao umo ndani ya heba ya mwanajamii katika sura ya utashi wake wa nusura. Utashi huu wa nusura ndio unajidhihirisha katika mkusanyiko wa mbinu mbalimbali za kuutafutia nusura. Uso huu ulio ndani ya heba ndio unaoukilia vipengele vyote vinavyoorodheshwa. Aidha, uso huu ndio unaomsukuma mwanajamii mpya kufanya jitihada ya kujifunza huu uso wa nje. Uhusiano wa usababisho kati ya utashi wa nusura na mbinu za maisha zinazodhihirika ni kitu cha msingi katika kuchochea, kuimarisha na/au kuhamasisha maendeleo ya jamii. Kwa maneno mengine, ncha mbili hizi zinazokamilisha fasili zinasaidia kuona uhusiano wa karibu kati ya utamaduni na maendeleo ya jamii.
Maendeleo ya jamii
Tunapochukulia kuwa utamaduni una nyuso mbili, yaani utashi wa nusura na mbinu za kuipata nusura hiyo, inawezekana kusema maendeleo ya jamii yoyote ni mabadiliko ya utamaduni wake, na hasa, kwa usahihi zaidi, ni  mabadiliko ya mbinu za kupatia nusura. Mabadiliko ya mbinu hizo huanzia kwenye utashi. Huanza na hisia za kutosheleza kwa mbinu hizo za kuipatia jamii nusura yake. Baada ya kuridhika kuwa mbinu zinazotumika zina udhaifu, jamii hufanya bidii ya kuondoa zile zilizochakaa na kuingiza mpya. Mbinu mpya zinapoingia katika jamii, ndipo jamii inayohusika inasemekana kuwa imepiga hatua ya maendeleo.Kwa maana hii, jitihada zozote za kuiletea jamii maendeleo huanza na tathmini ya kina ya utamaduni wa jamii inayohusika, hususan, mbinu za maitikio ya changamoto za mazingira zinakidhi kwa kiasi gani haja ya jamii hiyo ya kujitafutia nusura. Tathmini hii itaelekeza ni vipengee gani katika ‘mashine’ ya maendeleo vimechakaa na kwa hivyo vinahitaji kubadilishwa. Mbinu mpya za utunzaji wa mazingira, kwa mfano, huibukia ndani ya utamaduni wa jamii kuhisi kuwa maitikio ya zile za zamani ya changamoto hizo hayaleti tija inayolingana na mahitaji.
Jambo la msingi hapa ni kwamba ni lazima jamii ihisi kwamba kuna tatizo. Endapo jamii, kwa macho yake ya utamaduni, haihisi kuwa liko tatizo, jitihada zote za kuleta maendeleo hukwama. Mathalan, sina hakika kama heba ya Tanzania inahisi kuwa uzazi wa watoto wengi ni tatizo. Mradi wa Uzazi wa mpango utafanikiwa ikiwa heba ya jamii itagundua na kukubali kuwa, kuwa na watoto wengi katika familia ni tatizo.
Umuhimu wa kuangalia maendeleo ya jamii kwa mwanga huu umetiliwa mkazo katika Mkutano Mkuu wa sera za utamaduni ulimwenguni (1982). Mkutano huo wa Mexico ulidhihirisha kwa kauli moja haja ya kuweka mnasaba kati ya maendeleo na utamaduni. Mkutano ulizingatia na kutangaza kwamba:
Quote:Maendeleo ya kweli ni yale yanayotokana na hisia na dhamira za mabadiliko za wanajamii. Kwa maana hiyo maendeleo ya jamii yatakuwa matokeo ya juhudi za wanajamii. (uk. 18). (Tafsiri ya mwandishi)
Kwa kuangalia kampeni nyingi za nchi, ni rahisi kuona kuwa, yaliyo matatizo kwa wenzetu, yamefanywa kuwa matatizo kwetu. Aidha, kwa kuwa suala la utamaduni halina kipaumbele, nchi imejitumbukiza katika miradi mbalimbali ambayo mara nyingi haielekei kukabili changamoto halisi za mazingira ya jamii. Kampeni kama Twende na wakati na Uzazi wa mpango, zinafungamana zaidi na heba za jamii za nje kuliko heba ya Tanzania Ni dhahiri kuwa, Tanzania haitafuti maendeleo ya kijamii kwa kurekebisha heba yake bali kwa kujilinganisha na kujifananisha na heba nyingine. Kujiangalia na kujirekebisha kwa kioo cha nje, au tuseme, kwa kutumia vigezo vya tamaduni za nje, kuna matokeo ya kutelekeza utamaduni wetu ambao, ndio mashine ya maendeleo ya kweli.
Elimu na lugha
Zinapokubalika, fasili za utamaduni na maendeleo ya jamii zinadokeza kwa nguvu, umuhimu wa elimu na lugha katika maendeleo. Ikiwa ndani ya utamaduni mna mfumo wa maarifa au mbinu mbalimbali zinazoleta arabuni ya utashi wa nusura ya jamii, na ikiwa maendeleo ya jamii ni mabadiliko ya utamaduni, ni dhahiri kuwa elimu na lugha ni muhimu katika uhai wa mfumo wenyewe pamoja na maendeleo ya jamii. Mfumo huo hauwezi kuendelea kuwako bila ya kuwako kwa taratibu za kuurithisha kwa kizazi kipya. Taratibu hizo za kuurithisha mfumo wa maarifa na mbinu za nusura ndizo zinazoingia katika ajenda ya elimu.

Elimu kwa rai ya makala haya, iwe ya asili au ya kisasa, ina kazi kuu mbili. Zaidi ya kuwa mchakato wa kurithishia vipengee mbalimbali vya mfumo wa nusura ya jamii, lakini pia, mchakato huu humpatia kila mwanajamii fursa ya kugundua na kukuza vipawa vyake. Ni mfumo unaokuza akili ya mpokeaji hadi imepata uwezo wa kutanzua tata, kudadisi na/au kupata stadi za ubunifu. Elimu hii ndiyo ile ile inayofasiliwa na Nyerere (1967) kuwa mchakato wa kukuzia udadisi na wa kujengea fikra angavu.

Freire (1970) anaifasili elimu hii kuwa kitendo cha kitamaduni chenye kumleta mpokeaji kwenye uhuru. Kauli ya Freire inaobesha wazi kuwa Elimu ni utamaduni na utamaduni ni elimu. Tanzania kuwa na Wizara ya Elimu na Utamaduni ni kuonesha kuwa dhana ya utamaduni haijaeleweka. Aidha, kwa mujibu wa Freire, kitendo hicho cha kitamaduni kitakuwa hakina maana ikiwa hakimpi mpokeaji kujua na badala yake humpa kukariri mambo tu.

Elimu, na hasa ile ambayo ni chipukizi la utamaduni wa jamii, ni mchakato muhimu na wenye nguvu za kusukuma gurudumu la maendeleo. Lakini kama wanavyodai Costa na Garmston (1994) elimu hiyo ni sharti iwe na makusudi mahususi. Hapana budi iwe na ‘mtu wa ndoto’ anayeaniwa nayo;

Quote:Ni lazima elimu ikuze uwezo wa kufikiri kwa unyofu na uangavu. Impe mpokeaji uwezo wa kuunganisha chanzo na sababu za matukio na kutoa maamuzi razini (uk 77) (Tafsiri ya mwandishi)
Haya, kwa kiasi kikubwa, ndiyo yanayotajwa na Nyerere anapofafanua mtu wake wa ndoto kielimu (mtajwa). Yeye pamoja nao wote wanasisitiza kuwako kwa falsafa ambayo itaongoza mchakato mzima wa elimu. Kutokuwako kwa falsafa ya elimu iliyo hai nchini kumesababisha matatizo ya aina mbalimbali ambayo yanaelekea kuunyima mchakato wa elimu Tanzania uwezo wa kumuumba mtu wa ndoto tuliyemtaja.
Mchakato wa elimu wenye uwezo wa kutoa bidhaa ya aina iliyoelezwa, ni ule ambao unatumia lugha inayoruhusu makusano (interaction) baina ya walimu na wanafunzi, walimu na walimu na wanafunzi na wanafunzi. Matumizi ya lugha ya Kiingereza katika elimu ya sekondari yametunyima bidhaa hii. Walimu na wanafunzi hawaonani kifikra, hawakusani wala hawajadiliani. Kwa miaka mingi, Kiswahili kwa macho ya serikali Tanzania hakistahiki na wala hakiwezi kumudu mawasiliano ya kitaalam. Viongozi na watu wengine wanalitamka jambo hili bila ya ‘ashakum’ wala ‘astaghafiru’. Kinachoumiza roho ni kwamba, kama tutakavyoona hivi punde, dai hili si sahihi kabisa. Aidha, hata kama lingalikuwa kweli, lisingalitangazwa kwa mikogo hiyo. Kwa kuwa lugha huakisi akili ya jamii nzima, inaposemwa lugha yake haimudu hili au lile ni kifani cha kusema akili ya jamii hiyo ni ndogo kuliko ya jamii nyingine. Sina hakika kama jamii hii iko tayari kujipuuza hivi ili iendelee kupuuzwa. Vinginevyo tunajitia katika ushahidi kuwa mnyonge huanza kujinyonga mwenyewe.
Lugha ya kufundishia

Kwa muongo mzima huu, kuanzia 1987 hadi 1997, taifa kwa sehemu kubwa, limeendelea kutoelewa vipengee vya msingi vinavyosukuma mbele gurudumu la maendeleo. Hakuna dalili zozote zinazoonesha nafasi ya utamaduni, na hususan lugha, katika kurutubisha vito vya taifa kwa upande mmoja na kwa maendeleo ya taifa kwa upande wa pili. Taifa limeshindwa, hadi sasa, kugundua ubadhirifu wa vipawa vya taifa shuleni. Ingawa Kiingereza hakijulikani, bado serikali imeshikilia kidinindi kiendelee kuwa lugha ya kufundishia elimu ya sekondari. Inatia huzuni, na pengine aibu, kuona kuwa Tanzania inaamini kuwa mtoto wa nchi hii atakuwa amesharabu Kiingereza baada ya kupewa saa 800 za kujifunza lugha hiyo katika shule ya msingi (ang. Mochiwa 1991).


Kutojulikana kwa Kiingereza si suala la utafiti tena. Wataalam mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wamelieleza taifa hili kwamba lugha hii haijulikani kwa kiwango cha mawasiliano katika elimu ya sekondari (ang. Mlama na Matteru, 1977, Criper & Donald 1984, Rubagumya 1990). Isitoshe, tume ya Rais (1982) ilipendekeza kitumike Kiswahili badala ya Kiingereza lakini, serikali ililifumbia macho pendekezo hilo.


Hali hii inaonesha kuwa serikali ya Tanzania haiendeshi mambo yake kisayansi badala yake inafuata ushauri wa kihisia usiozingatia hali halisi. Ushauri huo wa kihisia unaelekea kuitisha serikali kwa kutangaza matatizo makubwa yatakayoikumba nchi endapo itaamua kuingiza Kiswahili ndani ya madarasa ya sekondari. Baadhi ya matatizo ni ya hhakika na mengine ni ya kufikirika. Tujipe fursa ya kuyaangalia.


Matatizo ya kutumia Kiswahili

Matatizo au vikwazo vinavyotajwa sana tunaposhauri kuongezeka kwa matumizi ya Kiswahili katika uhai wa taifa hili ni mengi. Aidha, sababu za kushikilia matumizi ya Kiingereza katika shule za sekondari ni nyingi. Lakini Maghimbi (1995) angepata nafasi ya kutangaza sababu za kushikilia Kiingereza na kutupilia mbali Kiswahili – mwenyewe sababu hizo anaziita Tasinifu – ametaja 25. Baadhi ya tasnifu hizo ni: kuogopa kuwa wa kwanza katika mabadiliko, ukosefu wa vitabu vya taaluma, gharama, kuanguka kwa viwango vya elimu nchini, kuvunjika kwa mashirikiano ya kitaalam na uchanga wa Kiswahili. Kwa makusudi ya makala haya matatizo haya yatawekwa katika matapo makuu mawili: nafsi ya lugha yenyewe na utekelezaji wa sera ya Kiswahili sekondari. Tutaanza na nafsi ya lugha.


Nafsi ya lugha
Hofu kubwa ambayo inasambazwa na washauri ina mwega ndani ya Kiswahili chenyewe. Kiswahili, inadaiwa, hakina msamiati. Ingawa dai hili ni kweli lakini inasaliti udhaifu wa aina tatu. Mosi, inaelekea wanaotangaza dai hili kwa pumzi zote, hawajui lugha ni nini. Kwa nafsi yake, lugha ni sarufi yake na si msamiati wake. Hawajui kwamba asilimia kubwa ya msamiati wa Kiingereza – lugha inayotukuzwa kupita kiasi – si wake; ni wa kusharabu. Hivyo basi, matumizi ya Kiswahili katika nyanja za elimu hayawezi kuleta matatizo kwani, ikiwa kitapungukiwa na msamiati, Kiswahili kinaweza kuchukua/kutohoa maneno kama ilivyofanyika katika ukuaji wa Kiingereza. Kinachotakiwa kubadilika si msamiati bali sarufi. Wanafunzi shuleni hawashindwi kwa sababu ya msamiati mgumu bali wanashindwa na sarufi ngumu ya Kiingereza.
Pili, njia ya kuondoa tatizo la msamiati, washauri wanasema, ni kuahirisha kwanza matumizi ya Kiswahili ili uundwe msamiati kwanza, Ushauri huu hudhihirisha kutojua kuwa lugha, kama ulivyo utamaduni, hujirekebisha kwa kulingana na mahitaji mapya. Isitoshe, maana ya ushauri huu ni kutaka Tanzania itayarishe Kiswahili kwa matumizi yatakayotangazwa baadaye. Ushauri huu, zaidi ya kuhuzunisha, unapingana na maumbile. Maneno na semi hujengwa na wazungumzaji wenyewe katika hizo shughuli zao. Mkemia atazua maneno kwa kulingana na kile anachokiona akilini mwake au tuseme katika taaluma yake. Wasio na utaalamu wa kemia hawawezi kuratili hali halisi ya taaluma hiyo. Kwa maana hii, tunapozungumzia mabadiliko ya lugha ya kufundishia, tunatangaza changamoto kwa wataalamu wote – wakemia, wafizikia, wahandisi n.k – wajenge msamiati na semi mwafaka kwa taaluma zao. Kwa mantiki hii hata kesho Kiswahili kingeweza kuingia katika maabara ya shule ya sekondari maadam walimu ni Watanzania.
Tatu, washauri hao wanasahau kuwa vinavyoelea vimeundwa. Ikiwa lugha yetu ina kasoro zozote ni juu yetu sote kusimama kidete kuirekebisha katika hima ya kujiletea maendeleo yetu. Kuijenga lugha hii ikawa chombo chenye uwezo wa kuchanuza mikondo yote ya fikra za wanajamii ni hatua muhimu katika maendeleo.Aidha, ikiwa lugha ni miongoni mwa mbinu za jamii za utashi nusura, kwa kufanya hivyo, jamii hujijengea mtandao wa mawasiliano utakaolea changilizi ya maarifa. Taifa ambalo watu wake wamegawanyika kimawasiliano hawana changilizi ya maarifa. Maana, inagawa Kiswahili kinazungumzwa na wote, lakini fikra na mijadala ya kitaalamu, hivi sasa, haina mikondo katika lugha hii. Hivyo, kama Waaarabu wa Pemba, Kiingereza ndicho kilemba cha wasomi na asiye na kilemba hicho hafaidiki na mazungumzo yao.
Hofu nyingine maarufu iliyoenea na inaendelea kusambazwa na washauri inahusiana na kukosekana kwa vitabu vya kitaaluma. Wataalamu wetu – pengine pamoja na sisi wenyewe – wanagwaya wanapoichungulia maktaba ya Kiswahili ilivyosinyaa. Wanadai kwamba, vitabu vyote vya kitaaluma vimeandikwa kwa Kiingereza. Hivyo haitakuwa busara wala kwa faida yetu endapo tutaacha Kiingereza kitoke madarasani mwetu. Hofu hii nayo ni imara kwa kiasi fulani cha masafa. Lakini ikiangaliwa kwa jicho la karibu, itaonekana kuwa hoja hii inalegalega na inatia kiinimacho katika tatizo. Hii, kwa upande mwingine, ni hoja inayodai kuwa jambo linalotafakariwa haliwezekani mpaka Kiswahili kiwe na vitabu vyake vya kitaaluma. Kila mtu anajua kuwa kutokuwako kwa vitabu vya taaluma ni jambo la hakika. Lakini kama ilivyokuwa katika suala la msamiati, matatizo ya kukosekana kwa vitabu ni changamoto kwa wataalamu wetu. Wataalamu wetu wataanza kuandika vitabu vya taaluma zao baada ya kujua kuwa kuna wasomaji na/au wanunuzi.
Utaratibu wa kuanza kutumia Kiswahili katika sekondari, ninathubutu kusema, ndio ambao utajenga mwega wa usomi wenye manufaa. Sasa hivi wasomi wengi hawafikirii kuandika vitabu kwa sababu wanaweza kufanya kazi zao kwa kutegemea vitabu vya jamii nyingine. Hivyo kitendo cha kuanzisha mijadala ya kitaalam kwa Kiswahili kitaanza kutengua mihimili ya utegemezi wa kisomi.
Swali ambalo linakuja akilini haraka ni lile linalohusu vitabu vya kutumiwa wakati vya Kiswahili vinaandikwa. Aidha, kutokuwako na vitabu vya taaluma si suala la kuzua au la kukichukia Kiswahili. Namna ya kulikabili suala hili ni kukifanya Kiswahili kifundishie kwa sauti, Kiingereza kifundishie kimya kimya. Maana ya tamko hili ni kwamba Kiswahili kiendeshe majadiliano darasani na Kiingereza kiwapatie wasomi wetu maarifa kutoka vitabuni. Kwa maneno mengine Kiingereza kiendelee kuwa lugha ya maktaba. Utaratibu huu usiwe wa muda bali uwe wa kudumu katika jamii. Utaratibu huo utawataka wanafunzi wasome vitabu na marejeo mbalimbali kwa Kiingereza lakini ufundishaji, majadiliano, mazoezi na tathmini vifanyike kwa Kiswahili. Aidha, huu ndio utaratibu unaotumika katika ufundishaji wa Isimu katika Idara ya Kiswahili ya Chuo Kikuu.
Utaratibu wa kumlazimisha mwanafunzi aeleze maarifa yake kwa lugha asiyoijua, kama ilivyo sasa, hutupotezea watu wengi wenye vipawa. Katika makala fulani, (Mochiwa 1991:15) niliuliza swali: ikitokea kwamba mwanafunzi ameulizwa: What is ice? na akajibu kwa Kiswahili: ni maji yaliyoganda: tutasema amekosa au amepata? Tukisema amekosa, amekosa nini? Haya ni miongoni mwa matatizo yanayodhihirisha udhaifu wa sera yetu ya lugha katika elimu. Kwa sera hii wasio na vipawa vya kujifunza lugha hupotea hata kama wanavyo vingine ambavyo vingeleta tumaini jipya katika jamii. Kwa hekima ya Tanzania, mpaka sasa, kujua ni kujua Kiingereza na /au kwa Kiingereza.
Suala lililojadiliwa hivi punde ni suala la uhusiano wa lugha na elimu. Tumezoezwa kuchanganya elimu na lugha. Mtu anayemwaga Kiingereza vizuri hufikiriwa kuwa ana akili, tena amesoma sana. Maana, kama Whiteley (1971) alivyopata kutamka, kwetu, Kiingereza ni elimu, na elimu ni Kiingereza. Katika miaka kumi hii iliyopita, kigezo kikuu cha tathmimi ya watu ya kuanguka kwa kiwango cha elimu nchini ni udhaifu wa wanafunzi katika Kiingereza. Inadaiwa kuwa, watoto wanafika kidato cha nne bila uwezo wa kuandika barua ya mistari miwili ya Kiingereza. Kitu ambacho wangezingatia ni kwamba Kiingereza kimemzuia mwanafunzi asikuze uwezo wake wa kufikiri na kutanzua tata. Lakini badala ya kulizingatia tatizo hili wazazi wengi wanasikitika kuwa watoto wao wanajua Kiswahili tu, eti hii ni hasara!Wazazi wanaosema kuwa watoto wao wamepata hasara kwa kujua Kiswahili wanaendeleza fikra ya usawa wa Kiingereza na elimu. Lakini kinyume cha bahati, watoto wao hata hicho Kiswahili hawakijui! Aidha, kujua Kiingereza fasaha si usomi wala akili. Lugha ni suhula tu (facility) ya kuchanuzia yale tunayofikiri. Hivyo, katika tathmini ya elimu haitoshi kupima uwezo wa kusema tu bila ya kupima uzito wa lile linalosemwa pia. Tathmini sahihi ya viwango vya elimu ni lazima izingatie jinsi Kiingereza kilivyosahilisha au kuleta pingamizi katika uelewa wa wanafunzi. Kiingereza ni chanzo cha kuanguka kwa viwango vya elimu kwa sababu hakifai kwa matumizi ya lugha ya kufundishia.
Gharama
washauri wetu wameshikilia kidinindi kuwa kukiingiza Kiswahili katika madarasa ya sekondari kuna gharama kubwa na za namna mbalimbali. Miongoni mwa gharama hizo ni ile ya matayarisho. Watu wengi wanafikiri au ni ubinu wao wa kuchelewesha utekelezaji wa matumizi ya Kiswahili sekondari – ni lazima vitabu vyote, vya kiada na ziada, vifasiriwe kwa Kiswahili. Mradi huo utaligharimu taifa mabilioni ya fedha. Baadhi ya washauri, Maghimbi (1995) kwa mfano, wanatangaza kwa midomo mipana kwamba Kiswahili hakiwezi kuwa lugha ya kufundishia mpaka vitabu vyote vya kitaaluma vimefasiriwa na kuchapishwa. Kwa kweli ikiwa Tanzania inafikiri haiwezi kutumia Kiswahili katika shule za sekondari mpaka vitabu vyote vya taaluma vifasiriwe ni kana kwamba inasema Kiswahili hakitafundishia elimu ya sekondari.
Kwa nchi maskini kama yetu, kuamua kubadilisha lugha ya kufundishia ni ujuba ikiwa, mradi wa kufasiri vitabu ni muhimu kiasi hicho. Ilivyokuwa hakuna haja ya kufasiri kitabu chochote, hakuna sababu ya kuchelewesha hatua ya kukiingiza Kiswahili katika madarasa ya sekondari. Mabadiliko ya lugha ya kufundishia ni hatua muhimu na ya kwanza kabla ya kuingia katika mchakato wa maendeleo ya kijamii. Kwamba hadi leo tumo katika majadiliano ni dalili kuwa bado hatujapafahamu pa kuanzia safari yetu ya maendeleo.
Gharama nyingine kubwa iliyojizonga akilini mwa washauri wetu ni ule uwezekano wa kutoka kwenye kambi ya wasema Kiingereza. Itakumbukwa kwamba nchi za Kiafrika zimo katika makambi ya lugha za wale waliozitawala. Tanzania na nchi nyingine zilizotawaliwa na Waingereza ni za kambi ya Anglophone. Zilizotawaliwa na Wareno zimo katika kambi ya Lusophone na za Wafaransa ni za kambi ya Francophone. Kwa mtazamo huo washauri, kama Maghimbi (1995) wanafikiria haitakuwa salama kama tutatoka kwenye kambi ya Waingereza. Msingi wa rai hii uko mara mbili. Kwa upande mmoja, washauri wanalinda mazoea na kwa upande wa pili wanafirki kwamba Watanzania watakuwa wameandalika kwa masomo nchi za nje. Pengine inasemekana kuwa kuendeleza mtindo huu kunawapatia Watanzania uwezo wa kuwasiliana na watu wa nje.
Tathmini yagharama hizi inaonesha kuwa ushauri unaelekeza kwenye haja ya uanachama wa u-anglophone bila kujiuliza kama upo uwezekano wa kuupata. Isitoshe ushauri haukuzingatia kwamba kazi kubwa ya lugha katika elimu si kutufutia uanachama. Ushauri umeendelea kulifumbia macho suala la kutojulikana kwa Kiingereza nchini Anayetumia lugha kwa masomo au kutafuta urafiki ni yule anayejua lugha yenyewe. Je, ni nani ambaye, hadi sasa, hajui kwamba Kiingereza hakijulikani nchini kwa kiwango cha kuendeshea mawasiliano yanayoweza kuonesha fikra pevu?
Zaidi ya kufumbia macho suala la kutojulikana kwa Kiingereza, kuna ule ushauri wa kuwaandaa Watanzania kwa masomo ya nje ambao ni dhaifu. Hii ni kwa sababu, kwa hali ilivyo sasa hivi, si sahihi kufikiri kila penye asasi ya elimu patazungumzwa Kiingereza. Watanzania wamekwenda  China, Japani, Ujerumani na sehemu nyingine nyingi mbalimbali ambazo hazitumii Kiingereza. Ke bado watu wale wamesoma. Pengine ingekuwa bora kwa Mtanzania kujifunza lugha yoyote kule inakozungumzwa na wazawa wake kuliko tunavyofikiri tunajifunza Kiingereza hapa ambapo hakina wazungumzaji wazawa.
Hasara ya kung’ang’ania Kiingereza
Baada ya mjadala wa ushauri wa kutelekeza Kiswahili, kikabakia lugha ya kuuzia karanga kwa muda wote huu, ni vyema tutafakari kidogo hasara au tuseme, gharma ya kung’ang’ania Kiingereza. Gharama kubwa tunayobeba ni kuendeleea kwa kutenguka kwa elimu. Kiingereza kinaendelea kuzuia makusano kati ya walimu na wanafunzi na kwa hivyo umaizi wa ubongo wa mtoto haupati nafasi ya kuongezeka. Kwa maana hii, mchakato wa elimu mpaka sasa haujaweza kuwasaidia wanafunzi kujifunza kufikiri, na hasa kufikiri haraka haraka. Ingawa sina ushahidi wa kisayansi kuhusu jambo hili, lakini ninahisi kwamba, kwa kuwa hatukimiliki ipasavyo, tunapokitumia, Kiingereza kinapunguza kasi ya kufikiri. Kama Powell (1997) anavyosema, kujifunza lugha ni kupata mamlaka ya kutawala mazingira na kutawala ulimwengu wa uzoevu. Wanafunzi wasiojua Kiingereza watatarajiwa vipi kutawala mazingira yao au taaluma zao?
Kung’ang’ania Kiingereza katika kuendeshea maisha ya taifa hili kunawanyima wanajamii haki za msingi za binadamu. Nitachukua mifano kutokana na kuchungua sehemu tatu. Sehemu ya kwanza inahusu haki ya kuishi duniani. Hospitali zimesambazwa nchini kuhakikisha kuwa kila mwanajamii anapata huduma anapougua ili apone. Wahudumu wetu wamejifunza huduma hiyo kwa Kiingereza. Ikiwa sote tunajua kuwa Kiingereza hakifahamiki vizuri, tuna hakika gani kuwa Madaktari na Manesi wao wanaelewana? Lini taifa litagundua hatari ya unasibu wa lugha? Unasibu wa lugha ndio uliosababisha neno moja la Kiarabu lipokewe kwenye Kiingereza kuwa ‘risk’ kitu au tukio la hatari na katika Kiswahili ‘riziki’ kitu cha kukidhi haja! Ingawa sina takwimu,- na si rahisi kuzipata-lakini kuna uwezekano mkubwa wa kuwako kwa vifo ambavyo vimetokana na mawasiliano butu kati ya Daktari na Nesi, au kutoiva kikamilifu kwa Daktari au Nesi mwenyewe.
Sehemu ya pili inahusu sheria. Ninaambiwa mpaka leo, waheshimiwa wanasheria huweka kumbukumbu zao kwa lugha ya Kiingereza, hata kama washitaki na washitakiwa wametumia Kiswahili au lugha nyingine. Wao wameaminiwa kuwa ‘wafasiri’ wasiojikwaa! Lakini kwa mujibu wa ninavyojua dhati ya lugha, unasibu wake pamoja na matatizo yanayofafanuliwa katika nadharia za tafsiri (ang. Nida 1964), ninahisi kwa nguvu kuwa wako watu ambao wamezama magerezani kwa kutokana na mabadilikobadiliko haya ya lugha. Kosa la tafsiri linaumba hatia ya mshitakiwa. Jambo kama hili linapotokea, kuna mwanajamii mmoja ambaye atakuwa amenyimwa haki yake ya kimsingi. Ni dhahiri kwamba jamii inashindwa kulinda haki za watu.
Sehemu ya tatu inahusu haki ya kujiendeleza. Tanzania ilikuwa maarufu duniani kwa kuweka kipaumbele katika maendeleo ya elimu ya watu wazima. Kinyume cha bahati, jitihadi za mtu anayeanza kujielimisha haziwezi kuvuka elimu ya msingi. Hii ni kwa sababu akipita kiwango cha shule ya msingi hawezi kusonga mbele kwa kuwa hajui lugha ya Kiingereza. Jambo hili linazidi ugumu kwa kuwa mhitimu wa kisomo chenye manufaa atajiendeleza nje ya mazingira ya shule. Sasa ikiwa wanafunzi wa kidato cha kwanza, wenye miaka kumi na nne au kumi na tano, wanashindwa kujifunza Kiingereza mbele ya mwalimu wao, mtu aliyeanza kisomo cha manufaa na miaka arobaini ataweza kujifunza Kiingereza chini ya mwembe? Ikiwa hana Kiingereza, mwanakisomo atajiendelezaje? Kwa utaratibu wa sasa, matumizi ya Kiingereza yanazuia mienendo ya elimu nchini. Hivyo elimu si ya wote bali ni haki ya wachache, tena, wenye kipawa madhubuti cha lugha.
Suala hili lililojadiliwa hivi punde halimwathiri mtu mmoja mmoja tu, bali jamii nzima. Jamii inawazuia watu ambao, kama wangepata nafasi ya kujiendeleza, wangekuwa wabunifu na watundu wa manufaa kwa taifa. Ama, hali hii nayo inahuzunisha. Huenda taifa halipati wasiwasi kwa imani kuwa wavumbuzi au wagunduzi watapatikana Chuo Kikuu. Lakini, kwamba rai hii imepotoka, inaonekana kwa kusoma kwenye magazeti kuwa kuna watu vijijini wanaweza kutengeneza vitu vya kisasa kama silaha. Aidha, labda kwa sababu ya imani ileile ya wavumbuzi kuwa watu wa Chuo Kikuu, watu hawa wanapogundulika hupata misukosuko. Isingekuwa hivyo, watundu hawa wangepewa kipaumbele. Watu hawa, kwa kuonekana umuhimu wao kwa taifa, wangeengwaengwa na kubembeslezwa wajiunge na jeshi ili taifa lifaidike.
Makusudi yangu hapa ni kwamba si siku zote wavumbuzi watatoka vyuoni. Kuendelea na matumizi ya Kiingereza katika elimu ya juu ni kuziba uwezekano wa kupatikana kwa watu walio na vito muhimu kwa maendeleo ya taifa.
Pamoja na umaarufu wake – kwa herufi na harufu-Tanzania haiwezi kukipa Kiingereza kiti kikakaa hapa nchini kwa makusudi ya kuongeza ukuzaji wa umaizi wa Watanzania. Hii haina maana kuwa Kiingereza hakifai au hakitakiwi nchini. Haya si makusudi ya makala. Bali kinachokusudiwa hapa ni kwamba, kwa mazingira tuliyo nayo, upeo wa ufundishaji, muda na mbinu za ufundishaji, si rahisi kukifundisha kikajulikana ganda na kiini. Aidha, wataalamu wengi (Qorro, et al 1987, Trappes – Lomax et al (eds) 1982) wameonesha wazi kuwa Kiingereza hakiwezi kufundishwa hadi aliyefundishwa akafikia kiwango cha umilisi wa kuchambua fikra au viumbile dhahania. Ziko sababu nyingi zinazosababisha hali hii, lakini hapa tutachambua mbili: Muda na mazingira. Tutaanza na muda.
Muda
Tanzania haina budi kuelewa kuwa kufundisha na hasa kujifunza lugha kunataka muda mrefu. Kujua kuwa hivyo ndivyo, tujiulize mtoto mchanga anayejifunza lugha yake ya maziwa anahitaji muda gani. Mtaalam mmoja (ang. Hammerly 1982) alidai kuwa mtoto anatumia saa 18,000 za kujifunza lugha hiyo ya kwanza. Kwa kuwa suala hili halikutiwa ndani ya mizani zetu sawasawa, Tanzania inaona kuwa saa 800 za kujifunza Kiingereza (soma. Mochiwa 1991) katika shule ya msingi zinatosha. Baya zaidi ni kwamba, ilihali anapojifunza lugha ya kwanza mtoto anakutana nayo kwa wakati mwafaka, wakati ambao ubongo na hisia havijui kukataa wala kudharau, lakini mtoto wa shule ya msingi anakutana na Kiingereza kwa wakati usio mwafaka. Anakuwa amekwisha vuka umri wa kawaida wa kujifunza lugha.
Tunapoendelea kuwalinganisha watoto wawili hawa, tunaona kwamba anayejifunza lugha ya mama hana ratiba yoyote ya shughuli. Yeye hatumwitumwi na wala halazimishwi kujifunza kipengee fulani kilichomo mwenye muhtasari. Lakini huyu aliye shuleni hupewa hizo saa 800 za Kiingereza ndani ya ratiba ya masomo mengine. Kana kwamba hii haitoshi, hizo saa mia nane zimetawanywa kwa kipindi cha miaka mitano, kuanzia darasa la tatu hadi la saba. Yule mtoto aliye nyumbani ana saa nyingi na haziingiliwi na mambo mengine isipokuwa usingizi tu.
Tunapolinganisha muda huu mrefu wa kusharabu lugha, itakuwa hatuangalii mambo kiuhakikifu (objectively) kama tutatarajia Kiingereza kijengeke katika akili ya mtoto kwa muda huu mfupi. Ikiwa tunataka Kiingereza kijengeke basi inabidi ratiba ya shule isogelee hizo saa 18,000. Lakini hii ina maana kwamba, kwa muda wa miaka isiyopungua mitatu, Watanzania hawana budi wazamishwe kwenye programu ya Kiingereza. Kwa rai yangu hatua ya namna hii haiwezekani kwa sababu nyingi, lakini kubwa, ni gharama yake ya mali na muda.
Mazingira
Mtoto anapojifunza lugha ya kwanza anafunikwa na lugha anayojifunza. Mtoto anayejifunza Kiingereza shuleni hana bahati hiyo. Kwake, Kiingereza hakisikiki, maana hakitumiki kuongoza maisha ya kila siku. Hivyo, dafaa za kukisikia Kiingereza ni chache sana. Ni lugha ambayo itasikika darasani na si muktadha utakaomfanya mtoto aone jinsi lugha yenyewe inavyofanya mambo yaende.
Mazingira ya ufundishaji wa Kiingereza ni ya kuigiza heba ambayo haipo katika jamii. Maadamu ‘Kiingereza’ maana yake ni ‘kwa namna’ au kwa ‘mila ya’ au ‘mwenendo wa’ Waingereza, Kiingereza ndani ya mazingira ya Kiswahili kinahitaji jitihada kubwa za kukifanya kimee. Kujifunza namna au mwenendo wa Kiingereza kunahitaji uamuzi na nidhamu ya kisaikolojia. Heba hiyo hiyo iliyosisitizwiwa umuhimu wa kujivunia. Uswahili, Uafrika ndiyo hiyo hiyo inayoingizwa katika majaribu ya kuenenda naau kujifasili kwa Kiingereza. Migongano ya aina hii ndiyo inayosababisha elimu nchini Tanzania kuwa maigizo na si maisha.
Mwisho
Mchakato wa elimu katika Tanzania hauna tofauti na maigizo kwa sababu mbili. Kwanza, ingawa unatakiwa umfanye mpokeaji awe ‘huyo mtu wa ndoto’ lakini kwa kutokana na sera ya lugha iliyopo, mchakato wa elimu unamfanya mpokeaji awe KAMA ‘huyo mtu wa ndoto’ Mtu huyo wa ndoto si Mtanzania bali ni Mwingereza. Ilivyokuwa haiwezekani, Mngoni kuzaa Mzigua, vivyo hivyo Mtanzania hawezi kuzaa Mwingereza. Kwa mantiki hiyo, mchakato wa elimu unampeleka mtanzania kuzaa ‘Kizuu cha Mwingereza’ au Mmarekani, mpokeaji wa elimu ya Tanzania atakuwa anaingiza heba ya Kiingereza na/au Kimarekani kwa mwenendo wa fikra na msemo. Mpokeaji huyo hataishi kwa heba ya kwao bali ataishi kwa heba ya kuazima.
Pili, mpokeaji wa elimu hii atakuwa ana utapia elimu mkubwa kwa sababu ya pingamizi la lugha ambalo humkabili katika mchakato mzima. Hatapata kiwango cha weledi sawa na mtu wa ndoto ambaye Tanzania imemwekea. Katika mazingira haya, mfumo wa elimu unakuwa mchakato wa kuingia utumwani na si wa kumpatia uhuru kama unavyotarajiwa na Nyerere na Freire (op.cit). Anapoumaliza mfumo wa elimu, mpokeaji hatalingana na Mwingereza kwa uwezo wa kuchambua, kuwaza, kusasanya mambo wala kusasanyua. Kutokana na kuung’amua ukweli huu, mhitimu atasema moyoni mwake ‘Wazungu,wazungukeni!’
Zaidi ya kuufanya kuwa mchakato wa kuvuruga mfumo wa kujiamini wa mpokeaji sera ya lugha inamnyima mpokeaji haki za msingi za kibinadamu. Haki hizo ni pamoja na ya kujielimisha, ya mazingira ya kupata tiba isiyo na madhara kwake na ya kupata haki mbele ya sheria. Watanzania hawana hakika ya kukuza akili zao, ya kupata matibabu sahihi wala ya kutendewa haki wanapokabiliwa na daawa. Yote haya ndiyo matokeo ya maigizo ya kielimu yanayosababishwa na matumizi ya Kiingereza katika elimu. Wanaonufaika katika vurumai hii ni watu wenye kipawa cha lugha tu. Aidha vurumai hii hunufaisha sana mataifa ya nje kwa sababu kwao Watanzania ni ‘wateja’.
Mwl Maeda
Reply


Forum Jump:


Users browsing this thread: 1 Guest(s)